Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Ni Wenye Furaha Ingawa Wanateswa

Ni Wenye Furaha Ingawa Wanateswa

Ni Wenye Furaha Ingawa Wanateswa

“Wenye furaha ni ninyi wakati watu wanapowashutumu na Kuwatesa na kusema kwa uwongo kila namna ya jambo baya juu yenu kwa ajili yangu.”—MATHAYO 5:11.

1. Yesu aliwapa wafuasi wake uhakikisho gani kuhusu furaha na kuteswa?

YESU alipowatuma mitume wake mara ya kwanza wakahubiri Ufalme, aliwaonya kwamba wangepingwa. Aliwaambia: “Mtachukiwa na watu wote kwa sababu ya jina langu.” (Mathayo 10:5-18, 22) Hata hivyo, mapema katika Mahubiri yake ya Mlimani, aliwahakikishia mitume wake na wengine kwamba haingekuwa lazima upinzani huo uhatarishe furaha yao ya kutoka moyoni. Kwa kweli, Yesu alihusianisha hali ya kuwa na furaha na kuteswa kwa Wakristo! Kuteswa kungewezaje kuleta furaha?

Kuteseka kwa Ajili ya Uadilifu

2. Kulingana na Yesu na mtume Petro, ni kuteseka kwa aina gani huleta furaha?

2 Sababu ya nane ya kuwa na furaha ambayo Yesu alitaja ni: “Wenye furaha ni wale ambao wameteswa kwa ajili ya uadilifu, kwa kuwa ufalme wa mbinguni ni wao.” (Mathayo 5:10) Kuteseka kwenyewe si jambo linaloleta sifa. Mtume Petro aliandika: “Kuna sifa gani katika jambo ikiwa mnapofanya dhambi na kupigwa makofi, mnavumilia? Lakini ikiwa, mnapotenda mema na kuteseka, mnavumilia, jambo hilo ni lenye kukubalika kwa Mungu.” Naye aliongeza kusema: “Hata hivyo, yeyote kati yenu asiteseke kwa sababu yeye ni muuaji au mwizi au mtenda-maovu au mwenye kujiingiza katika mambo ya watu wengine. Lakini akiteseka kwa sababu yeye ni Mkristo, asione aibu, bali na aendelee kumtukuza Mungu katika jina hili.” (1 Petro 2:20; 4:15, 16) Kulingana na maneno ya Yesu kuteseka huleta furaha tunapovumilia kwa ajili ya uadilifu.

3. (a) Kuteswa kwa ajili ya uadilifu humaanisha nini? (b) Mateso yalikuwa na matokeo gani juu ya Wakristo wa mapema?

3 Uadilifu wa kweli hukadiriwa kulingana na jinsi mtu anavyoshika amri za Mungu na kufanya mapenzi yake. Kwa hiyo, kuteseka kwa ajili ya uadilifu humaanisha kuteseka kwa sababu mtu anapinga mkazo wa kuvunja kanuni au matakwa ya Mungu. Mitume waliteswa na viongozi Wayahudi kwa sababu walikataa kuacha kuhubiri katika jina la Yesu. (Matendo 4:18-20; 5:27-29, 40) Je, hilo lilipunguza shangwe yao au kufanya waache kuhubiri? Hata kidogo! ‘Walitoka mbele ya Sanhedrini, wakishangilia kwa sababu walikuwa wamehesabiwa kuwa wenye kustahili kuvunjiwa heshima kwa ajili ya jina lake. Na kila siku katika hekalu na nyumba kwa nyumba wakaendelea bila kuacha kufundisha na kutangaza habari njema juu ya Kristo, Yesu.’ (Matendo 5:41, 42) Mateso hayo yaliwaletea shangwe na kuongeza bidii yao katika kazi ya kuhubiri. Baadaye, Wakristo wa mapema waliteswa na Waroma kwa sababu ya kukataa kumwabudu maliki.

4. Wakristo huteswa kwa sababu zipi?

4 Siku hizi Mashahidi wa Yehova wameteswa kwa sababu ya kukataa kuacha kuhubiri “habari njema ya ufalme.” (Mathayo 24:14) Mikutano yao ya Kikristo inapopigwa marufuku, wao huwa tayari kuteseka badala ya kuacha kukusanyika pamoja kama Biblia inavyoamuru. (Waebrania 10:24, 25) Wameteswa kwa sababu ya msimamo wao wa Kikristo wa kutokuwamo au kwa kukataa kutumia damu kwa njia isiyofaa. (Yohana 17:14; Matendo 15:28, 29) Hata hivyo, msimamo huo kwa ajili ya uadilifu huwaletea watu wa Mungu leo amani nyingi ya akili na furaha.—1 Petro 3:14.

Kushutumiwa kwa Ajili ya Kristo

5. Sababu ya msingi ya kuteswa kwa watu wa Yehova leo ni ipi?

5 Sababu ya tisa ya kuwa na furaha ambayo Yesu alitaja katika Mahubiri yake ya Mlimani inahusu pia suala la kuteswa. Alisema: “Wenye furaha ni ninyi wakati watu wanapowashutumu na kuwatesa na kusema kwa uwongo kila namna ya jambo baya juu yenu kwa ajili yangu.” (Mathayo 5:11) Sababu ya msingi ya kuteswa kwa watu wa Yehova ni kwamba wao si sehemu ya mfumo huu mwovu wa mambo. Yesu aliwaambia hivi wanafunzi wake: “Kama mngekuwa sehemu ya ulimwengu, ulimwengu ungependa kilicho chake. Sasa kwa sababu ninyi si sehemu ya ulimwengu, bali nimewachagua ninyi kutoka ulimwenguni, kwa sababu hiyo ulimwengu unawachukia ninyi.” (Yohana 15:19) Vivyo hivyo, mtume Petro alisema: “Kwa sababu ninyi hamwendelei kukimbia pamoja nao katika mwendo huo kwenda kwenye dimbwi lilelile la chini la upotovu, wao wanashangaa na kuendelea kuwatukana ninyi.”—1 Petro 4:4.

6. (a) Kwa nini mabaki na waandamani wao hushutumiwa na kuteswa? (b) Je, shutuma hiyo hupunguza furaha yetu?

6 Tayari tumeona kwamba Wakristo wa mapema waliteswa kwa sababu walikataa kuacha kuhubiri katika jina la Yesu. Kristo aliwapa wafuasi wake kazi hii: “Mtakuwa mashahidi wangu . . . mpaka sehemu ya mbali zaidi ya dunia.” (Matendo 1:8) Mabaki waaminifu wa ndugu za Yesu waliotiwa mafuta, wakisaidiwa na waandamani wao washikamanifu wa “umati mkubwa,” wanafanya kazi hiyo kwa bidii. (Ufunuo 7:9) Kwa hiyo, Shetani anapigana vita “na wale waliobaki wa uzao wake [uzao wa “mwanamke,” sehemu ya kimbingu ya tengenezo la Mungu], wanaoshika amri za Mungu na walio na kazi ya kutoa ushahidi kumhusu Yesu.” (Ufunuo 12:9, 17) Tukiwa Mashahidi wa Yehova, tunatoa ushahidi kumhusu Yesu, ambaye sasa ni Mfalme anayetawala wa serikali ya Ufalme, ambayo itaharibu serikali za wanadamu zinazopinga ulimwengu mpya wa Mungu wenye uadilifu. (Danieli 2:44; 2 Petro 3:13) Sisi hushutumiwa na kuteswa kwa sababu hiyo, lakini tunafurahi kuteswa kwa ajili ya jina la Kristo.—1 Petro 4:14.

7, 8. Wapinzani walisema nini kwa uwongo juu ya Wakristo wa mapema?

7 Yesu alisema kwamba wafuasi wake wanapaswa kujiona kuwa na furaha hata wakati watu ‘wanaposema kwa uwongo kila namna ya jambo baya’ juu yao kwa ajili yake. (Mathayo 5:11) Hivyo ndivyo ilivyotukia kwa Wakristo wa mapema. Mtume Paulo alipozuiliwa huko Roma, yapata mwaka wa 59-61 W.K., viongozi Wayahudi wa huko walisema hivi kuhusu Wakristo: “Kweli kwa habari ya madhehebu hii tunajua kwamba kila mahali huwa inasemwa vibaya.” (Matendo 28:22) Paulo na Sila walishutumiwa kuwa “wameipindua dunia inayokaliwa,” wakitenda ‘kwa kupingana na maagizo ya Kaisari.’—Matendo 17:6, 7.

8 Mwanahistoria K. S. Latourette alisema hivi alipoandika kuhusu Wakristo wakati wa Milki ya Roma: “Walishutumiwa kwa mambo tofauti-tofauti. Kwa sababu Wakristo walikataa kuhusika katika sherehe za kipagani waliitwa wakana-Mungu. Kwa kuwa hawakujihusisha na mambo mengi yaliyofanywa katika jamii, kama vile sherehe za kipagani, vitumbuizo vya umma . . . walidhihakiwa kuwa wenye kuwachukia wanadamu. . . . Ilisemekana kwamba wanaume kwa wanawake walikutana pamoja usiku na kwamba walifanya ngono kiholela-holela. . . . Kwa kuwa [Ukumbusho wa kifo cha Kristo] uliadhimishwa na waamini peke yao, kulikuwa na uvumi kwamba Wakristo walidhabihu kwa ukawaida watoto wachanga, wakanywa damu yao, na kula nyama yao.” Isitoshe, kwa kuwa Wakristo wa mapema walikataa kumwabudu maliki, walishutumiwa kuwa maadui wa Serikali.

9. Wakristo wa karne ya kwanza waliitikiaje shutuma za uwongo zilizotolewa juu yao, na hali ikoje leo?

9 Shutuma hizo za uwongo hazikuwazuia Wakristo wa mapema kutimiza kazi yao ya kuhubiri habari njema ya Ufalme. Mnamo mwaka wa 60-61 W.K., Paulo alisema juu ya “habari njema” ambayo ilikuwa ‘ikizaa matunda na kuongezeka katika ulimwengu’ na ambayo ilikuwa ‘imehubiriwa katika uumbaji wote ulio chini ya mbingu.’ (Wakolosai 1:5, 6, 23) Ndivyo ilivyo leo. Mashahidi wa Yehova wanashutumiwa kwa uwongo sawa na Wakristo wa karne ya kwanza. Hata hivyo, leo kazi ya kuhubiri ujumbe wa Ufalme inaendelea, nayo inawaletea furaha nyingi wale wanaoifanya.

Wanafurahi Kuteswa Kama Vile Manabii

10, 11. (a) Yesu alimaliziaje mazungumzo yake kuhusu sababu ya tisa ya kuwa na furaha, na kwa nini? (b) Kwa nini manabii waliteswa? Toa mifano.

10 Yesu alimalizia mazungumzo yake kuhusu sababu ya tisa ya kuwa na furaha kwa kusema: “Shangilieni . . . , kwa maana hivyo ndivyo walivyowatesa manabii waliokuwa kabla yenu.” (Mathayo 5:12) Manabii waliotumwa na Yehova kuwaonya Waisraeli wasio waaminifu walipokewa vibaya na mara nyingi wakateswa. (Yeremia 7:25, 26) Mtume Paulo alithibitisha jambo hilo kwa kuandika: “Nami nitasema nini zaidi? Kwa maana nitakosa wakati nikiendelea kusimulia juu ya . . . manabii wengine, ambao kupitia imani . . . walipata jaribu lao kwa dhihaka na mapigo kwa mijeledi, kwa kweli, zaidi ya hayo, kwa vifungo na magereza.”—Waebrania 11:32-38.

11 Wakati wa utawala wa Mfalme Ahabu mwovu na mke wake Yezebeli, manabii wengi wa Yehova waliuawa kwa upanga. (1 Wafalme 18:4, 13; 19:10) Nabii Yeremia alitiwa katika mikatale na baadaye akatupwa ndani ya tangi lenye matope. (Yeremia 20:1, 2; 38:6) Nabii Danieli alitupwa katika shimo la simba. (Danieli 6:16, 17) Manabii hao wote wa kabla ya Ukristo waliteswa kwa sababu walitetea ibada safi ya Yehova. Manabii wengi waliteswa na viongozi wa kidini Wayahudi. Yesu aliwaita waandishi na Mafarisayo “wana wa wale waliowaua manabii.”—Mathayo 23:31.

12. Kwa nini sisi Mashahidi wa Yehova huona kuwa ni heshima kuteswa kama vile manabii wa kale?

12 Leo, mara nyingi sisi Mashahidi wa Yehova huteswa kwa sababu ya kuhubiri kwa bidii habari njema ya Ufalme. Maadui wetu hutushutumu kwamba sisi “huwalazimisha watu wageuze imani yao,” lakini tunajua kwamba waabudu waaminifu wa Yehova waliokuwa kabla yetu walikabili shutuma kama hizo. (Yeremia 11:21; 20:8, 11) Tunaona ni heshima kuteswa kwa sababu ileile iliyofanya manabii waaminifu wa kale wateswe. Mwanafunzi Yakobo aliandika hivi: “Akina ndugu, wachukueni manabii kuwa kielelezo cha kupatwa na uovu na kuonyesha subira, wale waliosema katika jina la Yehova. Tazama! Tunawatangaza kuwa wenye furaha wale ambao wamevumilia.”—Yakobo 5:10, 11.

Sababu Kuu za Kuwa na Furaha

13. (a) Kwa nini hatuvunjwi moyo na mateso? (b) Ni nini hutuwezesha kusimama imara, na hilo huthibitisha nini?

13 Badala ya kuvunjwa moyo na mateso, tunafarijika kujua kwamba tunafuata hatua za manabii, Wakristo wa mapema, na Yesu Kristo mwenyewe. (1 Petro 2:21) Tunapata uradhi mkubwa sana kutoka katika Maandiko, kama inavyoonyeshwa na maneno yafuatayo ya mtume Petro: “Wapendwa, msishangazwe juu ya moto unaowaka katikati yenu, unaowapata ninyi ili kuwa jaribu, kana kwamba jambo geni linawapata. Ikiwa mnashutumiwa kwa ajili ya jina la Kristo, ninyi ni wenye furaha, kwa sababu ile roho ya utukufu, yaani roho ya Mungu, inatulia juu yenu.” (1 Petro 4:12, 14) Tunajua kutokana na mambo ambayo yametupata kwamba tunaweza tu kusimama imara tunapopatwa na mateso kwa sababu roho ya Yehova inatulia juu yetu na kutuimarisha. Utegemezo wa roho takatifu huthibitisha kwamba Yehova anatubariki, na hilo hutuletea furaha nyingi.—Zaburi 5:12; Wafilipi 1:27-29.

14. Tuna sababu zipi za kushangilia tunapoteswa kwa ajili ya uadilifu?

14 Sababu nyingine inayofanya tuwe na furaha tunapopingwa na kuteswa kwa ajili ya uadilifu ni kwamba hilo huthibitisha tunaishi kama Wakristo wa kweli wenye ujitoaji-kimungu. Mtume Paulo aliandika: “Wote wanaotamani kuishi kwa ujitoaji-kimungu katika ushirika na Kristo Yesu watateswa pia.” (2 Timotheo 3:12) Tunafurahi sana kujua kwamba kudumisha utimilifu chini ya jaribu huandaa jibu zaidi kwa dai la Shetani kwamba viumbe wote humtumikia Yehova kwa faida za kibinafsi. (Ayubu 1:9-11; 2:3, 4) Tunashangilia kwamba tunashiriki, hata kama ni kwa kiwango kidogo, katika kutetewa kwa enzi kuu ya Yehova yenye uadilifu.—Methali 27:11.

Rukeni kwa Shangwe kwa Sababu ya Thawabu

15, 16. (a) Yesu alitupa sababu gani ya ‘kushangilia na kuruka kwa shangwe’? (b) Ni thawabu gani ambayo Wakristo watiwa-mafuta wanatarajia kupokea huko mbinguni, nao “kondoo wengine,” ambao ni waandamani wao, watathawabishwaje?

15 Yesu alitoa sababu nyingine ya kuwa na shangwe tunaposingiziwa na kuteswa kama manabii wa kale. Alipokuwa akimalizia mazungumzo yake kuhusu sababu ya tisa ya kuwa na furaha, alisema: “Shangilieni na kuruka kwa shangwe, kwa kuwa thawabu yenu ni kubwa mbinguni.” (Mathayo 5:12) Mtume Paulo aliandika: “Mshahara ambao dhambi hulipa ni kifo, lakini zawadi ambayo Mungu hutoa ni uzima wa milele kupitia Kristo Yesu Bwana wetu.” (Waroma 6:23) Naam, ‘thawabu hiyo kubwa’ ni uzima, nao si mshahara tunaoweza kufanyia kazi. Ni zawadi ya bure. Yesu alisema kwamba thawabu hiyo iko “mbinguni” kwa sababu inatoka kwa Yehova.

16 Watiwa-mafuta hupokea “taji la uzima,” yaani, uhai usioweza kufa huko mbinguni pamoja na Kristo. (Yakobo 1:12, 17) “Kondoo wengine,” ambao wana tumaini la kuishi duniani wanatazamia kwa hamu kupata uzima wa milele katika paradiso ya kidunia. (Yohana 10:16; Ufunuo 21:3-5) “Thawabu” hiyo si malipo kwa kazi ambayo jamii hizo mbili hufanya. Watiwa-mafuta na “kondoo wengine” hupokea thawabu yao kutokana na “fadhili nyingi zaidi zisizostahiliwa,” za Yehova, jambo lililomfanya mtume Paulo aseme: “Mungu apewe shukrani kwa ajili ya zawadi yake ya bure isiyoelezeka.”—2 Wakorintho 9:14, 15.

17. Kwa nini tunaweza kuwa na furaha tunapoteswa na “kuruka kwa shangwe” kwa njia ya mfano?

17 Mtume Paulo aliwaandikia hivi Wakristo ambao, baada ya muda mfupi, baadhi yao wangeteswa kwa ukatili na Maliki Nero: “Tufurahi tukiwa katika dhiki, kwa kuwa tunajua kwamba dhiki hutokeza uvumilivu; nao uvumilivu, hali yenye kukubaliwa; nayo hali yenye kukubaliwa, tumaini, nalo tumaini halikatishi tamaa.” Pia aliongeza: “Shangilieni katika tumaini. Vumilieni chini ya dhiki.” (Waroma 5:3-5; 12:12) Hata tumaini letu liwe la kimbingu au la kidunia, thawabu yetu ya kuwa waaminifu chini ya majaribu ni kubwa sana kuliko chochote tunachostahili kupata. Shangwe yetu kuhusu tarajio la kuishi milele ili kumtumikia na kumsifu Baba yetu mwenye upendo, Yehova, chini ya Mfalme wetu, Yesu Kristo haina kifani. Sisi ‘huruka kwa shangwe’ kwa njia ya mfano.

18. Mataifa yanatarajiwa kufanya nini mwisho ukaribiapo, naye Yehova atafanya nini?

18 Katika nchi fulani, Mashahidi wa Yehova wameteswa na bado wanateswa. Katika unabii wake kuhusu umalizio wa mfumo wa mambo, Yesu aliwaonya hivi Wakristo wa kweli: “Mtachukiwa na mataifa yote kwa sababu ya jina langu.” (Mathayo 24:9) Tunapokaribia mwisho, Shetani atafanya mataifa yaonyeshe chuki yao juu ya watu wa Yehova. (Ezekieli 38:10-12, 14-16) Hilo litadhihirisha wakati wa Yehova wa kutenda. “Hakika nitajitukuza mwenyewe na kujitakasa mwenyewe na kujijulisha mwenyewe mbele ya macho ya mataifa mengi; nao watalazimika kujua kwamba mimi ni Yehova.” (Ezekieli 38:23) Hivyo, Yehova atalitakasa jina lake kuu na kuwakomboa watu wake kutoka katika mateso. Kwa hiyo, “mwenye furaha ni mtu anayeendelea kuvumilia.”—Yakobo 1:12.

19. Tunapaswa kufanya nini tunapongojea ile ‘siku kuu ya Yehova’?

19 Ile ‘siku kuu ya Yehova’ inapozidi kukaribia, acheni tushangilie kwa sababu ‘tumehesabiwa kuwa wenye kustahili kuvunjiwa heshima’ kwa ajili ya jina la Yesu. (2 Petro 3:10-13; Matendo 5:41) Kama Wakristo wa mapema, na tuendelee “bila kuacha kufundisha na kutangaza habari njema juu ya Kristo” na serikali yake ya Ufalme huku tukingojea thawabu yetu katika ulimwengu mpya wa Yehova wenye uadilifu.—Matendo 5:42; Yakobo 5:11.

Kwa Kupitia

• Inamaanisha nini kuteseka kwa ajili ya uadilifu?

• Mateso yalikuwa na matokeo gani juu ya Wakristo wa mapema?

• Kwa nini tunaweza kusema kwamba Mashahidi wa Yehova wanateswa kama manabii wa kale?

• Kwa nini tunaweza ‘kushangilia na kuruka kwa shangwe’ tunapoteswa?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 16, 17]

“Wenye furaha ni ninyi wakati watu wanapowashutumu na kuwatesa”

[Hisani]

Group in prison: Chicago Herald-American