Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Jihadhari na Desturi Zisizompendeza Mungu

Jihadhari na Desturi Zisizompendeza Mungu

Jihadhari na Desturi Zisizompendeza Mungu

KATIKA ua mdogo, kuna jeneza lililo wazi chini ya jua kali la Afrika. Waombolezaji wanapopita kando yake ili kuonyesha huzuni yao, mzee mmoja anasimama. Akiwa na macho yaliyojaa majonzi, anainama karibu na uso wa mfu huyo na kuanza kusema: “Kwa nini hukuniambia kuwa unaenda? Kwa nini uliniacha hivi? Kwa kuwa sasa umerudi, je, utaendelea kunisaidia?”

Katika sehemu nyingine ya Afrika, mtoto anazaliwa. Hakuna mtu anayeruhusiwa kumwona mtoto huyo. Kwa kawaida, mtoto huwekwa ndani ya nyumba nao watu wasio washiriki wa familia hawaruhusiwi kumwona mpaka baada ya sherehe ya kumpa jina.

Kwa watu fulani, kusema na mfu au kumficha mtoto aliyezaliwa asionwe na wengine huenda ikaonekana kuwa tabia ya kiajabu-ajabu. Hata hivyo, katika tamaduni na jamii fulani, tabia na maoni ya watu kuelekea kifo na kuzaliwa huathiriwa na imani thabiti kwamba wafu wako hai na wana ufahamu.

Imani hiyo ni yenye nguvu sana hivi kwamba imekuwa sehemu muhimu ya mila na desturi zinazohusu karibu sehemu zote za maisha. Kwa mfano, watu wengi huamini kwamba hatua muhimu maishani mwa mtu, yaani, kuzaliwa, kubalehe, kufunga ndoa, kuzaa, na kifo ni hatua za kutoka hali moja ya maisha kuelekea makao ya roho ya wazazi waliokufa. Inaaminika kwamba huko, mfu huendelea kuwa na uvutano wenye nguvu katika maisha ya wale aliowaacha, naye anaweza kuendelea kuishi na kuzaliwa upya.

Ili kuhakikisha kwamba anapita salama kutoka hali moja ya maisha hadi ile nyingine, desturi na mila mbalimbali hufanywa. Desturi hizo zinaathiriwa na imani ya kwamba kitu fulani ndani yetu huendelea kuishi baada ya kifo. Wakristo wa kweli huepuka desturi yoyote ile inayohusiana na imani hiyo. Kwa nini?

Wafu Wako Katika Hali Gani?

Biblia inaeleza wazi hali ya wafu. Inasema hivi: “Walio hai wanajua kwamba watakufa; lakini wafu, hawajui lolote kamwe . . . Upendo wao na chuki yao na wivu wao tayari zimepotea . . . Hakuna kazi, wala utungaji wala ujuzi wala hekima katika Kaburi, mahali unapokwenda.” (Mhubiri 9:5, 6, 10) Waabudu wa kweli wa Mungu wamethamini sana ukweli huo wa msingi wa Biblia. Wameelewa kwamba nafsi inaweza kufa na kuharibiwa. (Ezekieli 18:4) Pia, wamejua kwamba roho za wafu haziendelei kuishi. (Zaburi 146:4) Nyakati za kale, Yehova aliwaamuru kwa mkazo watu wake wajitenga kabisa na desturi au mila zozote ambazo zilihusiana na imani ya kwamba wafu wana ufahamu nao wanaweza kuwaathiri walio hai.—Kumbukumbu la Torati 14:1; 18:9-13; Isaya 8:19, 20.

Vivyo hivyo, Wakristo wa karne ya kwanza waliepuka desturi au mila yoyote ambayo ilihusiana na mafundisho ya dini ya uwongo. (2 Wakorintho 6:15-17) Leo, Mashahidi wa Yehova, wawe wametoka katika jamii, kabila, au malezi gani, wamekataa mila na desturi ambazo zinahusiana na mafundisho ya uwongo kwamba kitu fulani huendelea kuishi baada ya mtu kufa.

Tukiwa Wakristo, ni nini kinachoweza kutuongoza kuamua ikiwa tutafuata desturi fulani au la? Ni lazima tufikirie kwa makini kama desturi hiyo ina uhusiano wowote na mafundisho yasiyopatana na Maandiko kama vile imani ya kwamba roho za wafu huwaathiri walio hai. Zaidi ya hayo, tunapaswa kufikiria ikiwa kushiriki kwetu katika desturi au sherehe kama hizo kutawakwaza wengine wanaojua yale ambayo Mashahidi wa Yehova wanaamini na kufundisha. Tukiwa na hayo akilini, acheni tuchunguze mambo mawili ambayo huwahangaisha watu wengi, yaani, kuzaliwa na kifo.

Sherehe za Kuzaliwa na Kumpa Mtoto Jina

Desturi nyingi zinazohusiana na kuzaliwa kwa mtoto zinafaa. Hata hivyo, katika maeneo ambako kuzaliwa kwa mtoto huonwa kuwa hatua ya kutoka katika makao ya roho ya wazazi waliokufa hadi kwenye ulimwengu wa wanadamu, Wakristo wa kweli wanapaswa kuwa waangalifu. Kwa mfano, katika sehemu fulani za Afrika, mtoto aliyezaliwa huwekwa ndani ya nyumba naye hapewi jina mpaka kipindi fulani cha wakati kipite. Ingawa kipindi hicho cha kungojea huenda kikatofautiana kulingana na mahali, mwishoni mwa kipindi hicho kunakuwa na sherehe ya kumpa mtoto jina, na wakati huo mtoto hutolewa nje na kuonyeshwa rasmi kwa watu wa ukoo na marafiki. Wakati huo, jina la mtoto hutangazwa rasmi.

Kikieleza maana ya desturi hiyo, kitabu Ghana—Understanding the People and Their Culture kinasema: “Wakati wa siku saba za kwanza za maisha yake, mtoto huonwa kuwa katika ‘safari’ ya kutoka ulimwengu wa roho na kuelekea kwenye maisha duniani. . . . Kwa kawaida, mtoto huwekwa ndani ya nyumba nao watu wasio washiriki wa familia hawaruhusiwi kumwona.”

Kwa nini kuna kipindi cha kungoja kabla ya sherehe ya kumpa mtoto jina? Kitabu Ghana in Retrospect kinaeleza: “Kabla ya siku ya nane, mtoto haonwi kuwa binadamu. Anahusianishwa kwa kadiri fulani na ulimwengu wa roho ambako ametoka.” Kitabu hicho kinaendelea kusema: “Kwa kuwa jina ndilo humfanya mtoto awe binadamu, wakati mume na mke wanapohofu kwamba mtoto wao atakufa, kwa kawaida hawatampa jina mpaka wawe na hakika kwamba ataishi. . . . Kwa hiyo, sherehe hiyo ya kutoka hali moja ya maisha hadi nyingine, ambayo nyakati nyingine huitwa kumtoa mtoto nje, huonwa kuwa yenye matokeo makubwa kwa mtoto na wazazi wake. Hiyo ndiyo sherehe ambayo humwingiza mtoto katika ushirika au ulimwengu wa wanadamu.”

Kwa kawaida, mzee wa ukoo ndiye husimamia sherehe hiyo ya kumpa mtoto jina. Mambo yanayofanyika wakati wa sherehe hiyo hutofautiana kulingana na mahali, lakini mara nyingi hutia ndani kumwagwa kwa toleo la kinywaji, kusali kwa roho za wazazi waliokufa ili kuwashukuru kwamba mtoto amefika salama, na mila na desturi nyingine.

Kutangazwa kwa jina la mtoto ndilo tukio muhimu la sherehe hiyo. Ingawa wazazi ndio wenye daraka la kumpa mtoto wao jina, mara nyingi watu wengine wa ukoo huwa na uvutano mkubwa kuhusu jina atakalopewa mtoto. Huenda majina mengine yakawa na maana yenye fumbo katika lugha ya kienyeji, kama vile “alienda na akarudi,” “Mama amerudi mara ya pili,” au “Baba amerudi tena.” Majina mengine yana maana ambayo imekusudiwa kuwazuia wazazi waliokufa wasimrudishe tena mtoto aliyezaliwa katika ulimwengu wa wafu.

Bila shaka, hakuna ubaya wowote katika kufurahia kuzaliwa kwa mtoto. Kumpa mtoto jina la mtu mwingine na kumpa jina ambalo linahusiana na hali za kuzaliwa kwake ni desturi zinazokubalika, na kuamua wakati wa kumpa mtoto jina ni uamuzi wa kibinafsi. Hata hivyo, Wakristo wanaotaka kumpendeza Mungu huwa waangalifu kuepuka desturi au sherehe yoyote ambayo itafanya watu wafikiri kwamba wanakubaliana na maoni ya kwamba mtoto aliyezaliwa ni “mgeni” anayepita kutoka ulimwengu wa roho wa wazazi waliokufa hadi ulimwengu wa walio hai.

Isitoshe, ingawa wengi katika jamii huona sherehe ya kumpa mtoto jina kuwa desturi muhimu ya kutoka hali moja ya maisha hadi ile nyingine, Wakristo wanapaswa kufikiria dhamiri za watu wengine na jinsi watu wasioamini watakavyoliona jambo hilo. Kwa mfano, wengine wangefikia mkataa gani ikiwa familia ya Kikristo ingemficha mtoto wao asionekane na watu hadi sherehe ya kumpa jina ifanywe? Watu wangekuwa na maoni gani ikiwa mtoto angepewa majina yanayopingana na madai yao ya kuwa walimu wa ile kweli ya Biblia?

Hivyo, wanapoamua jinsi na wakati wa kuwapa watoto wao majina, Wakristo wanajitahidi ‘kufanya mambo yote kwa utukufu wa Mungu’ ili wasiwakwaze wengine. (1 Wakorintho 10:31-33) Wao ‘hawaweki kando amri ya Mungu kusudi wabaki na mapokeo’ ambayo yamekusudiwa hasa kuwaheshimu wafu. Badala yake, wanamheshimu na kumtukuza Yehova, Mungu aliye hai.—Marko 7:9, 13.

Kupita Kutoka Kifo Hadi Uhai

Sawa na kuzaliwa, watu wengi huona kifo kuwa njia ya kutoka hali moja ya maisha hadi nyingine; mfu anahama kutoka ulimwengu wa wanadamu hadi makao yasiyoonekana ya roho za wafu. Wengi huamini kwamba wasipofanya desturi na mila fulani za mazishi mtu anapokufa, roho za wazazi waliokufa ambao hudhaniwa kuwa wenye nguvu za kuwaadhibu au kuwathawabisha walio hai, zitakasirika. Imani hiyo inaathiri sana jinsi mazishi hupangwa na kuendeshwa.

Mazishi ambayo yanakusudiwa kumtuliza mfu mara nyingi hutia ndani mambo mengi yanayohusu hisia, yaani, kulia kupita kiasi na kupiga kelele mbele ya maiti na pia kufanya sherehe zenye shangwe baada ya mazishi. Mara nyingi katika sherehe hizo za mazishi, watu hula bila kujizuia, hulewa, na kucheza muziki kwa sauti kubwa. Sherehe za mazishi huonwa kuwa muhimu sana hivi kwamba hata familia zilizo maskini sana hujitahidi kukusanya pesa za kutosha ili kuandaa “mazishi yanayofaa” hata ingawa huenda hilo likatokeza shida na madeni.

Kwa miaka mingi, Mashahidi wa Yehova wamefunua waziwazi desturi za mazishi zinazopingana na Biblia. * Desturi hizo zinatia ndani makesha, kumwagwa kwa kinywaji, kusema na mfu na kumwomba mambo fulani, sherehe za kukumbuka siku za mazishi, desturi nyingine zinazotegemea imani ya kwamba kitu fulani ndani ya mtu huendelea kuishi baada ya kifo. Desturi hizo ambazo hazimletei Mungu heshima ni “najisi,” na “udanganyifu mtupu” unaotegemea “pokeo la wanadamu” wala si kweli ya Neno la Mungu.—Isaya 52:11; Wakolosai 2:8.

Mkazo wa Kufuata Desturi

Imekuwa vigumu kwa wengi kuepuka desturi, hasa katika nchi ambako kuheshimu wafu huonwa kuwa jambo muhimu sana. Kwa sababu ya kutofuata desturi hizo, Mashahidi wa Yehova hutiliwa shaka au hushutumiwa kuwa wanaojitenga na watu na wasioheshimu wafu. Uchambuzi na mkazo mkali umefanya Wakristo fulani waogope kuwa tofauti, ingawa wana uelewaji sahihi wa kweli ya Biblia. (1 Petro 3:14) Baadhi yao wamehisi kwamba desturi hizo ni sehemu ya utamaduni wao na kwamba haziwezi kuepukwa kabisa. Hata hivyo, wengine wamefikiri kwamba kukataa kufuata desturi huenda kukawafanya watu wa Mungu wachukiwe na jumuiya.

Hatupendi kuwaudhi wengine bila sababu. Hata hivyo, Biblia hutuonya kwamba kusimama thabiti upande wa kweli kutatufanya tuchukiwe na ulimwengu uliotengwa mbali na Mungu. (Yohana 15:18, 19; 2 Timotheo 3:12; 1 Yohana 5:19) Tunachukua msimamo huo kwa hiari tukijua kwamba ni lazima tuwe tofauti na wale walio katika giza la kiroho. (Malaki 3:18; Wagalatia 6:12) Kama vile Yesu alivyompinga Shetani alipomshawishi kufanya jambo lisilompendeza Mungu, sisi pia hupinga mkazo wa kufanya mambo yasiyompendeza Mungu. (Mathayo 4:3-7) Badala ya kuwaogopa wanadamu, Wakristo wa kweli wanahangaikia kwanza kumpendeza Yehova Mungu na kumheshimu yeye kuwa Mungu wa kweli. Wanafanya hivyo kwa kutolegeza viwango vya Biblia vya ibada safi kwa sababu ya mkazo kutoka kwa wengine.—Methali 29:25; Matendo 5:29.

Kumheshimu Yehova kwa Jinsi Tunavyowaona Wafu

Ni jambo la kawaida kuumia sana kihisia mtu tumpendaye anapokufa. (Yohana 11:33, 35) Kumkumbuka mpendwa aliyekufa na kumfanyia mazishi ya heshima ni njia inayofaa ya kuonyesha upendo wetu. Hata hivyo, Mashahidi wa Yehova huvumilia huzuni kubwa inayosababishwa na kifo bila kujiingiza katika desturi zozote zisizompendeza Mungu. Hilo si jambo rahisi kwa wale ambao wamelelewa katika tamaduni ambako watu huogopa sana wafu. Inaweza kuwa vigumu kudumisha usawaziko tunapohisi uchungu unaotokana na kifo cha mtu wetu wa karibu. Hata hivyo, Wakristo waaminifu huimarishwa na Yehova, “Mungu wa faraja yote,” nao wananufaika na msaada wenye upendo kutoka kwa waamini wenzao. (2 Wakorintho 1:3, 4) Imani yao yenye nguvu kwamba wafu wasiojua lolote na ambao wako katika kumbukumbu la Mungu wataishi tena siku fulani, huwapa Wakristo wa kweli kila sababu ya kujitenga kabisa na desturi za mazishi zisizo za Kikristo ambazo zinapinga ukweli kuhusu ufufuo.

Je, hatufurahi kwamba Yehova ametuita “kutoka katika giza kuingia katika nuru yake ya ajabu”? (1 Petro 2:9) Tunaposhangilia kuzaliwa kwa mtoto na kuvumilia huzuni ya kifo, na tuazimie kufanya yaliyo sawa na upendo wetu mwingi kwa Yehova Mungu utuchochee sikuzote ‘kuendelea kutembea kama watoto wa nuru.’ Na tusiruhusu kamwe kuchafuliwa kiroho na desturi zisizo za Kikristo ambazo hazimpendezi Mungu.—Waefeso 5:8.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 23 Tafadhali ona broshua Roho za Wafu—Je! Zaweza Kukusaidia au Kukuumiza? Je! Ziko Kweli? na Je, Umeipata Barabara Inayoongoza Kwenye Uhai wa Milele? zilizochapishwa na Mashahidi wa Yehova.