Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Hukumu ya Yehova Itakuja Juu ya Waovu

Hukumu ya Yehova Itakuja Juu ya Waovu

Hukumu ya Yehova Itakuja Juu ya Waovu

“Jitayarishe kukutana na Mungu wako.”—AMOSI 4:12.

1, 2. Kwa nini tunaweza kuwa na uhakika kwamba Mungu atakomesha uovu?

JE, Yehova atakomesha uovu na mateso katika dunia hii? Swali hilo linafaa zaidi sasa kuliko wakati mwingine wowote hasa tangu mwanzoni mwa karne hii ya 21. Inaonekana kwamba kila mahali, tunaona mwanadamu akimtendea mwanadamu mwenzake kwa ukatili. Lo! Tunatamani sana ulimwengu usio na jeuri, ugaidi, na ufisadi!

2 Jambo la kufurahisha ni kwamba tunaweza kuwa na uhakika kabisa kwamba Yehova atakomesha uovu. Sifa za Mungu mwenyewe zinatuhakikishia kwamba yeye atachukua hatua dhidi ya waovu. Yehova ni mwadilifu na mwenye haki. Katika Zaburi 33:5, Neno lake linatuambia hivi: “Anapenda uadilifu na haki.” Zaburi nyingine inasema: “Mtu yeyote anayependa jeuri nafsi [ya Yehova] hakika inamchukia.” (Zaburi 11:5) Bila shaka, Yehova, Mungu mwenye nguvu zote, ambaye anapenda uadilifu na haki, hatavumilia milele mambo ambayo anachukia.

3. Ni nini kitakachokaziwa tunapochunguza zaidi unabii wa Amosi?

3 Fikiria sababu nyingine inayotuhakikishia kwamba Yehova ataondoa uovu. Matendo yake ya zamani yanatuhakikishia jambo hilo. Mifano yenye kutokeza kuhusu jinsi Yehova alivyowachukulia hatua watu waovu inapatikana katika kitabu cha Biblia cha Amosi. Kuchunguza zaidi unabii wa Amosi kutakazia mambo matatu kuhusu hukumu ya Mungu. Kwanza, sikuzote Mungu huwahukumu tu watu wanaostahili kuhukumiwa. Pili, hukumu hiyo haiepukiki. Na tatu, Yehova hawezi kamwe kuwaharibu waadilifu pamoja na waovu, bali huwaonyesha rehema watu wanaotubu na wenye mwelekeo unaofaa.—Waroma 9:17-26.

Sikuzote Mungu Huwahukumu Wale Wanaostahili Kuhukumiwa

4. Yehova alimtuma Amosi wapi, na kwa kusudi gani?

4 Katika siku za Amosi, tayari taifa la Israeli lilikuwa limegawanyika na kuwa falme mbili, yaani, Yuda, ufalme wa kusini wa makabila mawili, na Israeli, ufalme wa kaskazini wa makabila kumi. Yehova alimpa Amosi utume wa kuwa nabii, na kumtuma kutoka mji wake wa Yuda aende Israeli. Akiwa huko, Mungu angemtumia kutangaza hukumu yake.

5. Amosi alianza kutoa unabii dhidi ya mataifa gani, na ni sababu gani moja iliyofanya yastahili hukumu kali ya Mungu?

5 Amosi hakuanza kazi yake kwa kutangaza hukumu ya Yehova dhidi ya ufalme wa kaskazini wa Israeli uliopotoka. Badala yake, alianza kwa kutangaza hukumu kali ya Mungu dhidi ya mataifa sita yaliyozunguka Israeli. Mataifa hayo yalikuwa Siria, Ufilisti, Tiro, Edomu, Amoni, na Moabu. Lakini je, kwa kweli, mataifa hayo yalistahili hukumu kali ya Mungu? Bila shaka. Sababu moja ni kwamba, mataifa hayo yalikuwa maadui shupavu wa watu wa Yehova.

6. Kwa nini Mungu angeleta msiba juu ya Siria, Ufilisti, na Tiro?

6 Kwa mfano, Yehova aliwashutumu Wasiria ‘kwa sababu ya kupura Gileadi.’ (Amosi 1:3) Wasiria walichukua eneo fulani la Gileadi—eneo la Israeli lililokuwa upande wa mashariki wa Mto Yordani—nao wakawaumiza vibaya watu wa Mungu waliokuwa huko. Namna gani Ufilisti na Tiro? Wafilisti walikuwa na hatia ya kuwachukua Waisraeli waliohamishwa, au waliotekwa, na kuwauza kwa Waedomu, na baadhi ya Waisraeli walidhibitiwa na wafanya-biashara ya utumwa wa Tiro. (Amosi 1:6, 9) Hebu wazia jambo hilo—kuwauza watu wa Mungu utumwani! Basi haishangazi kwamba Yehova angeleta msiba juu ya Siria, Ufilisti, na Tiro!

7. Mataifa ya Edomu, Amoni, na Moabu yalikuwa na uhusiano gani na Israeli, lakini yaliwatendeaje Waisraeli?

7 Mataifa ya Edomu, Amoni, Moabu, na Israeli yalikuwa na uhusiano fulani. Mataifa hayo yote matatu yalikuwa na uhusiano wa kiukoo na Waisraeli. Waedomu walitokana na Abrahamu kupitia Esau, ndugu pacha ya Yakobo. Kwa hiyo, kwa njia fulani walikuwa ndugu za Waisraeli. Waamoni na Wamoabu walikuwa wazao wa Loti, mpwa wa Abrahamu. Lakini, je, Edomu, Amoni, na Moabu waliwatendea Israeli, watu wao wa ukoo, kwa njia ya kindugu? Sivyo hata kidogo! Edomu lilitumia upanga bila huruma juu ya “ndugu yake mwenyewe,” nao Waamoni waliwatendea Waisraeli waliokuwa mateka kwa ukatili sana. (Amosi 1:11, 13) Ingawa Amosi hataji moja kwa moja kwamba Wamoabu waliwatendea vibaya watu wa Mungu, Wamoabu walipinga Israeli tangu zamani. Adhabu juu ya mataifa hayo matatu yenye ukoo mmoja ingekuwa kali. Yehova angeleta uharibifu mkali juu yao.

Hukumu ya Mungu Haiepukiki

8. Kwa nini hukumu ya Mungu dhidi ya mataifa sita yaliyozunguka Israeli haikuepukika?

8 Ni wazi kwamba, yale mataifa sita yaliyozungumziwa mapema katika unabii wa Amosi yalistahili hukumu kali ya Mungu. Isitoshe, hayangeweza kuepuka hukumu hiyo. Kuanzia Amosi sura ya 1, mstari wa 3, na kuendelea hadi sura ya 2, mstari wa 1, Yehova anasema hivi mara sita: “Sitaizuia.” Kupatana na neno lake, hakuacha kuyahukumu mataifa hayo. Kulingana na historia, ni wazi kwamba kila moja kati ya mataifa hayo lilipata msiba. Angalau manne kati yao—Ufilisti, Moabu, Amoni, na Edomu—mwishowe yalitokomea kabisa!

9. Wakaaji wa Yuda walistahili nini, na kwa nini?

9 Kisha Amosi anaelekeza unabii wake kwa taifa la saba, eneo lake la nyumbani la Yuda. Huenda watu waliomsikiliza Amosi katika ufalme wa kaskazini wa Israeli walishangaa kumsikia akitangaza hukumu juu ya ufalme wa Yuda. Kwa nini wakaaji wa Yuda walistahili hukumu kali? ‘Kwa sababu walikataa sheria ya Yehova,’ lasema andiko la Amosi 2:4. Yehova hakusahau jinsi walivyoipuuza Sheria yake kimakusudi. Kulingana na Amosi 2:5, alitabiri: “Nitapeleka moto ndani ya Yuda, nao utaiteketeza minara ya makao ya Yerusalemu.”

10. Kwa nini watu wa Yuda hawangeweza kuepuka ole?

10 Watu wa Yuda wasio waaminifu hawangeweza kuepuka ole ambao ungekuja. Kwa mara ya saba, Yehova alisema: “Sitaizuia.” (Amosi 2:4) Watu wa Yuda walipata adhabu iliyotabiriwa wakati Wababiloni walipoharibu nchi yao mwaka wa 607 K.W.K. Kwa mara nyingine tena tunaona kwamba waovu hawawezi kuepuka hukumu ya Mungu.

11-13. Amosi alitoa unabii hasa juu ya taifa gani, na kulikuwa na ukandamizaji wa aina gani huko?

11 Nabii Amosi alikuwa ametoka tu kutangaza hukumu ya Yehova juu ya mataifa saba. Hata hivyo, yeyote aliyewazia kwamba nabii huyo alikuwa amemaliza kutoa unabii wake, alikuwa amekosea sana. Amosi hakuwa amemaliza! Alikuwa amepewa utume hasa wa kutangaza ujumbe mkali wa hukumu juu ya ufalme wa kaskazini wa Israeli. Taifa la Israeli lilistahili hukumu kali ya Mungu kwa sababu taifa hilo lilikuwa limeharibika sana kiadili na kiroho.

12 Unabii wa Amosi ulifunua ukandamizaji ambao ulikuwa jambo la kawaida katika ufalme wa Israeli. Andiko la Amosi 2:6, 7 linasema hivi kuhusu jambo hilo: “Yehova amesema hivi, ‘Kwa sababu ya maasi matatu ya Israeli, na kwa sababu ya manne, sitaizuia, kwa sababu waliuza mtu mwadilifu kwa sababu tu ya fedha, na maskini kwa bei ya pea moja ya viatu. Wanatamani sana mavumbi ya dunia yaliyo kwenye vichwa vya watu wa hali ya chini; nao huipotosha njia ya watu wapole.’”

13 Waadilifu walikuwa wakiuzwa “kwa sababu tu ya fedha,” labda ikimaanisha kwamba waamuzi ambao walipokea rushwa ya fedha, walikuwa wakiwaadhibu wale wasio na hatia. Wakopeshaji walikuwa wakiwauza maskini utumwani kwa bei ya “pea moja ya viatu,” labda ili kulipa deni fulani dogo tu. Watu wakatili ‘walitamani sana,’ au walitafuta kwa bidii kuwashusha sana “watu wa hali ya chini” hivi kwamba maskini hao walitupa mavumbi juu ya vichwa vyao wenyewe, ambayo ni ishara ya mfadhaiko, maombolezo, au fedheha. Ufisadi ulikuwa umeenea sana hivi kwamba “watu wapole” hawakuwa na tumaini la kutendewa haki yoyote.

14. Ni nani waliokuwa wakitendewa vibaya katika ufalme wa Israeli wa makabila kumi?

14 Ona wale waliokuwa wakitendewa vibaya. Walikuwa waadilifu, maskini, watu wa hali ya chini, na wakaaji wapole wa nchi hiyo. Agano la Sheria ambalo Yehova alifanya kati yake na Israeli lilitaka watu wasio na ulinzi na maskini waonyeshwe huruma. Lakini, badala yake, hali za watu hao katika ufalme wa Israeli wa makabila kumi zilikuwa mbaya sana.

“Jitayarishe Kukutana na Mungu Wako”

15, 16. (a) Kwa nini Waisraeli walionywa: “Jitayarishe kukutana na Mungu wako”? (b) Andiko la Amosi 9:1, 2 linaonyeshaje kwamba waovu hawangeweza kuepuka kutekelezwa kwa hukumu ya Mungu? (c) Ni nini kilichoupata ufalme wa Israeli wa makabila kumi mwaka wa 740 K.W.K.?

15 Kwa kuwa kulikuwa na ukosefu mwingi wa adili na dhambi nyingine huko Israeli, nabii Amosi alikuwa na sababu nzuri ya kulionya hivi taifa hilo lenye kuasi: “Jitayarishe kukutana na Mungu wako.” (Amosi 4:12) Waisraeli waasi hawangeweza kuepuka hukumu ya Mungu iliyokuwa ikikaribia kwa sababu kwa mara ya nane, Yehova alitangaza: “Sitaizuia.” (Amosi 2:6) Mungu alisema hivi kuhusu waovu ambao huenda wangejaribu kujificha: “Hakuna yeyote kati yao anayekimbia atakayefanikiwa kukimbia, na hakuna yeyote kati yao anayeponyoka ambaye atafanikiwa kutoroka. Wakichimba chini kuingia katika Kaburi, toka humo mkono wangu mwenyewe utawachukua; nao wakienda juu mbinguni, toka huko nitawashusha chini.”—Amosi 9:1, 2.

16 Waovu hawangeweza kuepuka hukumu ya Yehova juu yao kwa kuchimba “chini kuingia katika Kaburi,” jambo linaloonyesha kwa njia ya mfano jitihada za kujificha katika sehemu za chini zaidi za dunia. Wala hawangeweza kuepuka hukumu ya Mungu kwa ‘kwenda juu mbinguni,’ yaani, kwa kujaribu kujificha katika milima mirefu. Onyo la Yehova lilikuwa wazi: Hakuna maficho ambayo yeye hawezi kuyafikia. Haki ya Mungu ilidai ufalme wa Israeli utozwe hesabu kwa ajili ya matendo yake maovu. Na wakati huo wa kutoza hesabu ulifika. Katika mwaka wa 740 K.W.K., karibu miaka 60 baada ya Amosi kuandika unabii wake, ufalme wa Israeli ulianguka mikononi mwa Waashuru waliovamia.

Hukumu ya Mungu Huchagua

17, 18. Amosi sura ya 9 hufunua nini kuhusu rehema ya Mungu?

17 Unabii wa Amosi umetusaidia kuona kwamba sikuzote wale wanaohukumiwa na Mungu wanastahili hukumu hiyo, nayo haiepukiki. Pia kitabu cha Amosi kinaonyesha kwamba hukumu ya Yehova huchagua. Mungu anaweza kuwapata waovu popote wanapojificha na kutekeleza hukumu yake juu yao. Anaweza pia kuwapata wale wanaotubu na wanyoofu—wale anaochagua kuwaonyesha rehema. Jambo hilo linakaziwa vizuri sana katika sura ya mwisho ya kitabu cha Amosi.

18 Kulingana na Amosi sura ya 9, mstari wa 8, Yehova alisema: “Sitaiangamiza kabisa nyumba ya Yakobo.” Kama inavyoonyeshwa katika mstari wa 13 hadi 15, Yehova aliahidi kwamba ‘angekusanya na kurudisha mateka’ wa watu wake. Watu hao wangeonyeshwa rehema na kupata usalama na ufanisi. Yehova alitabiri kwamba “anayelima atampita anayevuna.” Hebu wazia jambo hilo—mavuno yangekuwa mengi sana hivi kwamba majira ya kulima na kupanda yangefika kabla ya mavuno mengine kukusanywa ghalani!

19. Ni nini kilichotokea kwa mabaki wa Israeli na Yuda?

19 Tunaweza kusema kwamba hukumu ya Yehova juu ya waovu huko Yuda na Israeli ilikuwa yenye kuchagua kwa kuwa wale waliotubu na wenye mwelekeo unaofaa walionyeshwa rehema. Katika utimizo wa ahadi ya kurudishwa inayotajwa katika Amosi sura ya 9, mabaki wenye kutubu wa Israeli na Yuda walirudi kutoka utekwani Babiloni mwaka wa 537 K.W.K. Walipofika katika nchi yao waliyoipenda, walirudisha tena ibada safi. Pia walijenga upya nyumba zao na kupanda mizabibu na bustani chini ya hali zenye usalama.

Hukumu Kali ya Yehova Itakuja!

20. Tunapaswa kuwa na uhakika gani tunapochunguza ujumbe wa hukumu uliotangazwa na Amosi?

20 Tunapochunguza ujumbe wa hukumu ya Mungu ambao Amosi alitangaza, tunapaswa kuwa na hakika kwamba Yehova atakomesha uovu uliopo siku zetu. Kwa nini tunaweza kuamini hivyo? Kwanza, mifano hiyo ya zamani kuhusu jinsi Yehova alivyowatendea waovu inaonyesha jinsi atakavyofanya katika siku zetu. Pili, kutekelezwa kwa hukumu ya Mungu dhidi ya ufalme ulioasi wa Israeli kunatupa uhakikisho kwamba Mungu ataleta uharibifu juu ya dini zinazojiita za Kikristo ambazo ni sehemu inayolaumika zaidi ya “Babiloni Mkubwa,” milki ya ulimwengu ya dini ya uwongo.—Ufunuo 18:2.

21. Kwa nini dini zinazojiita za Kikristo zinastahili hukumu kali ya Mungu?

21 Bila shaka, dini zinazojiita za Kikristo zinastahili hukumu kali ya Mungu. Ni wazi kwamba kuna upotovu mwingi wa kidini na kiadili katika dini hizo. Dini zinazojiita za Kikristo pamoja na sehemu nyingine ya ulimwengu wa Shetani zinastahili hukumu ya Yehova. Hukumu hiyo pia haiwezi kuepukika, kwa kuwa wakati itakapotekelezwa, maneno haya ya Amosi sura ya 9, mstari wa 1, yatatimia: “Hakuna yeyote kati yao anayekimbia atakayefanikiwa kukimbia, na hakuna yeyote kati yao anayeponyoka ambaye atafanikiwa kutoroka.” Naam, hata waovu wajifiche wapi, Yehova atawapata.

22. Ni mambo gani kuhusu hukumu ya Mungu yanayofafanuliwa kwenye 2 Wathesalonike 1:6-8?

22 Sikuzote hukumu ya Mungu ni yenye kustahili, haiepukiki, nayo huchagua. Tunaweza kuona hilo katika maneno haya ya mtume Paulo: “Ni jambo la uadilifu kwa upande wa Mungu kuwalipa dhiki wale wanaowafanyia ninyi dhiki, lakini, kwenu ninyi mnaopata dhiki, kitulizo pamoja nasi wakati wa ufunuo wa Bwana Yesu kutoka mbinguni pamoja na malaika zake wenye nguvu katika mwali wa moto, anapoleta kisasi juu ya wale wasiomjua Mungu na wale wasiotii habari njema juu ya Bwana wetu Yesu.” (2 Wathesalonike 1:6-8) “Ni jambo la uadilifu kwa upande wa Mungu” kuwalipa wale wanaostahili hukumu kali kwa sababu ya kuwaletea dhiki watiwa-mafuta wake. Hukumu hiyo haitaepukika, kwa kuwa waovu hawataokoka ‘ufunuo wa Yesu pamoja na malaika zake wenye nguvu katika mwali wa moto.’ Pia hukumu ya Mungu itakuwa yenye kuchagua kwa kuwa Yesu ataleta kisasi “juu ya wale wasiomjua Mungu na wale wasiotii habari njema.” Na kutekelezwa kwa hukumu ya Mungu kutawafariji wale wanaopatwa na dhiki.

Tumaini kwa Wanyoofu

23. Tunaweza kupata tumaini na faraja gani katika kitabu cha Amosi?

23 Unabii wa Amosi una ujumbe wa faraja na tumaini kwa watu wenye mwelekeo unaofaa. Kama ilivyotabiriwa katika kitabu cha Amosi, Yehova hakuwaangamiza kabisa watu wake wa nyakati za kale. Mwishowe, aliwakusanya mateka wa Israeli na Yuda, akawarudisha katika nchi yao na kuwapa usalama na ufanisi mwingi. Hilo linamaanisha nini siku zetu? Jambo hilo hufanya tuwe na hakika kwamba wakati hukumu ya Mungu itakapotekelezwa, Yehova atawapata waovu popote pale walipojificha, naye atawapata wale wanaostahili rehema zake, popote pale wanapoishi katika dunia hii.

24. Watumishi wa Yehova wa siku hizi wamebarikiwa katika njia zipi?

24 Tunapongojea Yehova atekeleze hukumu juu ya waovu, tunajionea nini tukiwa watumishi wake waaminifu? Yehova anatubariki kwa ufanisi mwingi wa kiroho. Tuna ibada ambayo haina uwongo na upotovu unaotokana na mafundisho ya uwongo ya dini zinazojiita za Kikristo. Pia, Yehova ametupa chakula kingi cha kiroho. Hata hivyo, kumbuka kwamba baraka hizi nyingi kutoka kwa Yehova huandamana na madaraka makubwa. Mungu anatazamia tuwaonye wengine kuhusu hukumu inayokuja. Tunatamani kufanya yote tuwezayo ili kuwatafuta wale walio na “mwelekeo unaofaa kwa ajili ya uzima wa milele.” (Matendo 13:48) Naam, tunatamani kuwasaidia watu wengi iwezekanavyo wanufaike na ufanisi wa kiroho tunaofurahia sasa. Nasi tunataka waokoke Mungu atakapotekeleza hukumu yake inayokaribia juu ya waovu. Bila shaka, ili kunufaika na baraka hizo, ni lazima tuwe na hali ya moyo inayofaa. Kama tutakavyoona katika makala inayofuata, jambo hilo pia limekaziwa katika unabii wa Amosi.

Ungejibuje?

• Unabii wa Amosi huonyeshaje kwamba sikuzote hukumu kali ya Yehova ni yenye kustahili?

• Amosi anatoa uthibitisho gani ili kuonyesha kwamba hukumu ya Mungu haiwezi kuepukika?

• Kitabu cha Amosi huonyeshaje kwamba hukumu ya Mungu ni yenye kuchagua?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 16, 17]

Ufalme wa Israeli haukuepuka hukumu ya Mungu

[Picha katika ukurasa wa 18]

Mwaka wa 537 K.W.K., mabaki wa Israeli na Yuda walirudi kutoka utekwani Babiloni