Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Sema Neno la Mungu kwa Ujasiri

Sema Neno la Mungu kwa Ujasiri

Sema Neno la Mungu kwa Ujasiri

“Nenda, watolee unabii watu wangu.”—AMOSI 7:15.

1, 2. Amosi alikuwa nani, nayo Biblia husema nini kumhusu?

SHAHIDI mmoja wa Yehova alipokuwa akihubiri, alikutana na kuhani fulani. Kuhani huyo akapaaza sauti na kusema: ‘Koma kuhubiri! Ondoka hapa!’ Shahidi huyo alifanya nini? Je, alitii amri hiyo, au aliendelea kusema neno la Mungu kwa ujasiri? Unaweza kupata jibu kwa swali hilo kwa sababu shahidi huyo aliandika mambo yaliyompata katika kitabu chenye jina lake—kitabu cha Biblia cha Amosi. Hata hivyo, kabla hatujaendelea kuzungumza mengi kuhusu jinsi alivyokutana na kuhani huyo, acheni tupate habari fulani kuhusu malezi ya Amosi.

2 Amosi alikuwa nani? Aliishi wapi? Aliishi wakati gani? Tunapata majibu ya maswali hayo katika andiko la Amosi 1:1, ambapo tunasoma: “Maneno ya Amosi, aliyekuwa kati ya wafugaji wa kondoo kutoka Tekoa, . . . katika siku za Uzia mfalme wa Yuda, na katika siku za Yeroboamu mwana wa Yoashi, mfalme wa Israeli.” Amosi alikuwa mkaaji wa Yuda. Alizaliwa katika mji wa Tekoa uliokuwa kilometa 16 kusini ya Yerusalemu. Aliishi mwishoni mwa karne ya tisa K.W.K., Mfalme Uzia alipokuwa akitawala huko Yuda na Yeroboamu wa Pili alipokuwa mfalme wa yale makabila kumi ya Israeli. Amosi alikuwa mfugaji wa kondoo. Andiko la Amosi 7:14 linasema kwamba Amosi hakuwa “mchungaji” tu bali alikuwa pia “mminyaji wa tini za mikuyu.” Kwa hiyo, alifanya kazi ya kuvuna katika kipindi fulani cha mwaka. Aliminya, au kutoboa tini za mikuyu. Kazi hiyo ilifanywa ili tini ziive haraka. Ilikuwa kazi yenye kuchosha sana.

“Nenda, Watolee Unabii”

3. Kujifunza kumhusu Amosi kunatusaidiaje tunapohisi kwamba hatustahili kuhubiri?

3 Amosi alisema hivi waziwazi: “Mimi sikuwa nabii, wala sikuwa mwana wa nabii.” (Amosi 7:14) Amosi hakuzaliwa akiwa mwana wa nabii wala hakuzoezwa kuwa nabii. Hata hivyo, kati ya watu wote wa Yuda, Yehova alimchagua Amosi ili afanye kazi Yake. Wakati huo, Mungu hakuchagua mfalme mwenye nguvu, kuhani mwenye elimu, wala mkuu mwenye utajiri. Jambo hilo linatufunza somo linalotutia moyo. Huenda tusiwe na cheo kikubwa wala elimu ya juu. Lakini je, hilo lapaswa kufanya tuhisi kwamba hatustahili kulihubiri neno la Mungu? Sivyo hata kidogo! Yehova anaweza kutuzoeza tustahili kuhubiri ujumbe wake—hata katika maeneo magumu. Kwa kuwa Yehova alimzoeza Amosi, kila mtu aliye na hamu ya kusema neno la Mungu kwa ujasiri anaweza kujifunza jambo fulani kutokana na mfano wa nabii huyo aliyekuwa jasiri.

4. Kwa nini ilikuwa vigumu kwa Amosi kutoa unabii huko Israeli?

4 Yehova alimwamuru hivi Amosi: “Nenda, watolee unabii watu wangu Israeli.” (Amosi 7:15) Mgawo huo ulikuwa mgumu. Wakati huo, ufalme wa Israeli wa makabila kumi ulikuwa na amani, usalama, na ufanisi wa kimwili. Wengi walikuwa na ‘nyumba za wakati wa baridi kali’ na pia ‘nyumba za wakati wa kiangazi,’ ambazo hazikujengwa kwa matofali ya kawaida tu, bali kwa “mawe yaliyochongwa” ya bei ghali. Wengine walikuwa na vyombo vya kifahari vilivyopambwa kwa pembe za tembo, nao walikunywa divai iliyozalishwa katika “mashamba ya mizabibu yenye kupendeza.” (Amosi 3:15; 5:11) Kwa sababu hiyo, watu wengi hawakujali chochote. Kwa kweli, huenda ikawa eneo ambalo Amosi aligawiwa lilifanana sana na maeneo ambayo baadhi yetu tunahubiri.

5. Waisraeli fulani walikuwa wakifanya mambo gani yasiyo ya haki?

5 Hakukuwa na ubaya wowote kwa Waisraeli kuwa na mali. Hata hivyo, Waisraeli fulani walijirundikia utajiri kupitia njia zisizo za haki. Matajiri walikuwa ‘wakiwapunja watu wa hali ya chini’ na ‘kuwaponda walio maskini.’ (Amosi 4:1) Wafanya-biashara mashuhuri, waamuzi, na makuhani walishirikiana kuwapunja maskini. Sasa acheni turudi katika siku za Amosi na kuona mambo ambayo watu hao walikuwa wakifanya.

Sheria ya Mungu Yavunjwa

6. Wafanya-biashara Waisraeli waliwapunja wengine jinsi gani?

6 Kwanza tunaenda sokoni. Huko, wafanya-biashara wasio wanyoofu walifanya ‘efa kuwa ndogo’ na “kuifanya shekeli kuwa kubwa,” na hata wakauza “takataka tupu” kama ngano. (Amosi 8:5, 6) Wafanya-biashara hao waliwapunja wanunuzi kwa kuwauzia bidhaa duni, kwa kiasi kisicho kamili, na kwa bei ya juu mno. Baada ya wafanya-biashara hao kuwapunja na kuwaacha wakiwa maskini kabisa, watu hao walilazimika kujiuza wawe watumwa. Halafu, wafanya-biashara hao waliwanunua “kwa bei ya pea moja ya viatu.” (Amosi 8:6) Hebu wazia! Wafanya-biashara hao wenye pupa waliwaona Waisraeli wenzao kuwa wasio na thamani, waliwaona kama viatu tu! Hilo liliwashushia sana heshima watu maskini na kuivunja Sheria ya Mungu. Na bado, wafanya-biashara haohao waliishika “sabato.” (Amosi 8:5) Naam, walikuwa watu wa dini kijuujuu tu.

7. Ni nini kilichowawezesha wafanya-biashara Waisraeli wavunje Sheria ya Mungu?

7 Kwa nini wafanya-biashara hao hawakuadhibiwa kwa kuvunja Sheria ya Mungu, ambayo inaamuru: “Mpende mwenzako kama wewe mwenyewe”? (Mambo ya Walawi 19:18) Wafanya-biashara hao walifaulu kwa sababu wale waliopaswa kuhakikisha kwamba Sheria inafuatwa, yaani, waamuzi walishirikiana pamoja nao katika uhalifu. Kwenye lango la jiji, ambapo kesi zilisikilizwa, waamuzi ‘walichukua pesa za hongo, na kuwafukuza maskini langoni.’ Badala ya kuwalinda maskini, waamuzi hao walipewa rushwa ili wawasaliti. (Amosi 5:10, 12) Kwa hiyo, waamuzi pia waliipuuza Sheria ya Mungu.

8. Makuhani waovu walijifanya hawaoni jambo gani?

8 Wakati huohuo, makuhani wa Israeli walikuwa wakifanya nini? Ili kupata jibu, tunapaswa kuelekeza fikira zetu mahali pengine. Ona dhambi ambazo makuhani waliruhusu “katika nyumba ya miungu yao”! Kupitia Amosi, Mungu alisema: “Mwanamume na baba yake wanamwendea msichana yuleyule, kwa kusudi la kulitia unajisi jina langu takatifu.” (Amosi 2:7, 8) Hebu wazia jambo hilo! Baba Mwisraeli na mwana wake walifanya uasherati na kahaba yuleyule wa hekaluni. Na makuhani hao waovu walijifanya hawaoni ukosefu huo wa adili!—Mambo ya Walawi 19:29; Kumbukumbu la Torati 5:18; 23:17.

9, 10. Waisraeli walikuwa na hatia ya kuvunja Sheria gani za Mungu, na hali hiyo inafananaje na siku zetu?

9 Akitaja mwenendo mwingine wenye dhambi, Yehova alisema hivi: “Nao hujinyoosha kando ya kila madhabahu juu ya mavazi yaliyotwaliwa kama rehani, na divai ya wale ambao wametozwa wao huinywa katika nyumba ya miungu yao.” (Amosi 2:8) Naam, makuhani na watu kwa ujumla walipuuza sheria iliyoandikwa katika Kutoka 22:26, 27, iliyosema kwamba nguo ambayo imechukuliwa rehani ilipaswa kurudishwa kabla ya usiku kuingia. Badala yake, waliitumia kama blanketi la kulalia huku wakila na kunywa kwenye karamu za miungu ya uwongo. Nao walitumia fedha walizowatoza maskini kununua divai ili kuinywa katika sherehe za dini za uwongo. Lo! Jinsi walivyopotoka kutoka katika njia ya ibada safi!

10 Waisraeli walikuwa wakivunja bila haya zile amri mbili kuu za Sheria, yaani, kumpenda Yehova na kuwapenda wanadamu wenzao. Kwa hiyo, Mungu alimtuma Amosi awashutumu kwa ukosefu wao wa uaminifu. Leo, mataifa ya ulimwengu, kutia ndani yale yanayojiita ya Kikristo, huonyesha hali iliyopotoka kama Israeli la kale. Ingawa watu fulani wanaendelea kuwa na mali, wengine wengi wameachwa wakiwa maskini kabisa na kuumizwa kihisia moyo na vitendo viovu vya viongozi wasio wanyoofu wa mashirika makubwa ya kibiashara, siasa, na dini za uwongo. Lakini Yehova anawahangaikia wale wanaoteseka na ambao wanachochewa kumtafuta. Kwa hiyo, amewapa watumishi wake wa siku hizi kazi kama ile ya Amosi, yaani, kuhubiri neno Lake kwa ujasiri.

11. Tunaweza kujifunza nini kutokana na mfano wa Amosi?

11 Kwa sababu kazi yetu inafanana na ile ya Amosi, tutanufaika sana kwa kuchunguza mfano wake. Kwa kweli, Amosi anatuonyesha (1) ujumbe tunaopaswa kuhubiri, (2) jinsi tunavyopaswa kuhubiri, na (3) kwa nini wapinzani hawawezi kukomesha kazi yetu ya kuhubiri. Acheni tuyachunguze mambo hayo, moja baada ya lingine.

Jinsi Tunavyoweza Kumwiga Amosi

12, 13. Yehova alionyeshaje kwamba alichukizwa na Waisraeli, nao waliitikiaje?

12 Tukiwa Mashahidi wa Yehova, sisi hukazia fikira huduma yetu ya Kikristo ya kuhubiri kuhusu Ufalme na kufanya wanafunzi. (Mathayo 28:19, 20; Marko 13:10) Hata hivyo, sisi pia huhubiri kuhusu maonyo ya Mungu, kama vile Amosi alivyotangaza kwamba Yehova angeleta hukumu kali juu ya waovu. Kwa mfano, andiko la Amosi 4:6-11 linaonyesha tena na tena jinsi Yehova alivyochukizwa na Waisraeli. Aliwapa watu “upungufu wa mkate,” ‘akazuia mvua isiwanyeshee,’ akawapiga kwa “kuunguza na kwa ukungu,” na kutuma kati yao “tauni.” Je, mambo hayo yalifanya Waisraeli watubu? “Hamkurudi kwangu,” Mungu akasema. Kwa kweli, Waisraeli walimkataa Yehova tena na tena.

13 Yehova aliwaadhibu Waisraeli hao wasiotubu. Hata hivyo, kwanza walipokea onyo la kinabii. Kupatana na hilo, Mungu alitangaza hivi: “Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova hatafanya lolote isipokuwa awe amewafunulia watumishi wake manabii jambo lake la siri.” (Amosi 3:7) Mungu alimfunulia Noa kwamba Gharika ingekuja naye akamwagiza atoe onyo. Vivyo hivyo, Yehova alimwambia Amosi atoe onyo la mwisho. Kwa kusikitisha, Waisraeli walipuuza ujumbe huo kutoka kwa Mungu, nao hawakuchukua hatua inayofaa.

14. Siku zetu zinafananaje na wakati wa Amosi?

14 Bila shaka utakubali kwamba katika siku zetu kuna mambo yanayofanana sana na ya wakati wa Amosi. Yesu Kristo alitabiri kwamba kungekuwa na misiba mingi wakati wa mwisho. Pia, alitabiri kuhusu kazi ya kuhubiri ambayo ingefanywa ulimwenguni pote. (Mathayo 24:3-14) Hata hivyo, kama ilivyokuwa katika siku za Amosi, watu wengi leo wanapuuza ujumbe wa Ufalme na pia ishara ya nyakati. Watu hao watapatwa na kile kilichowapata Waisraeli ambao hawakutubu. Yehova aliwaonya hivi: ‘Jitayarisheni kukutana na Mungu wenu.’ (Amosi 4:12) Waisraeli walikutana na Mungu kwa kupatwa na hukumu yake kali wakati jeshi la Ashuru lilipowashinda. Leo, ulimwengu huu usiomwogopa Mungu ‘utakutana na Mungu’ kwenye Har–Magedoni. (Ufunuo 16:14, 16) Hata hivyo, maadamu subira ya Yehova ingalipo, tunawahimiza hivi watu wengi iwezekanavyo: ‘Mtafuteni Yehova, mwendelee kuishi.’—Amosi 5:6.

Kukabiliana na Upinzani Kama Alivyofanya Amosi

15-17. (a) Amazia alikuwa nani, naye aliitikiaje matangazo ya Amosi? (b) Amazia alitoa madai gani dhidi ya Amosi?

15 Tunaweza kumwiga Amosi si katika yale tunayohubiri tu bali pia jinsi tunavyohubiri. Jambo hilo linakaziwa katika sura ya 7, ambapo tunaelezwa kuhusu kuhani aliyetajwa mwanzoni mwa mazungumzo yetu. Alikuwa “Amazia kuhani wa Betheli.” (Amosi 7:10) Jiji la Betheli lilikuwa kituo cha dini ya uasi-imani ya Israeli, ambayo ilihusisha ibada ya ndama. Kwa hiyo, Amazia alikuwa kuhani wa dini rasmi ya taifa hilo. Yeye alitendaje aliposikia matangazo ya ujasiri ya Amosi?

16 Amazia alimwambia hivi Amosi: “Ewe mwonaji, nenda, kimbia uende zako kwenye nchi ya Yuda, ukale mkate huko, na huko unaweza kutoa unabii. Lakini usiendelee tena kutoa unabii katika Betheli, kwa maana ni mahali patakatifu pa mfalme, napo ni nyumba ya ufalme.” (Amosi 7:12, 13) Ni kana kwamba Amazia alisema: ‘Nenda zako nyumbani! Sisi tuna dini yetu.’ Alijaribu pia kuichochea serikali ipige marufuku kazi ya Amosi, akimwambia hivi Mfalme Yeroboamu wa Pili: “Amosi amepanga hila juu yako ndani ya nyumba ya Israeli.” (Amosi 7:10) Naam, Amazia alimshtaki Amosi kwamba alikuwa ametenda kosa la uhaini! Alimwambia mfalme hivi: “Amosi amesema hivi, ‘Kwa upanga Yeroboamu atakufa; naye Israeli bila shaka ataenda uhamishoni kutoka katika nchi yake mwenyewe.’”—Amosi 7:11.

17 Katika mstari huo mmoja, Amazia alisema mambo matatu yenye kupotosha. Alisema: “Amosi amesema hivi.” Lakini Amosi hakudai kamwe kwamba yeye ndiye chanzo cha unabii huo. Badala yake, sikuzote alikuwa akisema: “Yehova amesema.” (Amosi 1:3) Amosi pia alishtakiwa kwamba alisema: “Kwa upanga Yeroboamu atakufa.” Hata hivyo, kama inavyoonyeshwa katika Amosi 7:9, Amosi alikuwa ametoa unabii huu: “Nami [Yehova] nitasimama kuipiga nyumba ya Yeroboamu kwa upanga.” Mungu alikuwa amehukumu “nyumba” ya Yeroboamu, au uzao wake. Isitoshe, Amazia alidai kwamba Amosi alikuwa amesema: “Israeli bila shaka ataenda uhamishoni.” Lakini pia Amosi alikuwa ametabiri kwamba Mwisraeli yeyote ambaye angemrudia Mungu angebarikiwa. Basi ni wazi kwamba Amazia alitumia taarifa zenye kupotosha ili kazi ya kuhubiri ya Amosi ipigwe marufuku na serikali.

18. Kuna ufanani gani kati ya mbinu alizotumia Amazia na zile zinazotumiwa na viongozi wa kidini leo?

18 Je, umeona ufanani kati ya mbinu alizotumia Amazia na zile ambazo wapinzani wa watu wa Yehova hutumia leo? Kama vile Amazia alivyojaribu kumnyamazisha Amosi, ndivyo makasisi, na maaskofu wa siku zetu wanavyojaribu kuzuia kazi ya kuhubiri ya watumishi wa Yehova. Amazia alimshtaki Amosi kwa uwongo kwamba ametenda kosa la uhaini. Vivyo hivyo, leo makasisi fulani huwashtaki Mashahidi wa Yehova kwa uwongo kwamba wao ni tisho kwa usalama wa taifa. Na kama vile Amazia alivyomwendea mfalme ili apate msaada wa kupigana na Amosi, ndivyo viongozi wa kidini wanavyowaendea rafiki zao wa kisiasa ili wapate msaada wa kuwatesa Mashahidi wa Yehova.

Wapinzani Hawawezi Kukomesha Kazi Yetu ya Kuhubiri

19, 20. Amosi aliitikiaje upinzani wa Amazia?

19 Amosi aliitikiaje upinzani wa Amazia? Kwanza, Amosi alimwuliza kuhani huyo hivi: “Je, unasema, ‘Usitoe unabii juu ya Israeli’?” Kisha, bila kusita-sita nabii wa Mungu mwenye ujasiri alisema maneno ambayo Amazia hakutaka kusikia. (Amosi 7:16, 17) Amosi hakutishika. Huo ni mfano bora kama nini kwetu! Sisi tutamtii Mungu wetu na kusema neno lake, hata katika nchi ambako akina Amazia wa siku hizi wanachochea mateso makali. Kama Amosi, sisi tunaendelea kutangaza: “Yehova amesema hivi.” Nao wapinzani hawataweza kamwe kukomesha kazi yetu ya kuhubiri, kwa kuwa “mkono wa Yehova” u pamoja nasi.—Matendo 11:19-21.

20 Amazia alipaswa kujua kwamba vitisho vyake havingefanikiwa. Tayari Amosi alikuwa ameeleza ni kwa nini hakuna mtu yeyote duniani ambaye angeweza kumzuia asiseme—na hilo ndilo jambo la tatu tunalotaka kuzungumzia. Kulingana na Amosi 3:3-8, Amosi alitumia mfululizo wa maswali na mifano ili kuonyesha kwamba hakuna jambo linalotendeka bila sababu. Kisha, akaonyesha matumizi haya: “Kuna simba ambaye amenguruma! Ni nani hataogopa? Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova amesema! Ni nani ambaye hatatoa unabii?” Yaani, Amosi aliwaambia wasikilizaji wake: ‘Kama vile mnavyoogopa msikiapo simba akinguruma, ndivyo na mimi ninavyolihubiri neno la Mungu nisikiapo utume wa Yehova wa kwenda kuhubiri.’ Kumwogopa au kumheshimu sana Yehova, kulimchochea Amosi aseme kwa ujasiri.

21. Sisi huitikiaje amri ya Mungu ya kuhubiri habari njema?

21 Sisi pia tunausikia utume wa Yehova wa kuhubiri. Sisi huitikiaje? Kama Amosi na wafuasi wa mapema wa Yesu, kwa msaada wa Yehova, tunasema neno lake kwa ujasiri. (Matendo 4:23-31) Hatutanyamazishwa na mateso yanayochochewa na wapinzani wala kutojali kwa watu tunaowahubiria. Huku wakionyesha bidii kama ile ya Amosi, Mashahidi wa Yehova ulimwenguni pote wanachochewa kuendelea kutangaza habari njema kwa ujasiri. Tuna daraka la kuwaonya watu kuhusu hukumu ya Yehova inayokuja. Hukumu hiyo inahusisha nini? Swali hilo litajibiwa katika makala inayofuata.

Ungejibuje?

• Amosi alitimiza kazi aliyopewa na Mungu chini ya hali gani?

• Kama Amosi, tunapaswa kuhubiri nini?

• Tunapaswa kuhubiri tukiwa na mtazamo gani?

• Kwa nini wapinzani hawawezi kukomesha kazi yetu ya kutoa ushahidi?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 10]

Mungu alimchagua Amosi, mminyaji wa tini za mikuyu kufanya kazi Yake

[Picha katika ukurasa wa 13]

Kama Amosi, je, unatangaza ujumbe wa Yehova kwa ujasiri?