Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Washikamanifu na Imara Zamani na Sasa

Washikamanifu na Imara Zamani na Sasa

Washikamanifu na Imara Zamani na Sasa

Kuna mji mdogo unaoitwa Wisła ambao uko kusini mwa Poland, karibu na mpaka wake na Slovakia na Jamhuri ya Cheki. Ingawa huenda hujawahi kusikia kuhusu mji wa Wisła, mji huo una historia ambayo yaelekea itawavutia Wakristo wa kweli. Ni historia inayoonyesha utimilifu na bidii kwa ajili ya ibada ya Yehova. Jinsi gani?

MJI wa Wisła uko katika eneo maridadi lenye milima ambako unaweza kuona vizuri milima hiyo yenye kuvutia sana. Vijito vyenye kutiririka kwa kasi huungana na Mto Vistula, ambao hujipinda-pinda kupitia milima na mabonde yenye misitu. Uchangamfu wa wenyeji na pia hali ya hewa ya kipekee, hufanya mji wa Wisła uwe kituo maarufu cha matibabu, mahali pa kwenda likizo wakati wa kiangazi, au kutembelea wakati wa baridi kali.

Inaonekana kwamba kijiji cha kwanza kupewa jina hilo kilianzishwa miaka ya 1590. Kiwanda cha kupasulia mbao kilijengwa, na muda si muda sehemu za milima zisizo na miti zilikuwa na walowezi, waliofuga kondoo na ng’ombe na pia kulima. Lakini watu hao wa kawaida waliathiriwa na mabadiliko ya haraka ya kidini. Eneo hilo liliathiriwa sana na marekebisho ya kidini yaliyoanzishwa na Martin Luther, nayo Dini ya Wafuasi wa Luther ikawa “dini ya Serikali mwaka wa 1545,” kulingana na mtafiti Andrzej Otczyk. Hata hivyo, vile Vita vya Miaka 30 na yale Marekebisho Makubwa ya Kanisa Katoliki yaliyofuata yalibadili hali kabisa. Otczyk aendelea kusema, “Mnamo mwaka wa 1654, makanisa yote yalitwaliwa kutoka kwa Waprotestanti, ibada yao ikapigwa marufuku, nazo Biblia na vitabu vingine vya kidini vikatwaliwa.” Hata hivyo, wenyeji wengi waliendelea kuwa wafuasi wa Luther.

Mbegu za Kwanza za Kweli ya Biblia

Jambo la kufurahisha ni kwamba marekebisho mengine ya kidini yaliyo muhimu zaidi yalikuwa karibu kutokea. Mnamo mwaka wa 1928, mbegu za kwanza kabisa za kweli ya Biblia zilipandwa na Wanafunzi wawili wa Biblia wenye bidii, kama Mashahidi wa Yehova walivyoitwa wakati huo. Mwaka uliofuata, Jan Gomola alifika Wisła akiwa na kinanda kilichotumiwa kucheza sahani za santuri zilizokuwa na hotuba za Biblia. Kisha akaelekea kwenye bonde lililokuwa karibu ambako alipata mtu mwenye kusikiliza kwa makini—Andrzej Raszka, wa mlimani aliyekuwa mfupi, mwenye nguvu, na mwenye moyo mnyoofu. Mara moja Raszka alitoa Biblia yake ili kuthibitisha mambo yaliyosemwa katika hotuba hizo zilizorekodiwa. Kisha akasema kwa mshangao: “Ndugu yangu, hatimaye nimeipata kweli! Nimekuwa nikitafuta majibu tangu nilipokuwa nikipigana Vita vya Kwanza vya Ulimwengu!”

Akiwa na furaha tele, Raszka alimpeleka Gomola kwa rafiki zake Jerzy na Andrzej Pilch, ambao waliitikia vizuri ujumbe wa Ufalme. Andrzej Tyrna, ambaye alikuwa amejifunza kweli za Biblia huko Ufaransa, aliwasaidia watu hao waongeze ujuzi wao wa ujumbe wa Mungu. Baada ya muda mfupi wakabatizwa. Ili kusaidia kikundi kidogo cha Wanafunzi wa Biblia huko Wisła, akina ndugu kutoka miji iliyo karibu walitembea huko katikati ya miaka ya 1930. Kulikuwa na matokeo mazuri sana.

Wapya wenye kupendezwa walimiminika kwa wingi. Familia za wenyeji ambao walikuwa wafuasi wa Luther walikuwa na desturi ya kusoma Biblia nyumbani mwao. Kwa hiyo, walipofahamu hoja za Biblia zenye kusadikisha kuhusu fundisho la moto wa mateso na Utatu, wengi wangeweza kutofautisha ukweli na uwongo. Familia nyingi ziliamua kuacha kufuata mafundisho ya kidini ya uwongo. Hivyo, kutaniko la Wisła lilikua, na kufikia mwaka wa 1939, likawa na washiriki wapatao 140. Hata hivyo, jambo la kushangaza ni kwamba watu wengi wazima katika kutaniko hilo hawakuwa wamebatizwa. “Hii haimaanishi kwamba wahubiri hao wasiobatizwa hawakuweza kuchukua msimamo upande wa Yehova,” asema Helena, mmoja wa Mashahidi hao wa zamani. Anaongeza kusema: “Walidumisha utimilifu wao baada ya kukabili majaribu ya imani muda mfupi baadaye.”

Namna gani watoto? Waliona kwamba wazazi wao wamepata kweli. Franciszek Branc anasema: “Baba yangu alipotambua kwamba amepata kweli, alianza kuikazia kwangu na kwa ndugu yangu. Nilikuwa na umri wa miaka minane naye ndugu yangu alikuwa na miaka kumi. Baba alikuwa akituuliza maswali rahisi kama vile: ‘Mungu ni nani, na jina lake ni nani? Ni habari gani unazojua kumhusu Yesu Kristo?’ Ilitubidi kuandika majibu yetu na kuyathibitisha kwa kutumia mistari ya Biblia.” Shahidi mwingine anasema: “Kwa kuwa wazazi wangu walikubali ujumbe wa Ufalme kwa hiari na kuacha kushirikiana na Kanisa la Lutheri mwaka wa 1940, nilikabili upinzani na kupigwa shuleni. Ninawashukuru wazazi wangu kwa kunifundisha kanuni za Biblia. Jambo hilo lilinisaidia sana kukabiliana kwa mafanikio na hali hizo ngumu.”

Imani Yajaribiwa

Vita vya Pili vya Ulimwengu vilipozuka nao Wanazi wakatwaa eneo hilo, waliazimia kuwaangamiza kabisa Mashahidi wa Yehova. Mwanzoni, watu wazima—hasa akina baba—walitiwa moyo watie sahihi orodha fulani iliyoonyesha kwamba wao ni raia wa Ujerumani ili wapate manufaa fulani. Mashahidi walikataa kuwaunga mkono Wanazi. Ndugu wengi na watu wenye kupendezwa wenye umri wa kujiunga na jeshi walitatanika: Wangeweza kujiunga na jeshi, au wangeweza kudumisha msimamo mkali wa kutokuwamo lakini waadhibiwe vikali. “Kukataa utumishi wa kijeshi kulimaanisha kupelekwa kwenye kambi ya mateso, labda Auschwitz,” asema Andrzej Szalbot aliyekamatwa na Gestapo mwaka wa 1943. “Sikuwa nimebatizwa bado, lakini nilijua uhakikisho ambao Yesu alitupatia kwenye Mathayo 10:28, 29. Nilijua kwamba nikifa kwa sababu ya imani yangu katika Yehova, ataweza kunifufua.”

Mapema mwaka wa 1942, Wanazi waliwakamata ndugu 17 kutoka Wisła. Baada ya miezi mitatu, 15 kati yao walikufa huko Auschwitz. Mashahidi wengine waliobaki Wisła waliathiriwaje na jambo hilo? Badala ya kukana imani yao, jambo hilo liliwatia moyo washikamane na Yehova bila kulegea! Miezi sita iliyofuata, idadi ya wahubiri huko Wisła iliongezeka maradufu. Baada ya muda mfupi, wengi zaidi walikamatwa. Kwa ujumla, ndugu 83, watu wenye kupendezwa, na watoto waliathiriwa na kikosi chenye nguvu kilichotumiwa na Hitler. Kati yao, 53 walipelekwa kwenye kambi za mateso (hasa Auschwitz) au kwenye kambi za kazi ngumu katika migodi na machimbo huko Poland, Ujerumani, na Bohemia.

Washikamanifu na Imara

Huko Auschwitz, Wanazi walijaribu kuwashawishi Mashahidi kwamba watawapa uhuru mara moja. Askari mmoja wa SS alimwambia ndugu fulani hivi: “Ukitia tu sahihi hati ya kuonyesha kwamba umewakana Wanafunzi wa Biblia, tutakuachilia, nawe utaenda nyumbani.” Aliambiwa jambo hilo mara nyingi, lakini ndugu huyo aliendelea kuwa mwaminifu kwa Yehova. Kwa sababu hiyo, alipigwa, akadhihakiwa, na kupelekwa kwenye kambi za kazi ngumu huko Auschwitz na Mittelbau-Dora, Ujerumani. Kabla tu ya ukombozi, ndugu huyo aliponea chupuchupu kufa wakati kambi alimokuwa amezuiliwa ilipopigwa makombora.

Paweł Szalbot, Shahidi aliyekufa hivi karibuni, alikumbuka hivi pindi moja: “Wakati wa kuhojiwa, askari wa Gestapo waliniuliza mara nyingi kwa nini sikujiunga na jeshi la Ujerumani na kukataa kusema Heil Hitler.” Baada ya kueleza msimamo wake wa Kikristo wa kutokuwamo akitumia Biblia, alipelekwa kufanya kazi katika kiwanda cha kutengeneza silaha. “Bila shaka, dhamiri yangu haingeniruhusu kufanya kazi hiyo, kwa hiyo walinipeleka nikafanye kazi kwenye mgodi.” Bado, aliendelea kuwa mwaminifu.

Wale ambao hawakufungwa gerezani—wanawake na watoto—waliwatumia vifurushi vya chakula wale waliokuwa Auschwitz. “Wakati wa kiangazi tulichuma matunda madogo mekundu ya porini kisha tukayabadilisha kwa ngano,” asema ndugu mmoja aliyekuwa kijana wakati huo. “Akina dada walioka mikate na kuiloweka ndani ya mafuta. Kisha tukawapelekea waamini wenzetu waliokuwa gerezani mikate hiyo kwa kiasi kidogo-kidogo.”

Kwa ujumla, Mashahidi 53 waliokuwa watu wazima kutoka Wisła walipelekwa kwenye kambi za mateso na kupewa kazi ngumu, 38 kati yao walikufa.

Kizazi Kipya Chatokea

Pia watoto wa Mashahidi wa Yehova waliathiriwa na ukandamizaji wa Wanazi. Baadhi yao walipelekwa pamoja na mama zao kwenye kambi za muda huko Bohemia. Wengine walitenganishwa na wazazi wao na kupelekwa kwenye kambi ya watoto yenye sifa mbaya huko Lodz.

Watatu kati ya watoto hao wanasema: “Tukiwa watoto kumi, sisi ndio tuliokuwa kikundi cha kwanza kupelekwa Lodz na Wajerumani. Tulikuwa na umri kati ya miaka mitano na miaka tisa. Tulitiana moyo kwa kusali na kuzungumzia habari za Biblia. Haikuwa rahisi kuvumilia.” Mnamo mwaka wa 1945, watoto hao wote walirudi nyumbani. Walikuwa hai lakini walikuwa wamekonda na kuvurugika. Hata hivyo, hakuna jambo lililovunja utimilifu wao.

Ni Nini Kilichotukia Baadaye?

Vita vya Pili vya Ulimwengu vilipokaribia kwisha, bado Mashahidi kutoka Wisła walikuwa na imani yenye nguvu na tayari kuendelea tena na azimio lao la kuhubiri kwa bidii. Vikundi vya akina ndugu walitembelea watu walioishi umbali wa kilometa 40 hivi kutoka Wisła, wakihubiri na kugawanya vichapo vinavyotegemea Biblia. “Punde si punde, kulikuwa na makutaniko matatu yenye bidii katika mji wetu,” asema Jan Krzok. Hata hivyo, uhuru wa kidini haukuendelea kwa muda mrefu.

Serikali ya Kikomunisti ambayo ilichukua mahali pa Wanazi ilipiga marufuku kazi ya Mashahidi wa Yehova huko Poland mwaka wa 1950. Hivyo, ndugu wenyeji walihitaji kufanya huduma yao kwa werevu. Nyakati nyingine waliwatembelea watu nyumbani kwao kwa kujifanya kuwa wanataka kununua mifugo au nafaka. Kwa kawaida mikutano ya Kikristo ilifanywa usiku, katika vikundi vidogo-vidogo. Hata hivyo, askari wa kulinda usalama waliwakamata waabudu wengi wa Yehova, na kuwashtaki kuwa wanafanyia kazi shirika la ujasusi la nchi fulani ya kigeni—dai hilo halikuwa na msingi wowote. Maofisa fulani walimtisha Paweł Pilch kwa dharau hivi: “Hitler hakuvunja utimilifu wenu, lakini sisi tutauvunja.” Hata hivyo, aliendelea kuwa mshikamanifu kwa Yehova, kwa kufungwa miaka mitano. Mashahidi wachache wenye umri mdogo walipokataa kutia sahihi hati fulani ya chama cha kisoshalisti, walifukuzwa shuleni au kazini.

Yehova Hakuwaacha

Hali ya kisiasa ilibadilika mwaka wa 1989, na Mashahidi wa Yehova wakatambuliwa kisheria nchini Poland. Waabudu wa Yehova walio imara huko Wisła walifanya kazi yao kwa bidii, kama inavyoonyeshwa na idadi ya mapainia, au wahudumu wa wakati wote. Ndugu na dada wapatao 100 kutoka eneo hilo wameanza utumishi wa upainia. Kwa hiyo, haishangazi kwamba mji huo umepewa jina la utani, Kiwanda cha Mapainia.

Biblia inasema hivi kuhusu jinsi Mungu alivyowasaidia watumishi wake zamani: “Kama Yehova hangekuwa upande wetu watu waliposimama dhidi yetu, ndipo wangetumeza hata tukiwa hai.” (Zaburi 124:2, 3) Ingawa katika nyakati zetu hali ya kutojali na mwenendo usio wa adili wa ulimwengu umeenea sana kati ya watu, waabudu wa Yehova huko Wisła wanajitahidi kudumisha utimilifu wao nao wanabarikiwa sana. Vizazi vilivyofuata vya Mashahidi katika eneo hilo wanaweza kuthibitisha ukweli wa maneno haya ya mtume Paulo: “Ikiwa Mungu yuko upande wetu, ni nani atakayekuwa dhidi yetu?”—Waroma 8:31.

[Picha katika ukurasa wa 26]

Emilia Krzok pamoja na watoto wake Helena, Emilia, na Jan walipelekwa kwenye kambi ya muda huko Bohemia

[Picha katika ukurasa wa 26]

Alipokataa utumishi wa kijeshi, Paweł Szalbot alipelekwa akafanye kazi kwenye migodi

[Picha katika ukurasa wa 27]

Akina ndugu walipotumwa na kufa huko Auschwitz, bado kazi iliendelea kukua huko Wisła

[Picha katika ukurasa wa 28]

Paweł Pilch na Jan Polok walipelekwa kwenye kambi ya vijana huko Lodz

[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 25]

Berries and flowers: © R.M. Kosinscy / www.kosinscy.pl