Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

“Hema la Wanyoofu Litasitawi”

“Hema la Wanyoofu Litasitawi”

“Hema la Wanyoofu Litasitawi”

DHORUBA ya Har–Magedoni itakapotokea na kuukomesha mfumo mwovu wa mambo wa Shetani, “nyumba ya watu waovu itaharibiwa.” Namna gani “hema la wanyoofu”? Kwa kweli, katika ulimwengu mpya wa Mungu “litasitawi.”—Methali 14:11.

Hata hivyo, wasio na lawama watalazimika kuendelea kuishi pamoja na waovu hadi wakati ambapo ‘waovu watakatiliwa mbali kutoka duniani nao wenye hila kung’olewa kutoka ndani yake.’ (Methali 2:21, 22) Je, wanyoofu wanaweza kusitawi chini ya hali hizo? Mstari wa 1 hadi 11 wa sura ya 14 ya kitabu cha Biblia cha Methali huonyesha kwamba tukiacha hekima iongoze maneno na matendo yetu, tunaweza kuwa na ufanisi na utulivu kwa kadiri fulani hata sasa.

Hekima Inapojenga Nyumba

Akizungumza kuhusu jinsi mwanamke anavyoweza kuwa na uvutano juu ya familia yake, Mfalme Sulemani wa Israeli la kale anasema: “Mwanamke mwenye hekima kwelikweli amejenga nyumba yake, lakini aliye mpumbavu huibomoa kwa mikono yake mwenyewe.” (Methali 14:1) Mwanamke aliye na hekima huijengaje nyumba yake? Mwanamke mwenye hekima huheshimu mpango wa Mungu wa ukichwa. (1 Wakorintho 11:3) Haathiriwi na roho ya kujitegemea ambayo imeenea katika ulimwengu huu wa Shetani. (Waefeso 2:2) Yeye hujitiisha kwa mume wake na husema mambo mazuri kumhusu, na hivyo kufanya wengine wazidi kumheshimu mume wake. Mwanamke mwenye hekima hujishughulisha sana kuwafundisha watoto wake mambo ya kiroho na mambo mengine maishani. Yeye hufanya kazi kwa bidii kwa faida ya watu wa nyumbani mwake, na hivyo kufanya nyumba kuwa mahali penye kupendeza na pa starehe kwa ajili ya familia. Yeye husimamia mambo kwa busara na kutumia pesa kwa uangalifu. Kwa kweli, mwanamke mwenye hekima huchangia ufanisi na utulivu wa nyumba yake.

Mwanamke mpumbavu haheshimu mpango wa Mungu wa ukichwa. Yeye haogopi kusema mambo mabaya kumhusu mume wake. Badala ya kutumia vizuri pesa za familia zinazopatikana kwa shida, yeye huzitapanya. Yeye pia hupoteza wakati. Kwa sababu hiyo, nyumba yake si safi na nadhifu, nao watoto hutaabika kimwili na kiroho. Naam, mpumbavu hubomoa nyumba yake.

Ni nini huamua kama mtu ni mwenye hekima au ni mpumbavu? Methali 14:2 inasema: “Anayetembea katika unyoofu wake anamwogopa Yehova, lakini mtu mpotovu anamdharau Yeye katika njia zake.” Mtu mnyoofu humwogopa Mungu wa kweli, na “kumwogopa Yehova ni mwanzo wa hekima.” (Zaburi 111:10) Mtu mwenye hekima kwelikweli anajua kwamba ni wajibu wake ‘kumwogopa Mungu wa kweli na kushika amri zake.’ (Mhubiri 12:13) Kwa upande mwingine, mpumbavu hufuata njia ambayo haipatani na viwango vya Mungu vya uadilifu. Njia zake zimepotoka. Mtu kama huyo humdharau Mungu, naye husema moyoni mwake: “Hakuna Yehova.”—Zaburi 14:1.

Midomo Inapolindwa na Hekima

Tunaweza kusema nini kuhusu usemi wa mtu mwenye kumwogopa Yehova na wa yule anayemdharau? “Fimbo ya majivuno imo katika kinywa cha mpumbavu,” mfalme anasema, “lakini midomo ya wenye hekima itawalinda.” (Methali 14:3) Kwa kuwa anakosa hekima inayotoka juu, mtu mpumbavu si mwenye kufanya amani wala mwenye usawaziko. Hekima inayoongoza hatua zake ni ya kidunia, ya kinyama, ya roho waovu. Anasema kwa ugomvi na kiburi. Majivuno ya kinywa chake husababisha matatizo mengi kwake mwenyewe na kwa wengine.—Yakobo 3:13-18.

Midomo ya mtu mwenye hekima humlinda, na hivyo kumletea uradhi na furaha. Jinsi gani? Maandiko yanasema: “Kuna mtu anayesema bila kufikiri kama kwa upanga unaochoma, lakini ulimi wa mwenye hekima huponya.” (Methali 12:18) Mtu mwenye hekima hasemi bila kufikiri na maneno yake hayaumizi. Moyo wake hutafakari ili kujibu. (Methali 15:28) Maneno yake yaliyofikiriwa vizuri huponya, yaani, huwatia moyo wale waliovunjika moyo nayo huburudisha wale wanaokandamizwa. Badala ya kuwakasirisha wengine, midomo yake huendeleza amani na utulivu.

Hekima Inapoongoza Kazi za Kibinadamu

Kisha, Sulemani anataja methali fulani yenye kupendeza ambayo yaonekana inazungumzia uhitaji wa kufikiria faida na hasara za kufanya kazi fulani. Anasema: “Mahali pasipo na ng’ombe hori ni safi, lakini mazao ni mengi kwa sababu ya nguvu za ng’ombe-dume.”Methali 14:4.

Kikieleza kuhusu maana ya methali hiyo, kitabu kimoja cha kitaalamu kinasema: “Hori lililo tupu huonyesha kwamba hakuna ng’ombe wa kulisha na hivyo hakuna kazi ya kusafisha na kuwatunza wanyama hao, na gharama zitapungua. Lakini ‘faida’ hiyo inaonyeshwa kuwa bure katika m[stari] wa 4b: inaonekana kwamba asipotumia ng’ombe-dume, hakutakuwa na mavuno mengi.” Lazima mkulima aamue kwa hekima.

Je, si kweli kwamba kanuni ya methali hiyo inaweza kutumika pia wakati tunapofikiria kubadili kazi, kuchagua aina fulani ya nyumba, kununua gari, kupata mnyama wa nyumbani, na kadhalika? Mtu mwenye hekima atafikiria faida na hasara na kukadiria kama kwa kweli kazi hiyo ilihitaji jitihada na gharama hizo.

Shahidi Anapokuwa Mwenye Hekima

Sulemani anaendelea kusema: “Shahidi mwaminifu ni yule ambaye hatasema uwongo, lakini shahidi wa uwongo husema uwongo mtupu.” (Methali 14:5) Bila shaka, uwongo wa shahidi wa uwongo unaweza kutokeza madhara makubwa. Nabothi Myezreeli aliuawa kwa mawe kwa sababu watu wawili wasiofaa kitu walitoa ushahidi wa uwongo juu yake. (1 Wafalme 21:7-13) Na je, si kweli kwamba mashahidi wa uwongo walijitokeza dhidi ya Yesu, na hivyo kusababisha kifo chake? (Mathayo 26:59-61) Mashahidi wa uwongo pia walitoa ushahidi juu ya Stefano—mwanafunzi wa kwanza wa Yesu kuuawa kwa sababu ya imani yake.—Matendo 6:10, 11.

Huenda mtu mwongo asigunduliwe kwa muda fulani, lakini fikiria wakati wake ujao. Biblia inasema kwamba Yehova humchukia “shahidi wa uwongo anayesema uwongo.” (Methali 6:16-19) Mtu kama huyo atatupwa ndani ya lile ziwa linalowaka moto na kiberiti, yaani, kifo cha pili—pamoja na watenda-maovu kama vile wauaji, waasherati, na waabudu-sanamu.—Ufunuo 21:8.

Shahidi mwaminifu hasemi uwongo baada ya kuapa kusema ukweli. Ushahidi wake haupotoshwi na uwongo. Hata hivyo, hilo halimaanishi kwamba analazimika kutoa habari zote kwa wale ambao huenda wanataka kuwadhuru watu wa Yehova kwa njia yoyote ile. Wazee wa ukoo Abrahamu na Isaka hawakutoa habari zote kwa watu fulani ambao hawakumwabudu Yehova. (Mwanzo 12:10-19; 20:1-18; 26:1-10) Rahabu wa Yeriko aliwaelekeza vibaya watu waliotumwa na mfalme. (Yoshua 2:1-7) Yesu Kristo mwenyewe alijizuia kutoa habari zote ikiwa kufanya hivyo kungetokeza tu madhara. (Yohana 7:1-10) Alisema: “Msiwape mbwa kitu kitakatifu, wala msitupe lulu zenu mbele ya nguruwe.” Kwa nini? Ili kwamba ‘wasigeuke na kuwararua ninyi.’—Mathayo 7:6.

‘Ujuzi Unapokuwa Jambo Rahisi’

Je, kila mtu anaweza kupata hekima? Methali 14:6 inasema: “Mtu mwenye dhihaka ametafuta hekima, asiipate; lakini kwa mtu mwenye uelewaji, ujuzi ni jambo rahisi.” Huenda mtu mwenye dhihaka akatafuta hekima, lakini hawezi kuipata hekima ya kweli. Kwa kuwa mdhihaki hupuuza mambo ya Mungu kwa ukaidi, yeye hukosa kutimiza takwa la msingi la kuwa na hekima, yaani, ujuzi sahihi kumhusu Mungu wa kweli. Kiburi na ukaidi wake humzuia kujifunza kumhusu Mungu na hivyo kupata hekima. (Methali 11:2) Kwa nini basi ajishughulishe kutafuta hekima? Methali hiyo haitoi jibu, lakini labda yeye hufanya hivyo ili wengine wafikiri kwamba ana hekima.

“Ujuzi ni jambo rahisi” kwa mtu mwenye uelewaji. Uelewaji unafafanuliwa kuwa ‘uwezo wa akili wa kushika mambo,’ ‘uwezo wa kutambua jinsi habari ndogo-ndogo zinavyohusiana na habari yote kwa ujumla.’ Ni uwezo wa kuhusianisha sehemu mbalimbali za habari fulani na kuona jambo lote, si sehemu fulani tu. Methali hiyo inasema kwamba mtu aliye na uwezo huo hupata ujuzi kwa urahisi.

Kwa habari hiyo, fikiria jinsi wewe mwenyewe ulivyopata ujuzi wa kweli za Biblia. Ulipoanza kujifunza Biblia, yaelekea sana kwamba mafundisho ya msingi kuhusu Mungu, ahadi zake, na Mwana wake yalikuwa kati ya kweli za kwanza ulizojifunza. Mwanzoni, hukuona uhusiano uliopo kati ya mafundisho hayo. Lakini ulipoendelea kujifunza, ulianza kuelewa habari mbalimbali ulizosoma na kuona waziwazi jinsi zinavyohusiana na kusudi kuu la Yehova kuelekea wanadamu na dunia. Ulianza kuona jinsi kweli za Biblia zinavyopatana na akili na zinavyohusiana. Sasa ikawa rahisi kwako kujifunza na kukumbuka mambo mapya kwa kuwa ungeweza kuona jinsi yanayovyohusiana na habari yote.

Mfalme mwenye hekima anaonya kuhusu mahali ambapo ujuzi hauwezi kupatikana. Anasema: “Toka mbele ya mjinga, kwa maana hakika hutaweza kuona midomo ya ujuzi.” (Methali 14:7) Mtu mpumbavu hana ujuzi wa kweli. Midomo yake haina ujuzi. Tunashauriwa tutoke mbele ya mtu kama huyo, na ni jambo la hekima kukaa mbali naye. Yeyote “anayeshirikiana na wajinga atapatwa na mabaya.”—Methali 13:20.

Sulemani anaendelea kusema: “Hekima ya mwerevu ni kuelewa njia yake, lakini upumbavu wa wajinga ni udanganyifu.” (Methali 14:8) Mtu mwenye hekima hufikiria matendo yake. Yeye huchunguza uamuzi ulio mbele yake na kufikiria kwa uangalifu matokeo ya kila uamuzi. Yeye huchagua njia yake kwa hekima. Namna gani mtu mpumbavu? Yeye huchagua njia ya upambavu, huku akiamini kwamba anajua yale anayofanya na kwamba anafanya uchaguzi mzuri. Upumbavu wake humpotosha.

Hekima Inapoongoza Mahusiano

Mtu anayeongozwa na hekima ana mahusiano yenye amani na wengine. Mfalme wa Israeli anasema: “Wale wanaodhihaki hatia ni wapumbavu, lakini kuna makubaliano kati ya wanyoofu.” (Methali 14:9) Mtu mpumbavu hajihisi kuwa mwenye hatia. Ameharibu mahusiano nyumbani na penginepo kwa sababu ‘anadharau kuwa na kosa’ na kutafuta amani. (Zaire Swahili Bible) Mtu mnyoofu yuko tayari kusamehe makosa ya wengine. Yuko tayari kuomba msamaha na kufanya mapatano anapowakosea wengine. Kwa kuwa anafuatia amani, yeye huwa na uhusiano mzuri na wenye kudumu pamoja na wengine.—Waebrania 12:14.

Sulemani anaonyesha sababu nyingine inayoharibu mahusiano ya kibinadamu. Anasema: “Moyo unajua uchungu wa nafsi ya mtu mwenyewe, wala hapana mgeni atakayejiingiza katika kushangilia kwake.” (Methali 14:10) Je, sikuzote tunaweza kuwaeleza wengine hisia zetu za ndani kabisa iwe ni za huzuni au za shangwe na kuwaambia waziwazi jinsi tunavyohisi? Na je, sikuzote mtu mwingine anaweza kuelewa kabisa jinsi tunavyohisi? Jibu la maswali yote mawili ni la.

Kwa mfano, fikiria hisia za mtu anayetaka kujiua. Mara nyingi mtu anayehisi hivyo hawezi kumweleza waziwazi hisia hizo mshiriki fulani wa familia au rafiki. Na sikuzote wengine hawawezi kutambua kwamba marafiki wao wana hisia hizo. Hatuhitaji kuhisi kuwa wenye hatia ikiwa hatutambui ishara hizo na hivyo kukosa kutoa msaada unaohitajiwa. Pia methali hii inatufundisha kwamba ingawa ni jambo lenye kufariji kutafuta msaada kutoka kwa rafiki mwenye huruma ili kututegemeza kihisia, faraja ambayo wanadamu wanaweza kutoa ina mipaka. Huenda tukahitaji kumtegemea tu Yehova tunapovumilia matatizo fulani.

“Vitu Vyenye Thamani na Utajiri Vimo Nyumbani Mwake”

Mfalme wa Israeli anasema: “Nyumba ya watu waovu itaharibiwa, lakini hema la wanyoofu litasitawi.” (Methali 14:11) Huenda mtu mwovu akasitawi katika mfumo huu wa mambo na kuishi katika nyumba nzuri, lakini vitu hivyo vitamfaidije ikiwa yeye hatakuwapo tena? (Zaburi 37:10) Kwa upande mwingine, huenda makao ya mtu mnyoofu yakawa ya hali ya chini. Lakini “vitu vyenye thamani na utajiri vimo nyumbani mwake,” yasema Zaburi 112:3. Ni vitu gani hivyo?

Maneno na matendo yetu yanapoongozwa na hekima, tunakuwa na “utajiri na utukufu” ambao hupatikana kupitia hekima. (Methali 8:18) Utajiri na utukufu huo unatia ndani uhusiano wenye amani pamoja na Mungu na wanadamu wenzetu, afya nzuri na furaha, na utulivu wa kadiri fulani. Naam, “hema la wanyoofu” linaweza kusitawi hata sasa.

[Picha katika ukurasa wa 27]

Mwanamke mwenye hekima huijenga nyumba yake

[Picha katika ukurasa wa 28]

“Ulimi wa mwenye hekima huponya”