Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Wewe Unatambua Furaha Inayotokana na Kutoa?

Je, Wewe Unatambua Furaha Inayotokana na Kutoa?

Je, Wewe Unatambua Furaha Inayotokana na Kutoa?

DADA mmoja mwaminifu alikuwa ametumika kwa miaka 50 hivi katika utumishi wa Kikristo. Ingawa uzee ulikuwa umefanya awe dhaifu, alikuwa ameazimia kufika kwenye Jumba la Ufalme lililokuwa limejengwa karibuni. Akijiegemeza kwenye mkono wa ndugu Mkristo aliyemsaidia, aliingia ndani ya jumba na kutembea polepole, lakini moja kwa moja hadi kwenye sanduku la michango. Alitumbukiza pesa ambazo alikuwa amehifadhi ili atoe mchango kwa ajili ya Jumba hilo jipya la Ufalme. Ingawa hangeweza kufanya kazi ya kujenga jumba lenyewe, alitaka kusaidia.

Mwanamke huyo Mkristo anatukumbusha yule ‘mjane maskini’ ambaye Yesu alimwona akitumbukiza sarafu mbili ndogo katika masanduku ya hazina ya hekalu. Hatuelezwi kuhusu hali zake, lakini mwanamke yeyote ambaye hakuwa na mume wakati huo angepatwa na matatizo mengi ya kifedha. Kwa kweli, Yesu alimsikitikia kwa sababu alielewa hali yake kabisa. Akimtumia kama mfano kwa wanafunzi wake, alitaja kwamba mchango wake mdogo uliwakilisha “vyote alivyokuwa navyo, riziki yake yote.”—Marko 12:41-44.

Kwa nini mwanamke mwenye uhitaji kama mjane huyu atoe dhabihu kama hiyo? Ni wazi kwamba alikuwa amejitoa kabisa kwa Yehova Mungu, ambaye hekalu la Yerusalemu lilikuwa kitovu cha ibada yake. Alitaka kuendeleza utumishi mtakatifu ingawa hangeweza kufanya mengi. Na lazima awe alipata shangwe kubwa kwa kuchanga alichoweza.

Kutoa ili Kutegemeza Kazi ya Yehova

Sikuzote kutoa vitu vya kimwili na fedha kumekuwa sehemu muhimu ya ibada ya kweli, na utoaji huo hutokeza shangwe kubwa. (1 Mambo ya Nyakati 29:9) Katika Israeli la kale, michango ilitumiwa kulirembesha hekalu na pia kuendeleza shughuli zote zilizohusiana na ibada ya Yehova zilizofanyiwa humo kila siku. Sheria ilitaja wazi kwamba wana wa Israeli walipaswa kuchangia sehemu ya kumi ya mazao yao ili kuwategemeza Walawi, ambao walihudumu katika hekalu. Lakini Walawi pia walipaswa kumtolea Yehova sehemu ya kumi ya mapato waliyopokea.—Hesabu 18:21-29.

Ingawa Wakristo waliwekwa huru kutokana na matakwa ya agano la Sheria, bado kanuni ya kwamba watumishi wa Mungu watoe mali za kimwili ili kutegemeza ibada ya kweli haijabadilika. (Wagalatia 5:1) Kwa kuongezea, Wakristo wa karne ya kwanza walitoa michango yao kwa shangwe ili kushughulikia mahitaji ya ndugu zao. (Matendo 2:45, 46) Mtume Paulo aliwakumbusha Wakristo kwamba kwa kadiri ileile ambayo Mungu aliwapa vitu vizuri kwa ukarimu, wao pia walipaswa kuwa wakarimu kuelekea wengine. Aliandika hivi: “Uwape maagizo wale walio matajiri katika mfumo wa mambo wa sasa wasitake makuu, na waweke tumaini lao, si katika utajiri usio hakika, bali katika Mungu, ambaye hutupa sisi vitu vyote kwa wingi ili tuvifurahie; wafanye mema, wawe matajiri katika matendo mazuri, wawe wakarimu, tayari kushiriki, wakijiwekea wenyewe kwa usalama hazina ya msingi mzuri kwa ajili ya wakati ujao, ili waushike imara uzima ulio wa kweli.” (1 Timotheo 6:17-19; 2 Wakorintho 9:11) Kwa kweli, kutokana na mambo aliyojionea, Paulo angeweza kuthibitisha maneno haya ya Yesu: “Kuna furaha zaidi katika kutoa kuliko ilivyo katika kupokea.”—Matendo 20:35.

Utoaji wa Kikristo Leo

Leo, watumishi wa Yehova wanaendelea kutumia mali zao za kimwili ili kusaidiana na kutegemeza kazi ya Mungu. Hata walio maskini huchanga wanachoweza. “Mtumwa mwaminifu na mwenye busara” anajua kwamba ana wajibu mbele za Yehova wa kutumia michango yote hiyo kwa njia bora kabisa. (Mathayo 24:45) Michango hutumiwa kuendesha ofisi za tawi, kutafsiri na kuchapisha Biblia na vichapo vya Biblia, kupangia mikutano mikubwa ya Kikristo, kuzoeza na kutuma waangalizi wasafirio na wamishonari, kuandaa msaada wakati wa misiba, na pia kwa mambo mengine mengi muhimu. Acheni tufikirie sababu moja kati ya hizo—kutoa michango ya kujenga sehemu za ibada.

Mashahidi wa Yehova hukutana mara kadhaa kwa juma katika Majumba yao ya Ufalme ili wanufaike na elimu ya kiroho na ushirika unaofaa. Hata hivyo, katika nchi nyingi hali za kiuchumi haziwaruhusu Mashahidi wenyeji kujenga Majumba yao ya Ufalme bila kupata msaada wa kifedha kwanza. Basi, katika mwaka wa 1999, Mashahidi wa Yehova walianzisha programu ya kutumia pesa kutoka nchi zenye utajiri ili zitumiwe kusaidia kujenga Majumba ya Ufalme katika nchi maskini. Isitoshe, maelfu ya wajitoleaji wametumia wakati na stadi zao, mara nyingi wakifanya kazi katika sehemu za mashambani katika nchi hizo. Wakati wa ujenzi, ndugu wenyeji hujifunza stadi za kujenga na za kudumisha jumba, nayo Hazina ya Majumba ya Ufalme huwasaidia kununua vifaa vinavyohitajiwa. Mashahidi wanaotumia majumba hayo mapya wanashukuru sana kwamba waamini wenzao walitoa wakati na pesa zao. Mashahidi hao pia hutoa michango kila mwezi ili kudumisha Jumba hilo jipya la Ufalme na kusaidia kurudisha gharama za ujenzi, na hivyo kusaidia kujenga Majumba mengi zaidi ya Ufalme.

Majumba ya Ufalme hujengwa kwa kutumia mbinu na vifaa vya mahali yanapojengwa. Ingawa majumba hayo hayana madoido, yanavutia na kustarehesha. Mpango huo wa ujenzi ulipoanza mwaka wa 1999, nchi 40 hivi zilizo maskini zilihusishwa. Tangu wakati huo, mpango huo umepanuliwa ili kutia ndani nchi kama hizo 116, zinazohusisha zaidi ya nusu ya makutaniko yote ya Mashahidi wa Yehova ulimwenguni. Katika miaka mitano iliyopita, zaidi ya Majumba ya Ufalme 9,000 yamejengwa chini ya mpango huo. Huo ni wastani wa zaidi ya majumba mapya 5 kila siku! Bado katika nchi hizo 116, kuna uhitaji wa Majumba mapya ya Ufalme 14,500. Kwa baraka za Yehova na kupitia utayari na ukarimu wa Mashahidi ulimwenguni pote, inatarajiwa kwamba kutakuwa na pesa za kutosheleza uhitaji huo.—Zaburi 127:1.

Majumba ya Ufalme Huchangia Ukuzi

Jitihada hiyo kubwa imekuwa na matokeo gani juu ya Mashahidi wenyeji na juu ya kazi ya kuhubiri Ufalme? Katika sehemu nyingi, kuna ongezeko kubwa sana katika hudhurio la mikutano baada ya Jumba la Ufalme jipya kujengwa. Mfano mzuri unapatikana katika ripoti ifuatayo kutoka Burundi: “Jumba la Ufalme hujaa punde tu baada ya kujengwa. Kwa mfano, Jumba moja la Ufalme lilijengwa kwa ajili ya kutaniko lililokuwa na wastani wa wahudhuriaji 100 katika mikutano yao. Jumba lao jipya linatoshea watu 150. Kufikia wakati jumba hilo lilipomalizika, watu 250 walikuwa wakihudhuria mikutano.”

Kwa nini kumekuwa na ongezeko hilo? Kwanza kabisa, watu hutilia shaka vikundi vya watangazaji wa Ufalme ambao hukutana chini ya mti au uwanjani kwa sababu ya kukosa mahali rasmi pa kukutania. Katika nchi fulani, vita vya kikabila vimehusianishwa na vikundi vidogo kama hivyo vya kidini, nayo sheria hutaka mikutano yote ya kidini ifanywe ndani ya nyumba ya ibada.

Pia, kuwa na majumba yao wenyewe huwasaidia Mashahidi wa Yehova kuonyesha watu kwamba wao si wafuasi wa kasisi fulani. Ofisi ya tawi ya Mashahidi wa Yehova kule Zimbabwe iliandika hivi: “Zamani, akina ndugu huku walikuwa wakikutana katika nyumba za kibinafsi, na wenyeji walikuwa wakilitambulisha kutaniko na mwenye nyumba. Wangesema kwamba ndugu hao walikuwa wafuasi wa kanisa la Bw. Fulani wa fulani. Sasa yote hayo yanabadilika watu wanapoona ishara zilizoandikwa waziwazi, ‘Jumba la Ufalme la Mashahidi wa Yehova’ zikitambulisha kila jumba.”

Watoaji Wenye Shangwe

Mtume Paulo aliandika, “Mungu humpenda mtoaji mchangamfu.” (2 Wakorintho 9:7) Bila shaka, michango mikubwa inasaidia sana. Lakini sehemu kubwa ya michango inayotolewa kwa ajili ya kazi ya Mashahidi wa Yehova hupatikana katika masanduku ya michango ya Majumba ya Ufalme. Michango yote ni muhimu nayo haipuuzwi, iwe mikubwa au midogo. Kumbuka kwamba Yesu aliketi mahali ambapo angeweza kumwona yule mjane akitumbukiza sarafu zake mbili ndogo. Yehova na malaika walimwona pia. Hata hatujui jina la mjane huyo, lakini Yehova alihakikisha kwamba tendo lake la kujidhabihu limeandikwa katika Biblia kwa wakati wote.

Zaidi ya kujenga Majumba ya Ufalme, michango yetu hutegemeza sehemu nyingine muhimu za kazi ya Ufalme. Kushirikiana katika njia hii kunatupatia sababu ya kushangilia na kuwa “matajiri kwa maonyesho mengi ya shukrani kwa Mungu.” (2 Wakorintho 9:12) Ndugu zetu kule Benin wanaripoti hivi: “Kila siku sala nyingi za shukrani humwendea Yehova kwa sababu ya msaada wa kifedha tunaopata kutoka kwa undugu wa kimataifa.” Wakati uleule, sote tunaoshiriki katika kutegemeza kazi ya Ufalme tunapata shangwe inayotokana na utoaji wa Kikristo!

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 22, 23]

Jinsi Ambavyo Wengine Hutoa Michango

MICHANGO KWA AJILI YA KAZI YA ULIMWENGUNI POTE

Wengi hutenga kiasi fulani cha pesa ambacho wao hutia katika masanduku ya michango yaliyoandikwa, “Michango kwa Ajili ya Kazi ya Ulimwenguni Pote–Mathayo 24:14.”

Kila mwezi, makutaniko hutuma pesa hizo kwenye ofisi ya Mashahidi wa Yehova iliyo katika nchi yao. Michango ya hiari ya pesa inaweza kutumwa moja kwa moja kwenye Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania, c/o Office of the Secretary and Treasurer, 25 Columbia Heights, Brooklyn, New York 11201-2483, au kwenye ofisi ya tawi ya nchi yenu. Cheki za benki zinapaswa kuonyesha kwamba zitalipwa kwa shirika la “Watch Tower.” Vito au vitu vingine vyenye thamani vinaweza kuchangwa vilevile. Barua fupi inayoonyesha kwamba vitu hivyo ni zawadi ya moja kwa moja inapaswa kuambatanishwa na michango hiyo.

MPANGO WA MICHANGO YENYE MASHARTI

Pesa zinaweza kutolewa kwa amana kwa ajili ya shirika la Watch Tower. Hata hivyo, zinaweza kurudishwa iwapo zitaitishwa. Kwa habari zaidi, tafadhali wasiliana na Ofisi ya Katibu na Mweka-Hazina kwa kutumia anwani iliyoonyeshwa hapa juu.

UTOAJI ULIOPANGWA

Mbali na zawadi za moja kwa moja za pesa au vitu vyenye thamani na michango yenye masharti, kuna njia nyinginezo za kutoa kwa ajili ya kazi ya Ufalme duniani pote. Hizo zinatia ndani:

Bima: Watch Tower inaweza kutajwa kuwa mfaidikaji wa hati ya bima ya maisha au wa malipo ya kustaafu kazi au ya uzeeni.

Akiba za Benki: Akaunti za benki, hati za amana, au akiba za pesa za kustaafu za mtu mmoja-mmoja zinaweza kuwekwa zikiwa amana, au kulipwa wakati wa kifo, kwa Watch Tower, kulingana na matakwa ya benki za kwenu.

Hisa na Dhamana: Hisa na dhamana zinaweza kuchangwa kwa Watch Tower zikiwa zawadi ya moja kwa moja.

Ardhi na Nyumba: Ardhi au nyumba zinazoweza kuuzwa zinaweza kutolewa zikiwa zawadi ya moja kwa moja au zawadi yenye masharti, yaani, mtoaji anaweza kuendelea kuishi humo hadi kifo chake. Julisha ofisi ya tawi katika nchi yako kabla ya kuchanga ardhi au nyumba.

Malipo-Mwaka: Huo ni mpango wa kutoa pesa, hisa na amana, ziwe mali za Watch Tower. Yule anayetoa mchango huo, au mtu fulani aliyechaguliwa na mtoaji, hupata kiasi fulani cha pesa kila mwaka maishani mwake. Mtoaji hupunguziwa kodi ya serikali mwaka ule ambapo mpango huo unaanzishwa.

Wasia na Amana: Watch Tower inaweza kuachiwa urithi wa mali au pesa kwa njia ya wasia halali, au Watch Tower inaweza kutajwa kuwa mfaidikaji wa mkataba wa amana. Kuwa na amana inayofaidi tengenezo la kidini kunaweza kupunguza kwa kiasi fulani kodi ambayo hutozwa na serikali.

Kama vile usemi “utoaji uliopangwa” unavyodokeza, michango ya aina hii kwa kawaida hutaka mtoaji afanye mipango hususa. Watch Tower Society imetayarisha broshua ya Kiingereza na Kihispania yenye kichwa Charitable Planning to Benefit Kingdom Service Worldwide, ili kuwasaidia watu wanaotamani kuendeleza kazi inayofanywa na Mashahidi wa Yehova ulimwenguni pote kwa njia ya utoaji uliopangwa. Broshua hiyo iliandikwa ili kutoa habari kuhusu njia mbalimbali za kutoa zawadi sasa au kama urithi mtu anapokufa. Baada ya kusoma broshua hiyo na kushauriana na washauri wao wa mambo ya sheria na kodi, watu wengi wameweza kusaidia kutegemeza kazi ya Mashahidi wa Yehova ulimwenguni pote, na kupunguziwa kodi wanapofanya hivyo. Unaweza kupata broshua hiyo kwa kuiomba moja kwa moja kutoka kwenye Charitable Planning Office.

Kwa habari zaidi unaweza kuwasiliana na Charitable Planning Office, ama kwa kuandika ama kwa kupiga simu, kwenye anwani iliyoonyeshwa hapa chini, ama kwenye ofisi ya tawi ya nchi yako.

Mashahidi wa Yehova

P.O. Box 47788

00100 GPO Nairobi

Kenya

Simu: (02) 573211

[Picha katika ukurasa wa 20, 21]

Sehemu mpya za kukutania na zile za zamani za Mashahidi wa Yehova

Zambia

Jamhuri ya Afrika ya Kati