Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Unapaswa Kuamuaje Yaliyo Sawa na Yaliyo Makosa?

Unapaswa Kuamuaje Yaliyo Sawa na Yaliyo Makosa?

Unapaswa Kuamuaje Yaliyo Sawa na Yaliyo Makosa?

NI NANI aliye na haki ya kuweka viwango vya yaliyo sawa na yaliyo makosa? Swali hilo lilizushwa mwanzoni kabisa mwa historia ya wanadamu. Kitabu cha Biblia cha Mwanzo kinaonyesha kwamba Mungu alichagua mti fulani uliokuwa ukikua katika bustani ya Edeni uwe “mti wa ujuzi wa mema na mabaya.” (Mwanzo 2:9) Mungu aliwaagiza wanadamu wawili wa kwanza wasile matunda ya mti huo. Hata hivyo, Shetani Ibilisi ambaye ni adui wa Mungu, alidokeza kwamba ikiwa wangekula matunda ya mti huo, macho yao ‘yangefunguliwa’ nao ‘wangekuwa kama Mungu, wakijua mema na mabaya.’—Mwanzo 2:16, 17; 3:1, 5; Ufunuo 12:9.

Adamu na Hawa walikabili uamuzi fulani—je, wangepaswa kukubali viwango vya Mungu vya mema na mabaya au wangepaswa kufuata viwango vyao wenyewe? (Mwanzo 3:6) Waliamua kutomtii Mungu na kula matunda ya mti huo. Tendo hilo rahisi lilimaanisha nini? Kwa kukataa kuheshimu mipaka waliyowekewa na Mungu, walidai kwamba wao na wazao wao wangeishi vizuri zaidi kwa kujiwekea viwango vyao wenyewe vya yaliyo sawa na yaliyo makosa. Wanadamu wamefaulu kadiri gani kwa kujaribu kujitwika mamlaka hayo ya Mungu?

Maoni Yanayotofautiana

Baada ya kuchunguza mafundisho ya wanafalsafa mashuhuri kwa karne nyingi, kichapo Encyclopædia Britannica kinasema kwamba tangu wakati wa mwanafalsafa Mgiriki Socrates hadi karne ya 20, kumekuwa na “mijadala ya mara kwa mara kuhusu maana kamili ya kiwango cha yaliyo sawa na yaliyo makosa.”

Kwa mfano, Sophists walikuwa kikundi mashuhuri cha walimu Wagiriki wa karne ya tano K.W.K. Walifundisha kwamba viwango vya yaliyo sawa na yaliyo makosa viliamuliwa na maoni ya wengi. Mmoja wa walimu hao alisema: “Mambo yoyote yanayoonekana kuwa yanafaa kiadili na yenye kukubalika kwa kila jiji, ni mazuri tu kwa jiji hilo, mradi tu wakaaji wa jiji hilo wanayaona kuwa mazuri.” Kwa kufuata kiwango hicho, Jodie, aliyetajwa katika makala iliyotangulia, anapaswa kuchukua pesa hizo, kwa kuwa yaelekea watu wengi katika jumuiya au “jiji” lake, wangefanya hivyo.

Immanuel Kant, mwanafalsafa mashuhuri wa karne ya 18 alikuwa na maoni tofauti. Gazeti Issues in Ethics linasema: “Immanuel Kant na wengine kama yeye . . . walikazia haki ya mtu ya kujiamulia mwenyewe.” Kulingana na falsafa ya Kant, mradi Jodie havunji haki za wengine, yeye ndiye angeamua jambo la kufanya. Hapaswi kutegemea maoni ya wengi ili kuamua viwango atakavyofuata.

Kwa hiyo, Jodie alishughulikiaje hali hiyo yenye kutatanisha? Alifuata njia ya tatu. Alifuata mafundisho ya Yesu Kristo, ambaye viwango vyake vya maadili vimesifiwa na Wakristo na watu wasio Wakristo pia. Yesu alifundisha: “Kwa hiyo, mambo yote mnayotaka watu wawatendee ninyi, lazima mwatendee wao pia vivyo hivyo.” (Mathayo 7:12) Mteja wake alishangaa kupokea dola 82,000, kutoka kwa Jodie. Alipoulizwa kwa nini hakuchukua pesa hizo, Jodie alieleza kwamba yeye ni mmoja wa Mashahidi wa Yehova, kisha akasema: “Pesa hizo hazikuwa zangu.” Jodie aliona umuhimu wa kutii maneno ya Yesu yaliyoandikwa katika Biblia kwenye Mathayo 19:18: “Usiibe.”

Je, Maoni ya Wengi Ni Mwongozo Unaotegemeka?

Huenda watu fulani wakasema kwamba Jodie alikuwa mjinga kwa kuwa mnyoofu sana. Lakini maoni ya wengi si mwongozo unaotegemeka. Kwa mfano, ikiwa ungeishi katika jamii inayoamini kwamba kutoa watoto dhabihu kunakubalika, kama jamii nyingine zilivyoamini hapo awali, je, hilo lingefanya uone zoea hilo kuwa linafaa? (2 Wafalme 16:3) Namna gani ikiwa ungezaliwa katika jamii ambayo huona kula nyama ya binadamu kuwa jambo linalofaa? Je, hilo lingemaanisha kwamba si kosa kula nyama ya binadamu? Kwa kuwa tu jambo fulani linapendwa na watu wengi hiyo haimaanishi kwamba jambo hilo ni sawa. Zamani sana, Biblia ilitoa onyo dhidi ya mtego huo, ikisema: “Usiufuate umati kwa ajili ya makusudio maovu.”—Kutoka 23:2.

Yesu Kristo alionyesha sababu nyingine ya kujihadhari ili tusifuate maoni ya wengi kama mwongozo wa yaliyo sawa na yaliyo makosa. Alimfunua Shetani kuwa “mtawala wa ulimwengu.” (Yohana 14:30; Luka 4:6) Shetani hutumia cheo chake kupotosha “dunia nzima inayokaliwa.” (Ufunuo 12:9) Kwa hiyo, ukijiwekea viwango vya yaliyo sawa na yaliyo makosa kwa kutegemea tu maoni ya wengi, huenda ukawa unafuata maoni ya Shetani kuhusu maadili, na bila shaka jambo hilo lingetokeza msiba.

Je, Unaweza Kutegemea Maoni Yako Mwenyewe?

Basi, je, kila mtu anapaswa kujiamulia mwenyewe yaliyo sawa na yaliyo makosa? Biblia inasema: “Usitegemee uelewaji wako mwenyewe.” (Methali 3:5) Kwa nini? Kwa sababu wanadamu wote wamerithi kasoro ya asili ambayo inaweza kupotosha maoni yao. Adamu na Hawa walipomwasi Mungu, walikubali viwango vya msaliti mwenye ubinafsi Shetani na kumchagua yeye kuwa baba yao wa kiroho. Kisha wakawapitishia wazao wao tabia fulani—moyo wenye hila ambao unaweza kutambua yaliyo sawa lakini wenye mwelekeo wa kufuatia yaliyo makosa.—Mwanzo 6:5; Waroma 5:12; 7:21-24.

Kikizungumzia maadili, kichapo Encyclopædia Britannica, kinasema: “Haishangazi kwamba watu wanajua jambo wanalopaswa kufanya lakini wanafanya lile linalowapendeza. Limekuwa tatizo kubwa sana kuwapa watu wanaofuata maadili ya nchi za Magharibi sababu za kufanya yaliyo sawa.” Biblia husema hivi kwa usahihi: “Moyo ni wenye hila kuliko kitu kingine chochote nao ni hatari. Ni nani anayeweza kuujua?” (Yeremia 17:9) Je, unaweza kumtumaini mtu ambaye anajulikana kuwa mwenye hila na hatari?

Ni kweli kwamba, hata watu wasiomwamini Mungu wanaweza kujiendesha kwa njia ya uadilifu na kutunga kanuni za maadili zinazofaa na zenye kuheshimika. Hata hivyo, mara nyingi kanuni bora zilizo katika mifumo yao ya sheria huonyesha tu viwango vya Biblia vya maadili. Ingawa huenda watu hao wakakana kuwepo kwa Mungu, mawazo yao huonyesha kwamba wana uwezo wa kiasili wa kudhihirisha utu wa Mungu. Kama Biblia isemavyo, hilo linathibitisha kwamba, mwanadamu aliumbwa “kwa mfano wa Mungu.” (Mwanzo 1:27; Matendo 17:26-28) Mtume Paulo anasema: “Wao ndio wanaoonyesha kuwa yaliyomo katika sheria yameandikwa ndani ya mioyo yao.”—Waroma 2:15.

Bila shaka, kuna tofauti kati ya kujua yaliyo sawa; na kuwa na nguvu za kiadili za kufanya yaliyo sawa. Mtu hupataje nguvu za kiadili zinazohitajiwa? Kwa kuwa matendo huchochewa na moyo, kusitawisha upendo kwa Mtungaji wa Biblia, Yehova Mungu, kunaweza kumsaidia mtu awe na nguvu hizo.—Zaburi 25:4, 5.

Kupata Nguvu za Kutenda Mema

Hatua ya kwanza katika kujifunza kumpenda Mungu ni kutambua jinsi amri zake zinavyofaa na zinavyotumika. Mtume Yohana anasema: “Maana kumpenda Mungu humaanisha hivi, kwamba tuzishike amri zake; na bado amri zake si mzigo mzito.” (1 Yohana 5:3) Kwa mfano, Biblia ina mashauri yanayofaa ambayo yanaweza kuwasaidia vijana kutambua jambo linalofaa na lililo kosa wanapoamua kama wanapaswa kutumia vileo, dawa za kulevya, au kufanya ngono kabla ya ndoa. Biblia inaweza kuwasaidia watu waliooana wajue jinsi ya kutatua matatizo yao na pia inaweza kuwaandalia wazazi mwongozo wa kulea watoto. * Vinapofuatwa, viwango vya Biblia vya maadili huwanufaisha vijana kwa wazee, bila kujali jamii, elimu, au utamaduni wao.

Kama vile unavyopata nguvu za kufanya kazi kwa kula chakula kinachofaa, kusoma Neno la Mungu hukupa nguvu za kuishi kupatana na kanuni zake. Yesu alifananisha maneno ya Mungu na mkate unaotegemeza uhai. (Mathayo 4:4) Pia alisema: “Chakula changu ni mimi kufanya mapenzi yake aliyenituma.” (Yohana 4:34) Kula chakula cha kiroho cha neno la Mungu kulimsaidia Yesu ashinde vishawishi na kufanya maamuzi ya hekima.—Luka 4:1-13.

Huenda mwanzoni ukaona ni vigumu kula chakula cha kiroho cha Neno la Mungu na kufuata viwango vyake. Lakini kumbuka kwamba ulipokuwa mdogo, labda hukupenda ladha ya vyakula fulani vilivyokufaa. Ili kupata nguvu, ilikubidi ujifunze kupendezwa na vyakula hivyo vinavyofaa. Vivyo hivyo, huenda ikakuchukua muda kupendezwa na viwango vya Mungu. Ukiendelea kujitahidi, utaanza kupendezwa navyo na kuwa na nguvu za kiroho. (Zaburi 34:8; 2 Timotheo 3:15-17) Utajifunza kumpenda Yehova na kuchochewa ‘kufanya mema.’—Zaburi 37:3.

Huenda usijikute kamwe katika hali kama ile ya Jodie. Hata hivyo, kila siku unafanya maamuzi madogo na makubwa yanayohusu maadili. Kwa hiyo, Biblia inakuhimiza: “Mtegemee Yehova kwa moyo wako wote wala usitegemee uelewaji wako mwenyewe. Mtambue yeye katika njia zako zote, naye atanyoosha mapito yako.” (Methali 3:5, 6) Kujifunza kumtegemea Yehova kutakunufaisha sasa na pia kukupa nafasi ya kuishi milele kwa sababu kumtii Yehova Mungu huongoza kwenye uzima.—Mathayo 7:13, 14.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 18 Shauri linalofaa kutoka katika Biblia kuhusu habari hii na nyingine muhimu linapatikana katika vitabu Maswali Ambayo Vijana Huuliza—Majibu Yafanyayo Kazi na Siri ya Kupata Furaha ya Familia, vilivyochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

[Blabu katika ukurasa wa 6]

Huenda maoni ya wengi yakaathiriwa na viumbe wa roho wasioonekana

[Picha katika ukurasa wa 5]

Katika historia yote, wanafalsafa wamejadili suala la yaliyo sawa na yaliyo makosa

SOCRATES

KANT

CONFUCIUS

[Hisani]

Kant: From the book The Historian’s History of the World; Socrates: From the book A General History for Colleges and High Schools; Confucius: Sung Kyun Kwan University, Seoul, Korea

[Picha katika ukurasa wa 7]

Biblia haitusaidii tu kutambua yaliyo sawa na yaliyo makosa bali pia hutuchochea kufanya yaliyo sawa