Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Tutapata Kuwa na Usalama wa Kweli?

Je, Tutapata Kuwa na Usalama wa Kweli?

Je, Tutapata Kuwa na Usalama wa Kweli?

KWA ujumla, watu hufurahia kutazama watoto wakicheza pamoja na wazazi wao wenye upendo. Watoto huhisi wakiwa salama kabisa wanapokuwa na wazazi wanaowajali. Hata hivyo, ni watoto wachache sana ambao hufurahia hali kama hiyo. Badala yake, baadhi yao huhangaika kila siku kuhusu kupata mahali pa kulala usiku. Je, kuna tumaini lolote kwa watoto hao wasio na makao na watu wengine wanaoishi bila usalama?

Ingawa huenda wakati ujao ukaonekana kuwa usio na tumaini, Neno la Mungu hutoa tumaini. Nabii Isaya alitabiri kwamba siku moja watu wote wataishi kwa usalama kabisa. Aliandika: “Hakika wao watajenga nyumba na kukaa ndani yake; na hakika wao watapanda mashamba ya mizabibu na kula matunda yake. Hawatajenga na mtu mwingine akae ndani yake; hawatapanda na mtu mwingine ale.”—Isaya 65:21, 22.

Lakini je, tuna sababu nzuri ya kuwa na tumaini hilo, licha ya kwamba sikuzote neno “tumaini” halimaanishi kuwa na uhakika? Kwa mfano, nchini Brazili, mara nyingi mtu husikia usemi huu: “A esperança é a última que morre.” Kihalisi usemi huo unamaanisha, “Tumaini ndilo hufa mwisho.” Hiyo inamaanisha kwamba watu wengi huendelea kuwa na tumaini hata wakati ambapo hawana sababu nzuri ya kuwa na tumaini. Hata hivyo, Mungu wetu aliye hai anatupa tumaini lililo tofauti. Mtume Paulo aliandika: “Yeyote anayemwamini [Mungu] hatakata tamaa.” (Waroma 10:11) Unabii wa Biblia ambao tayari umetimizwa hutupa uhakika kwamba ahadi nyingine zote za Yehova Mungu zitatimizwa pia. Zitakapotimizwa, hali ambazo hulazimisha watoto waishi barabarani zitatoweka.

Hata leo, shauri la Biblia lenye kutumika linaweza kuwasaidia wale wasio na tumaini la kuboresha maisha yao na kupata usalama wa kweli. Hilo linawezekanaje? Mashahidi wa Yehova katika eneo unamoishi watafurahi kukusaidia kupata jibu la swali hilo.