Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Watumishi wa Yehova Wenye Furaha

Watumishi wa Yehova Wenye Furaha

Watumishi wa Yehova Wenye Furaha

“Wenye furaha ni wale wanaotambua uhitaji wao wa kiroho.”—MATHAYO 5:3.

1. Furaha ya kweli ni nini, nayo huonyesha nini?

WATU wa Yehova huthamini sana hali yao yenye furaha. Mtunga-zaburi Daudi alisema: “Wenye furaha ni watu ambao Mungu wao ni Yehova.” (Zaburi 144:15) Furaha ni kuchangamka kwa ajili ya jambo lenye kupendeza. Furaha kuu zaidi, inayogusa hisia zetu za ndani kabisa, hutokana na kule kufahamu kwamba tumekubaliwa na Yehova. (Methali 10:22) Furaha hiyo huonyesha kwamba tuna uhusiano wa karibu na Baba yetu wa mbinguni na kutambua kwamba tunafanya mapenzi yake. (Zaburi 112:1; 119:1, 2) Inapendeza kwamba Yesu alitaja sababu tisa zinazoweza kutufanya tuwe na furaha. Kuchunguza sababu za kuwa na furaha katika makala hii na ile inayofuata kutatusaidia tufahamu ni kwa kadiri gani tunaweza kuwa na furaha ikiwa tutamtumikia kwa uaminifu Yehova, yule “Mungu mwenye furaha.”—1 Timotheo 1:11.

Kutambua Uhitaji Wetu wa Kiroho

2. Ni pindi gani Yesu alizungumzia furaha, na ni yapi yaliyokuwa maneno yake ya utangulizi?

2 Mnamo mwaka wa 31 W.K., Yesu alitoa mojawapo ya hotuba maarufu zaidi kuwahi kutolewa. Inaitwa Mahubiri ya Mlimani kwa sababu Yesu aliitoa kwenye mlima ulioelekeana na Bahari ya Galilaya. Injili ya Mathayo inasema: “[Yesu] alipouona umati akapanda mlimani; na baada ya kuketi wanafunzi wake wakamjia; naye akafungua kinywa chake na kuanza kuwafundisha, akisema: ‘Wenye furaha ni wale wanaotambua uhitaji wao wa kiroho, kwa kuwa ufalme wa mbinguni ni wao.’” Maneno ya Yesu ya utangulizi yanapotafsiriwa kihalisi, yanasema: “Wenye furaha ni wale walio maskini wa roho.” (Mathayo 5:1-3; Kingdom Interlinear) Tafsiri ya Today’s English Version inasema: “Wenye furaha ni wale wanaotambua kwamba wao ni maskini kiroho.”

3. Kuwa wanyenyekevu huchangiaje furaha yetu?

3 Katika Mahubiri yake ya Mlimani, Yesu alisema kwamba mtu anakuwa mwenye furaha zaidi ikiwa anatambua kwamba ana uhitaji wa kiroho. Wakristo wanyenyekevu, wanaotambua kabisa hali yao yenye dhambi, humwomba Yehova msamaha kwa msingi wa dhabihu ya fidia ya Kristo. (1 Yohana 1:9) Hivyo, wao hupata amani ya akili na furaha ya kweli. “Mwenye furaha ni mtu ambaye amesamehewa maasi yake, ambaye dhambi yake imefunikwa.”—Zaburi 32:1; 119:165.

4. (a) Ni katika njia zipi tunaweza kuonyesha kwamba tunatambua uhitaji wetu wa kiroho na wa wengine? (b) Ni nini huongeza furaha yetu tunapotambua uhitaji wetu wa kiroho?

4 Kutambua uhitaji wetu wa kiroho hutuchochea tusome Biblia kila siku, tupate manufaa kamili kutokana na chakula cha kiroho kinachotolewa “kwa wakati unaofaa” na “mtumwa mwaminifu na mwenye busara,” na tuhudhurie mikutano ya Kikristo kwa ukawaida. (Mathayo. 24:45; Zaburi 1:1, 2; 119:111; Waebrania 10:25) Upendo kwa jirani hufanya tutambue uhitaji wa kiroho wa wengine na kutuchochea tuwe wenye bidii katika kuhubiri na kufundisha habari njema ya Ufalme. (Marko 13:10; Warumi 1:14-16) Tunapata furaha kwa kuwaeleza wengine kweli za Biblia. (Matendo 20:20, 35) Furaha yetu huongezeka tunapotafakari kuhusu tumaini zuri la Ufalme na baraka ambazo Ufalme huo utaleta. Tumaini la “kundi dogo” la Wakristo watiwa-mafuta ni kupata uhai usioweza kufa huko mbinguni wakiwa sehemu ya serikali ya Ufalme ya Kristo. (Luka 12:32; 1 Wakorintho 15:50, 54) Nao “kondoo wengine” wana tumaini la kupata uzima wa milele katika paradiso duniani chini ya serikali hiyo ya Ufalme.—Yohana 10:16; Zaburi 37:11; Mathayo 25:34, 46.

Jinsi Wanaoomboleza Wanavyoweza Kuwa na Furaha

5. (a) Maneno “wale wanaoomboleza” yanamaanisha nini? (b) Watu hao wanaoomboleza hufarijiwaje?

5 Maneno yanayohusu furaha ambayo Yesu alifuatia kutaja yanaonekana kama yanajipinga. Alisema: “Wenye furaha ni wale wanaoomboleza, kwa kuwa watafarijiwa.” (Mathayo 5:4) Mtu anawezaje kuomboleza na wakati huohuo awe na furaha? Ili kuelewa maana ya maneno ya Yesu, tunahitaji kufikiria anazungumza kuhusu maombolezo ya aina gani. Mwanafunzi Yakobo anaeleza kwamba hali yetu wenyewe yenye dhambi inapaswa kutufanya tuomboleze. Aliandika: “Safisheni mikono yenu, ninyi watenda-dhambi, na takaseni mioyo yenu, ninyi wenye kusitasita. Iweni na taabu na kuomboleza na kulia. Kicheko chenu na kigeuzwe kuwa maombolezo, na shangwe yenu kuwa huzuni. Jinyenyekezeni machoni pa Yehova, naye atawainua ninyi.” (Yakobo 4:8-10) Wale wanaosikitishwa kikweli na hali yao yenye dhambi hufarijika wanapotambua kwamba wanaweza kusamehewa dhambi wakionyesha imani katika dhabihu ya fidia ya Kristo na kuonyesha toba ya kweli kwa kufanya mapenzi ya Yehova. (Yohana 3:16; 2 Wakorintho 7:9, 10) Hivyo wanaweza kuwa na uhusiano mzuri na Yehova na kuwa na tumaini la kuishi milele ili kumtumikia na kumsifu. Hiyo huwaletea furaha nyingi ya moyoni.—Waroma 4:7, 8.

6. Wengine huomboleza katika maana gani, nao hufarijiwaje?

6 Pia maneno ya Yesu yanatia ndani wale wanaoomboleza kwa sababu ya hali zenye kuchukiza zilizopo duniani. Yesu alisema kuwa maneno haya ya unabii wa Isaya 61:1, 2, yanamhusu: “Roho ya Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova iko juu yangu, kwa sababu Yehova amenitia mafuta niwatangazie wapole habari njema. Amenituma kufunga majeraha ya waliovunjika moyo, . . . kuwafariji wote wanaoomboleza.” Utume huo unawahusu pia Wakristo watiwa-mafuta walio duniani leo, ambao huutekeleza wakisaidiwa na waandamani wao, “kondoo wengine.” Wote wanashiriki katika kazi ya kutia alama kwa njia ya mfano kwenye mapaji ya nyuso za “watu wanaougua na kulia kwa sababu ya machukizo yote yanayofanywa katikati yake [Yerusalemu lililoasi, linalofananisha dini zinazojiita za Kikristo].” (Ezekieli 9:4) Watu hao wanaoomboleza hufarijiwa na “habari njema ya ufalme.” (Mathayo 24:14) Wanafurahi kujua kwamba hivi karibuni ulimwengu mpya wa Yehova wenye uadilifu utachukua mahali pa mfumo mwovu wa mambo wa Shetani.

Wenye Furaha Ni Wale Walio na Tabia-Pole

7. Neno “tabia-pole” halimaanishi nini?

7 Yesu aliendelea na Mahubiri yake ya Mlimani kwa kusema: “Wenye furaha ni wale walio na tabia-pole, kwa kuwa watairithi dunia.” (Mathayo 5:5) Nyakati nyingine tabia-pole huonwa kuwa udhaifu. Hata hivyo, sivyo ilivyo. Akieleza maana ya neno linalotafsiriwa “tabia-pole,” msomi mmoja wa Biblia aliandika hivi: “Sifa kuu ya mtu mwenye tabia-pole ni kwamba yeye hujizuia sana. Sifa hiyo haimaanishi kutojikakamua, kuongozwa na hisia tu, wala utulivu ambao hutokana na kutojiingiza katika jambo fulani. Ni nguvu zenye kuzuiwa.” Yesu alisema hivi kujihusu: “Mimi ni mwenye tabia-pole na mnyenyekevu moyoni.” (Mathayo 11:29) Hata hivyo, Yesu alikuwa jasiri katika kutetea kanuni za uadilifu.—Mathayo 21:12, 13; 23:13-33.

8. Sifa ya tabia-pole inahusianishwa kwa ukaribu na nini, na kwa nini tunahitaji sifa hiyo tunaposhughulika na wengine?

8 Kwa hiyo, tabia-pole inahusianishwa kwa ukaribu na kujizuia. Kwa kweli, mtume Paulo aliorodhesha tabia-pole pamoja na kujizuia alipotaja “matunda ya roho.” (Wagalatia 5:22, 23) Sifa ya tabia-pole inapaswa kusitawishwa kwa msaada wa roho takatifu. Ni sifa ya Kikristo ambayo huchangia amani pamoja na wasioamini kutia ndani wale walio kutanikoni. Paulo aliandika: “Jivikeni upendo mwororo wenye huruma, fadhili, unyenyekevu wa akili, upole, na ustahimilivu. Endeleeni kuvumiliana na kusameheana kwa hiari.”—Wakolosai 3:12, 13.

9. (a) Kwa nini kuwa mwenye tabia-pole hakuhusishi tu mahusiano yetu na wengine? (b) Watu wenye tabia-pole ‘watairithi dunia’ jinsi gani?

9 Hata hivyo, tabia-pole haihusu tu mahusiano yetu na wanadamu wengine. Sisi huonyesha kwamba tuna tabia-pole tunapojitiisha kwa hiari chini ya enzi kuu ya Yehova. Yesu Kristo ndiye kielelezo kikuu cha sifa hiyo kwa kuwa alipokuwa duniani alionyesha tabia-pole na kujitiisha kikamili kwa mapenzi ya Baba yake. (Yohana 5:19, 30) Yesu hasa anarithi dunia, kwa kuwa yeye ndiye Mtawala wa dunia aliyewekwa rasmi. (Zaburi 2:6-8; Danieli 7:13, 14) Anashiriki urithi huo akiwa na wale 144,000 walio ‘warithi pamoja naye,’ ambao wamechaguliwa “kati ya wanadamu” ili ‘watawale wakiwa wafalme juu ya dunia.’ (Waroma 8:17; Ufunuo 5:9, 10; 14:1, 3, 4; Danieli 7:27) Kristo pamoja na watawala wenzake watatawala mamilioni ya wanaume na wanawake walio mfano wa kondoo, ambao watapata utimizo wenye furaha wa unabii huu wa zaburi: “Wapole wataimiliki dunia, nao watapata furaha yao tele katika wingi wa amani.”—Zaburi 37:11; Mathayo 25:33, 34, 46.

Wenye Furaha Ni Wale Walio na Njaa kwa Ajili ya Uadilifu

10. Ni katika njia gani moja wale ‘walio na njaa na kiu kwa ajili ya uadilifu’ hutoshelezwa?

10 Sababu nyingine ya kuwa na furaha iliyotajwa na Yesu alipokuwa akizungumza kwenye mlima huo wa Galilaya ilikuwa: “Wenye furaha ni wale walio na njaa na walio na kiu kwa ajili ya uadilifu, kwa kuwa watashibishwa.” (Mathayo 5:6) Yehova ndiye huwawekea Wakristo kiwango cha uadilifu. Hivyo basi, wale walio na njaa na kiu kwa ajili ya uadilifu wana njaa na kiu ya kupata mwongozo wa Mungu. Watu hao wanatambua vizuri hali yao ya dhambi na kutokamilika, nao wanatamani kuwa na msimamo unaokubalika mbele za Yehova. Wao hufurahi kama nini wanapojifunza katika Neno la Mungu kwamba wakitubu na kutafuta msamaha kwa msingi wa dhabihu ya fidia ya Kristo, wataweza kuwa na nafasi ya kupata msimamo wenye uadilifu mbele za Mungu!—Matendo 2:38; 10:43; 13:38, 39; Waroma 5:19.

11, 12. (a) Wakristo watiwa-mafuta hupataje kuwa waadilifu? (b) Kiu ya waandamani wa watiwa-mafuta kwa ajili ya uadilifu hutoshelezwaje?

11 Yesu alisema kwamba watu hao wangekuwa na furaha kwa kuwa “watatoshelezwa.” (Mathayo 5:6, Kingdom Interlinear) Wakristo watiwa-mafuta ambao wamepewa mwito wa ‘kutawala wakiwa wafalme’ pamoja na Kristo mbinguni wanatangazwa kuwa “waadilifu kwa ajili ya uzima.” (Waroma 5:1, 9, 16-18) Yehova huwafanya kuwa wana wa kiroho. Wanakuwa warithi pamoja na Kristo, na kupewa mwito wa kuwa wafalme na makuhani katika serikali ya Ufalme wa mbinguni.—Yohana 3:3; 1 Petro 2:9.

12 Waandamani wa watiwa-mafuta bado hawajatangazwa kuwa waadilifu kwa ajili ya uzima. Hata hivyo, kupitia imani yao katika damu iliyomwagwa ya Kristo, Yehova huwahesabu kuwa waadilifu kwa kadiri fulani. (Yakobo 2:22-25; Ufunuo 7:9, 10) Wao huhesabiwa kuwa waadilifu wakiwa rafiki za Yehova nao wana taraja la kukombolewa wakati wa “dhiki kuu.” (Ufunuo 7:14) Chini ya “mbingu mpya,” kiu yao kwa ajili ya uadilifu itatoshelezwa hata zaidi wakati ambapo watakuwa sehemu ya dunia mpya ambamo “uadilifu utakaa.”—2 Petro 3:13; Zaburi 37:29.

Wenye Furaha Ni Wale Walio na Rehema

13, 14. Tunawezaje kuonyesha rehema katika njia halisi, nasi tutanufaikaje?

13 Yesu aliendelea kusema hivi katika Mahubiri yake ya Mlimani: “Wenye furaha ni wale walio na rehema, kwa kuwa wataonyeshwa rehema.” (Mathayo 5:7) Katika maana ya kisheria, rehema inaeleweka kuwa inarejelea huruma ya hakimu ambaye huepuka kumpa mkosaji adhabu kamili inayokubalika na sheria. Hata hivyo, katika Biblia, maneno ya awali yanayotafsiriwa “rehema” hurejelea hasa kuonyesha fadhili au sikitiko linalowaletea kitulizo wale walio katika hali mbaya. Hivyo, wale walio na rehema huonyesha huruma. Mfano wa Yesu kuhusu Msamaria mwenye ujirani ni kielelezo kizuri cha mtu “aliyemtendea kwa rehema” mtu mwenye uhitaji.—Luka 10:29-37.

14 Ili kupata furaha inayotokana na kuwa mwenye rehema, tunahitaji kuwafanyia mambo yenye fadhili wale wenye uhitaji. (Wagalatia 6:10) Yesu aliwahurumia watu aliowaona. ‘Aliwasikitikia, kwa sababu walikuwa kama kondoo wasio na mchungaji. Naye akaanza kuwafundisha mambo mengi.’ (Marko 6:34) Yesu alitambua kwamba uhitaji wa kiroho ndio muhimu zaidi kwa wanadamu. Sisi pia tunaweza kuonyesha huruma na rehema kwa kuwaeleza wengine kile wanachohitaji zaidi, yaani, “habari njema ya ufalme.” (Mathayo 24:14) Pia tunaweza kuwasaidia Wakristo wenzetu wenye umri mkubwa, wajane, na mayatima na ‘kusema kwa kuzifariji nafsi zilizohuzunika.’ (1 Wathesalonike 5:14; Methali 12:25; Yakobo 1:27) Hilo litatuletea furaha na pia Yehova ataturehemu.—Matendo 20:35; Yakobo 2:13.

Walio Safi Moyoni na Wanaofanya Amani

15. Tunawezaje kuwa safi moyoni na wenye kufanya amani?

15 Yesu alitaja sababu ya sita na ya saba ya kuwa na furaha kama ifuatavyo: “Wenye furaha ni wale walio safi moyoni, kwa kuwa watamwona Mungu. Wenye furaha ni wale wanaofanya amani, kwa kuwa wataitwa ‘wana wa Mungu.’” (Mathayo 5:8, 9) Moyo safi ni ule ambao umetakata kiadili na kiroho na ambao umeungana katika ujitoaji kwa Yehova. (1 Mambo ya Nyakati 28:9; Zaburi 86:11) Wale wanaofanya amani huishi kwa amani pamoja na ndugu zao Wakristo na, ikiwa wanaweza, pamoja na majirani wao. (Waroma 12:17-21) Wao ‘hutafuta amani na kuifuatilia.’—1 Petro 3:11.

16, 17. (a) Kwa nini watiwa-mafuta huitwa “wana wa Mungu,” nao ‘humwonaje Mungu’? (b) “Kondoo wengine” ‘humwonaje Mungu’? (c) “Kondoo wengine” watakuwa “wana wa Mungu” katika maana kamili lini na jinsi gani?

16 Wale wanaofanya amani ambao ni safi moyoni, wanaahidiwa kwamba “wataitwa ‘wana wa Mungu’” nao “watamwona Mungu.” Wakristo watiwa-mafuta huzaliwa kwa roho naye Yehova huwafanya kuwa “wana” wakiwa wangali duniani. (Waroma 8:14-17) Wanapofufuliwa ili wawe na Kristo mbinguni, wao hutumika mbele za Yehova na kumwona kihalisi.—1 Yohana 3:1, 2; Ufunuo 4:9-11.

17 “Kondoo wengine” wenye kufanya amani humtumikia Yehova chini ya Mchungaji Mwema, Kristo Yesu, ambaye anakuwa ‘Baba yao wa Milele.’ (Yohana 10:14, 16; Isaya 9:6) Wale watakaopita mtihani wa mwisho baada ya Utawala wa Miaka Elfu wa Kristo watafanywa kuwa wana wa kidunia wa Yehova na “kuwa na uhuru wenye utukufu wa watoto wa Mungu.” (Waroma 8:21; Ufunuo 20:7, 9) Wanapongojea kwa hamu jambo hilo, wao humwita Yehova Baba yao, kwa kuwa wanajiweka wakfu kwake, na kumtambua kuwa Mpaji-Uhai wao. (Isaya 64:8) Kama vile Ayubu na Musa wa nyakati za kale, wanaweza ‘kumwona Mungu’ kwa macho ya imani. (Ayubu 42:5; Waebrania 11:27) Kupitia ‘macho ya mioyo yao’ na ujuzi sahihi kumhusu Mungu, wanaona sifa nzuri za Yehova na kujitahidi kumwiga kwa kufanya mapenzi yake.—Waefeso 1:18; Waroma 1:19, 20; 3 Yohana 11.

18. Kulingana na sababu za kwanza saba za kuwa na furaha ambazo Yesu alitaja, leo ni nani wanaopata furaha ya kweli?

18 Tumeona kwamba wale wanaotambua uhitaji wao wa kiroho, wale wanaoomboleza, wale walio na tabia-pole, wale walio na njaa na kiu kwa ajili ya uadilifu, wale walio na rehema, wale walio safi moyoni, na wale wanaofanya amani hupata furaha ya kweli katika kumtumikia Yehova. Hata hivyo, sikuzote wao wamepatwa na upinzani na hata wameteswa. Je, jambo hilo huvuruga furaha yao? Swali hilo litazungumziwa katika makala inayofuata.

Kwa Kupitia

• Wale wanaotambua uhitaji wao wa kiroho hupata furaha gani?

• Wale wanaoomboleza hufarijiwa katika njia zipi?

• Tunaonyeshaje tabia-pole?

• Kwa nini tunapaswa kuwa wenye rehema, safi moyoni, na wenye kufanya amani?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 10]

“Wenye furaha ni wale wanaotambua uhitaji wao wa kiroho”

[Picha katika ukurasa wa 10]

“Wenye furaha ni wale walio na rehema”

[Picha katika ukurasa wa 10]

“Wenye furaha ni wale walio na njaa na walio na kiu kwa ajili ya uadilifu”