Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Mambo Makuu Katika Kitabu cha Yoshua

Mambo Makuu Katika Kitabu cha Yoshua

Neno la Yehova Liko Hai

Mambo Makuu Katika Kitabu cha Yoshua

WAKIWA wamepiga kambi kwenye Nchi Tambarare ya Moabu mwaka wa 1473 K.W.K., lazima Waisraeli wawe walisisimuka kusikia maneno haya: “Jitayarishieni chakula, kwa kuwa siku tatu kutoka sasa mtavuka huu mto Yordani ili kuingia na kuimiliki nchi ambayo Yehova Mungu wenu anawapa ninyi mpate kuimiliki.” (Yoshua 1:11) Ile miaka 40 ambayo wangekaa nyikani inakaribia kwisha.

Zaidi ya miaka 20 hivi baadaye, kiongozi Yoshua asimama katikati ya nchi ya Kanaani na kuwatangazia hivi wanaume wazee wa Israeli: “Oneni, niliwagawia kwa kura mataifa haya yanayobaki yawe urithi kwa ajili ya makabila yenu, na mataifa yote ambayo nilikatilia mbali, kuanzia Yordani mpaka Bahari Kuu upande wa magharibi. Na Yehova Mungu wenu ndiye aliyeendelea kuwasukuma mbali kutoka mbele yenu, naye akawanyang’anya miliki yao kwa ajili yenu, nanyi mkaimiliki nchi yao, kama vile Yehova Mungu wenu alivyokuwa amewaahidi ninyi.”—Yoshua 23:4, 5.

Kitabu cha Yoshua ambacho kiliandikwa na Yoshua mnamo mwaka wa 1450 K.W.K., kinasimulia mambo ya kihistoria yenye kusisimua yaliyotukia miaka hiyo 22. Tunapokaribia kuingia katika dunia mpya iliyoahidiwa, hali yetu inafanana na ile ya wana wa Israeli ambao walikuwa tayari kuimiliki Nchi ya Ahadi. Basi na tuchunguze kwa makini kitabu cha Yoshua.—Waebrania 4:12.

HADI KWENYE “NCHI TAMBARARE ZA JANGWA LA YERIKO”

(Yoshua 1:1–5:15)

Kwa kweli, Yoshua anapokea mgawo muhimu Yehova anapomwambia hivi: “Musa mtumishi wangu amekufa; basi simama sasa, vuka huu mto Yordani, wewe na watu hawa wote, mwingie katika nchi ambayo ninawapa wao, wana wa Israeli.”! (Yoshua 1:2) Yoshua ana mgawo wa kuongoza taifa lenye watu milioni kadhaa kuingia Nchi ya Ahadi. Ili kujitayarisha, anawatuma wapelelezi wawili kwenda Yeriko—jiji litakalokuwa la kwanza kushindwa. Rahabu, yule kahaba ambaye amesikia juu ya kazi za Yehova zenye nguvu alizofanya kwa niaba ya watu wake, anaishi jijini humo. Anawalinda na kuwasaidia wapelelezi hao, nao wanamwahidi kwamba atahifadhiwa.

Wapelelezi wanaporudi, Yoshua na Waisraeli wako tayari kuendelea na safari yao na kuvuka Yordani. Ingawa mto huo unafurika hadi kwenye kingo zake, hicho si kizuizi kwa kuwa Yehova anafanya mkondo wa maji ulio upande wa juu wa mto uinuke kama bwawa la maji na ule wa upande wa chini uelekee katika Bahari ya Chumvi. Baada ya kuvuka Yordani, Waisraeli wanapiga kambi huko Gilgali, karibu na Yeriko. Siku nne baadaye, jioni ya Nisani 14 siku ya Abibu, wanaadhimisha sikukuu ya Pasaka kwenye nchi tambarare za jangwa la Yeriko. (Yoshua 5:10) Siku inayofuata, wanaanza kula baadhi ya mazao ya nchi hiyo, nayo mana inakoma. Wakati huo, Yoshua anawatahiri wanaume wote waliozaliwa nyikani.

Maswali ya Kimaandiko Yajibiwa:

2:4, 5—Kwa nini Rahabu anawaelekeza vibaya wanaume wa mfalme ambao wanawatafuta wapelelezi? Rahabu anahatarisha uhai wake kwa kuwaficha wapelelezi hao kwa sababu amesitawisha imani katika Yehova. Kwa hiyo, hayuko chini ya wajibu wowote kuwaeleza wanaume wanaokusudia kuwadhuru watu wa Mungu mahali walipo wapelelezi. (Mathayo 7:6; 21:23-27; Yohana 7:3-10) Kwa kweli, Rahabu ‘alitangazwa kuwa mwadilifu kwa matendo,’ kutia ndani tendo la kuwaelekeza vibaya wajumbe wa mfalme.—Yakobo 2:24-26.

5:14, 15—“Mkuu wa jeshi la Yehova” ni nani? Yaelekea mkuu anayekuja kumwimarisha Yoshua wakati Nchi ya Ahadi inapoanza kutwaliwa, ni “Neno,” yaani, Yesu Kristo kabla hajawa mwanadamu. (Yohana 1:1; Danieli 10:13) Ni jambo lenye kuimarisha kama nini kuwa na uhakika kwamba Yesu Kristo aliyetukuzwa yuko pamoja na watu wa Mungu leo wanapoendelea na vita vya kiroho!

Mambo Tunayojifunza:

1:7-9. Ili tufanikiwe katika mambo ya kiroho, tunapaswa kusoma Biblia kila siku, kutafakari yale inayosema na kutumia mambo tunayojifunza.

1:11. Yoshua anawaambia watu watayarishe chakula na vitu vya lazima badala ya kungojea Mungu kizembe awaandalie vitu hivyo. Shauri la Yesu kwamba tusihangaikie mambo ya lazima maishani, pamoja na ahadi ya kwamba “mtaongezewa hivi vitu vingine vyote” halimaanishi kwamba hatupaswi kufanya jitihada yoyote ya kujitegemeza.—Mathayo 6:25, 33.

2:4-13. Baada ya kusikia kuhusu kazi kuu za Yehova na kutambua kwamba wakati huo ulikuwa wa hatari, Rahabu anaamua kuwaunga mkono waabudu wa Yehova. Ikiwa umekuwa ukijifunza Biblia kwa muda fulani na unatambua kwamba tunaishi katika “siku za mwisho,” je, hupaswi kuamua kumtumikia Mungu?—2 Timotheo 3:1.

3:15. Kwa kuwa wapelelezi waliotumwa Yeriko wanaleta ripoti nzuri, Yoshua anatenda haraka bila kungojea maji ya Yordani yapungue. Tunapaswa kutenda kwa ujasiri kuhusiana na mambo ya ibada ya kweli badala ya kusitasita hadi hali zionekane kuwa zinafaa zaidi.

4:4-8, 20-24. Mawe 12 yaliyotolewa chini ya mto Yordani yangekuwa ukumbusho kwa Israeli. Matendo ya Yehova ya kuwakomboa watu wake leo kutokana na maadui wao pia ni ukumbusho wa kwamba yuko pamoja nao.

USHINDI WAENDELEA

(Yoshua 6:1–12:24)

Jiji la Yeriko ‘limefungwa imara, hakuna mtu anayetoka nje wala kuingia ndani.’ (Yoshua 6:1) Jiji hilo lingetekwaje? Yehova anamwonyesha Yoshua mbinu. Punde si punde, kuta zinaporomoka nalo jiji linaharibiwa. Rahabu tu pamoja na watu wa nyumbani mwake ndio wanaookoka.

Ushindi unaofuata ni dhidi ya jiji la kifalme la Ai. Wapelelezi waliotumwa huko wanaripoti kwamba jiji hilo lina wakaaji wachache, kwa hiyo ni wanaume wachache tu wanaohitajiwa ili kulipiga. Hata hivyo, askari-jeshi wapatao 3,000 ambao walitumwa kushambulia jiji hilo wanawatoroka wanaume wa Ai. Kwa nini? Yehova hayuko pamoja na Waisraeli. Akani wa kabila la Yuda alifanya dhambi Yeriko lilipovamiwa. Baada ya kushughulikia jambo hilo, Yoshua anashambulia Ai tena. Mfalme wa Ai yuko tayari kupigana na Waisraeli kwa kuwa aliwahi kuwashinda pindi moja. Lakini kwa kuwa wanaume wa Ai wana uhakika kwamba watawashinda Waisraeli, Yoshua anatumia mbinu fulani na kuliteka jiji lao.

Gibeoni ni ‘jiji kubwa—kubwa kuliko Ai, na wanaume wake wote ni wenye nguvu.’ (Yoshua 10:2) Hata hivyo, baada ya kusikia kuhusu ushindi wa Yoshua dhidi ya Yeriko na Ai, wanaume wa Gibeoni wanamdanganya Yoshua afanye agano la amani pamoja nao. Mataifa jirani yanaona uasi huo kuwa tisho kwao. Wafalme watano wa mataifa hayo wanaungana na kushambulia Gibeoni. Israeli lawaokoa Wagibeoni na kuwashinda kabisa washambuliaji hao. Ushindi mwingine ambao Israeli lilipata Yoshua alipokuwa kiongozi unatia ndani majiji yaliyo kusini na magharibi, na vilevile wafalme wa kaskazini walioungana. Wafalme wote walioshindwa ambao walikuwa upande wa magharibi ya Yordani ni 31.

Maswali ya Kimaandiko Yajibiwa:

10:13Jambo hilo lisilo la kawaida linawezekanaje? “Je, jambo lolote ni kubwa mno isivyo kawaida kwa Yehova,” Muumba wa mbingu na dunia? (Mwanzo 18:14) Yehova akitaka anaweza kufanya dunia isizunguke hivi kwamba mtu akiwa duniani ataona ni kana kwamba jua na mwezi zimesimama. Au anaweza kuacha dunia na mwezi ziendelee kuzunguka lakini apinde miali ya jua na mwezi ili nuru kutoka kwa mianga hiyo iendelee kuangaza. Vyovyote iwavyo, “hakuna siku ambayo imepata kuwa kama hiyo” katika historia ya wanadamu.—Yoshua 10:14.

10:13Kitabu cha Yashari ni nini? Kitabu hicho kinatajwa tena kwenye 2 Samweli 1:18 kuhusiana na shairi linaloitwa “Upinde”—wimbo wa huzuni unaohusu Mfalme Sauli wa Israeli na mwana wake Yonathani. Labda kitabu hicho kilikuwa mkusanyo wa nyimbo na mashairi yaliyohusu matukio yaliyokumbukwa katika historia ya Waisraeli na yaelekea Waebrania walikifahamu vizuri.

Mambo Tunayojifunza:

6:26; 9:22, 23. Laana iliyotamkwa na Yoshua wakati Yeriko lilipokuwa likiharibiwa inatimizwa miaka 500 hivi baadaye. (1 Wafalme 16:34) Laana ya Noa kwa mjukuu wake wa kiume Kanaani inatimizwa Wagibeoni wanapokuwa wafanyakazi. (Mwanzo 9:25, 26) Sikuzote neno la Yehova hutimia.

7:20-25. Huenda watu fulani wakaona wizi wa Akani kuwa jambo dogo, labda wakisema kwamba haukuwadhuru wengine. Huenda wakawa na maoni hayohayo kuhusu wizi mdogo na makosa madogo-madogo yanayokiuka sheria ya Biblia. Hata hivyo, tunapaswa kuwa kama Yoshua katika azimio letu la kupinga uvutano wa kufanya mambo yaliyo kinyume cha sheria au yasiyo ya adili.

9:15, 26, 27. Tunapaswa kuchukua kwa uzito mapatano tunayofanya na kutimiza ahadi zetu.

YOSHUA AFANYA KAZI YAKE KUBWA YA MWISHO

(Yoshua 13:1–24:33)

Sasa akikaribia umri wa miaka 90, Yoshua anaanza kugawanya nchi hiyo. Ni kazi kubwa kwelikweli! Makabila ya Rubeni na Gadi na nusu ya kabila la Manase tayari yamepokea urithi wao mashariki ya Yordani. Makabila yanayobaki yanapewa urithi upande wa magharibi kwa kupigwa kwa kura.

Maskani inajengwa huko Shilo katika eneo la Efraimu. Kalebu anapokea jiji la Hebroni, naye Yoshua anapokea Timnath-sera. Walawi wanapewa majiji 48, kutia ndani majiji 6 ya makimbilio. Wakiwa njiani kurudi kwenye urithi wao mashariki ya Yordani, mashujaa wa vita wa Rubeni, Gadi, na nusu ya kabila la Manase wanajenga madhabahu “kubwa yenye kuonekana wazi.” (Yoshua 22:10) Makabila yaliyo magharibi ya Yordani yanaona jambo hilo kuwa tendo la uasi-imani na karibu vita vya kikabila vitokee, lakini umwagaji wa damu unazuiwa kwa sababu ya mawasiliano mazuri.

Baada ya Yoshua kuishi Timnath-sera kwa muda fulani, anawaita wanaume wazee, vichwa, waamuzi, na maofisa wa Israeli na kuwahimiza wawe jasiri na kuendelea kuwa waaminifu kwa Yehova. Baadaye, Yoshua anakusanya makabila yote ya Israeli huko Shekemu. Akiwa huko, anazungumzia tena matendo ya Yehova tangu wakati wa Abrahamu na kuendelea, na kuwahimiza tena ‘wamwogope Yehova na kumtumikia kwa njia isiyo na kosa na katika kweli.’ Watu wanachochewa kujibu hivi: “Yehova, Mungu wetu, ndiye tutakayemtumikia, na sauti yake ndiyo tutakayoisikiliza!” (Yoshua 24:14, 15, 24) Baada ya mambo hayo, Yoshua afa akiwa na umri wa miaka 110.

Maswali ya Kimaandiko Yajibiwa:

13:1Je, andiko hili linapingana na yale yanayosemwa kwenye Yoshua 11:23? La, kwa kuwa kumilikiwa kwa Nchi ya Ahadi kulihusisha mambo mawili: kwanza, vita vya kitaifa ambavyo kupitia hivyo wafalme 31 wa nchi ya Kanaani walishindwa na nguvu za Wakanaani kumalizwa, na pili makabila na watu mmoja-mmoja walishinda na kumiliki kikamili nchi hiyo. (Yoshua 17:14-18; 18:3) Ingawa wana wa Israeli hawakuwafukuza Wakanaani wote kabisa, wale waliobaki hawakuwa tisho kwa usalama wa Israeli. (Yoshua 16:10; 17:12) Andiko la Yoshua 21:44 linasema: “Yehova akawapa pumziko kuwazunguka pande zote.”

24:2Je, Tera, baba ya Abrahamu alikuwa mwabudu-sanamu? Hapo mwanzo, Tera hakuwa mwabudu wa Yehova Mungu. Yaelekea aliabudu mungu-mwezi aliyeitwa Sin—mungu aliyekuwa maarufu huko Uru. Kulingana na mapokeo ya Kiyahudi, huenda hata Tera alitengeneza sanamu. Hata hivyo, Abrahamu anapotii amri ya Mungu na kuondoka Uru, Tera anaambatana naye hadi Harani.—Mwanzo 11:31.

Mambo Tunayojifunza:

14:10-13. Ingawa ana umri wa miaka 85, Kalebu anaomba kazi ngumu ya kuwafukuza watu katika eneo la Hebroni. Eneo hilo linakaliwa na Waanakimu—watu wakubwa isivyo kawaida. Kwa msaada wa Yehova, shujaa huyo wa vita mwenye uzoefu anafanikiwa, na Hebroni lawa jiji la makimbilio. (Yoshua 15:13-19; 21:11-13) Kielelezo cha Kalebu kinatutia moyo tusiogope migawo migumu ya kiroho.

22:9-12, 21-33. Tunapaswa kuwa waangalifu ili kuepuka kuelewa vibaya nia ya wengine.

“Halikukosa Kutimia Hata Neno Moja”

Anapokuwa mzee, Yoshua anawaambia hivi wanaume wa Israeli wenye madaraka: “Halikukosa kutimia hata neno moja kati ya maneno yote mema ambayo Yehova Mungu wenu amewaambia ninyi. Yote yametimia kwenu.” (Yoshua 23:14) Simulizi la kihistoria la Yoshua linafafanua jambo hilo waziwazi kama nini!

Mtume Paulo aliandika hivi: “Mambo yote yaliyoandikwa zamani yaliandikwa ili kutufundisha sisi, ili kupitia uvumilivu wetu na kupitia faraja kutokana na Maandiko tuwe na tumaini.” (Waroma 15:4) Tunaweza kuwa na uhakika kwamba tumaini letu katika ahadi za Mungu si bure. Hakuna ahadi itakayokosa kutimia; zote zitatimia.

[Ramani katika ukurasa wa 10]

(Ona mpangilio kamili katika nakala iliyochapishwa)

Nchi iliyotwaliwa Yoshua alipokuwa kiongozi

BASHANI

GILEADI

ARABA

NEGEBU

Mto Yordani

Bahari ya Chumvi

B.M. la Yaboki

B.M. la Arnoni

Hasori

Madoni

Lasharoni

Shimroni

Yokneamu

Dori

Megido

Kedeshi

Taanaki

Heferi

Tirsa

Afeki

Tapua

Betheli

Ai

Gilgali

Yeriko

Gezeri

Yerusalemu

Makeda

Yarmuthi

Adulamu

Libna

Lakishi

Egloni

Hebroni

Debiri

Aradi

[Picha katika ukurasa wa 9]

Je, unajua kwa nini Rahabu, yule kahaba alitangazwa kuwa mwadilifu?

[Picha katika ukurasa wa 10]

Yoshua aliwahimiza Waisraeli ‘wamwogope Yehova na kumtumikia’

[Picha katika ukurasa wa 12]

Wizi wa Akani haukuwa kosa dogo—ulikuwa na matokeo mabaya sana

[Picha katika ukurasa wa 12]

“Kwa imani kuta za Yeriko zilianguka.”—Waebrania 11:30