Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Dumisha Maoni Yaliyosawazika Kuhusu Kutumia Kileo

Dumisha Maoni Yaliyosawazika Kuhusu Kutumia Kileo

Dumisha Maoni Yaliyosawazika Kuhusu Kutumia Kileo

“Divai ni mdhihaki, kileo husababisha msukosuko, na kila mtu anayepotezwa nacho hana hekima.”—METHALI 20:1.

1. Mtunga-zaburi alionyeshaje shukrani zake kwa baadhi ya zawadi nzuri kutoka kwa Yehova?

MWANAFUNZI Yakobo aliandika hivi: “Kila zawadi njema na kila tuzo kamilifu hutoka juu, kwa maana hushuka kutoka kwa Baba wa mianga ya mbinguni.” (Yakobo 1:17) Akichochewa na shukrani kwa zawadi nyingi nzuri kutoka kwa Mungu, mtunga-zaburi aliimba hivi: “Anafanya majani mabichi yachipuke kwa ajili ya wanyama, na mimea ili itumikie wanadamu, ili chakula kitokezwe duniani, na divai ambayo hufanya moyo wa mwanadamu anayeweza kufa ushangilie, kuufanya uso ung’ae kwa mafuta, na mkate unaotegemeza moyo wa mwanadamu anayeweza kufa.” (Zaburi 104:14, 15) Divai na vileo vingine ni zawadi nzuri kutoka kwa Mungu, kama vile mimea, mkate, na mafuta. Tunapaswa kuzitumiaje?

2. Tutazungumzia maswali gani kuhusu kutumia kileo?

2 Zawadi inayofurahisha huwa nzuri inapotumiwa tu kwa njia inayofaa. Kwa mfano, asali “ni njema” lakini “si vizuri kula asali nyingi mno.” (Methali 24:13; 25:27) Ingawa huenda ikafaa kunywa “divai kidogo,” kutumia kileo vibaya ni tatizo kubwa. (1 Timotheo 5:23) Biblia huonya hivi: “Divai ni mdhihaki, kileo husababisha msukosuko, na kila mtu anayepotezwa nacho hana hekima.” (Methali 20:1) Hata hivyo, mtu anawezaje kupotezwa na kileo? * Ni kiwango gani cha divai kinachopita kiasi? Ni maoni gani yaliyosawazika kuhusiana na jambo hilo?

‘Mtu Anawezaje Kupotezwa’ na Kileo?

3, 4. (a) Ni nini kinachoonyesha kwamba Biblia hushutumu kunywa kileo mpaka mtu alewe? (b) Ni nini baadhi ya dalili za ulevi?

3 Katika Israeli la kale, mwana aliyekuwa mlafi na mlevi asiyetubu alipaswa kuuawa kwa kupigwa mawe. (Kumbukumbu la Torati 21:18-21) Mtume Paulo aliwaonya Wakristo hivi: “Mwache kuchangamana katika ushirika pamoja na mtu yeyote anayeitwa ndugu ambaye ni mwasherati au mtu mwenye pupa au mwabudu-sanamu au mtukanaji au mlevi au mnyang’anyi, hata msile chakula pamoja na mtu wa namna hiyo.” Ni wazi kwamba Maandiko yanashutumu kunywa kileo mpaka mtu alewe.—1 Wakorintho 5:11; 6:9, 10.

4 Ikieleza dalili za ulevi, Biblia husema: “Usiitazame divai inapotoa rangi nyekundu, inapochemka katika kikombe, inaposhuka taratibu. Mwisho wake inauma kama nyoka, nayo hutoa sumu kama nyoka. Macho yako mwenyewe yataona mambo mageni, nao moyo wako mwenyewe utasema mambo yaliyopotoka.” (Methali 23:31-33) Kunywa kupita kiasi huuma kama nyoka mwenye sumu na kusababisha ugonjwa, kuvurugika kiakili na hata kupoteza fahamu. Mlevi anaweza kuona “mambo mageni” katika maana ya kwamba anaweza kusikia sauti zisizokuwepo au kuota ndoto za mchana. Huenda pia akakosa kujizuia kusema na kufanya mambo yaliyopotoka ambayo kwa kawaida hangefanya.

5. Kunywa kileo kupita kiasi ni hatari jinsi gani?

5 Namna gani ikiwa mtu anakunywa kileo lakini anakuwa mwangalifu asinywe kupita kiasi ili wengine wasione kwamba amelewa? Watu fulani hawaonyeshi sana dalili za kulewa hata baada ya kunywa sana. Hata hivyo, kufikiri kwamba zoea hilo halina madhara ni kujidanganya. (Yeremia 17:9) Hatua kwa hatua, huenda mtu akawa mzoefu wa kileo na kuwa ‘mtumwa wa divai nyingi sana.’ (Tito 2:3) Mwandishi Caroline Knapp anasema hivi kuhusu jinsi mtu huwa mzoefu wa kileo: “Mtu huwa mzoefu polepole, hatua kwa hatua, na kisiri-siri.” Kwa kweli, kutumia kileo kupita kiasi ni mtego usioonekana.

6. Kwa nini mtu anapaswa kujiepusha kula na kunywa kileo kupita kiasi?

6 Pia fikiria onyo hili la Yesu: “Jiangalieni ninyi wenyewe kwamba mioyo yenu isilemewe kamwe na kula kupita kiasi na kunywa sana na mahangaiko ya maisha, na kwa ghafula siku hiyo iwe juu yenu mara moja kama mtego. Kwa maana itakuja juu ya wale wote wanaokaa juu ya uso wa dunia yote.” (Luka 21:34, 35) Si lazima mtu anywe mpaka alewe kabla ya kuanza kusinzia na kuwa mvivu—kimwili na kiroho pia. Itakuwaje siku ya Yehova ikimpata katika hali hiyo?

Mambo Yanayoweza Kusababishwa na Kutumia Kileo Vibaya

7. Kwa nini kutumia kileo vibaya hakupatani na agizo linalotajwa kwenye 2 Wakorintho 7:1?

7 Kutumia kileo kupita kiasi kunaweza kusababisha hatari nyingi za kimwili na za kiroho pia. Kutumia kileo vibaya hutokeza magonjwa kama vile ule unaoua chembe za ini, uvimbe wa ini, na magonjwa mengine yanayoathiri mfumo wa neva kama vile kitetemeshi cha ulevi. Kutumia kileo vibaya kwa muda mrefu kunaweza pia kusababisha kansa, kisukari, na magonjwa fulani ya moyo na tumbo. Bila shaka, kutumia kileo vibaya hakupatani na agizo hili la Kimaandiko: “Acheni tujisafishe wenyewe kila unajisi wa mwili na roho, tukiukamilisha utakatifu katika kumwogopa Mungu.”—2 Wakorintho 7:1.

8. Kulingana na Methali 23:20, 21, ni nini kinachoweza kutokea kwa kutumia kileo vibaya?

8 Pia kutumia kileo vibaya kunaweza kufanya mtu atumie pesa vibaya au hata apoteze kazi. Mfalme Sulemani wa Israeli la kale alionya: “Usiwe kati ya watu wanaokunywa divai mno, kati ya watu wanaokula nyama kwa ulafi.” Kwa nini? Alieleza hivi: “Kwa maana mlevi na mlafi watakuwa maskini, na kusinzia kutamvika mtu nguo zilizopasuka.”—Methali 23:20, 21.

9. Kwa nini ni jambo la hekima kuepuka kunywa kileo ikiwa utaendesha gari?

9 Kikitaja hatari nyingine, kichapo The Encyclopedia of Alcoholism kinasema: “Uchunguzi umeonyesha kwamba kileo hufanya ustadi wa kuendesha gari upungue, kutia ndani kutenda kwa haraka, viungo kufanya kazi kwa upatano, kuwa macho, uwezo wa kuona vizuri na kuamua.” Kuendesha gari ukiwa mlevi kunaweza kusababisha msiba. Nchini Marekani peke yake, makumi ya maelfu ya watu hufa na mamia ya maelfu hujeruhiwa katika aksidenti zinazosababishwa na madereva walevi. Vijana ambao hawana uzoefu wa kuendesha gari na pia wa kunywa kileo ndio huathiriwa hasa na hatari hiyo. Je, mtu anaweza kuendesha gari akiwa amekunywa sana na wakati huohuo adai kwamba anaheshimu uhai kuwa zawadi kutoka kwa Yehova Mungu? (Zaburi 36:9) Kwa kuwa uhai ni mtakatifu, ingefaa mtu asinywe kileo chochote ikiwa ataendesha gari.

10. Kileo kinaweza kuathirije akili yetu, na kwa nini jambo hilo ni hatari?

10 Kutumia kileo kupita kiasi hudhuru watu kimwili na kiroho pia. Biblia inasema: “Divai na divai tamu ndivyo vinavyoondoa kusudi jema.” (Hosea 4:11) Kileo huathiri akili. “Mtu anapokunywa,” chasema kichapo kimoja cha Taasisi ya Kitaifa ya Dawa za Kulevya ya Marekani, “kileo hufyonzwa kupitia mfumo wa kumeng’enya chakula hadi kwenye damu na kufika haraka kwenye ubongo. Kinaanza kufanya sehemu za ubongo ambazo hudhibiti fikira na hisia zifanye kazi polepole. Mtu hushindwa kujidhibiti.” Katika hali hiyo, ni rahisi ‘tupotee,’ tujiendeshe kwa njia isiyofaa na watu wa jinsia tofauti, na kutumbukia katika vishawishi vingi.—Methali 20:1.

11, 12. Kutumia kileo kupita kiasi kunaweza kusababisha madhara gani ya kiroho?

11 Isitoshe, Biblia inaagiza hivi: “Kama mnakula au mnakunywa au mnafanya jambo lingine lolote, fanyeni mambo yote kwa utukufu wa Mungu.” (1 Wakorintho 10:31) Je, kunywa kileo kingi humtukuza Mungu? Bila shaka, Mkristo hangependa kujulikana kuwa mnywaji kupindukia. Kuwa mlevi kupindukia hakumtukuzi Yehova, bali huliletea jina lake suto.

12 Namna gani ikiwa Mkristo anakunywa kupita kiasi na hivyo kumkwaza mwamini mwenzake, au mwanafunzi mpya? (Waroma 14:21) Yesu alionya: “Yeyote anayemkwaza mmoja wa hawa wadogo wanaoniamini, ingekuwa afadhali afungiwe shingoni jiwe la kusagia kama lile ambalo huzungushwa na punda na azamishwe katika bahari kuu.” (Mathayo 18:6) Mtu anayekunywa kupita kiasi anaweza pia kupoteza mapendeleo katika kutaniko. (1 Timotheo 3:1-3, 8) Kutumia kileo vibaya kunaweza pia kusababisha mgogoro katika familia.

Tunawezaje Kuepuka Hatari Mbalimbali?

13. Ni jambo gani lililo muhimu katika kuepuka kutumia kileo vibaya?

13 Siri moja ya kuepuka hatari za kutumia kileo vibaya ni kujua tofauti kati ya kunywa kwa kiasi na kunywa kupita kiasi bali si tofauti kati ya kunywa kupita kiasi na kulewa. Ni nani anayeweza kukuamulia kiasi cha kileo kinachokufaa na kiwango kinachopita kiasi? Kwa kuwa kuna mambo mengi yanayohusika, hakuna sheria inayotaja kiwango kinachopita kiasi. Kila mtu anapaswa kujiwekea mipaka na kutovuka mipaka hiyo. Ni nini kitakachokusaidia kuamua kiwango kinachokufaa? Je, kuna kanuni inayoweza kutumika kama mwongozo?

14. Ni kanuni gani itakayokuongoza kujiwekea mipaka kati ya kiasi cha kileo kinachokufaa na kiwango kinachopita kiasi?

14 Biblia inasema: “Linda hekima inayotumika na uwezo wa kufikiri, nazo zitakuwa uzima kwa nafsi yako na kitu chenye kuvutia shingoni pako.” (Methali 3:21, 22) Kwa hiyo, kanuni inayopaswa kutuongoza ni hii: Kiasi chochote cha kileo ambacho kinapunguza uwezo wako wa kufanya maamuzi na wa kufikiri ni kingi mno. Lakini unapaswa kujichunguza kwa unyoofu na kutambua mipaka yako!

15. Ni wakati gani huenda likawa jambo la hekima kutokunywa hata kidogo?

15 Katika hali fulani, huenda likawa jambo la hekima kutokunywa hata kidogo. Kwa sababu kileo kinaweza kudhuru kijusi, huenda mwanamke mja-mzito akaepuka kabisa kunywa kileo. Je, halingekuwa jambo la fadhili kuepuka kunywa mbele ya mtu ambaye amekuwa na tatizo la kutumia kileo vibaya au mtu ambaye dhamiri yake haimruhusu kunywa? Yehova aliwaamuru hivi wale waliokuwa wakitumika kama makuhani kwenye maskani: ‘Msinywe divai wala kileo . . . mnapoingia ndani ya hema la mkutano, msije mkafa.’ (Mambo ya Walawi 10:8, 9) Kwa hiyo, epuka kunywa kileo kabla tu ya kuhudhuria mikutano ya Kikristo, kushiriki katika huduma, na unapotimiza madaraka mengine ya kiroho. Isitoshe, katika nchi ambazo zinakataza matumizi ya vileo au zinaruhusu matumizi ya vileo kwa watu ambao wamepitisha umri fulani, Wakristo wanapaswa kutii sheria za nchi.—Waroma 13:1.

16. Unapaswa kuamuaje jambo la kufanya unapopewa kileo?

16 Unapopewa kileo, swali la kwanza unalopaswa kujiuliza ni: ‘Je, ninapaswa kunywa?’ Ukiamua kunywa, kumbuka mipaka uliyojiwekea na usiivuke. Usishawishiwe na ukarimu wa mkaribishaji wako. Jihadhari na sherehe ambazo vileo hutolewa kwa wingi, kama vile kwenye karamu za harusi. Katika nchi nyingi, watoto wanaruhusiwa na sheria kunywa vileo. Ni daraka la wazazi kuwafundisha watoto wao kuhusu kutumia kileo na kusimamia jinsi wanavyokitumia.—Methali 22:6.

Unaweza Kudhibiti Tatizo Hilo

17. Ni nini kinachoweza kukusaidia kutambua kama una tatizo la kutumia kileo vibaya?

17 Je, una tatizo la kutumia vibaya divai na vileo? Uwe na hakika kwamba ikiwa unafanya dhambi ya siri ya kutumia kileo vibaya, punde si punde itakuathiri. Kwa hiyo, jichunguze kwa unyoofu. Jiulize maswali haya ya kujichunguza: ‘Je, ninakunywa mara nyingi kuliko nilivyozoea? Je, nimeanza kutumia vileo vikali? Je, mimi hunywa vileo ili kuepuka wasiwasi, mkazo, au matatizo? Je, mshiriki fulani wa familia au rafiki ametaja tatizo langu la kunywa kupita kiasi? Je, kutumia kileo kupita kiasi kumesababisha matatizo katika familia yangu? Je, ninaona ni vigumu kumaliza juma, mwezi, au miezi kadhaa bila kunywa kileo? Je, mimi huwaficha wengine kiasi cha divai au kileo ninachotumia?’ Namna gani ikiwa unajibu ndiyo kwa baadhi ya maswali hayo? Usiwe kama ‘mtu anayeutazama uso wake wa asili katika kioo na kusahau mara moja yeye ni mtu wa namna gani.’ (Yakobo 1:22-24) Chukua hatua za kurekebisha tatizo hilo. Unaweza kufanya nini?

18, 19. Unawezaje kuacha kutumia kileo kupita kiasi?

18 Mtume Paulo aliwahimiza hivi Wakristo: “Msiwe mkilewa divai, ambayo ina upotovu ndani yake, bali endeleeni kujazwa na roho.” (Waefeso 5:18) Amua kiwango ambacho kimepita kiasi na ujiwekee mipaka inayofaa. Azimia kutopita mipaka hiyo; jizuie. (Wagalatia 5:22, 23) Je, una marafiki ambao hukukaza unywe kupita kiasi? Jihadhari. Biblia inasema: “Anayetembea na watu wenye hekima atakuwa na hekima, lakini anayeshirikiana na wajinga atapatwa na mabaya.”—Methali 13:20.

19 Ikiwa unatumia kileo ili kuepuka tatizo fulani, kabili tatizo hilo moja kwa moja. Matatizo yanaweza kutatuliwa kwa kutumia shauri kutoka kwa Neno la Mungu. (Zaburi 119:105) Usisite kuomba msaada kutoka kwa mzee Mkristo unayemtumaini. Tumia kikamili maandalizi ambayo Yehova ametoa ili kujenga hali yako ya kiroho. Imarisha uhusiano wako na Mungu. Sali kwake kwa ukawaida hasa kuhusu udhaifu wako. Msihi Mungu ‘asafishe figo zako na moyo wako.’ (Zaburi 26:2) Kama ilivyozungumziwa katika makala iliyotangulia, jitahidi kadiri uwezavyo kutembea katika njia ya utimilifu.

20. Unaweza kuchukua hatua gani ili kutatua tatizo lenye kuendelea la kutumia kileo kupita kiasi?

20 Namna gani tatizo la kunywa kupita kiasi likiendelea licha ya jitihada zako? Basi unapaswa kufuata shauri hili la Yesu: “Mkono wako ukikufanya ukwazike, ukate; ni afadhali uingie katika uzima ukiwa kilema kuliko kwenda ukiwa na mikono miwili na kuingia katika Gehena.” (Marko 9:43) Suluhisho ni: Usinywe hata kidogo. Hivyo ndivyo mwanamke mmoja ambaye tutamwita Irene alivyoazimia kufanya. Yeye anasema hivi: “Baada ya kuepuka kunywa kileo kwa miaka miwili na nusu hivi, nilianza kujiambia kwamba pengine sitaathiriwa nikinywa kidogo tu ili kuona kama ninaweza kujizuia. Lakini mara tu ninapohisi hivyo, mimi husali kwa Yehova mara moja kuhusu jambo hilo. Nimeazimia kutokunywa kileo hadi mfumo mpya au labda sitakunywa hata wakati huo.” Kuepuka kunywa kileo kabisa si jambo kubwa likilinganishwa na uzima katika ulimwengu mpya wa Mungu wenye uadilifu.—2 Petro 3:13.

“Kimbieni kwa Namna ya Kwamba Mweze Kupata Tuzo”

21, 22. Ni nini kinachoweza kutuzuia tusifike kwenye mstari wa kumalizia katika mbio ya uzima, na tunaweza kuepukaje kizuizi hicho?

21 Akilinganisha maisha ya Mkristo na mbio au shindano, mtume Paulo alisema: “Je, hamjui kwamba wakimbiaji katika mbio wote hukimbia, lakini ni mmoja tu anayepokea tuzo? Kimbieni kwa namna ya kwamba mweze kupata tuzo. Zaidi ya hayo, kila mtu anayeshiriki katika shindano hujizuia katika mambo yote. Basi wao, bila shaka, hushindana ili wapate taji linaloharibika, lakini sisi ili tupate taji lisiloharibika. Kwa hiyo, jinsi ninavyokimbia si bila uhakika; jinsi ninavyoelekeza ngumi zangu ni ili nisiwe nikipiga hewa; lakini naupigapiga mwili wangu na kuuongoza kama mtumwa, ili, baada ya mimi kuwahubiria wengine, mimi mwenyewe nisikataliwe kwa njia fulani.”—1 Wakorintho 9:24-27.

22 Tuzo hupewa wale tu wanaofanikiwa kumaliza shindano. Kutumia kileo vibaya kunaweza kutuzuia tusifike kwenye mstari wa kumalizia katika mbio ya uzima. Lazima tujizuie. Ili tukimbie kwa uhakika, tunapaswa kujiepusha kutumia “divai kupita kiasi.” (1 Petro 4:3) Badala yake, tunahitaji kujizuia katika mambo yote. Kuhusiana na kunywa vileo, ni jambo la hekima “kukataa kabisa kutomwogopa Mungu na tamaa za kilimwengu na tuishi kwa utimamu wa akili na uadilifu na ujitoaji-kimungu.”—Tito 2:12.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 2 Katika makala hii, “kileo” kinarejelea bia, divai, na pombe nyingine kali.

Je, Unakumbuka?

• Kutumia kileo vibaya kunahusisha nini?

• Ni madhara gani hutokana na kutumia kileo vibaya?

• Unawezaje kuepuka hatari za kutumia kileo vibaya?

• Mtu anawezaje kukabiliana na tatizo la kutumia kileo vibaya?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 19]

Divai “hufanya moyo wa mwanadamu anayeweza kufa ushangilie”

[Picha katika ukurasa wa 20]

Tunapaswa kujua mipaka yetu na kutoivuka

[Picha katika ukurasa wa 21]

Jiwekee mpaka mapema wa kutotumia kileo kupita kiasi

[Picha katika ukurasa wa 22]

Sali kwa Yehova kwa ukawaida kuhusu udhaifu wako

[Picha katika ukurasa wa 23]

Wazazi wana daraka la kufundisha watoto wao kuhusu kutumia kileo