Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Jinsi ya Kuwalinda Watoto Wako Kupitia Hekima ya Mungu

Jinsi ya Kuwalinda Watoto Wako Kupitia Hekima ya Mungu

Jinsi ya Kuwalinda Watoto Wako Kupitia Hekima ya Mungu

KILA siku miili yetu hupigana. Lazima ipigane na vijidudu, vimelea, na virusi vingi. Tunashukuru kwamba wengi wetu tumerithi mfumo wa kinga ambao hutulinda na mashambulizi kama hayo na kutukinga na maradhi mengi ya kuambukiza.

Vivyo hivyo, Wakristo wanapaswa kupigana na maoni na kanuni zisizo za Kimaandiko na pia dhidi ya uvutano unaoweza kuharibu afya yetu ya kiroho. (2 Wakorintho 11:3) Ili kupinga mashambulizi hayo ya kila siku dhidi ya mioyo na akili zetu, tunahitaji kusitawisha uwezo wa kujikinga tusishambuliwe kiroho.

Uwezo wa kujikinga tusishambuliwe kiroho ni muhimu hasa kwa watoto wetu kwa kuwa hawazaliwi wakiwa na uwezo huo ambao unaweza kupinga roho ya ulimwengu. (Waefeso 2:2) Watoto wanapokua, ni muhimu wazazi wawasaidie kusitawisha uwezo wa kujikinga ili wasishambuliwe kiroho. Uwezo huo unategemea nini? Biblia inasema: “Yehova mwenyewe anatoa hekima; . . . atailinda njia ya washikamanifu wake.” (Methali 2:6, 8) Hekima ya Mungu inaweza kulinda njia ya vijana ambao huenda wakaathiriwa na mashirika mabaya, msongo wa marika, au vitumbuizo visivyofaa. Wazazi wanawezaje kufuata mwongozo wa Yehova na kukazia hekima ya Mungu?

Kutafuta Ushirika Wenye Kujenga

Ni jambo linaloeleweka kwamba, vijana hupenda kushirikiana na vijana wenzao, lakini kushirikiana tu na watu wengine wasio na ujuzi hakutafanya mtu awe na hekima ya Mungu. “Ujinga umefungwa pamoja na moyo wa mvulana,” yaonya methali. (Methali 22:15) Hivyo basi, wazazi fulani wamewasaidiaje watoto wao kutumia hekima ya Mungu kwa habari ya mashirika?

Baba mmoja anayeitwa Don * alisema: “Wavulana wetu walitumia wakati mwingi pamoja na marika wao, lakini mara nyingi walitumia muda huo nyumbani mwetu, tukiwepo. Sikuzote nyumba yetu ilikuwa wazi kuwapokea vijana wengi daima ambao tuliwalisha na kufanya wahisi kuwa wamestarehe. Tulifurahi kuvumilia makelele na vurugu katika nyumba yetu ili watoto wetu wafurahie mazingira salama.”

Brian na Mary wana watoto watatu wazuri lakini wanakiri kwamba haijawa rahisi kuwalea. Walisema: “Katika kutaniko letu, hakukuwa na vijana wengi wanaokaribia umri wa miaka 20 ambao wangeshirikiana na binti yetu Jane. Hata hivyo, alikuwa na rafiki mmoja aliyeitwa Susan, ambaye alikuwa kijana mwenye urafiki na mchangamfu. Ingawa hivyo, wazazi wake walimpa uhuru mwingi zaidi kuliko ule tuliompa Jane. Susan aliruhusiwa kurudi nyumbani usiku zaidi kuliko Jane, kuvaa nguo fupi zaidi, kusikiliza muziki usiofaa, na kutazama sinema zisizofaa. Kwa muda mrefu, haikuwa rahisi Jane kuelewa maoni yetu. Jane aliona wazazi wa Susan kuwa wenye kuelewa mambo zaidi, hali alituona sisi kuwa wakali mno. Jane aling’amua tu kwamba uthabiti wetu ulimlinda wakati Susan alipojikuta matatani. Tulifurahi sana kwa kutolegeza msimamo wetu kuhusu mambo tuliyoona kuwa yanamfaa binti yetu.”

Kama Jane, vijana wengi wamejifunza hekima ya kutafuta mwongozo wa wazazi wao kuhusiana na mashirika. “Sikio linalosikiliza karipio la uzima hukaa kati ya watu wenye hekima,” yasema methali. (Methali 15:31) Hekima ya Mungu huwaongoza vijana watafute marafiki wanaojenga.

Kukabiliana na Msongo wa Kuwa Kama Wengine

Msongo wa marika unahusiana sana na mashirika. Uwezo wa watoto wetu wa kujikinga huathiriwa daima na msongo wa kuwa kama wengine. Kwa kuwa ni kawaida ya vijana kutaka kukubaliwa na marika wao, msongo wa marika unaweza kufanya wawe kama walimwengu.—Methali 29:25.

Biblia inatukumbusha kwamba “ulimwengu unapitilia mbali na pia tamaa yake.” (1 Yohana 2:17) Hivyo, wazazi hawapaswi kuwaruhusu watoto wao waathiriwe kupita kiasi na maoni ya ulimwengu. Wanawezaje kuwasaidia watoto wao wafikiri kwa njia ya Kikristo?

“Sikuzote binti yangu alitaka kuvaa mavazi kama ya vijana wengine,” akasema Richard. “Kwa hiyo tulizungumza naye kuhusu faida na hasara za mambo aliyoomba kufanya. Hata kuhusiana na mitindo tuliyoona kuwa inafaa, tulifuata shauri tulilosikia miaka kadhaa iliyopita, ‘Mtu mwenye hekima hawi wa kwanza kufuata mtindo fulani mpya wala hawi wa mwisho kuuacha.’”

Mama mmoja anayeitwa Pauline alikabiliana na msongo wa marika kwa njia nyingine. Anakumbuka: “Nilipendezwa na mambo yaliyowapendeza watoto wangu na nilienda chumbani mwao kwa ukawaida ili kuzungumza nao. Kuwa na mazungumzo nao kwa muda mrefu kuliniwezesha kurekebisha mawazo yao na kuwasaidia wafikirie mambo kwa njia nyingine.”

Msongo wa marika utakuwepo daima, kwa hiyo yaelekea wazazi wataendelea kujitahidi ‘kupindua mawazo ya kilimwengu’ na kuwasaidia watoto wao wazifanye fikira zao ‘mateka ili zimtii Kristo.’ (2 Wakorintho 10:5) Lakini kwa ‘kudumu katika sala,’ wazazi na watoto wataimarishwa ili kumaliza kazi hii muhimu.—Waroma 12:12; Zaburi 65:2.

Uvutano Wenye Nguvu wa Vitumbuizo

Uvutano wa tatu ambao huenda wazazi wakauona kuwa mgumu kukabiliana nao ni vitumbuizo. Kwa kawaida, watoto hupenda kucheza. Pia watoto wengi wenye umri mkubwa hupenda kujifurahisha. (2 Timotheo 2:22) Lakini tamaa hiyo ikitoshelezwa kwa njia isiyo ya hekima inaweza kudhoofisha uwezo wa watoto wa kujikinga wasishambuliwe kiroho. Kwa kawaida hatari hutokea hasa katika njia mbili.

Kwanza, vitumbuizo vingi hudhihirisha viwango vya maadili vilivyopotoka vya ulimwengu. (Waefeso 4:17-19) Hata hivyo, kwa kawaida vitumbuizo hivyo hufanywa kwa njia yenye kusisimua na kuvutia. Hiyo hutokeza hatari kwa vijana ambao huenda wasione mitego hiyo.

Pili, muda unaotumiwa kujitumbuiza unaweza pia kusababisha matatizo. Wengine huona kujifurahisha kuwa jambo muhimu zaidi maishani na hivyo kutumia wakati wao mwingi na nguvu zao nyingi kufanya hivyo. Methali inaonya kwamba “si vizuri kula asali nyingi mno.” (Methali 25:27) Vivyo hivyo, vitumbuizo vinavyopita kiasi vitapunguza hamu ya kula chakula cha kiroho na kusababisha uvivu wa kiakili. (Methali 21:17; 24:30-34) Kufurahia ulimwengu huu kikamili kutazuia vijana ‘wasiushike uzima ulio wa kweli,’ yaani, uzima wa milele katika ulimwengu mpya wa Mungu. (1 Timotheo 6:12, 19) Wazazi wamekabilianaje na tatizo hilo?

Mari Carmen, mama ya binti watatu alisema: “Tulitaka binti zetu wawe na tafrija inayofaa na kujifurahisha. Kwa hiyo sikuzote tulifanya tafrija tukiwa familia, nao pia walishirikiana na marafiki kutanikoni. Lakini tulifanya tafrija kwa kiasi. Tulilinganisha tafrija na tamutamu—ni kitamu lakini si chakula kikuu. Walijifunza kuwa wafanyakazi nyumbani, shuleni, na kutanikoni.”

Don na Ruth walifanya mipango hususa ya kuwa na vitumbuizo. “Tulizoea kutenga siku ya Jumamosi kuwa siku ya familia,” wakaeleza. “Tulikuwa tukienda mahubiri asubuhi, tunaenda kuogelea alasiri, na kula chakula maalum jioni.”

Maelezo ya wazazi hao yanaonyesha manufaa ya kuwa na usawaziko katika kuandaa vitumbuizo vinavyofaa na kutoviruhusu vivuruge maisha ya Mkristo.—Mhubiri 3:4; Wafilipi 4:5.

Mtumaini Yehova

Bila shaka, inachukua miaka mingi kusitawisha uwezo wa kujikinga tusishambuliwe kiroho. Watoto hawawezi kupata kwa njia ya kimuujiza hekima ya Mungu ambayo itawachochea kumtumaini Baba yao wa mbinguni. Badala yake, lazima wazazi ‘waendelee kuwalea katika nidhamu na mwongozo wa akilini wa Yehova.’ (Waefeso 6:4) ‘Mwongozo huo wa akilini’ unamaanisha kuwasaidia watoto waone mambo kama Mungu anavyoyaona. Wazazi wanawezaje kutimiza jambo hilo?

Ili kufanikiwa, ni muhimu kuwa na funzo la Biblia la familia kwa ukawaida. Funzo hilo ‘hufunua macho ya watoto ili wapate kutazama mambo ya ajabu kutoka katika sheria ya Mungu.’ (Zaburi 119:18) Diego alichukua funzo la familia kwa uzito sana na hivyo akawasaidia watoto wake wamkaribie Yehova. “Nilijitayarisha kikamili kwa ajili ya funzo,” akasema. “Kwa kufanya utafiti katika vichapo vya Biblia, nilijifunza kuwasaidia watoto wangu wawaone watu wanaotajwa katika Biblia kuwa halisi. Niliwatia moyo watoto wajilinganishe na watu hao waaminifu. Hilo liliwakumbusha watoto wangu waziwazi mambo yanayompendeza Yehova.”

Watoto pia hujifunza katika hali zisizo rasmi. Musa aliwahimiza wazazi wazungumze juu ya vikumbusho vya Yehova ‘wanapoketi katika nyumba yao na wanapotembea barabarani na wanapolala na wanapoamka.’ (Kumbukumbu la Torati 6:7) Baba mmoja alisema: “Mtoto wangu huhitaji wakati kufunua yale yaliyo moyoni mwake. Tunapotembea au kufanya kazi pamoja, mwishowe yeye hujieleza waziwazi. Kwenye pindi hizo, sisi huzungumzia mambo yanayotufaidi sote.”

Pia sala zinazotolewa na wazazi huwa na matokeo makubwa kwa watoto wao. Watoto wanapowasikia wazazi wao wakimwomba Mungu kwa unyenyekevu awasaidie na kuwasamehe, wanachochewa ‘waamini kwamba yeye yuko.’ (Waebrania 11:6) Wazazi wengi ambao wamefanikiwa wametaja umuhimu wa sala za familia, baadhi ya sala hizo zinatia ndani masuala ya shule na mambo mengine yanayowahangaisha watoto wao. Baba mmoja alisema kwamba sikuzote mke wake husali pamoja na watoto kabla hawajaondoka kwenda shuleni.—Zaburi 62:8; 112:7.

“Na Tusife Moyo Katika Kufanya Yaliyo Mema”

Wazazi wote hukosea nao huenda wakasikitika kuhusu jinsi walivyoshughulikia hali fulani. Hata hivyo, Biblia inatuhimiza tuendelee kujaribu, bali “tusife moyo katika kufanya yaliyo mema.”—Wagalatia 6:9.

Hata hivyo, huenda wazazi wakakata tamaa nyakati fulani wanapokosa kuwaelewa watoto wao. Ni rahisi kukata kauli kwamba kizazi hiki ni tofauti na kigumu. Lakini kwa kweli, leo watoto wana udhaifu uleule ambao vizazi vya zamani vilikuwa nao, nao wanakabili vishawishi vilevile ingawa huenda ikawa mkazo wa kufanya mabaya umeongezeka. Kwa hiyo, baba mmoja baada ya kumrekebisha mwana wake, alitumia maneno mororo na kuongezea hivi kwa fadhili: “Moyo wako unataka tu kufanya mambo ambayo moyo wangu ulitaka kufanya nilipokuwa na umri kama wako.” Huenda wazazi wasijue mengi kuhusu kompyuta, lakini wanajua vizuri sana kuhusu maelekeo ya mwili wetu usio mkamilifu.—Mathayo 26:41; 2 Wakorintho 2:11.

Labda watoto fulani husitasita kukubali mwongozo wa wazazi wao na hata hukataa nidhamu wanayopewa. Hata hivyo, kwa mara nyingine tena, ni muhimu kuwa mvumilivu. Licha ya kuonyesha mwelekeo wa kukataa au kukaidi nidhamu mwanzoni, mwishowe watoto wengi huikubali. (Methali 22:6; 23:22-25) Matthew, kijana Mkristo ambaye sasa anatumika kwenye ofisi moja ya tawi ya Mashahidi wa Yehova, alisema: “Nilipokuwa tineja, nilihisi kwamba wazazi wangu waliniwekea vizuizi visivyo vya lazima. Niliwaza, ikiwa wazazi wa rafiki zangu wamekubali jambo fulani, kwa nini wazazi wangu wasilikubali? Na nilikasirika sana nyakati nyingine waliponiadhibu kwa kutoniruhusu niende kuendesha mtumbwi—jambo nililopenda. Hata hivyo, ninapokumbuka mambo hayo, ninatambua kwamba nidhamu ambayo wazazi wangu walinipa ilikuwa yenye matokeo na pia muhimu. Ninashukuru kwamba walinipa mwongozo niliohitaji kwa wakati barabara.”

Ni kweli kwamba, ingawa huenda nyakati nyingine watoto wetu wakalazimika kuwa katika mazingira yasiyofaa kiroho, bado wanaweza kuwa Wakristo wazuri. Kama Biblia inavyoahidi, hekima ya Mungu inaweza kuwasaidia wasitawishe uwezo wa kujikinga wasishambuliwe kiroho. “Hekima inapoingia moyoni mwako na ujuzi kupendeza nafsi yako, uwezo wa kufikiri utakutunza, utambuzi utakulinda, ili kukukomboa kutoka katika njia mbaya.”—Methali 2:10-12.

Si rahisi kubeba mtoto tumboni kwa miezi tisa. Nayo miaka 20 inayofuata huenda kwa kadiri fulani ikasababisha maumivu ya kihisia-moyo na pia furaha. Lakini kwa kuwa wanawapenda watoto wao, wazazi Wakristo hujitahidi kadiri wawezavyo kuwalinda watoto wao kupitia hekima ya Mungu. Wao huhisi hivi kuhusu watoto wao kama vile mtume Yohana aliyezeeka alivyohisi kuhusu watoto wake wa kiroho: “Sina sababu nyingine kubwa zaidi ya kuwa na shukrani kuliko mambo haya, kwamba niwe nikisikia watoto wangu wanaendelea kutembea katika kweli.”—3 Yohana 4.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 7 Baadhi ya majina katika makala hii yamebadilishwa.

[Picha katika ukurasa wa 24]

“Sikuzote nyumba yetu ilikuwa wazi kuwapokea vijana wengi daima”

[Picha katika ukurasa wa 25]

Pendezwa na mambo yanayowapendeza watoto wako

[Picha katika ukurasa wa 26]

“Nilijitayarisha kikamili kwa ajili ya funzo”