Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Vijana Acheni wazazi wenu wawasaidie kulinda mioyo yenu!

Vijana Acheni wazazi wenu wawasaidie kulinda mioyo yenu!

Vijana Acheni wazazi wenu wawasaidie kulinda mioyo yenu!

UNAFIKIRI ni kazi gani iliyo ngumu zaidi ambayo nahodha hukabili? Je, ni kuvuka bahari kubwa kwa usalama? Kwa kawaida sivyo. Meli nyingi huvunjika karibu na ufuo, si baharini. Kwa kweli, inaweza kuwa hatari zaidi kuegesha meli kuliko kuelekeza ndege itue. Kwa nini?

Kabla ya nahodha kuegesha meli yake, anapaswa kuepuka hatari zote zinazoweza kuwa katika bandari fulani. Anapaswa kujua mikondo ya bahari huku akiepuka kugonga meli nyingine. Pia anapaswa kukwepa kingo za mchanga, miamba, au mabaki yaliyofichika chini ya maji. Na hatari kubwa hata zaidi inaweza kuwa hiyo ndiyo mara yake ya kwanza kufika kwenye bandari hiyo.

Ili kukabiliana na matatizo hayo, huenda nahodha mwenye busara akaomba msaada kutoka kwa rubani anayefahamu vizuri bandari hiyo. Rubani husimama kando ya nahodha katika chumba au jukwaa la kuendeshea meli na kutoa mwongozo wa kitaalamu. Wao hufikiria pamoja hatari wanazoweza kukabili kuielekeza meli kupitia njia yoyote nyembamba hadi bandarini.

Mashauri ya kitaalamu ya rubani yanaonyesha msaada muhimu unaopatikana kwa vijana Wakristo ambao wanalazimika kukabiliana na hali ngumu maishani. Msaada huo ni upi? Kwa nini matineja wanauhitaji?

Na tuendelee na ule mfano wa meli. Ikiwa wewe ni kijana, kwa njia fulani unafanana na nahodha wa meli kwa kuwa mwishowe itakubidi kuchukua daraka kuhusiana na maisha yako. Nayo kazi ya wazazi wako ni kama ile ya rubani wa meli wanapojitahidi kukuongoza kukabiliana na hali ngumu sana zitakazotokea maishani. Hata hivyo, unapokuwa tineja, huenda ukaona ni vigumu kukubali shauri la wazazi wako. Kwa nini?

Mara nyingi, tatizo huhusiana na moyo. Moyo wako wa mfano unaweza kukuchochea utamani mambo unayokatazwa au kupinga jambo lolote unalohisi kuwa linakunyima uhuru. Biblia inasema, “Mwelekeo wa moyo wa mwanadamu ni mbaya tangu ujana wake na kuendelea.” (Mwanzo 8:21) Yehova anakuambia waziwazi kwamba utakabiliana na jaribu. Anaonya, “Moyo ni wenye hila kuliko kitu kingine chochote nao ni hatari.” (Yeremia 17:9) Mbali na kusitawisha tamaa mbaya kisiri, moyo unaweza kumdanganya kijana afikiri kwamba anajua mengi zaidi kuliko wazazi wake, hata ingawa wao wana uzoefu mwingi zaidi. Hata hivyo, kuna sababu nzuri za kutafuta msaada kutoka kwa wazazi wako unapokabiliana na miaka migumu ya utineja.

Kwa Nini Uwatii Wazazi Wako?

Zaidi ya yote, Yehova, aliye Mwanzilishi wa familia, anakuambia kwamba unapaswa kufuata mwongozo wa wazazi wako. (Waefeso 3:15) Kwa kuwa Mungu amewapa wazazi wako daraka la kukutunza, anakushauri hivi: “Enyi watoto, watiini wazazi wenu Kikristo maana hili ni jambo jema.” (Waefeso 6:1-3, BHN; Zaburi 78:5) Ingawa huenda ikawa sasa wewe ni tineja, bado wazazi wako wana daraka la kukuongoza, nawe una wajibu wa kuwasikiliza. Mtume Paulo alipoandika kwamba watoto wanapaswa kuwatii wazazi wao, alitumia neno la Kigiriki linaloweza kuhusisha watoto wa umri wowote. Kwa mfano, kama inavyotajwa katika Mathayo 23:37, Yesu aliwaita wakaaji wa Yerusalemu “watoto,” hata ingawa wengi wao walikuwa watu wazima.

Watu wengi wenye imani wa nyakati za kale waliendelea kuwatii wazazi wao muda mrefu hata baada ya kuwa watu wazima. Ingawa Yakobo alikuwa mtu mzima, alielewa kwamba alipaswa kutii amri ya baba yake ya kuepuka kuoa mwanamke asiye mwabudu wa Yehova. (Mwanzo 28:1, 2) Ni wazi kwamba Yakobo pia alikuwa ameona jinsi wazazi wake walivyokerwa sana na uamuzi wa ndugu yake wa kuoa wanawake wapagani wa Kanaani.—Mwanzo 27:46.

Mbali na wajibu waliopewa na Mungu wa kukuongoza, yaelekea wazazi wako Wakristo ndio washauri bora zaidi. Hiyo ni kwa sababu hasa wanakujua vizuri sana na bila shaka wamekuonyesha upendo usio na ubinafsi kwa miaka mingi. Kama nahodha wa meli, wao huzungumza kutokana na yale ambayo wamejionea. Wao wenyewe wamepatwa na “tamaa zinazotukia ujanani.” Na wakiwa Wakristo wa kweli, wameona manufaa ya kufuata kanuni za Biblia.—2 Timotheo 2:22.

Kupitia msaada wa watu wenye uzoefu, unaweza kufanikiwa kukabiliana na hali ngumu sana. Kwa mfano, fikiria uhusiano wako pamoja na watu wa jinsia tofauti. Wazazi Wakristo wanaweza kukuongozaje katika jambo hili la kibinafsi?

Kuvutiwa na Watu wa Jinsia Tofauti

Marubani huwashauri manahodha wasikaribie kingo za mchanga. Kingo za mchanga ni laini na hatari pia, kwa kuwa hazibaki mahali palepale. Vivyo hivyo, wazazi wako watataka ujiepushe na hali zinazoweza kukunasa kihisia-moyo. Kwa mfano, wazazi wanajua kwamba hisia kuelekea watu wa jinsia tofauti huwa nyingi na si rahisi kuzieleza. Lakini zinapoamshwa, hisia hizo zinaweza kukuletea madhara.

Kielelezo cha Dina kinaonyesha hatari ya kukaribia sana hali yenye kuhatarisha. Labda udadisi na tamaa ya kujifurahisha ndiyo mambo yaliyomchochea Dina kufanya urafiki na wasichana Wakanaani, ambao bila shaka maadili yao yalikuwa yamepotoka. Hali ya kujifurahisha ambayo mwanzoni ilionekana kuwa isiyo na madhara yoyote, punde si punde ilitokeza jambo la kuhuzunisha—alilalwa kinguvu na kijana “mwenye kuheshimika zaidi” mjini.—Mwanzo 34:1, 2, 19.

Hatari hizo ni nyingi hata zaidi katika nyakati hizi tunamoishi ambapo ngono inakaziwa sana. (Hosea 5:4) Huenda vijana wengi wakafanya ufikiri kwamba inapendeza sana kujifurahisha na watu wa jinsia tofauti. Huenda ukasisimuliwa na wazo la kuwa pamoja na mtu fulani anayekuvutia. Lakini wazazi wenye upendo watajaribu kukulinda usishirikiane na vijana wasioheshimu viwango vya Mungu.

Laura anakiri kwamba matineja wanaweza kupotoshwa na udadisi wasione hatari. “Wasichana wa darasa langu wanaponiambia kwamba walicheza dansi hadi usiku wa manane pamoja na wavulana wenye kuvutia, hilo husikika kuwa jambo lisiloweza kusahaulika. Ninajua kwamba mara nyingi wao hutilia chumvi habari hizo, lakini bado ninahisi nikivutiwa na mambo hayo na kufikiri kwamba labda ninanyimwa raha fulani. Ingawa ninajua kwamba wazazi wangu wanafanya vizuri kutoniruhusu kwenda sehemu kama hizo, bado ninavutiwa.”

Meli haina breki, kwa hiyo inachukua muda mrefu kabla ya kusimama. Wazazi wanajua kwamba tamaa ni kama meli. Kitabu cha Methali humlinganisha mtu anayeongozwa na hisia zisizodhibitiwa, na ng’ombe-dume anayeelekezwa machinjoni. (Methali 7:21-23) Hungependa kupatwa na jambo kama hilo ambalo litakufanya upatwe na madhara ya kihisia-moyo na ya kiroho. Wazazi wako wanaweza kutambua wakati moyo wako unapoanza kukupotosha kuhusiana na habari hii, nao wanaweza kukushauri ifaavyo. Je, utaonyesha hekima kwa kuwasikiliza na hivyo kuepuka hatari?—Methali 1:8; 27:12.

Pia unahitaji utegemezo wa wazazi wako inapokubidi kukabiliana na msongo wa marika. Wanaweza kukusaidiaje?

Uvutano Wenye Kushawishi wa Marika Wako

Mkondo wa maji wenye nguvu unaweza kufanya meli ipoteze mwelekeo. Ili kuepuka mkondo huo, meli inapaswa kuelekezwa upande mwingine. Vivyo hivyo, usipochukua hatua, uvutano wenye kushawishi wa vijana wengine unaweza kufanya upoteze mwelekeo wa kiroho.

Kama vile mambo yaliyompata Dina yanavyoonyesha, ‘ukishirikiana na wajinga, utapatwa na mabaya.’ (Methali 13:20) Kumbuka kwamba Biblia hutumia neno “mjinga” kurejelea mtu asiyemjua Yehova au anayeamua kutotembea katika njia zake.

Hata hivyo, huenda isiwe rahisi kukataa maoni au mazoea ya wanadarasa wenzako. María José anasema: “Nilitaka kukubaliwa na vijana wengine. Kwa kuwa sikutaka wafikiri kwamba mimi ni tofauti, niliiga karibu kila kitu walichofanya.” Huenda ukaathiriwa na marika wako bila kutambua—katika muziki unaochagua, mavazi, au hata namna ya kuzungumza. Labda unahisi kustarehe unapokuwa na vijana wa rika lako. Hilo ni jambo la kawaida, lakini utaathiriwa na uvutano wao wenye nguvu, ambao unaweza kuleta madhara.—Methali 1:10-16.

Caroline anakumbuka magumu aliyokabili miaka michache iliyopita: “Nilipokuwa na umri wa miaka 13, wasichana wengi nilioshirikiana nao walikuwa na marafiki wa kiume, na kwa miaka kadhaa nilikabili msongo usiokoma wa kuiga kielelezo chao. Hata hivyo, mama yangu aliniongoza wakati huo mgumu. Alinisikiliza kwa muda wa saa nyingi, akijadiliana nami, na kunisaidia nione umuhimu wa kutokuwa na urafiki kama huo hadi nikomae zaidi.”

Kama mama ya Caroline, huenda wazazi wako wakahisi kwamba wana wajibu wa kukuonya kuhusu msongo wa marika au hata kukukataza mambo fulani au marafiki fulani. Nathan anakumbuka jinsi alivyobishana na wazazi wake mara kadhaa kuhusiana na mambo hayo. “Mara nyingi marafiki wangu walinialika nishirikiane nao,” anasema, “lakini wazazi wangu hawakutaka nifuatane na umati au niende kwenye karamu kubwa zisizosimamiwa vizuri. Wakati huo, singeweza kuelewa kwa nini wazazi wengine hawakuwa na sheria nyingi kama wazazi wangu.”

Hata hivyo, baadaye Nathan alielewa sababu. “Ninajua kwamba kuhusiana na kisa changu, ‘ujinga ulikuwa umefungwa pamoja na moyo wa mvulana,’” anakiri. “Ujinga huo hujitokeza kwa urahisi wavulana wanapokuwa pamoja katika vikundi. Mvulana mmoja huanza kufanya jambo fulani baya, mwingine hufanya jambo baya zaidi, na wa tatu hufanya hali iwe mbaya hata zaidi. Punde si punde, wote wanachochewa kufanya jambo hilo baya. Hata vijana wanaodai kumtumikia Yehova wanaweza kuangukia mtego huo.”—Methali 22:15.

Nathan na María José walipingana na mioyo yao wakati wazazi wao walipowakataza kufanya mambo fulani yaliyopendekezwa na marika wao. Hata hivyo, walisikiliza, na baadaye walifurahi kufanya vile walivyoambiwa. Methali inasema: “Tega sikio lako usikie maneno ya wenye hekima, ili kuutia moyo wako katika ujuzi wangu.”—Methali 22:17.

Wanastahili Kuheshimiwa

Ni vigumu kuelekeza meli ambayo imeinama upande mmoja, na ikiinama sana, inaweza kuzama kwa urahisi. Kwa sababu ya kutokamilika kwetu, sote tuna mwelekeo wa ubinafsi na wa kutaka kufanya mambo ambayo tumekatazwa. Licha ya maelekeo hayo, bado vijana wanaweza kufanikiwa maishani, ikiwa watafuata mwongozo wa wazazi wao kwa makini.

Kwa mfano, wazazi wako wanaweza kukusaidia ukatae wazo la kwamba kuna barabara nyingine katikati ya ile barabara nyembamba inayoongoza kwenye uzima na ile pana inayoongoza kwenye uharibifu. (Mathayo 7:13, 14) Pia ni jambo lisilopatana na akili kufikiri kwamba unaweza kufurahia kidogo jambo baya bila kuvunja sheria za Mungu, kana kwamba unaweza “kuonja” dhambi bila kuimeza. Wale wanaojaribu kufuata mwenendo huo ‘wanayumba-yumba juu ya maoni mawili tofauti’—kumtumikia Yehova kwa kiwango fulani lakini pia kuupenda ulimwengu na vitu vilivyo katika ulimwengu—na wanaweza kuzama kiroho kwa urahisi. (1 Wafalme 18:21; 1 Yohana 2:15) Kwa nini tunaweza kuzama kiroho kwa urahisi? Kwa sababu ya maelekeo yetu yenye dhambi.

Tamaa zetu zenye dhambi huwa zenye nguvu zaidi tunapojiachilia. ‘Moyo wetu wenye hila’ hautatosheka tu kwa “kuonja” dhambi. Utadai tufanye zaidi. (Yeremia 17:9) Tunapoanza kupeperuka kiroho pole kwa pole, ulimwengu unakuwa na uvutano mkubwa zaidi juu yetu. (Waebrania 2:1) Huenda usitambue kwamba unainama kiroho, lakini yaelekea wazazi wako Wakristo watatambua. Ni kweli kwamba huenda wasijifunze kompyuta kwa urahisi kama wewe, lakini wanajua mengi zaidi kuliko wewe kuhusu moyo wenye hila. Nao wanataka kukusaidia ‘uuongoze moyo wako katika njia’ inayoweza kuelekeza kwenye uzima.—Methali 23:19.

Bila shaka, usitarajie wazazi wako waamue mambo kwa ukamilifu wanapohitaji kukupa mwongozo kuhusiana na masuala magumu kama vile muziki, vitumbuizo, na kujipamba. Huenda wazazi wako wasiwe na hekima kama ya Sulemani au na subira kama ya Ayubu. Kama rubani wa meli, huenda nyakati nyingine wakawa wenye tahadhari kupita kiasi ili kuepuka hatari. Hata hivyo, mwongozo wao unaweza kuwa wenye thamani ikiwa utasikiliza ‘nidhamu ya baba yako, na kutoacha sheria ya mama yako.’—Methali 1:8, 9.

Vijana wengine wanaweza kuongea kwa dharau kuhusu wazazi wao. Hata hivyo, ikiwa wazazi wako wanajitahidi kufuata Maandiko, wao ni kama rubani wa meli, wako pamoja nawe chini ya hali zozote, unapokabili hatari za kila namna. Kama nahodha wa meli ambaye hushauriwa na rubani mwenye uzoefu, unahitaji kuongozwa na wazazi wako, katika njia ya hekima. Thawabu za kufanya hivyo hazina kifani.

“Hekima inapoingia moyoni mwako na ujuzi kupendeza nafsi yako, uwezo wa kufikiri utakutunza, utambuzi utakulinda, ili kukukomboa kutoka katika njia mbaya, na kutoka kwa mtu anayesema mambo mapotovu, kutoka kwa wale wanaoacha mapito ya unyoofu ili watembee katika njia za giza . . . Kwa maana wanyoofu ndio watakaokaa duniani, na wasio na lawama ndio watakaobaki ndani yake.”—Methali 2:10-13, 21.

[Picha katika ukurasa wa 22]

Uvutano wa vijana wengine unaweza kufanya upoteze mwelekeo wa kiroho

[Picha katika ukurasa wa 23]

Kumbuka mambo yaliyompata Dina

[Picha katika ukurasa wa 24]

Kama vile nahodha wa meli hutafuta mashauri ya rubani mwenye uzoefu, vijana wanapaswa kutafuta mwongozo wa wazazi

[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 24]

Photo: www.comstock.com