Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Je, maneno ya Stefano kwenye Matendo 7:59 yanayoonyesha kwamba sala zinapaswa kuelekezwa kwa Yesu?

Andiko la Matendo 7:59 linasema: “Wakaendelea kumtupia Stefano mawe huku akiomba na kusema: ‘Bwana Yesu, pokea roho yangu.’” Kwa kuwa Biblia inasema kwamba Yehova ni “Msikiaji wa sala,” maneno hayo yametokeza maswali mengi katika akili za watu fulani. (Zaburi 65:2) Je, kwa kweli Stefano alisali kwa Yesu? Je, hilo linaonyesha kwamba Yesu ni sawa na Yehova?

Tafsiri ya King James Version inasema kwamba Stefano alikuwa “akimwita Mungu.” Basi, haishangazi kwamba watu wengi wanafikia mkataa uliofikiwa na mfafanuzi wa Biblia Matthew Henry aliyesema: “Hapa Stefano anasali kwa Kristo, sisi pia tunapaswa kufanya hivyo.” Hata hivyo, maoni hayo ni yenye makosa. Kwa nini?

Kitabu Barnes’ Notes on the New Testament kinakubali hivi waziwazi: “Neno Mungu halipatikani katika maandishi ya awali, nalo halikupaswa kutafsiriwa. Halipatikani katika [maandishi] au tafsiri zozote za kale.” Neno “Mungu” liliingiaje katika mstari huo? Msomi Abiel Abbot Livermore alitaja jambo hilo kuwa “ubaguzi wa kidini wa watafsiri.” Hivyo, tafsiri nyingi za kisasa huondoa mstari huo bandia unaomtaja Mungu.

Hata hivyo, tafsiri nyingi husema kwamba Stefano “alisali” kwa Yesu. Nayo maelezo ya chini katika tafsiri ya New World Translation yanaonyesha kwamba neno “alisihi” pia linaweza kumaanisha “ombi; sala.” Je, hilo halingeonyesha kwamba Yesu ni Mungu Mweza-Yote? Hapana. Kichapo Vine’s Expository Dictionary of Old and New Testament Words kinaeleza kwamba katika muktadha huu, neno la awali la Kigiriki, e·pi·ka·leʹo, linamaanisha: “Kuita, kusihi; . . . kukata rufani kwa wenye mamlaka.” Paulo alitumia neno hilohilo aliposema: “Ninakata rufani kwa Kaisari!” (Matendo 25:11) Basi kwa kufaa, tafsiri ya The New English Bible inasema kwamba Stefano “alimwita” Yesu.

Ni nini kilichomchochea Stefano asihi hivyo? Kulingana na Matendo 7:55, 56, Stefano, ‘akiwa amejaa roho takatifu, alikaza macho mbinguni, akaona utukufu wa Mungu na wa Yesu akiwa amesimama kwenye mkono wa kuume wa Mungu.’ Kwa kawaida, Stefano angeelekeza maombi yake kwa Yehova katika jina la Yesu. Lakini alipomwona Yesu aliyefufuliwa katika maono, yaelekea Stefano alijihisi huru kumsihi moja kwa moja, akisema: “Bwana Yesu, pokea roho yangu.” Stefano alijua kwamba Yesu alikuwa amepewa mamlaka ya kuwafufua wafu. (Yohana 5:27-29) Hivyo, alimwomba Yesu ahifadhi roho yake, au uhai wake, hadi siku ambayo Yesu atamfufua kwenye uhai usioweza kufa huko mbinguni.

Je, maneno hayo mafupi ya Stefano yalituwekea kielelezo cha kuelekeza sala kwa Yesu? La, hasha. Kwanza kabisa, Stefano alitofautisha waziwazi Yesu na Yehova, kwa kuwa masimulizi yanasema kwamba alimwona Yesu akiwa “amesimama kwenye mkono wa kuume.” Pia, hali hizo zilikuwa za kipekee. Kisa kingine tu kama hicho ambapo maneno yanaelekezwa kwa Yesu ni kile cha mtume Yohana, ambaye pia alielekeza maneno yake moja kwa moja kwa Yesu alipomwona katika maono.—Ufunuo 22:16, 20.

Ingawa kwa kufaa Wakristo leo huelekeza sala zao zote kwa Yehova Mungu, wao pia wana imani isiyotikisika kwamba Yesu ndiye “ufufuo na uzima.” (Yohana 11:25) Kama vile ilivyomtegemeza Stefano, ndivyo imani katika uwezo wa Yesu wa kuwafufua wafuasi wake inavyoweza kutusaidia na kututegemeza nyakati za shida.