Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Kutaniko la Kikristo huonaje ulafi?

Neno la Mungu hushutumu ulevi na ulafi kuwa tabia zisizowafaa wale wanaomtumikia Mungu. Kwa hiyo, kutaniko la Kikristo humwona mlafi asiyetaka kubadilika kwa njia ileile linavyomwona mtu aliye na zoea la ulevi. Mlevi au mlafi hawezi kuwa mshiriki wa kutaniko la Kikristo.

Methali 23:20, 21 inasema: “Usiwe kati ya watu wanaokunywa divai mno, kati ya watu wanaokula nyama kwa ulafi. Kwa maana mlevi na mlafi watakuwa maskini, na kusinzia kutamvika mtu nguo zilizopasuka.” Katika Kumbukumbu la Torati 21:20 tunasoma kuhusu mtu “mkaidi na mwasi,” ambaye kulingana na Sheria ya Musa alistahili kuuawa. Kulingana na mstari huo, mtu huyo mwasi na asiyetubu alikuwa “mlafi na mlevi.” Ni wazi kwamba katika Israeli la kale, ulafi ulionwa kuwa zoea lisilofaa kwa waliotaka kumtumikia Mungu.

Hata hivyo, mlafi ni mtu wa aina gani, nayo Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo husema nini kuhusu ulafi? Mlafi ni mtu ambaye “sikuzote hula na kunywa kwa pupa.” Hivyo, ulafi ni aina ya pupa, nalo Neno la Mungu hutuambia kwamba “watu wenye pupa” ni kati ya wale ambao hawataurithi Ufalme wa Mungu. (1 Wakorintho 6:9, 10; Wafilipi 3:18, 19; 1 Petro 4:3) Kwa kuongezea, wakati mtume Paulo alipowaonya Wakristo kuhusu kujihusisha katika “matendo ya mwili,” alitaja pia “vipindi vya kulewa, karamu za kupindukia, na mambo kama hayo.” (Wagalatia 5:19-21) Mara nyingi, kula kupita kiasi huambatana na vipindi vya kulewa na karamu za kupindukia. Isitoshe, ulafi pia unatiwa ndani ya “mambo kama hayo” ambayo Paulo alitaja. Kama ilivyo kuhusiana na ‘matendo mengine ya mwili,’ Mkristo anayejulikana sana kuwa mlafi na anayekataa kwa ukaidi kubadili tabia yake yenye pupa, anapaswa kuondolewa katika kutaniko.—1 Wakorintho 5:11, 13. *

Ingawa Neno la Mungu huonyesha kwamba mlevi ni sawa na mlafi, ni rahisi zaidi kumtambua mlevi kuliko mlafi. Kwa kawaida ishara za ulevi huonekana waziwazi. Hata hivyo, ni vigumu sana kuthibitisha kwamba mtu ni mlafi kwa sababu haiwezi kujulikana tu kwa kumtazama. Kwa hiyo, ili kushughulikia hali zinazohusu ulafi, wazee wa kutaniko wanahitaji kuwa waangalifu sana na wenye utambuzi.

Kwa mfano, kunenepa kupita kiasi kunaweza kuwa ishara ya ulafi, lakini si lazima iwe hivyo sikuzote. Mtu anaweza kunenepa kupita kiasi kwa sababu ya ugonjwa. Pia hali hiyo inaweza kurithiwa. Tunapaswa pia kukumbuka kwamba kunenepa kupita kiasi ni hali ya mwili, huku ulafi ukiwa ni mtazamo wa akili. Kunenepa kupita kiasi hufafanuliwa kuwa hali ya kuwa na mafuta mengi sana mwilini, hali ulafi ni pupa au kutojizuia unapokula. Hivyo ulafi hauamuliwi na unene wa mtu bali unaamuliwa na mtazamo wake kuelekea chakula. Mtu anaweza kuwa na unene wa kadiri au hata awe mwembamba lakini bado awe mlafi. Kwa kuongezea, watu wa sehemu mbalimbali wana maoni tofauti kuhusu uzito au umbo linalofaa.

Tunawezaje kutambua kwamba mtu ni mlafi? Mlafi hushindwa kujizuia kwa ukawaida, akila kwa pupa na hata kupita kiasi hivi kwamba anaanza kujihisi vibaya au hata anakuwa mgonjwa. Kutojizuia kwake kunaonyesha kwamba hana ufikirio kabisa kuhusu suto analoleta juu ya jina la Yehova na juu ya watu Wake. (1 Wakorintho 10:31) Kwa upande mwingine, si lazima mtu anayekula kupita kiasi mara chache tu, aonwe kuwa “mtu mwenye pupa.” (Waefeso 5:5) Hata hivyo, kulingana na maoni yaliyo katika Wagalatia 6:1, huenda Mkristo wa aina hiyo akahitaji kusaidiwa. Paulo anasema: “Akina ndugu, hata mtu akijikwaa katika kosa fulani kabla ya yeye kulijua, ninyi mlio na sifa za kustahili kiroho jaribuni kumrekebisha upya mtu huyo katika roho ya upole.”

Kwa nini shauri la Biblia kuhusu kuepuka kula kupita kiasi ni muhimu hasa leo? Kwa sababu, Yesu alionya hivi hasa kuhusu siku zetu: “Jiangalieni ninyi wenyewe kwamba mioyo yenu isilemewe kamwe na kula kupita kiasi na kunywa sana na mahangaiko ya maisha, na kwa ghafula siku hiyo iwe juu yenu mara moja kama mtego.” (Luka 21:34, 35) Njia moja muhimu ya kuepuka mtindo wa maisha wenye kudhuru kiroho ni kujizuia kula kupita kiasi.

Kuwa na kiasi ni sifa ya Kikristo. (1 Timotheo 3:2, 11) Kwa hiyo, kwa kweli Yehova atawasaidia wote wanaojitahidi kwa unyoofu kutumia shauri la Biblia kuhusu kuwa wenye kiasi wanapokula na kunywa.—Waebrania 4:16.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 5 Ona “Maswali Kutoka kwa Wasomaji” katika toleo la Mnara wa Mlinzi la Mei 1, 1986.