Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Fuateni Kielelezo Kilichowekwa na Yesu

Fuateni Kielelezo Kilichowekwa na Yesu

Fuateni Kielelezo Kilichowekwa na Yesu

“Niliweka kielelezo kwa ajili yenu, ili, kama vile nilivyowafanyia ninyi, ninyi pia mfanye hivyo.”—YOHANA 13:15.

1. Kwa nini Yesu ni kielelezo cha kuigwa na Wakristo?

KATIKA historia yote ya wanadamu, ni mtu mmoja tu aliyeishi maisha yake yote bila kufanya dhambi. Mtu huyo ni Yesu. Mbali na Yesu, “hakuna mwanadamu asiyetenda dhambi.” (1 Wafalme 8:46; Waroma 3:23) Kwa sababu hiyo, Wakristo wa kweli humwona Yesu kuwa kielelezo kikamilifu cha kuigwa. Kwa kweli, Nisani 14, 33 W.K., muda mfupi kabla ya kifo chake, Yesu aliwaambia wafuasi wake wamwige. Alisema: “Niliweka kielelezo kwa ajili yenu, ili, kama vile nilivyowafanyia ninyi, ninyi pia mfanye hivyo.” (Yohana 13:15) Usiku huo wa mwisho, Yesu alitaja njia mbalimbali ambazo Wakristo wanapaswa kujitahidi kuwa kama yeye. Katika makala hii, tutazungumzia baadhi ya njia hizo.

Uhitaji wa Unyenyekevu

2, 3. Yesu alikuwa kielelezo kikamilifu cha unyenyekevu katika njia zipi?

2 Yesu alipowahimiza wanafunzi wake wafuate kielelezo alichoweka, alikuwa akizungumza hasa kuhusu unyenyekevu. Zaidi ya mara moja, alikuwa amewashauri wafuasi wake wawe wanyenyekevu, na katika usiku wa Nisani 14, alidhihirisha unyenyekevu wake kwa kuosha miguu ya mitume wake. Kisha Yesu akasema: “Ikiwa mimi, nijapokuwa Bwana na Mwalimu, niliiosha miguu yenu, ninyi pia mnapaswa kuoshana miguu.” (Yohana 13:14) Baadaye, aliwaambia mitume wake wafuate kielelezo alichoweka. Hicho kilikuwa kielelezo bora sana cha unyenyekevu.

3 Mtume Paulo anatuambia kwamba kabla ya Yesu kuja duniani, alikuwa “katika umbo la Mungu.” Hata hivyo, aliacha vyote na kuwa mwanadamu wa hali ya chini. Isitoshe, “alijinyenyekeza naye akawa mtiifu mpaka kifo, ndiyo, kifo juu ya mti wa mateso.” (Wafilipi 2:6-8) Ebu fikiria kidogo jambo hilo. Yesu, mtu wa pili kwa ukuu katika ulimwengu wote, alikubali kuwa mtu wa hali ya chini kuliko malaika, kuzaliwa akiwa kitoto hoi, kukua na kujitiisha chini ya wazazi wasio wakamilifu, na mwishowe kufa kama mhalifu aliyedharauliwa. (Wakolosai 1:15, 16; Waebrania 2:6, 7) Huo ni unyenyekevu ulioje! Je, tunaweza kuiga ‘mtazamo huo wa akili’ na kusitawisha “unyenyekevu wa akili” kama huo? (Wafilipi 2:3-5) Ndiyo, lakini si rahisi kufanya hivyo.

4. Ni mambo gani huwafanya wanadamu wawe na kiburi, na kwa nini kiburi ni hatari?

4 Kinyume cha unyenyekevu ni kiburi. (Methali 6:16-19) Kiburi kilimfanya Shetani aanguke. (1 Timotheo 3:6) Kiburi hukua kwa urahisi katika mioyo ya wanadamu, na kikishakua moyoni inakuwa vigumu kukiondoa. Watu huwa na kiburi kwa sababu ya nchi yao, rangi yao, mali zao, elimu yao, mafanikio yao, cheo chao katika jamii, sura yao, uwezo wao katika michezo, na mambo mengine mengi. Hata hivyo, mambo hayo yote si muhimu kwa Yehova. (1 Wakorintho 4:7) Na yakifanya tuwe na kiburi, yanaharibu uhusiano wetu pamoja naye. “Yehova yuko juu, hata hivyo yeye humwona mnyenyekevu; lakini yeye anamjua mwenye kiburi kutoka mbali tu.”—Zaburi 138:6; Methali 8:13.

Kuonyesha Unyenyekevu Tunapokuwa na Ndugu Zetu

5. Kwa nini wazee wanahitaji kuwa wanyenyekevu?

5 Hata yale tunayotimiza na mafanikio yetu katika utumishi wa Yehova na pia madaraka yetu kutanikoni hayapaswi kutufanya tuwe na kiburi. (1 Mambo ya Nyakati 29:14; 1 Timotheo 6:17, 18) Kwa kweli, kadiri tunavyokuwa na madaraka mazito zaidi ndivyo tunavyohitaji kuwa wanyenyekevu. Mtume Petro aliwahimiza wazee wasiwe ‘wakipiga ubwana juu ya wale ambao ni urithi wa Mungu, bali wawe vielelezo kwa kundi.’ (1 Petro 5:3) Wazee huwekwa rasmi kuwa watumishi na vielelezo, si mabwana wakubwa.—Luka 22:24-26; 2 Wakorintho 1:24.

6. Tunahitaji kuwa wanyenyekevu katika sehemu gani za maisha ya Kikristo?

6 Si wazee peke yao wanaohitaji kuonyesha unyenyekevu. Petro aliwaandikia hivi vijana ambao huenda wakawa na kiburi kwa sababu ya kuwa na akili nyepesi na miili yenye nguvu wanapolinganishwa na wazee: “Jifungeni unyenyekevu wa akili kuelekeana ninyi wenyewe, kwa sababu Mungu huwapinga wenye majivuno, lakini huwapa wanyenyekevu fadhili zisizostahiliwa.” (1 Petro 5:5) Naam, unyenyekevu kama wa Kristo ni muhimu kwa wote. Unyenyekevu unahitajiwa ili kuhubiri habari njema hasa tunapokabili ubaridi au uadui. Tunahitaji kuwa wanyenyekevu ili tukubali shauri au kurahisisha maisha yetu na hivyo kushiriki zaidi katika huduma. Isitoshe, tunahitaji unyenyekevu na pia ujasiri na imani tunapovumilia kuenezwa kwa habari za uwongo, tunaposhtakiwa mahakamani, au kuteswa kikatili.—1 Petro 5:6.

7, 8. Tunaweza kusitawisha unyenyekevu katika njia zipi?

7 Mtu anawezaje kushinda kiburi na kujiendesha ‘kwa unyenyekevu wa akili akiwaona wengine kuwa bora’ kuliko yeye? (Wafilipi 2:3) Anahitaji kujiona kama vile Yehova anavyomwona. Yesu alieleza mtazamo tunaopaswa kuwa nao aliposema: “Ninyi, pia, wakati mmefanya mambo yote mliyoagizwa, semeni, ‘Sisi ni watumwa wasiofaa kitu. Jambo ambalo tumefanya ndilo tulilopaswa kufanya.’” (Luka 17:10) Kumbuka kwamba hakuna jambo tunaloweza kufanya ambalo linaweza kulinganishwa na yale ambayo Yesu alifanya. Hata hivyo, Yesu alikuwa mnyenyekevu.

8 Isitoshe, tunaweza kumwomba Yehova atusaidie kusitawisha maoni yanayofaa kujihusu. Kama mtunga-zaburi, tunaweza kusali hivi: “Unifundishe wema, kuwa na akili na ujuzi, kwa maana nimeonyesha imani katika amri zako.” (Zaburi 119:66) Yehova atatusaidia kusitawisha maoni yanayofaa, yaliyosawazika kujihusu, naye atatubariki kwa kuwa wanyenyekevu. (Methali 18:12) Yesu alisema: “Yeyote yule anayejiinua atanyenyekezwa, na yeyote yule anayejinyenyekeza atainuliwa.”—Mathayo 23:12.

Maoni Yanayofaa Kuhusu Yaliyo Sawa na Yaliyo Makosa

9. Yesu alionaje yaliyo sawa na yaliyo makosa?

9 Licha ya kuishi kwa miaka 33 kati ya watu wasio wakamilifu, Yesu aliendelea ‘kuwa bila dhambi.’ (Waebrania 4:15) Kwa kweli, alipokuwa akitabiri kuhusu Masihi, mtunga-zaburi alisema hivi: “Umependa uadilifu nawe unachukia uovu.” (Zaburi 45:7; Waebrania 1:9) Wakristo hujitahidi kumwiga Yesu katika jambo hilo pia. Wanajua kutofautisha yaliyo sawa na yaliyo makosa, nao huchukia yaliyo makosa na kupenda yaliyo sawa. (Amosi 5:15) Hilo huwasaidia kushinda maelekeo yao ya asili yenye dhambi.—Mwanzo 8:21; Waroma 7:21-25.

10. Tukitenda “mambo maovu” bila kutubu, tutakuwa tukionyesha mtazamo gani?

10 Yesu alimwambia hivi Farisayo Nikodemo: “Yule ambaye huzoea kufanya mambo maovu huchukia nuru na haji kwenye nuru, ili matendo yake yasipate kukaripiwa. Lakini yule ambaye hufanya yaliyo ya kweli huja kwenye nuru, ili matendo yake yapate kufunuliwa kuwa tayari yamefanywa kupatana na Mungu.” (Yohana 3:20, 21) Fikiria: Yohana alimtambulisha Yesu kuwa “nuru ya kweli ambayo humpa nuru mtu wa kila namna.” (Yohana 1:9, 10) Hata hivyo, Yesu alisema kwamba tukizoea kufanya “mambo maovu,” yaani, mambo mabaya yasiyokubaliwa na Mungu, tunachukia nuru. Je, unaweza kuwazia ukimchukia Yesu na viwango vyake? Lakini hivyo ndivyo watu wanaozoea kutenda dhambi bila kutubu wanavyofanya. Labda hawafikiri kwamba wanamchukia Yesu na viwango vyake, lakini ni wazi kwamba Yesu anafikiri hivyo.

Jinsi ya Kusitawisha Maoni Kama ya Yesu Kuhusu Yaliyo Sawa na Yaliyo Makosa

11. Ni nini kinachohitajiwa ili tusitawishe maoni kama ya Yesu kuhusu yaliyo sawa na yaliyo makosa?

11 Tunahitaji kuelewa waziwazi maoni ya Yehova kuhusu yale yaliyo sawa na yaliyo makosa. Tunapata uelewaji huo tu kwa kujifunza Neno la Mungu, Biblia. Tunapojifunza, tunahitaji kusali hivi kama mtunga-zaburi: “Nijulishe njia zako, Ee Yehova; nifundishe mapito yako mwenyewe.” (Zaburi 25:4) Hata hivyo, kumbuka kwamba Shetani ni mdanganyifu. (2 Wakorintho 11:14) Anaweza kufanya lililo kosa lionekane kuwa lenye kukubalika kwa Mkristo asiyejihadhari. Hivyo, tunahitaji kutafakari sana mambo tunayojifunza na kutii shauri la “mtumwa mwaminifu na mwenye busara.” (Mathayo 24:45-47) Funzo, sala, na kutafakari mambo tunayojifunza kutatusaidia tuwe wakomavu na kuwa kati ya wale ambao “kwa kutumia, nguvu zao za ufahamu zimezoezwa kutofautisha yaliyo sawa na yaliyo makosa pia.” (Waebrania 5:14) Kisha tutakuwa na mwelekeo wa kuchukia yaliyo makosa na kupenda yaliyo sawa.

12. Ni shauri gani la Biblia hutusaidia tujiepushe na uasi-sheria?

12 Tukichukia yaliyo makosa, hatutaruhusu tamaa ya mabaya ikue ndani ya mioyo yetu. Mtume Yohana aliandika hivi miaka mingi baada ya kifo cha Yesu: “Msiwe mkiupenda ulimwengu au vitu vilivyo katika ulimwengu. Yeyote akiupenda ulimwengu, kumpenda Baba hakumo ndani yake; kwa sababu kila kitu kilicho katika ulimwengu—tamaa ya mwili na tamaa ya macho na mtu kujionyesha mali yake maishani—hakitokani na Baba, bali hutokana na ulimwengu.”—1 Yohana 2:15, 16.

13, 14. (a) Kwa nini kupenda vitu vya ulimwengu ni hatari kwa Wakristo? (b) Tunawezaje kuepuka kusitawisha upendo wa vitu vya ulimwengu?

13 Huenda wengine wakafikiri kwamba si kila kitu ulimwenguni ni kibaya. Hata ingawa hilo ni kweli, ulimwengu na vitu vyake vyenye kuvutia vinaweza kutukengeusha kwa urahisi tuache kumtumikia Yehova. Na hakuna chochote katika ulimwengu huu ambacho kinaweza kutusaidia tumkaribie Mungu. Hivyo, tukisitawisha upendo wa vitu vya ulimwengu, hata vitu ambavyo huenda si vibaya, tutakuwa hatarini. (1 Timotheo 6:9, 10) Isitoshe, kwa kweli mambo mengi katika ulimwengu ni mabaya na yanaweza kutupotosha. Ikiwa tunatazama sinema au vipindi vya televisheni vinavyoonyesha jeuri, ufuatiaji wa vitu vya kimwili, au uasherati, tunaweza kuanza kukubali mambo hayo na baadaye kushawishiwa nayo. Tukishirikiana na watu ambao kusudi lao kuu ni kuboresha hali yao ya maisha au wanaotafuta nafasi za kuanzisha biashara, mambo hayo yanaweza kuanza kuwa muhimu zaidi kwetu pia.—Mathayo 6:24; 1 Wakorintho 15:33.

14 Kwa upande mwingine, ikiwa tunapendezwa sana na Neno la Yehova, hatutavutiwa sana na “tamaa ya mwili na tamaa ya macho na mtu kujionyesha mali yake maishani.” Isitoshe, ikiwa tutashirikiana na wale wanaotanguliza Ufalme wa Mungu, tutakuwa kama wao na kupenda mambo wanayopenda na kuepuka mambo wanayojiepusha nayo.—Zaburi 15:4; Methali 13:20.

15. Kama ilivyokuwa kwa habari ya Yesu, kupenda uadilifu na kuchukia uasi-sheria kutatuimarishaje?

15 Kuchukia uasi-sheria na kupenda uadilifu kulimsaidia Yesu aendelee kukaza macho yake kwenye “shangwe iliyowekwa mbele yake.” (Waebrania 12:2) Hata sisi tunaweza kufanya hivyo. Tunajua kwamba “ulimwengu unapitilia mbali na pia tamaa yake.” Raha yoyote inayotokana na ulimwengu huu ni ya muda tu. Hata hivyo, “yeye anayefanya mapenzi ya Mungu anadumu milele.” (1 Yohana 2:17) Kwa sababu Yesu alifanya mapenzi ya Mungu, aliwafungulia wanadamu njia ya kupata uzima wa milele. (1 Yohana 5:13) Sote na tumwige na hivyo kunufaika na utimilifu wake.

Kuvumilia Mateso

16. Kwa nini Yesu aliwahimiza wafuasi wake wapendane?

16 Yesu alitaja njia nyingine ambayo wanafunzi wake wangemwiga, akisema: “Hii ndiyo amri yangu, kwamba mpendane kama vile nilivyowapenda ninyi.” (Yohana 15:12, 13, 17) Wakristo wana sababu nyingi za kuwapenda ndugu zao. Katika pindi hiyo, Yesu alikuwa akifikiria hasa chuki ambayo wanafunzi wake wangekabili kutoka katika ulimwengu. Alisema: “Ikiwa ulimwengu unawachukia ninyi, mnajua kwamba umenichukia mimi kabla ya kuwachukia ninyi. . . . Mtumwa si mkuu kuliko bwana wake. Ikiwa wamenitesa mimi, watawatesa ninyi pia.” (Yohana 15:18, 20) Naam, hata wanapoteswa, Wakristo ni kama Yesu. Wanahitaji kusitawisha kifungo cha upendo chenye nguvu kitakachowasaidia kuvumilia chuki hiyo.

17. Kwa nini ulimwengu unawachukia Wakristo wa kweli?

17 Kwa nini ulimwengu ungewachukia Wakristo? Kwa sababu kama Yesu, wao “si sehemu ya ulimwengu.” (Yohana 17:14, 16) Hawajiungi na jeshi wala kujihusisha na mambo ya kisiasa, nao hutii kanuni za Biblia kuhusu utakatifu wa uhai na kufuata viwango vya juu vya maadili. (Matendo 15:28, 29; 1 Wakorintho 6:9-11) Malengo yao makuu ni mambo ya kiroho wala si ya kimwili. Wanaishi katika ulimwengu, lakini kama Paulo alivyoandika, ‘hawautumii kwa ukamili.’ (1 Wakorintho 7:31) Ni kweli kwamba wengine wamevutiwa na viwango vya juu vya Mashahidi wa Yehova. Lakini Mashahidi wa Yehova hawalegezi msimamo wao ili kuvutia au kukubaliwa na wengi. Kwa sababu hiyo, wengi katika ulimwengu hawawaelewi, na wengi wanawachukia.

18, 19. Kwa kufuata kielelezo cha Yesu, Wakristo hukabilianaje na upinzani na mateso?

18 Mitume wa Yesu waliona chuki kubwa ya ulimwengu wakati Yesu alipokamatwa na kuuawa, nao waliona jinsi Yesu alivyokabili chuki hiyo. Wapinzani wa kidini wa Yesu walikuja kumkamata katika bustani ya Gethsemane. Petro alijaribu kumlinda Yesu kwa kutumia upanga, lakini Yesu akamwambia: “Rudisha upanga wako mahali pake, kwa maana wale wote wanaouchukua upanga wataangamia kwa upanga.” (Mathayo 26:52; Luka 22:50, 51) Katika nyakati za zamani, Waisraeli walipigana na adui zao kwa kutumia upanga. Lakini sasa mambo yalikuwa yamebadilika. Ufalme wa Mungu haukuwa “sehemu ya ulimwengu huu” nao haukuwa na mipaka ya kitaifa iliyohitaji kulindwa. (Yohana 18:36) Karibuni Petro angekuwa sehemu ya taifa la kiroho ambalo washiriki wake wangekuwa raia mbinguni. (Wagalatia 6:16; Wafilipi 3:20, 21) Kwa hiyo, kuanzia wakati huo na kuendelea, wafuasi wa Yesu wangekabili chuki na mateso kama Yesu alivyofanya, yaani, bila woga na kwa amani. Wakiwa na uhakika, wangeacha mambo yote mikononi mwa Yehova na kumtegemea awape nguvu za kuvumilia.—Luka 22:42.

19 Miaka kadhaa baadaye, Petro aliandika hivi: “Kristo aliteseka kwa ajili yenu, akiwaachia ninyi kielelezo ili mfuate hatua zake kwa ukaribu. . . . Alipokuwa akitukanwa, hakujibu kwa matukano. Alipokuwa akiteseka, hakutoa vitisho, bali aliendelea kujiweka mkononi mwa yule ambaye anahukumu kwa uadilifu.” (1 Petro 2:21-23) Kama vile Yesu alivyoonya, kwa miaka mingi, Wakristo wameteswa vikali. Kama ilivyokuwa katika karne ya kwanza, leo Wakristo wamefuata kielelezo cha Yesu na kuvumilia kwa uaminifu mambo mengi na hivyo kuonyesha kwamba wanadumisha utimilifu wao kwa amani. (Ufunuo 2:9, 10) Sote na tudumishe utimilifu wetu kwa amani tunapokabili mateso.—2 Timotheo 3:12.

“Mvaeni Bwana Yesu Kristo”

20-22. Wakristo ‘humvaa Bwana Yesu Kristo’ katika njia gani?

20 Paulo aliliandikia hivi kutaniko la Roma: “Mvaeni Bwana Yesu Kristo, na msiwe mkipanga kimbele kwa ajili ya tamaa za mwili.” (Waroma 13:14) Wakristo humvaa Yesu kama nguo kwa njia ya mfano. Wao hujitahidi sana kuonyesha sifa na matendo ya Bwana wao kadiri wawezavyo wakiwa wanadamu wasio wakamilifu.—1 Wathesalonike 1:6.

21 Tutafanikiwa ‘kumvaa Bwana Yesu Kristo’ ikiwa tutayafahamu maisha ya Bwana na kujitahidi kuishi jinsi alivyoishi. Tunaiga unyenyekevu wake, upendo wake wa uadilifu, chuki yake kuelekea uasi-sheria, upendo wake kwa ndugu zake, kutokuwa sehemu ya ulimwengu, na jinsi alivyovumilia mateso kwa subira. ‘Hatupangi kimbele kwa ajili ya tamaa za mwili,’ yaani, hatufanyi miradi ya kimwili au kutosheleza tamaa zetu za mwili kuwa lengo kuu maishani. Badala yake, tunapofanya uamuzi au kutatua tatizo fulani, sisi huuliza: ‘Yesu angefanyaje katika hali kama hii? Yeye angetaka nifanye nini?’

22 Mwishowe, tunamwiga Yesu kwa “kuhubiri habari njema” kwa bidii. (Mathayo 4:23; 1 Wakorintho 15:58) Pia katika njia hiyo, Wakristo hufuata kielelezo kilichowekwa na Yesu, na makala inayofuata itazungumzia jinsi wanavyofanya hivyo.

Je, Unaweza Kueleza?

• Kwa nini ni lazima Mkristo awe mnyenyekevu?

• Tunawezaje kusitawisha maoni yanayofaa kuhusu mambo yaliyo sawa na yaliyo makosa?

• Ni katika njia gani Wakristo humwiga Yesu wanapokabili upinzani na mateso?

• Inawezekanaje ‘kumvaa Bwana Yesu Kristo’?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 7]

Yesu aliweka kielelezo kikamilifu cha unyenyekevu

[Picha katika ukurasa wa 8]

Kila sehemu ya maisha ya Mkristo, kutia ndani kuhubiri, inahitaji unyenyekevu

[Picha katika ukurasa wa 9]

Shetani anaweza kufanya vitumbuizo visivyofaa vionekane kuwa vyenye kukubalika kwa Mkristo

[Picha katika ukurasa wa 10]

Kuwapenda ndugu zetu kutatuimarisha wakati wa upinzani