Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Tulifanya Uamuzi Thabiti wa Kuunga Mkono Utawala wa Mungu

Tulifanya Uamuzi Thabiti wa Kuunga Mkono Utawala wa Mungu

Simulizi la Maisha

Tulifanya Uamuzi Thabiti wa Kuunga Mkono Utawala wa Mungu

LIMESIMULIWA NA MICHAL ŽOBRÁK

Baada ya kukaa mwezi mmoja katika kifungo cha upweke, niliburutwa hadi kwa mhojaji fulani. Muda si muda, aligeuka rangi akawa mwekundu, kisha akasema: “Ninyi wapelelezi! Wapelelezi wa Marekani!” Kwa nini alikasirika hivyo? Alikuwa ametoka tu kuniuliza mimi ni wa dini gani, nami nikamjibu: “Mimi ni mmoja wa Mashahidi wa Yehova.”

JAMBO hilo lilitukia zaidi ya miaka 50 iliyopita. Wakati huo, nchi nilimoishi ilitawaliwa na Wakomunisti. Lakini muda mrefu kabla ya utawala huo, kazi yetu ya Kikristo ya kufundisha ilikuwa imepingwa vikali.

Vita Vyatuathiri Vikali

Vita vya Kwanza vya Ulimwengu vilipoanza mnamo 1914, nilikuwa na umri wa miaka minane. Wakati huo, kijiji chetu Zálužice, kilikuwa chini ya maliki wa Austria na Hungaria. Vita hivyo vilivuruga hali duniani na kwa ghafula vikanilazimisha kuchukua majukumu ya mtu mzima. Baba yangu aliyekuwa askari-jeshi, alikufa mwaka wa kwanza kabisa wa vita. Jambo hilo liliniacha mimi, mama yangu, na dada zangu wawili wadogo katika umaskini mkubwa. Muda si muda, nilijikuta nikiwa na majukumu mengi nyumbani na kwenye shamba letu dogo kwa kuwa mimi ndiye niliyekuwa mtoto wa kwanza wa kiume. Tangu utotoni, nilipenda dini sana. Mhudumu wa Kanisa letu la Kiprotestanti la Calvin hata alikuwa akiniomba nifundishe wanashule wenzangu kwa niaba yake wakati ambapo hakuwepo.

Sisi tulifurahi sana wakati Vita vya Kwanza vilipoisha mnamo 1918. Milki ya Austria na Hungaria ilikuwa imepinduliwa, nasi tukawa raia wa Jamhuri ya Chekoslovakia. Muda si muda, watu wengi wa eneo letu waliokuwa wamehamia Marekani walirudi nyumbani. Michal Petrík alikuwa mmoja wao, naye alikuja kijijini mwetu mwaka wa 1922. Alipotembelea familia fulani katika ujirani wetu, mimi na mama yangu tulialikwa.

Utawala wa Mungu Wapata Kuwa Halisi Kwetu

Michal alikuwa mwanafunzi wa Biblia, kama Mashahidi wa Yehova walivyoitwa wakati huo, naye alizungumzia masuala muhimu ya Biblia yaliyonivutia sana. Mojawapo ya mambo muhimu zaidi aliyozungumzia ni Ufalme wa Yehova unaokuja. (Danieli 2:44) Aliposema kwamba kungekuwa na mkutano wa Kikristo katika kijiji cha Záhor Jumapili iliyofuata, niliazimia kuhudhuria. Niliamka saa 10:00 za usiku na kutembea kilometa nane kwenda kwa binamu yangu kumwomba baiskeli. Baada ya kurekebisha gurudumu lililokuwa limetoboka, nilisafiri kilometa nyingine 24 hadi Záhor. Sikujua mkutano ungefanyiwa wapi, hivyo nikaanza kwenda polepole kwenye barabara moja. Ndipo nikatambua wimbo fulani wa Ufalme uliokuwa ukiimbwa katika nyumba fulani. Nilifurahi sana, nikaingia kwenye nyumba hiyo na kueleza kilichokuwa kimenileta huko. Nilikaribishwa kula kiamsha-kinywa pamoja na familia hiyo, kisha wakanipeleka kwenye mikutano. Ingawa ilinibidi kuendesha baiskeli na kutembea kilometa 32 zaidi ili kufika nyumbani, sikuhisi uchovu wowote.—Isaya 40:31.

Nilipendezwa sana na maelezo ya Mashahidi wa Yehova yaliyokuwa wazi na ambayo yalitegemea Biblia. Niliguswa moyo sana na tarajio la kufurahia kikamili maisha yenye kuridhisha chini ya utawala wa Mungu. (Zaburi 104:28) Mimi na mama yangu tuliamua kutuma barua ya kujiondoa katika kanisa letu. Jambo hilo lilileta vurugu kubwa kijijini mwetu. Wengine hata waliacha kuzungumza nasi kwa muda, lakini tulikuwa na ushirika mzuri pamoja na Mashahidi wa eneo letu waliokuwa wengi. (Mathayo 5:11, 12) Baada ya muda mfupi nilibatizwa katika Mto Uh.

Huduma Yawa Jambo la Kawaida Kwetu

Tulitumia kila nafasi kuhubiri kuhusu Ufalme wa Yehova. (Mathayo 24:14) Tulizingatia hasa mahubiri ya Jumapili ambayo yalipangwa vizuri. Kwa kawaida, watu waliamka mapema wakati huo, hivyo tulianza kuhubiri mapema. Hotuba ya watu wote ilitolewa baadaye siku hiyo. Nyakati nyingi walimu wa Biblia hawakutumia hati yoyote. Walizingatia hesabu ya watu waliopendezwa, malezi yao ya kidini, na mambo yaliyowahangaisha.

Kweli za Biblia tulizohubiri zilifungua macho ya watu wengi wenye mioyo minyoofu. Punde baada ya kubatizwa, nilihubiri katika kijiji cha Trhovište. Kwenye nyumba moja, nilizungumza na Bi. Zuzana Moskal, mwanamke mwenye fadhili na urafiki sana. Yeye na familia yake walikuwa wafuasi wa dini ya Calvin, ambayo pia ndiyo iliyokuwa dini yangu zamani. Ingawa aliifahamu Biblia, alikuwa na maswali mengi ya Biblia ambayo hakuwa amejibiwa. Tulizungumza naye kwa muda wa saa moja, nami nikamwachia kitabu, The Harp of God. *

Familia ya Moskal ilianza mara moja kusoma kitabu Harp katika vipindi vyao vya kawaida vya kusoma Biblia. Familia zaidi katika kijiji hicho zilianza kupendezwa, nazo zikaanza kuhudhuria mikutano yetu. Mhudumu wao aliyekuwa mfuasi wa Calvin aliwaonya vikali kutuhusu na kuhusu vichapo vyetu. Kisha baadhi ya watu waliopendezwa wakapendekeza kwamba kasisi huyo aje kwenye mikutano yetu na kukanusha mafundisho yetu katika mjadala wa hadharani.

Mhudumu huyo alikuja, lakini hakuweza kutoa hata hoja moja katika Biblia kuunga mkono mafundisho yake. Alisema hivi ili kujitetea: “Hatuwezi kuamini kila kitu katika Biblia. Iliandikwa na wanadamu, nayo maswali ya kidini yanaweza kufafanuliwa katika njia tofauti-tofauti.” Wakati huo wengi walifanya badiliko kubwa. Wengine walimwambia mhudumu huyo kwamba kama yeye haamini Biblia, wao hawangeenda tena kusikiliza mahubiri yake. Hivyo, waliacha Kanisa la Calvin, na wanakijiji wapatao 30 wakachukua msimamo thabiti kwa ajili ya kweli ya Biblia.

Lilikuwa jambo la kawaida kwetu kuhubiri habari njema ya Ufalme, kwa hiyo nilikuwa nikitafuta mwenzi kutoka familia yenye nguvu kiroho. Nilishirikiana katika huduma na Ján Petruška, aliyejifunza kweli huko Marekani. Binti yake Mária alinivutia kwa kuwa, kama babake, alikuwa tayari kumtolea kila mtu ushahidi. Tulioana mnamo 1936, na Mária akawa mwenzi wangu mwaminifu kwa miaka 50, hadi alipokufa mnamo 1986. Mwana wetu wa pekee, Eduard, alizaliwa mnamo 1938. Lakini wakati huo, vita vingine vilikuwa vinanukia huko Ulaya. Vingeathirije kazi yetu?

Msimamo Wetu wa Kikristo wa Kutokuwamo Wajaribiwa

Vita vya Pili vya Ulimwengu vilipoanza, Slovakia, ambayo ilikuwa nchi huru, ilikuwa chini ya utawala wa Nazi. Lakini serikali haikuchukua hatua yoyote hususa dhidi ya Mashahidi wa Yehova wakiwa tengenezo. Bila shaka, ilitubidi tufanye kazi kwa siri, navyo vichapo vyetu vilidhibitiwa. Hata hivyo, tuliendelea na kazi yetu kwa busara.—Mathayo 10:16.

Vita vilipopamba moto, niliitwa jeshini, ingawa nilikuwa na umri wa miaka zaidi ya 35. Kwa sababu ya msimamo wangu wa Kikristo wa kutokuwamo, nilikataa kupigana. (Isaya 2:2-4) Jambo la kufurahisha ni kwamba kabla ya wenye mamlaka kuamua wanifanyie nini, sote tuliokuwa na umri wa miaka zaidi ya 35 tuliachiliwa.

Tulitambua kwamba ilikuwa vigumu zaidi kwa ndugu zetu waliokuwa majijini kupata riziki kuliko sisi tulioishi mashambani. Tulitaka kugawana nao vyakula tulivyokuwa navyo. (2 Wakorintho 8:14) Hivyo, tulikuwa tukisafiri zaidi ya kilometa 500 kuvuka nchi hadi Bratislava, huku tukiwa tumebeba vyakula vingi iwezekanavyo. Urafiki na upendo wa Kikristo tuliositawisha wakati wa vita ulitutegemeza katika miaka migumu ya baadaye.

Kupata Kitia Moyo Tulichohitaji

Baada ya Vita vya Pili vya Ulimwengu, Slovakia ikawa tena sehemu ya Chekoslovakia. Kuanzia mwaka wa 1946 hadi 1948, makusanyiko ya kitaifa ya Mashahidi wa Yehova yalifanyiwa Brno ama Prague. Sisi tuliotoka mashariki mwa Slovakia tulisafiri kwa magarimoshi maalumu yaliyokodishwa kusafirisha wajumbe wa kusanyiko hilo. Unaweza kuyaita magarimoshi yenye kuimba kwa kuwa tuliimba wakati wote wa safari.—Matendo 16:25.

Ninakumbuka hasa kusanyiko la mwaka wa 1947 huko Brno, ambako waangalizi watatu Wakristo kutoka makao makuu ya ulimwengu, kutia ndani Ndugu Nathan H. Knorr walihudhuria. Ili kutangaza hotuba ya watu wote, wengi wetu tulitembea jijini tukiwa tumebeba mabango yaliyokuwa na kichwa cha hotuba hiyo. Mwana wetu Eduard, ambaye wakati huo alikuwa na umri wa miaka 9 tu, alihuzunika sana kwa kuwa hakupata bango. Kwa hiyo, ndugu walitengeneza mabango madogo kwa ajili yake na pia watoto wengine wengi. Watoto hao walifanya kazi nzuri sana ya kutangaza hotuba hiyo!

Mnamo Februari 1948, Wakomunisti walianza kutawala. Tulijua kwamba hatimaye serikali ingechukua hatua ya kuzuia huduma yetu. Kusanyiko moja lilifanywa huko Prague, Septemba 1948, nasi tuliogopa sana kwa kuwa tulidhani kwamba mikutano yetu ya hadharani ingepigwa marufuku tena, baada ya kukutana bila kizuizi chochote kwa miaka mitatu tu. Kabla ya kuondoka kwenye kusanyiko hilo, tulikubali azimio ambalo kwa sehemu lilisema: “Sisi Mashahidi wa Yehova ambao tumekusanyika pamoja . . ., tumeazimia kupanua utumishi huu wenye kuridhisha, na, kwa neema ya Bwana, kuendelea na utumishi huo katika majira yanayofaa na ya majaribu, na kutangaza Injili ya ufalme wa Mungu kwa bidii hata zaidi.”

“Maadui wa Serikali”

Miezi miwili tu baada ya kusanyiko la Prague, polisi wa siri walivamia makao ya Betheli karibu na Prague. Walinyakua makao hayo, wakatwaa vichapo vyovyote walivyopata, na kuwakamata Wanabetheli wote na ndugu wengine kadhaa. Na si hayo tu.

Usiku wa tarehe 3 na 4 Februari, 1952, maofisa wa usalama walisaka nchi yote na kuwakamata Mashahidi zaidi ya 100. Nilikuwa mmoja wao. Polisi waliamsha familia yangu yote mwendo wa saa tisa alfajiri. Waliniomba niandamane nao bila kunieleza chochote. Nilitiwa pingu na kufunikwa macho, kisha mimi pamoja na watu wengine tukatupwa nyuma ya lori. Niliishia katika kifungo cha upweke.

Hakuna mtu aliyezungumza nami kwa mwezi mmoja. Mtu pekee niliyeona ni mlinzi ambaye alisukuma chakula kidogo kupitia mwanya fulani kwenye mlango. Kisha nikaitwa na mhojaji aliyetangulia kutajwa. Baada ya kusema mimi ni jasusi, aliongeza: “Dini ni ujinga. Hakuna Mungu! Hatuwezi kuwaruhusu mwadanganye wafanyakazi wetu. Mtanyongwa au mfe gerezani. Na kama Mungu wenu angekuja hapa, tungemuua pia!”

Kwa kuwa wenye mamlaka walijua kwamba hapakuwa na sheria hususa iliyokataza utendaji wetu wa Kikristo, walitaka utendaji wetu uonekane kuwa unapingana na sheria zilizokuwepo kwa kuonyesha kwamba sisi tulikuwa “maadui wa Serikali” na majasusi wa nchi za kigeni. Ili kufanya hivyo, walihitaji kuvunja azimio letu na kutufanya “tukiri” mashtaka ya uwongo. Baada ya kuhojiwa usiku huo, sikuruhusiwa kulala. Baada ya saa chache, nilihojiwa tena. Wakati huu, mtu aliyenihoji alitaka nitie sahihi taarifa iliyosema: “Mimi nikiwa adui wa Jamhuri ya Watu wa Chekoslovakia sikujiunga na [shamba la ushirika] kwa sababu nilikuwa nikiwangojea Wamarekani.” Nilipokataa kutia sahihi taarifa hiyo ya uwongo, nilipelekwa kwenye seli ya urekebishaji tabia.

Nilikatazwa kulala, kujilaza chini, au hata kuketi. Ningeweza tu kusimama au kutembea-tembea. Nilipochoka, nililala kwenye sakafu. Kisha walinzi wakanirudisha kwenye ofisi ya mhojaji. “Utatia sahihi sasa?” mhojaji huyo akaniuliza. Nilipokataa tena, alinipiga tena usoni. Nilianza kutokwa na damu. Ndipo akawaambia walinzi kwa sauti nzito hivi: “Anataka kujiua. Mwe waangalifu sana asijiue!” Nilirudishwa kwenye kifungo cha upweke. Kwa muda wa miezi sita, mbinu hizo za kuhoji zilirudiwa mara nyingi. Hakuna ushawishi wa kimawazo wala jitihada za kunifanya nikiri kwamba nilikuwa adui wa Serikali zingeweza kupunguza azimio langu la kudumisha utimilifu wangu kwa Yehova.

Mwezi mmoja kabla ya kupelekwa mahakamani, mwendesha-mashtaka mmoja kutoka Prague alikuja na kuhoji kila mmoja wetu tukiwa ndugu 12. Aliniuliza hivi: “Utafanya nini mataifa ya Magharibi yakishambulia nchi yetu?” Nilimjibu, “Nitafanya vile nilivyofanya wakati nchi hii pamoja na Hitler waliposhambulia Muungano wa Sovieti. Sikupigana wakati huo, na sitapigana sasa kwa kuwa mimi ni Mkristo na siungi mkono upande wowote.” Kisha akaniambia: “Hatuwezi kuwavumilia Mashahidi wa Yehova. Tunahitaji askari-jeshi endapo mataifa ya Magharibi yatatushambulia, na tunahitaji askari-jeshi wa kuwakomboa wafanyakazi wetu huko Magharibi.”

Mnamo Julai 24, 1953, tulipelekwa mahakamani. Sote 12 tuliitwa mbele ya jopo la mahakimu, mmoja baada ya mwingine. Tulitumia nafasi hiyo kutoa ushahidi kuhusu imani yetu. Baada ya kujitetea kuhusiana na mashtaka ya uwongo dhidi yetu, mwanasheria mmoja alisimama na kusema: “Nimekuwa katika mahakama hii mara nyingi. Kwa kawaida, watu wengi hukiri makosa yao, hutubu, na hata kulia. Lakini watu hawa watatoka hapa wakiwa imara zaidi kuliko wakati walipokuja.” Baadaye, sote 12 tulipatikana na hatia ya kula njama dhidi ya Serikali. Nilihukumiwa kifungo cha miaka mitatu na mali yangu ikatwaliwa na Serikali.

Uzee Haujanizuia

Niliporudi nyumbani, bado polisi wa siri walikuwa wakinipeleleza. Licha ya hayo nilirudia utendaji wangu wa kiroho na kuwekwa kuwa msimamizi wa kutaniko letu. Ingawa tuliruhusiwa kuishi katika nyumba yetu iliyokuwa imetwaliwa na Serikali, tulirudishiwa nyumba hiyo kirasmi miaka 40 hivi baadaye, baada ya Ukomunisti kuporomoka.

Si mimi tu katika familia yetu niliyefungwa gerezani. Miaka mitatu tu baada ya kurudi nyumbani, Eduard aliitwa jeshini. Alipokataa kwa sababu ya dhamiri yake iliyozoezwa na Biblia, Eduard alitiwa gerezani. Miaka kadhaa baadaye, hata mjukuu wangu, Peter, alitiwa gerezani licha ya afya yake mbaya.

Mnamo 1989, utawala wa Kikomunisti huko Chekoslovakia uliporomoka. Nilifurahi kama nini kuweza kuhubiri nyumba kwa nyumba kwa uhuru baada ya miaka 40 ya marufuku! (Matendo 20:20) Nilifurahia aina hiyo ya utumishi kadiri afya yangu ilivyoniruhusu. Kwa kuwa sasa nina miaka 98, hali yangu ya afya imedhoofika, lakini ninafurahi kwamba bado ninaweza kuwahubiria watu juu ya ahadi tukufu za Yehova kuhusu wakati ujao.

Ninaweza kukumbuka viongozi 12 wa nchi tano tofauti ambao walitawala mji wetu wa nyumbani. Walitia ndani madikteta, marais, na mfalme mmoja. Hakuna hata mmoja wao aliyetoa utatuzi wa kudumu kwa matatizo yaliyowakumba watu chini ya utawala wao. (Zaburi 146:3, 4) Ninamshukuru Yehova kwa kuwa aliniruhusu kumjua nikiwa bado mdogo. Hivyo, niliweza kutambua suluhisho lake kupitia Ufalme wa Kimasihi na kuepuka ubatili wa kuishi bila Mungu. Nimehubiri kwa bidii habari zilizo bora kwa zaidi ya miaka 75, na hilo limefanya maisha yangu yawe na kusudi, uradhi, na tumaini zuri la kuishi milele duniani. Ningeomba nini kingine? *

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 14 Kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova na ambacho hakichapwi tena.

^ fu. 38 Inasikitisha kwamba hatimaye Ndugu Michal Žobrák aliishiwa na nguvu. Makala hii ilipokuwa ikitayarishwa ili kuchapwa, Žobrák alikufa akiwa mwaminifu na akiwa na uhakika katika tumaini la ufufuo.

[Picha katika ukurasa wa 26]

Punde baada ya arusi yetu

[Picha katika ukurasa wa 26]

Nikiwa na Eduard mapema miaka ya 1940

[Picha katika ukurasa wa 27]

Kutangaza kusanyiko huko Brno, mnamo 1947