Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kwa Nini Wengi Hutilia Shaka Kwamba Dini Inaweza Kuwaunganisha Wanadamu?

Kwa Nini Wengi Hutilia Shaka Kwamba Dini Inaweza Kuwaunganisha Wanadamu?

Kwa Nini Wengi Hutilia Shaka Kwamba Dini Inaweza Kuwaunganisha Wanadamu?

“MPENDE jirani yako.” (Mathayo 22:39) Kanuni hiyo muhimu ya mwenendo husifiwa na dini nyingi. Ikiwa dini hizo zingewafundisha wafuasi wake kuwapenda jirani zao, basi wafuasi hao wangeunganishwa na kuwa na umoja. Lakini, je, wewe umeona hivyo? Je, dini zinaweza kuwaunganisha watu? Uchunguzi uliofanywa hivi karibuni huko Ujerumani uliuliza swali hili: “Je, dini huwaunganisha watu, au yaelekea zinawatenganisha?” Kati ya wale waliojibu swali hilo, asilimia 22 walisema kwamba dini huwaunganisha watu, hali asilimia 52 walisema kwamba zinawagawanya, au kuwatenganisha. Huenda watu katika nchi yako wana maoni kama hayo.

Kwa nini watu wengi hawana imani sana kwamba dini inaweza kuwaunganisha wanadamu? Labda ni kwa sababu ya yale ambayo wamejifunza kutokana na matukio yaliyopita. Badala ya kuwaunganisha watu, mara nyingi dini imewatenganisha. Katika visa fulani, ukatili wenye kutisha umefanywa kwa kutumia dini kuwa kisingizio. Hebu fikiria visa vichache katika miaka 100 tu iliyopita.

Kuchochewa na Dini

Wakati wa vita vya pili vya ulimwengu, Wakroatia Wakatoliki na Waserbia Waothodoksi katika nchi za Balkani walipigana. Vikundi vyote viwili vilidai kuwa vinamfuata Yesu, ambaye aliwafundisha wafuasi wake wapende jirani yao. Hata hivyo, kama alivyosema mtafiti mmoja, mapigano hayo yalisababisha “mauaji mabaya sana ya raia yaliyowahi kutokea katika historia.” Ulimwengu ulishtushwa na vifo vya wanaume, wanawake, na watoto zaidi ya 500,000.

Mwaka wa 1947, bara la Hindi lilikuwa na watu wapatao milioni 400, hiyo ilikuwa asilimia 20 hivi ya watu wote duniani. Wengi wa watu hao walikuwa Wahindu, Waislamu, na Makalasinga. India ilipogawanywa, nchi ya Kiislamu ya Pakistan ilianzishwa. Wakati huo, mamia ya maelfu ya wakimbizi kutoka nchi zote mbili waliteketezwa kwa moto, wakapigwa, wakateswa, na kupigwa risasi katika mauaji ya watu wengi yaliyochochewa na dini.

Mbali na mauaji yenye kushtua yaliyotajwa, tisho la ugaidi lilionekana wazi mwanzoni mwa karne hii. Leo, ugaidi umefanya ulimwengu wote uwe katika hali ya tahadhari, na vikundi vingi vya kigaidi hudai kwamba vinashirikiana na dini fulani. Dini haionwi kuwa inachangia umoja. Badala yake, mara nyingi inahusianishwa na jeuri na migawanyiko. Kwa hiyo, haishangazi kwamba gazeti moja la Ujerumani FOCUS, lilifananisha dini kubwa ulimwenguni—dini ya Kiyahudi, dini ya Tao, Ubudha, Uhindu, Uislamu, Ukonfyushasi, na Ukristo—na baruti.

Mizozo ya Wenyewe kwa Wenyewe

Huku dini fulani zikipigana, nyingine zimekumbwa na mizozo ya wenyewe kwa wenyewe. Kwa mfano, katika miaka ya hivi karibuni, dini za Kikristo zimegawanywa na mijadala kuhusu mafundisho. Makasisi na watu wa kawaida huuliza: Je, kupanga uzazi kunaruhusiwa? Namna gani utoaji-mimba? Je, wanawake wawekwe rasmi kuwa makasisi? Kanisa linapaswa kuonaje ngono kati ya watu wa jinsia moja? Je, dini inapaswa kuunga mkono vita? Kwa sababu ya migawanyiko hiyo, wengi huuliza, ‘Dini inawezaje kuwaunganisha wanadamu ikiwa haiwezi kuwaunganisha wafuasi wake wenyewe?’

Ni wazi kwamba kwa ujumla dini imeshindwa kuchangia umoja. Lakini je, ni dini zote zilizo na migawanyiko? Je, kuna dini iliyo tofauti ambayo inaweza kuwaunganisha wanadamu wote?

[Picha katika ukurasa wa 3]

Polisi waliojeruhiwa wakati wa mapigano kati ya vikundi vya kidini huko India mwaka wa 1947

[Hisani]

Photo by Keystone/Getty Images