Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Watu Wanaweza Kuishi Muda Mrefu Kadiri Gani?

Watu Wanaweza Kuishi Muda Mrefu Kadiri Gani?

Watu Wanaweza Kuishi Muda Mrefu Kadiri Gani?

MACHI 3, 1513, mvumbuzi Mhispania Juan Ponce de León alifunga safari muhimu. Alisafiri kwa meli kutoka Puerto Riko akitumaini kufika kisiwa cha Bimini. Kulingana na hekaya, alikuwa akitafuta chemchemi ya kimuujiza—Chemchemi ya Ujana. Lakini safari yake ilimfikisha jimbo ambalo sasa ni Florida, Marekani. Bila shaka, hakuipata ile chemchemi ya ujana kwa kuwa hakuna chemchemi kama hiyo.

Leo, wanadamu kwa ujumla hawaishi zaidi ya miaka 70 au 80. Ingawa Biblia hutaja watu walioishi miaka mingi, kitabu 2002 Guinness Book of World Records husema kwamba mwanadamu aliyepata kuishi muda mrefu zaidi aliishi miaka 122 na siku 164. (Mwanzo 5:3-32) Hata hivyo, John Harris, mtaalamu wa elimu-maadili ya kibiolojia alisema hivi: “Utafiti mpya unaonyesha kwamba huenda ikawezekana kuwa na jamii ambayo haitazeeka au hata kufa.” Wataalamu wengi wa karne ya 21 huzungumza juu ya “hali ya kutoweza kufa kabisa,” “uhai usio na kikomo kufikia mwaka wa 2099,” “uwezekano wa chembe za mwili kuendelea kuongezeka bila kukoma,” na mambo kama hayo.

Katika kitabu chake The Dream of Eternal Life, Mark Benecke anasema hivi: “Karibu chembe zote za mwili hufanyizwa upya mara kadhaa maishani. . . . Baada ya miaka saba hivi, sisi huwa na mwili mpya kihalisi.” Hata hivyo, jambo hilo haliendelei milele kwa sababu chembe huacha kuongezeka baada ya kujigawanya mara ambazo zimeratibiwa. Benecke anasema kwamba kama chembe hazingeacha kujigawanya, “mwili wa binadamu ungeendelea kujifanyiza upya kwa muda mrefu sana—hata milele.”

Fikiria pia uwezo mkubwa ajabu wa ubongo wa mwanadamu. Sisi hutumia sehemu ndogo sana ya ubongo wetu wakati wa maisha yetu mafupi. Kulingana na kitabu Encyclopædia Britannica, ubongo wa mwanadamu “una uwezo mkubwa sana hivi kwamba mwanadamu hawezi kuutumia wote wakati wa maisha yake.” (Chapa ya 1976, Buku la 12, ukurasa wa 998) Kitabu How the Brain Learns, kilichoandikwa na David A. Sousa chasema hivi: “Kwa kweli, ubongo una uwezo usio na kikomo wa kuhifadhi habari.”—Ukurasa wa 78, Chapa ya Pili, haki ya kunakili 2001.

Kwa nini watafiti wameshindwa kupata sababu za kiasili zinazosababisha kifo? Na kwa nini ubongo wa mwanadamu una uwezo mkubwa hivyo? Je, inawezekana kwamba tuliumbwa ili tuendelee kujifunza milele? Kwa nini tunaweza kuwazia kuishi milele?

Biblia inasema: “Tena wakati usio na kipimo [Mungu] ameuweka ndani ya moyo wao, ili mwanadamu asiweze kugundua kazi ambazo Mungu wa kweli amefanya tangu mwanzo mpaka mwisho.” (Mhubiri 3:11) Maneno hayo yanaonyesha kwamba Mungu aliweka ndani yetu wazo la kuishi milele ili daima tuweze kujifunza mambo fulani kumhusu yeye na kazi zake. Ikiwa tungeishi kwa mabilioni ya miaka—naam, milele—tungeweza kujifunza daima mambo mengi sana kuhusu maajabu ya kazi za Mungu za uumbaji.

Maneno ya Yesu Kristo pia yanaonyesha kwamba wanadamu wanaweza kuishi milele. Alisema: “Uzima wa milele ndio huu, waendelee kupata ujuzi juu yako wewe, Mungu wa pekee wa kweli, na juu ya yule uliyemtuma, Yesu Kristo.” (Yohana 17:3) Namna gani wewe? Je, unataka kuishi milele?

[Picha katika ukurasa wa 3]

Juan Ponce de León alitafuta chemchemi ya ujana

[Hisani]

Ponce de León: Harper’s Encyclopædia of United States History