Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Roho waovu watakuwa wapi wakati wa Utawala wa Kristo wa Miaka Elfu?

Biblia haijibu waziwazi swali hilo. Hata hivyo, tunaweza kufikia mkataa wenye kupatana na akili kuhusu mahali ambapo roho waovu watakuwa wakati wa Utawala wa Kristo wa Miaka Elfu.

Akionyesha kimbele yale yatakayotukia mwanzoni na mwishoni mwa Miaka Elfu, mtume Yohana anasema: “Nikamwona malaika akishuka kutoka mbinguni mwenye ufunguo wa abiso na mnyororo mkubwa mkononi mwake. Naye akamkamata yule joka mkubwa, yule nyoka wa zamani, ambaye ni Ibilisi na Shetani, na kumfunga kwa miaka elfu. Naye akamtupa ndani ya abiso na kuifunga na kuitia muhuri juu yake, ili asipotoshe mataifa tena mpaka ile miaka elfu itakapokwisha. Baada ya mambo hayo yeye atafunguliwa kwa muda kidogo.” (Ufunuo 20:1-3) Mistari hiyo inazungumzia tu kutupwa kwa Shetani ndani ya abiso na baadaye kufunguliwa kwake kwa muda kidogo. Ingawa roho waovu hawatajwi, linaonekana kuwa jambo linalopatana na akili kufikia mkataa kwamba wakati malaika aliye na ufunguo wa abiso—Yesu Kristo aliyetukuzwa—atakapomkamata na kumtupa Ibilisi ndani ya abiso, atafanya vivyo hivyo kwa roho waovu pia.—Ufunuo 9:11.

Alipowekwa kuwa Mfalme mbinguni mwaka wa 1914, Yesu Kristo alichukua hatua ambayo ilikuwa na matokeo makubwa juu ya Shetani na roho waovu pia. Andiko la Ufunuo 12:7-9 linasema: “Vita vikatokea ghafula mbinguni: Mikaeli na malaika zake wakapigana na yule joka mkubwa, naye joka mkubwa na malaika zake [roho waovu] wakapigana lakini hakushinda, wala mahali hapakupatikana mbinguni kwa ajili yao tena. Kwa hiyo yule joka mkubwa akatupwa chini, yule nyoka wa zamani, yeye anayeitwa Ibilisi na Shetani, anayeipotosha dunia nzima inayokaliwa; akatupwa chini duniani, na malaika zake wakatupwa chini pamoja naye.” Tangu wakati huo, Shetani na roho wake waovu wamezuiliwa kwenye ujirani wa dunia. Ni jambo linalopatana na akili kuamini kwamba Yesu Kristo atakapozuia zaidi utendaji wa Shetani ili kuondoa uvutano wake mwovu duniani, atafanya vivyo hivyo kwa roho waovu pia.

Fikiria pia unabii wa kwanza kabisa wa Biblia. Tunasoma: “Nami [Mungu] nitaweka uadui kati yako [Shetani] na yule mwanamke [tengenezo la Yehova la kimbingu] na kati ya uzao wako [wa Shetani] na uzao wake [Yesu Kristo]. Yeye atakuponda kichwa nawe utamtia jeraha kwenye kisigino.” (Mwanzo 3:15) Kupondwa kwa nyoka kichwani kunatia ndani kutupwa kwa Shetani ndani ya abiso wakati wa Utawala wa Kristo wa Miaka Elfu. Pia unabii huo unaonyesha kwamba kuna uadui kati ya Yule anayeponda na uzao wa Shetani. Uzao huo, au tengenezo, unatia ndani sehemu isiyoonekana inayofanyizwa na malaika waovu, au roho waovu. Hivyo, ni jambo linalopatana na akili kukata kauli kwamba Yesu anapomtupa Shetani ndani ya abiso, anawafunga pia na kuwatupa roho waovu ndani ya abiso. Kwa kuwa roho waovu waliogopa sana kutupwa ndani ya abiso, hilo linaonyesha kwamba wanajua kuwa kuzuiliwa huko kunakaribia.—Luka 8:31.

Hata hivyo, je, inawezekana kwamba Ufunuo 20:1-3 haiwataji roho waovu kwa sababu wanaharibiwa kwenye Har-magedoni pamoja na sehemu inayoonekana ya uzao wa Shetani? Biblia inaonyesha kwamba huenda jambo hilo lisiwe kweli. Inasema hivi kuhusu yale yatakayompata Shetani mwishowe: “Ibilisi aliyekuwa akiwapotosha alitupwa ndani ya lile ziwa la moto na kiberiti, ambamo wote wawili, yule mnyama-mwitu na yule nabii wa uwongo, tayari walikuwa; nao watateswa mchana na usiku milele na milele.” (Ufunuo 20:10) Mnyama-mwitu na nabii wa uwongo ni serikali za dunia nazo ni sehemu inayoonekana ya tengenezo la Shetani. (Ufunuo 13:1, 2, 11-14; 16:13, 14) Zinaharibiwa kwenye Har–Magedoni, Ufalme wa Mungu unapoponda na kukomesha falme zote za ulimwengu. (Danieli 2:44) Biblia inataja “moto wa milele aliotayarishiwa Ibilisi na malaika zake.” (Mathayo 25:41) Shetani na roho wake waovu watatupwa ndani ya ‘ziwa lilelile la moto na kiberiti’ kama mnyama-mwitu na nabii wa uwongo katika maana ya kwamba wao pia wataharibiwa milele. Ikiwa sehemu isiyoonekana ya uzao wa Shetani, yaani, roho waovu ambao ni wenye nguvu zaidi kuliko sehemu inayoonekana ya uzao wa Shetani ingeharibiwa kwenye Har–Magedoni, bila shaka roho waovu wangetajwa kuwa tayari wamo katika lile ziwa la mfano pamoja na mnyama-mwitu na nabii wa uwongo. Kutotajwa kwao kwenye Ufunuo 20:10 kunaonyesha kwamba roho waovu hawataharibiwa kwenye Har-magedoni.

Kwa kuwa roho waovu hawatajwi waziwazi kuwa wametupwa ndani ya abiso, hawasemekani kihususa kuwa wamefunguliwa kutoka huko. Hata hivyo, watapatwa na jambo lilelile litakalompata Ibilisi. Baada ya kufunguliwa pamoja na Ibilisi na kushirikiana naye wakati wa lile jaribu la mwisho la wanadamu mwishoni mwa ile miaka elfu, roho waovu pia watatupwa ndani ya lile ziwa la moto na hivyo kupatwa na uharibifu wa milele.—Ufunuo 20:7-9.

Hivyo, ingawa andiko la Ufunuo 20:1-3 linazungumzia tu kukamatwa kwa Shetani na kutupwa ndani ya abiso la kutotenda, ni jambo linalopatana na akili kufikia mkataa kwamba malaika zake pia watafungwa na kutupwa ndani ya abiso. Wala Shetani wala majeshi yake ya roho waovu hawataruhusiwa kuzuia kutimizwa kwa kusudi la Mungu la kugeuza dunia kuwa paradiso na kuwafanya wanadamu wawe wakamilifu wakati wa Utawala wa Kristo wa Miaka Elfu.