Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kutumaini Utunzaji Wenye Upendo wa Yehova

Kutumaini Utunzaji Wenye Upendo wa Yehova

Simulizi la Maisha

Kutumaini Utunzaji Wenye Upendo wa Yehova

LIMESIMULIWA NA ANNA DENZ TURPIN

“Unapenda sana kuuliza maswali!” mama yangu akasema huku akitabasamu. Nilipokuwa msichana, niliwauliza wazazi wangu maswali mengi. Lakini Mama na Baba hawakunikemea kwa sababu ya udadisi wangu wa kitoto. Badala yake, walinifundisha kufikiri na kufanya maamuzi yanayotegemea dhamiri iliyozoezwa na Biblia. Mafundisho hayo yalikuwa yenye thamani sana baadaye. Siku moja, nilipokuwa na umri wa miaka 14, Wanazi walinitenganisha na wazazi wangu wapendwa, nami sikuwaona tena.

BABA yangu, Oskar Denz, na mama yangu, Anna Maria, waliishi Lörrach huko Ujerumani karibu na mpaka wa Uswisi. Walipokuwa vijana, walijihusisha sana na siasa nao walijulikana sana na kuheshimiwa katika jumuiya. Lakini katika mwaka wa 1922, muda mfupi tu baada ya kuoana, wazazi wangu walibadili maoni yao kuhusu siasa na miradi yao maishani. Mama alianza kujifunza Biblia na Wanafunzi wa Biblia, kama Mashahidi wa Yehova walivyoitwa wakati huo, naye alifurahi sana kujifunza kwamba Ufalme wa Mungu utaleta amani duniani. Punde si punde, Baba alijiunga naye katika funzo, nao wakaanza kuhudhuria mikutano ya Wanafunzi wa Biblia. Baba alimpa Mama kitabu cha kujifunza Biblia, The Harp of God, kama zawadi ya Krismasi mwaka huo. Nilizaliwa Machi 25, 1923 na nikawa mtoto wa pekee.

Ningali nakumbuka mambo tuliyofanya pamoja tukiwa familia kama vile kutembea kwenye msitu mtulivu wa Black Forest wakati wa kiangazi na Mama akinifundisha kazi za nyumbani. Bado ninaweza kukumbuka mama akiwa amesimama jikoni akinifundisha kupika. Wazazi wangu walinifundisha jambo muhimu zaidi, yaani, kumpenda na kumtumaini Yehova Mungu.

Kutaniko letu lilikuwa na wahubiri wa Ufalme 40 hivi wenye bidii. Wazazi wangu walikuwa na ustadi wa kutumia kila nafasi kuzungumza kuhusu Ufalme. Kwa sababu ya utendaji wao wa zamani katika jumuiya, waliweza kuwafikia watu kwa urahisi nao watu waliwasikiliza. Nilipokuwa na umri wa miaka saba, mimi pia nilitaka kuhubiri nyumba kwa nyumba. Mara yangu ya kwanza kuhubiri, yule niliyeandamana naye alinipa vichapo fulani, kisha akielekeza kidole kwenye nyumba moja, akaniambia, “Nenda, uone kama wangependa vichapo hivi.” Mwaka wa 1931, tulihudhuria kusanyiko la Wanafunzi wa Biblia huko Basel, Uswisi, ambako wazazi wangu walibatizwa.

Hali ya Vurugu Yageuka Kuwa Ukandamizaji

Wakati huo, Ujerumani ilikuwa katika hali ya vurugu kubwa, na vikundi mbalimbali vya kisiasa vilipigana kikatili barabarani. Usiku mmoja, niliamshwa na mayowe kutoka katika nyumba ya jirani. Vijana wawili walimuua kaka yao kwa uma wa kukusanyia nyasi kwa sababu hawakukubaliana na maoni yake ya kisiasa. Pia uadui dhidi ya Wayahudi uliongezeka na kuonekana wazi. Shuleni, msichana mmoja alisimama peke yake pembeni kwa sababu tu alikuwa Myahudi. Nilimsikitikia sana bila kujua kwamba muda si muda, mimi pia ningejikuta katika hali hiyo ya kutengwa.

Januari 30, 1933, Adolf Hitler alitawazwa kuwa waziri mkuu wa Ujerumani. Majengo mawili hivi kutoka mahali tulipoishi, tuliwaona Wanazi wakiweka kwa furaha bendera ya swastika juu ya makao makuu ya halmashauri ya jiji. Huko shuleni, mwalimu wetu mwenye shauku alitufunza kusema salamu ya Hitler, “Heil Hitler!” Alasiri hiyo nilimweleza Baba kuhusu jambo hilo. Akiwa na wasiwasi, alisema, “Jambo hilo halinifurahishi. ‘Heil’ inamaanisha wokovu. Tukisema ‘Heil Hitler!’ itamaanisha tunasema kwamba wokovu unatoka kwa Hitler wala si kwa Yehova. Si sawa kufanya hivyo, lakini wewe jiamulie mwenyewe utakalofanya.”

Wanashule wenzangu walinitenga kwa sababu nilikataa kumpigia Hitler saluti. Hata wavulana fulani walinipiga walimu walipokuwa hawatazami. Mwishowe waliacha kunisumbua, lakini hata rafiki zangu waliniambia kwamba baba zao waliwakataza kucheza nami eti kwa sababu nilikuwa mtu hatari sana.

Miezi miwili baada ya Wanazi kuanza kutawala Ujerumani, waliwapiga marufuku Mashahidi wa Yehova kwa sababu walikuwa hatari kwa Serikali. Kikosi chenye ukatili cha Hitler kilifunga Betheli huko Magdeburg na kupiga marufuku mikutano yetu. Lakini kwa sababu tuliishi karibu na mpaka, Baba alipata vibali vya kuturuhusu kuvuka mpaka hadi Basel ili kuhudhuria mikutano ya Jumapili. Mara nyingi alisema kwamba alitamani sana ndugu zetu huko Ujerumani wapate chakula hicho cha kiroho ili kiwasaidie kukabili wakati ujao kwa ujasiri.

Matembezi Hatari

Baada ya Betheli ya Magdeburg kufungwa, Julius Riffel aliyekuwa akifanya kazi huko alikuja Lörrach, alikozaliwa, ili kupanga jinsi kazi ya kuhubiri ingefanywa kisiri. Mara moja Baba alijitolea kusaidia. Alituketisha mimi na mama chini na kutueleza kwamba alikuwa amekubali kusaidia kuleta vichapo vya Biblia Ujerumani kutoka Uswisi. Alisema kwamba kazi hiyo ilikuwa hatari sana na angeweza kukamatwa wakati wowote. Hakutaka tuhisi kwamba ni lazima tujihusishe kwa sababu hilo lingekuwa hatari kwetu pia. Mara moja Mama akasema, “nitajiunga nawe.” Wote walinitazama, nami nikasema, “nitajiunga nanyi pia!”

Mama alifuma mfuko wenye ukubwa wa gazeti la Mnara wa Mlinzi. Aliingiza vichapo kwenye mwingilio uliokuwa upande mmoja wa mfuko huo kisha akaushona tena. Alishona mifuko ya siri kwenye nguo za Baba na pia akashona nguo mbili za ndani zenye kubana kuanzia kiunoni hadi mapajani ambamo mimi na yeye tuliweka vichapo vidogo vya Biblia. Kila mara tulipofanikiwa kuleta vichapo hivyo nyumbani, tulifurahi na kumshukuru Yehova. Tulificha vichapo hivyo darini.

Mwanzoni, Wanazi hawakutushuku. Hawakutuuliza maswali wala kupekua nyumba yetu. Hata hivyo, tuliamua kuwa na nambari ya siri 4711, ambayo tungetumia kuwaonya ndugu zetu wa kiroho wakati wa hatari. Nambari hiyo ilikuwa jina la marashi yaliyojulikana sana. Ilipokuwa hatari kuja nyumbani, tulitumia nambari hiyo kwa njia fulani kuwaonya. Baba pia aliwaambia watazame madirisha ya sebule yetu kabla ya kuingia kwenye jengo. Ikiwa dirisha la kushoto lilikuwa wazi, basi kulikuwa na hatari na hivyo hawangeingia.

Mwaka wa 1936 na 1937, askari wa Gestapo waliwakamata maelfu ya Mashahidi na kuwapeleka gerezani na kwenye kambi za mateso ambako walitendewa kijeuri na kinyama sana. Ofisi ya tawi huko Bern, Uswisi, ilianza kukusanya ripoti, kutia ndani ripoti zilizotolewa kambini kisiri, ambazo baadaye ziliandikwa na kuchapishwa katika kitabu kilichoitwa Kreuzzug gegen das Christentum (Mapambano Dhidi ya Ukristo) kilichofichua ukatili wa Wanazi. Tulifanya kazi hatari ya kupeleka ripoti hizo za siri hadi mpakani huko Basel. Ikiwa Wanazi wangetushika na hati hizo zilizopigwa marufuku, tungefungwa gerezani mara moja. Nililia niliposoma jinsi ndugu zetu walivyokuwa wakiteseka. Hata hivyo, sikuogopa. Nilikuwa na uhakika kwamba Yehova, wazazi wangu, na rafiki zangu wa karibu wangenitunza.

Nilimaliza shule nikiwa na umri wa miaka 14 na nikapata kazi ya ukarani katika duka moja la vifaa vya ujenzi. Kwa kawaida, tulisafirisha ripoti hizo za siri Jumamosi au Jumapili alasiri, wakati ambapo Baba hakuwa kazini na tulifanya hivyo kila baada ya majuma mawili. Tulionekana kama familia ya kawaida iliyokuwa katika matembezi yao ya mwisho-juma. Kwa miaka minne hivi, askari wa mpakani hawakutusimamisha au kutupekua. Lakini mambo yalibadilika siku moja Februari 1938.

Twagunduliwa!

Sitasahau kamwe sura ya baba yangu tulipopata rundo kubwa la vichapo mahali ambapo kwa kawaida tulichukua vichapo karibu na Basel. Kwa sababu familia nyingine iliyofanya kazi hiyo ya kubeba vichapo ilikuwa imekamatwa, tulilazimika kubeba vitabu vya ziada. Tulipofika mpakani, ofisa mmoja wa forodha alitushuku na hivyo akaagiza tupekuliwe. Alipopata vitabu hivyo, alitupeleka kwenye magari ya polisi yaliyokuwa yamesimama huku akituelekezea bunduki. Tulipokuwa tukiondoka na polisi hao kwa gari, Baba aliushika mkono wangu kwa nguvu na kuninong’onezea: “Usiwe msaliti. Usitaje jina la mtu yeyote!” “Sitataja,” nikamhakikishia. Tulipofika Lörrach, walimchukua baba yangu mpendwa. Nilimwona mara ya mwisho akiingia kwenye lango la gereza.

Kwa saa nne, askari wanne wa Gestapo walinihoji wakitaka niwaambie majina na anwani za Mashahidi wengine. Nilipokataa, ofisa mmoja alikasirika sana na kunitisha, “Tuna njia nyingine za kukufanya uongee!” Sikuwaambia chochote. Kisha wakaturudisha mimi na Mama nyumbani na kwa mara ya kwanza wakapekua nyumba yetu. Walimpeleka mama yangu korokoroni na kunipeleka kwa shangazi yangu na kumwagiza anitunze pasipo kujua kwamba yeye pia alikuwa Shahidi. Ingawa niliruhusiwa kwenda kazini, askari wanne wa Gestapo walisimamisha gari lao mbele ya nyumba ya shangazi yangu ili kuchunguza njia zangu zote huku polisi mmoja akishika doria kwenye kijia cha miguu.

Siku chache baadaye, wakati wa mapumziko ya chakula cha mchana, nilitoka nje na kumwona dada mmoja kijana akinijia akiwa anaendesha baiskeli yake. Aliponikaribia, alinitupia karatasi fulani. Nilidaka karatasi hiyo na kugeuka ili kuona kama Gestapo waliniona. Kwa kushangaza, nilipokuwa tu nikiidaka, askari hao walikuwa wakiangua kicheko.

Karatasi hiyo iliniagiza niende kwa wazazi wa dada huyo saa sita mchana. Lakini, kwa kuwa askari wa Gestapo walikuwa wakinichunguza, ningefanyaje hivyo bila kuwahatarisha wazazi wake? Niliwatazama wale askari wanne wa Gestapo na yule polisi aliyekuwa akishika doria barabarani. Sikujua la kufanya, hivyo nilimwomba Yehova kwa bidii anisaidie. Kwa ghafula, yule polisi alilikaribia gari la Gestapo na kuzungumza nao. Kisha akaingia ndani ya gari nao wakaondoka.

Mara tu shangazi yangu akatokea pembeni. Ilikuwa saa sita na kitu. Alisoma barua hiyo na kusema kwamba lingekuwa jambo la hekima kwenda kwenye nyumba ile kama tulivyoagizwa, huku akikata kauli kwamba ndugu walikuwa wamepanga kunipeleka Uswisi. Tulipofika huko, familia hiyo ilinijulisha kwa mtu ambaye sikumjua aliyeitwa Heinrich Reiff. Aliniambia kwamba alifurahi kuwa nilifika huko salama na angenisaidia nitorokee Uswisi. Aliniambia tukutane kwenye msitu fulani baada ya nusu saa.

Maisha ya Uhamishoni

Nilikutana na Ndugu Reiff, huku nikibubujikwa na machozi kwa sababu ya huzuni ya kuwaacha wazazi wangu. Mambo yalikuwa yametendeka haraka sana. Baada ya kuwa na wasiwasi kidogo, tuliungana na kikundi cha watalii na kuvuka mpaka na kuingia Uswisi salama.

Nilipofika kwenye ofisi ya tawi huko Bern, niliambiwa kwamba ndugu wa huko ndio waliofanya mipango ili niweze kutoroka. Kwa fadhili, walinipatia makao. Nilifanya kazi jikoni na nilifurahia sana kazi hiyo. Lakini ilikuwa vigumu sana kuishi uhamishoni, bila kujua kitakachowapata wazazi wangu ambao walikuwa wamefungwa kifungo cha miaka miwili kila mmoja. Nyakati nyingine, nilijawa na kihoro na wasiwasi hivi kwamba nilijifungia chooni na kulia. Lakini niliweza kuwasiliana na wazazi wangu kwa ukawaida nao walinitia moyo niendelee kuwa mwaminifu.

Kwa kuchochewa na imani ya wazazi wangu, nilijiweka wakfu kwa Yehova na kubatizwa Julai 25, 1938. Baada ya kufanya kazi Betheli kwa mwaka moja, nilienda kufanya kazi Chanélaz, shamba lililonunuliwa na ofisi ya tawi ya Uswisi ili kukuza chakula kwa ajili ya familia ya Betheli na pia kuwa makao ya ndugu waliokuwa wakitoroka mateso.

Kifungo cha wazazi wangu kilipomalizika mwaka wa 1940, Wanazi waliwaambia kwamba wangewaachilia huru ikiwa wangekana imani yao. Hawakubadili msimamo wao na hivyo wakapelekwa kwenye kambi za mateso, Baba alipelekwa Dachau naye Mama akapelekwa Ravensbrück. Wakati wa majira ya baridi kali ya mwaka wa 1941, mama yangu na Mashahidi wengine wa kike kambini walikataa kufanyia jeshi kazi. Waliadhibiwa kwa kuambiwa wasimame kwenye baridi kwa siku 3, mchana na usiku, na baadaye walifungiwa kwenye vyumba vyenye giza na kupewa chakula kidogo sana kwa siku 40. Kisha wakapigwa viboko. Mama alikufa Januari 31, 1942, majuma matatu baada ya kupigwa kikatili.

Baba alihamishwa kutoka kambi ya Dachau hadi Mauthausen huko Austria. Katika kambi hiyo, Wanazi waliwaua wafungwa kwa kuwanyima chakula na kuwapa kazi ngumu. Lakini miezi sita baada ya Mama kufa, Wanazi walimuua baba yangu wakitumia njia nyingine—majaribio ya kitiba. Madaktari kambini waliwaambukiza wafungwa ugonjwa wa kifua kikuu kimakusudi ili kufanya majaribio ya kitiba. Baadaye, waliwadunga wafungwa hao sindano yenye sumu moyoni. Hati rasmi za serikali zinasema kwamba kifo cha Baba kilisababishwa na “msuli dhaifu wa moyo.” Alikuwa na umri wa miaka 43. Nilijulishwa kuhusu mauaji hayo ya kikatili miezi kadhaa baadaye. Bado mimi hutokwa na machozi ninapowakumbuka wazazi wangu wapendwa. Hata hivyo, sasa kama ilivyokuwa wakati huo, ninafarijika kujua kwamba Mama na Baba, ambao walikuwa na tumaini la kwenda mbinguni, wako salama mikononi mwa Yehova.

Baada ya Vita vya Pili vya Ulimwengu, nilipata pendeleo la kuhudhuria darasa la 11 la Shule ya Gileadi (Watchtower Bible School of Gilead) huko New York. Nilifurahia sana kujifunza Biblia kwa makini kwa miezi mitano. Nilipohitimu mwaka wa 1948, nilitumwa nikatumikie nikiwa mishonari huko Uswisi. Muda mfupi baadaye, nilikutana na James L. Turpin, ndugu mwaminifu aliyehitimu darasa la tano la Gileadi. Alitumikia akiwa mwangalizi wa ofisi ya tawi ya kwanza huko Uturuki. Tulioana Machi 1951, na muda mfupi baadaye tukagundua kwamba tungepata mtoto! Tulihamia Marekani na binti yetu, Marlene akazaliwa Desemba mwaka huo.

Kwa miaka hiyo yote, mimi na Jim tumepata shangwe kubwa katika utumishi wetu wa Ufalme. Nakumbuka mwanafunzi mmoja wa Biblia, Penny, mwanamke kijana kutoka China ambaye alipenda sana kujifunza Biblia. Alibatizwa na baadaye akaolewa na Guy Pierce, ambaye sasa ni mshiriki wa Baraza Linaloongoza la Mashahidi wa Yehova. Marafiki wapendwa kama yeye wamesaidia kujaza pengo lililosababishwa na kifo cha wazazi wangu.

Mapema mwaka wa 2004, ndugu huko Lörrach, mji walikoishi wazazi wangu, walijenga Jumba jipya la Ufalme kwenye barabara ya Stich Street. Ili kutambua yale ambayo Mashahidi wa Yehova walikuwa wamefanya, Baraza la jiji liliamua kubadili jina la barabara hiyo na kuiita Denzstraße (Barabara ya Denz) kwa heshima ya wazazi wangu. Chini ya kichwa kikuu, “Kwa Ukumbusho wa Denz, Wenzi wa Ndoa Waliouawa,” gazeti moja la huko, Badische Zeitung lilisema kwamba wazazi wangu “waliuawa katika kambi ya mateso wakati wa Utawala wa Nazi kwa sababu ya imani yao.” Hatua hiyo ya baraza la jiji ilinigusa moyo sana ingawa ilikuwa badiliko ambalo sikutazamia.

Baba alikuwa akituambia kwamba tunapaswa kupanga mambo kimbele kana kwamba Har–Magedoni haingetukia maishani mwetu lakini tuishi kana kwamba ingekuja kesho. Sikuzote nimejaribu kufuata shauri hilo zuri. Si rahisi kuwa na subira na wakati uleule kutazamia kwa hamu wakati ujao, hasa sasa kwa kuwa siwezi kutoka nyumbani kwa sababu ya matatizo ya uzee. Hata hivyo, sijawahi kutilia shaka ahadi hii ya Yehova kwa watumishi wake wote walio waaminifu: “Mtegemee Yehova kwa moyo wako wote . . . Mtambue yeye katika njia zako zote, naye atanyoosha mapito yako.”—Methali 3:5, 6.

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 29]

MANENO YA KALE YENYE THAMANI

Mwanamke mmoja kutoka kijiji cha mbali alitembelea Lörrach katika miaka ya 1980. Wakati huo, watu wa mji huo walikuwa wakileta vyombo ambavyo hawakuvihitaji na kuviweka mahali fulani pa umma ili wengine wachukue chochote walichotaka. Mwanamke huyo alipata sanduku lenye vifaa vya kushonea na kulipeleka nyumbani. Baadaye, chini ya sanduku hilo, alipata picha fulani za msichana mdogo na barua ambazo ziliandikwa kwenye karatasi za kambi ya mateso. Mwanamke huyo alipendezwa sana na barua hizo naye akataka kujua msichana huyo mdogo aliyekuwa amesukwa nywele ni nani.

Siku moja katika mwaka wa 2000, mwanamke huyo aliona makala fulani katika gazeti kuhusu maonyesho ya kihistoria huko Lörrach. Makala hiyo ilieleza historia ya Mashahidi wa Yehova, kutia ndani familia yetu, wakati wa Utawala wa Nazi. Ilikuwa na picha zangu nikiwa kijana. Mwanamke huyo alipoona kwamba picha hizo zinafanana na zile alizokuwa nazo, aliwasiliana na mwandishi wa makala hiyo na kumweleza kuhusu barua 42 alizokuwa nazo. Majuma machache baadaye, nilipokea barua zote hizo. Wazazi wangu walimwandikia shangazi yangu barua hizo wakiulizia hali yangu. Hawakuacha kamwe kunihangaikia. Inastaajabisha kwamba barua hizo zilidumu kwa muda mrefu hivyo na kunifikia zaidi ya miaka 60 baadaye!

[Picha katika ukurasa wa 25]

Familia yetu yenye furaha ilitenganishwa Hitler alipoanza kutawala

[Hisani]

Hitler: U.S. Army photo

[Picha katika ukurasa wa 26]

1. Betheli ya Magdeburg

2. Askari wa Gestapo waliwakamata maelfu ya Mashahidi

[Picha katika ukurasa wa 28]

Mimi na Jim tumepata shangwe kubwa katika utumishi wetu wa Ufalme