Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Tulijifunza Kumtegemea Yehova Kikamili

Tulijifunza Kumtegemea Yehova Kikamili

Simulizi la Maisha

Tulijifunza Kumtegemea Yehova Kikamili

LIMESIMULIWA NA NATALIE HOLTORF

Ilikuwa Juni 1945. Siku fulani mwezi huo, mtu mmoja aliyeonekana kuwa mgonjwa alikuja nyumbani kwetu na kusimama kwa subira mbele ya mlango. Akiwa ameshtuka, Ruth, binti yangu mdogo aliniita kwa sauti na kusema: “Mama, kuna mgeni mlangoni!” Hakujua kwamba mgeni huyo alikuwa baba yake—mume wangu mpendwa, Ferdinand. Miaka miwili mapema, siku tatu tu baada ya Ruth kuzaliwa, Ferdinand alitoka nyumbani, akakamatwa na kupelekwa kwenye kambi ya mateso ya Nazi. Baada ya muda huo mrefu, mwishowe Ruth alikutana na baba yake, nayo familia yetu ikaungana tena. Mimi na Ferdinand tulikuwa na mambo mengi sana ya kuambiana!

FERDINAND alizaliwa mwaka wa 1909 katika jiji la Kiel, huko Ujerumani, nami nilizaliwa mwaka wa 1907 katika jiji la Dresden, pia huko Ujerumani. Nilipokuwa na umri wa miaka 12, familia yetu ilikutana kwa mara ya kwanza na Wanafunzi wa Biblia, kama Mashahidi wa Yehova walivyoitwa wakati huo. Niliacha Kanisa la Kiinjili nilipokuwa na umri wa miaka 19, na nikajiweka wakfu kwa Yehova.

Wakati huohuo, Ferdinand alihitimu chuo cha ubaharia naye akawa baharia. Wakati wa safari zake za baharini, alitafakari maswali kuhusu kuwako kwa Muumba. Alipokuwa Ujerumani baada ya safari yake, Ferdinand alimtembelea ndugu yake ambaye alikuwa Mwanafunzi wa Biblia. Ziara hiyo ilitosha kumsadikisha kwamba Biblia ilikuwa na majibu ya maswali ambayo yalikuwa yakimsumbua. Aliacha Kanisa la Kilutheri, na akaamua pia kuacha kazi ya baharia. Baada ya kushiriki siku ya kwanza katika kazi ya kuhubiri, alitamani sana kufanya kazi hiyo maisha yake yote. Usiku huohuo, Ferdinand alijiweka wakfu kwa Yehova. Alibatizwa Agosti 1931.

Afanya Kazi Akiwa Baharia na Mhubiri

Mnamo Novemba 1931, Ferdinand alisafiri kwa gari-moshi kwenda Uholanzi ili kusaidia katika kazi ya kuhubiri huko. Ferdinand alipomwambia ndugu aliyepanga kazi ya kuhubiri nchini kwamba alikuwa baharia, ndugu huyo alisema: “Wewe ndiye hasa mtu tunayehitaji!” Akina ndugu walikuwa wamekodi mashua ili kikundi cha mapainia (wahudumu wa wakati wote) kiwahubirie wale walioishi kwenye ukingo wa mto sehemu ya kaskazini ya nchi. Mashua hiyo ilikuwa na mabaharia watano, lakini hakuna hata mmoja wao aliyejua kuiendesha. Hivyo, Ferdinand akawa nahodha.

Miezi sita baadaye, Ferdinand aliombwa atumikie kama painia, huko Tilburg, kusini mwa Uholanzi. Ilikuwa karibu wakati huo kwamba nilifika huko Tilburg kutumikia nikiwa painia na nikakutana na Ferdinand. Mara moja tuliombwa tuhamie Groningen, sehemu ya kaskazini ya nchi. Huko, tulifunga ndoa mnamo Oktoba 1932, na tulifanya upainia huku tukifurahia fungate yetu katika nyumba iliyotumiwa na mapainia kadhaa.

Binti yetu Esther alizaliwa mnamo 1935. Ingawa hatukuwa na pesa nyingi, tuliazimia kuendelea na upainia. Tulihamia kijiji kimoja ambako tuliishi katika nyumba ndogo. Nilipokuwa nikimtunza mtoto nyumbani, mume wangu alikuwa akihubiri siku nzima. Siku iliyofuata tulibadilishana. Tuliendelea kufanya hivyo mpaka Esther alipokua vya kutosha ili kuandamana nasi katika mahubiri.

Muda mfupi baada ya hapo, hali ya kisiasa barani Ulaya ilikuwa yenye kutisha. Tulipata habari kuhusu jinsi Mashahidi walivyokuwa wakiteswa huko Ujerumani, na tulijua kwamba karibuni sisi pia tungetendewa vivyo hivyo. Tulijiuliza jinsi tungeweza kuvumilia mateso hayo makali. Mnamo 1938, serikali ya Uholanzi ilitoa amri ya kukataza wageni kufanya kazi ya kugawanya vichapo vya kidini. Ili kutusaidia kuendelea na huduma yetu, Mashahidi wa Uholanzi walitupa majina ya watu ambao walipendezwa na kazi yetu, nasi tuliweza kujifunza Biblia na baadhi yao.

Kusanyiko la Mashahidi wa Yehova lilipangwa karibu wakati huo. Ingawa hatukuwa na pesa za kununua tikiti ya kusafiri, tulitamani kuhudhuria kusanyiko hilo. Hivyo, tulianza safari ya siku tatu kwa baiskeli, Esther akiwa ameketi kwenye kiti kilichokuwa kwenye usukani wa baiskeli. Wakati wa usiku tulilala kwa Mashahidi walioishi kandokando ya barabara hiyo. Tulifurahi sana kuhudhuria kusanyiko letu la kwanza la kitaifa. Programu ilituimarisha kwa ajili ya majaribu yaliyokuwa mbele yetu. Zaidi ya yote, tulikumbushwa kumtegemea Mungu. Tuliongozwa na maneno haya ya Zaburi 31:6: “Lakini mimi, namtegemea Yehova.”

Tunawindwa na Wanazi

Mnamo Mei 1940, Wanazi walivamia Uholanzi. Muda mfupi baadaye Gestapo, au polisi wa siri wa Nazi, waliingia nyumbani mwetu kwa ghafula tulipokuwa tukipanga vichapo vya Biblia ili kuvisafirisha. Ferdinand alipelekwa kwenye makao makuu ya Gestapo. Mara kwa mara mimi na Esther tulimtembelea, na nyakati nyingine alihojiwa na kupigwa mbele yetu. Kwa ghafula mnamo Desemba, Ferdinand alifunguliwa, lakini uhuru wake ulikuwa wa muda mfupi tu. Jioni fulani tulipokuwa tukirudi nyumbani, tuliona gari la Gestapo karibu na nyumba yetu. Ferdinand alifaulu kukimbia lakini mimi na Esther tuliingia nyumbani. Gestapo walikuwa wakitungojea. Walimtaka Ferdinand. Usiku huohuo baada ya Gestapo kuondoka, polisi wa Uholanzi walikuja na kunikamata ili kunihoji. Siku iliyofuata, mimi na Esther tulienda kujificha katika nyumba ya familia ya Norder, wenzi wa ndoa ambao walikuwa Mashahidi waliobatizwa karibuni.

Kuelekea mwishoni mwa Januari 1941, wenzi wa ndoa mapainia waliokuwa wakiishi katika mashua walikamatwa. Siku iliyofuata mwangalizi mmoja wa mzunguko (mhudumu asafirie) pamoja na mume wangu waliingia ndani ya mashua hiyo ili kuchukua baadhi ya vitu vya wenzi hao wa ndoa, lakini watu walioshirikiana na Gestapo waliwavamia. Ferdinand alifaulu kuponyoka na kukimbia kwa baiskeli yake. Hata hivyo, mwangalizi wa mzunguko alishikwa na kupelekwa gerezani.

Ndugu waliosimamia kazi ya kuhubiri walimwomba Ferdinand achukue nafasi ya mwangalizi wa mzunguko. Hiyo ilimaanisha kwamba kila mwezi angekuwa nyumbani yapata siku tatu tu. Hilo lilitokeza jaribu lingine kwetu, lakini niliendelea na upainia. Gestapo walizidi kuwasaka Mashahidi, hivyo tulihama mara kwa mara. Mwaka wa 1942, tulihama mara tatu. Mwishowe, tulijikuta katika jiji la Rotterdam, mbali na mahali ambapo Ferdinand alikuwa akifanya huduma yake kisiri. Wakati huo, nilikuwa nikitarajia kujifungua mtoto wangu wa pili. Kwa fadhili, familia ya Kamp ambayo watoto wao wawili walikuwa wamepelekwa karibuni kwenye kambi ya mateso, walitukaribisha nyumbani kwao.

Twasakwa Sana na Gestapo

Mtoto wetu wa pili, Ruth, alizaliwa Julai 1943. Baada ya Ruth kuzaliwa, Ferdinand alikaa nasi kwa siku tatu, lakini ilibidi aondoke, na hiyo ndiyo ilikuwa mara ya mwisho kumwona kwa muda mrefu. Majuma matatu hivi baadaye, Ferdinand alikamatwa huko Amsterdam. Alipelekwa kwenye kituo cha Gestapo ambako waliweza kumtambua. Gestapo walimuuliza maswali mengi kwa kusudi la kumlazimisha atoe habari kuhusu kazi yetu ya kuhubiri. Lakini Ferdinand alikuwa tayari kuwaeleza tu kwamba yeye ni Shahidi wa Yehova na kwamba hakujiingiza katika utendaji wowote wa kisiasa. Maofisa wa Gestapo walikasirika kuona kwamba Ferdinand, ambaye alikuwa Mjerumani, hakuwa amejiandikisha jeshini, nao walitisha kumuua kwa kuwa waliomwona kuwa msaliti.

Katika miezi mitano iliyofuata, Ferdinand alizuiliwa gerezani ambako alitishwa kuuawa kwa kupigwa risasi. Hata hivyo, hakutikisika katika uaminifu wake kwa Yehova. Ni nini kilichomsaidia aendelee kuwa na nguvu kiroho? Ni Neno la Mungu, Biblia. Bila shaka, kwa kuwa Ferdinand alikuwa Shahidi, hakuruhusiwa kuwa na Biblia. Hata hivyo, wafungwa wengine wangeweza kuomba nakala moja. Hivyo, Ferdinand akamsadikisha mfungwa mwenzake aiombe familia yake imletee nakala moja ya Biblia. Mwanamume huyo alifanya hivyo. Miaka mingi baadaye, wakati wowote Ferdinand alipozungumza kuhusu jambo hilo, macho yake yaling’aa kwa furaha naye alisema: “Biblia hiyo iliniletea faraja iliyoje!”

Mapema Januari 1944, kwa ghafula Ferdinand alipelekwa kwenye kambi ya mateso ya Vught, huko Uholanzi. Kuhamishwa huko kusikotazamiwa kulimfaidi kwa kuwa alikutana na Mashahidi wengine 46. Nilipopata habari kwamba amehamishwa, nilifurahi sana kujua kwamba bado alikuwa hai!

Kuhubiri Bila Kuacha Katika Kambi ya Mateso

Maisha kambini yalikuwa magumu sana. Utapiamlo, ukosefu wa mavazi ya joto, na baridi kali yalikuwa mambo ya kawaida. Ferdinand alipatwa na ugonjwa wa tezi za koo. Baada ya kusimama nje kwenye baridi kali kwa muda mrefu akisubiri wafungwa waitwe kwa majina, alienda mahali pa kuwatunzia wagonjwa. Wagonjwa waliokuwa na homa na joto lililofikia nyuzi 40 za Selsiasi au zaidi waliruhusiwa kubaki huko. Lakini Ferdinand hakuruhusiwa kwa sababu kiasi cha joto la mwili wake kilikuwa nyuzi 39 za Selsiasi! Aliambiwa arudi kazini. Hata hivyo, wafungwa wenzake walimhurumia, wakamficha kwa vipindi vifupi-vifupi mahali penye joto. Alipata kitulizo zaidi hali ya hewa ilipokuwa yenye joto. Pia, wakati ndugu fulani walipopokea chakula, waliwagawia wengine, hivyo Ferdinand akapata nguvu kwa kadiri fulani.

Kabla mume wangu kufungwa gerezani, kuhubiri kulikuwa njia yake ya maisha, na aliendelea kuwaambia wengine kuhusu imani yake akiwa huko. Mara nyingi maofisa wa kambi walimdhihaki kwa sababu ya alama yake ya rangi ya zambarau, alama ambayo ilimtambulisha mfungwa kuwa ni Shahidi. Lakini Ferdinand aliona dhihaka hizo kuwa nafasi ya kuanzisha mazungumzo nao. Mwanzoni, eneo la kuhubiri la akina ndugu lilikuwa tu kambi za majeshi ambako waliishi hasa Mashahidi. Ndugu walijiuliza, ‘Tutawafikiaje wafungwa wengi zaidi?’ Bila kujua, wasimamizi wa kambi walitoa suluhisho. Jinsi gani?

Akina ndugu walikuwa wameficha vichapo vichache na pia Biblia 12. Siku moja walinzi waligundua baadhi ya vichapo hivyo, lakini hawangeweza kujua vilikuwa vya nani hasa. Hivyo, maofisa wa kambi waliamua kuvunja umoja wa Mashahidi. Hata hivyo, kama adhabu, ndugu wote walihamishwa na kupelekwa kwenye kambi nyingine ambazo hazikuwa na Mashahidi. Isitoshe, wakati wa chakula ndugu waliketi pamoja na wafungwa ambao hawakuwa Mashahidi. Mpango huo ulithibitika kuwa wenye manufaa. Sasa ndugu wangefanya kile ambacho walitamani kufanya, yaani, kuwahubiria wafungwa wengi iwezekanavyo.

Kulea Binti Wawili Nikiwa Pekee Yangu

Wakati huohuo, mimi na binti zangu wawili tulikuwa bado tukiishi huko Rotterdam. Kulikuwa na baridi kali sana mwaka 1943 na 1944. Nyuma ya nyumba yetu kulikuwa na kikosi cha askari Wajerumani wa kuangusha ndege. Mbele ya nyumba yetu kulikuwa na Bandari ya Waal ambayo majeshi ya Muungano yalitaka sana kuishambulia kwa makombora. Hapo hapakuwa mahali salama pa kujificha. Isitoshe, kulikuwa na upungufu wa chakula. Tulijifunza kumtegemea Yehova kikamili kuliko wakati mwingine wowote.—Methali 3:5, 6.

Esther mwenye umri wa miaka minane alisaidia familia yetu ndogo kwa kwenda kupanga mstari ili kupata posho. Hata hivyo, mara nyingi ilipofika zamu yake, alipata chakula kimekwisha. Siku moja alipoenda kutafuta chakula, alijikuta katikati ya mashambulizi ya ndege. Nilishikwa na wasiwasi niliposikia milipuko, lakini muda mfupi baadaye wasiwasi wangu ulibadilika na kuwa machozi ya furaha aliporudi bila kujeruhiwa na hata alirudi akiwa na viazi-sukari. Kwanza nilimuuliza, “kulitukia nini?” Kwa utulivu alijibu: “Mabomu yalipoanguka, nilifanya tu kama vile Baba alivyoniambia, nililala kifudifudi, nikaendelea kulala chini, na kusali. Na nikaokoka!”

Kwa sababu ya matamshi yangu ya Kijerumani, ilikuwa hatari kwangu kwenda dukani, kwa hiyo nilimtuma Esther aende kununua vitu. Askari Wajerumani walitambua jambo hilo nao wakaanza kumuuliza Esther maswali mengi. Lakini hakutoa siri yoyote. Nyumbani, nilimfundisha Esther Biblia, na kwa sababu hangeweza kwenda shule, nilimfundisha kusoma na kuandika na pia mambo mengine.

Esther alinisaidia pia katika huduma. Kabla ya kwenda kujifunza Biblia na mtu fulani, Esther alinitangulia ili kuhakikisha kwamba hakuna mtu yeyote aliyekuwa akituchunguza. Aliangalia ikiwa ishara ambazo tulikubaliana na mwanafunzi wa Biblia zilikuwa mahali pake. Kwa mfano, mtu ambaye nilimtembelea alipaswa kusimamisha kwa njia fulani chungu cha maua kwenye dirisha ili nijue kwamba ningeweza kuingia. Wakati wa funzo la Biblia, Esther alikaa nje ili kuchunguza dalili ya hatari huku akimsukuma Ruth akiwa ndani ya kigari cha mtoto.

Wapelekwa Sachsenhausen

Ferdinand alikuwa akiendeleaje? Mnamo Septemba 1944, yeye pamoja na ndugu wengine wengi walipelekwa kwa nguvu kwenye kituo cha gari-moshi ambako wafungwa 80 walifinyana ndani ya mabehewa. Kila gari lilikuwa na ndoo moja iliyotumiwa kama choo na ndoo nyingine ilikuwa ya maji ya kunywa. Safari hiyo ilichukua muda wa siku tatu mchana na usiku, na kulikuwa tu nafasi ya kusimama. Mabehewa hayo hayakuwa na madirisha ila tu matundu madogo hapa na pale. Mambo waliyopaswa kuvumilia, yaani, joto, njaa, na kiu na harufu mbaya, hayawezi kuelezeka.

Gari-moshi lilisimama taratibu kwenye kambi ya mateso ya Sachsenhausen yenye sifa mbaya. Wafungwa wote walinyang’anywa kila kitu isipokuwa tu Biblia ndogo 12 ambazo Mashahidi walichukua waliposafiri!

Ferdinand na ndugu wengine wanane walitumwa kwenye kambi iliyosimamiwa na Sachsenhausen huko Rathenow ili kufanya kazi katika kiwanda cha kutengenezea silaha za vita. Ingawa walitishwa kuuawa, ndugu walikataa kufanya kazi hiyo. Ili kutiana moyo kubaki imara, kila asubuhi walisoma pamoja andiko la Biblia, kama vile Zaburi 18:2, na hivyo wangeweza kulitafakari mchana wote. Hilo liliwasaidia kutafakari mambo ya kiroho.

Mwishowe, mngurumo wa mizinga ulitangaza kukaribia kwa majeshi ya Muungano na vikosi vya Urusi. Warusi ndio waliokuwa wa kwanza kufika kwenye kambi ambako Ferdinand na wenzake walikuwa. Waliwapa wafungwa chakula na kuwaamuru waondoke kambini. Mwishoni mwa Aprili 1945, jeshi la Warusi liliwaruhusu kwenda nyumbani.

Mwishowe Familia Yaungana

Mnamo Juni 15, Ferdinand alifika Uholanzi. Akina ndugu huko Groningen walimkaribisha kwa shauku. Punde si punde, aliambiwa kwamba tuko hai, na kwamba tunaishi mahali fulani nchini, nasi pia tukapokea habari kwamba amerudi. Kusubiri arudi kulionekana kuwa muda mrefu sana. Lakini mwishowe, siku moja Ruth, binti yangu mdogo aliniita kwa sauti na kusema: “Mama, kuna mgeni mlangoni!” Alikuwa mume wangu mpendwa na baba ya watoto wangu!

Kulikuwa na matatizo mengi yaliyohitaji kutatuliwa kabla hatujaanza tena kuishi maisha ya kawaida tukiwa familia. Hatukuwa na makao, nalo tatizo kubwa lilikuwa kupata kibali cha kukubaliwa tena kuishi Uholanzi kama wakaaji wa kudumu. Kwa kuwa tulikuwa Wajerumani, kwa miaka mingi watawala wa Uholanzi walituona kuwa watu wasiotakiwa na jamii. Ingawa hivyo, mwishowe, tuliweza kutulia na kuanza upya maisha tuliyoyapenda sana, yaani, kumtumikia Yehova pamoja tukiwa familia.

“Namtegemea Yehova”

Katika miaka ya baadaye, kila mara mimi na Ferdinand tulipokutana na baadhi ya marafiki wetu ambao walipitia nyakati hizo za shida kama sisi, tulikumbuka jinsi Yehova alivyotuongoza kwa upendo nyakati hizo ngumu. (Zaburi 7:1) Tulifurahi kwamba kwa miaka mingi, Yehova alituruhusu tushiriki katika kuendeleza kazi ya Ufalme. Mara nyingi tulizungumza pia jinsi tulivyofurahi kutumia ujana wetu katika utumishi mtakatifu wa Yehova.—Mhubiri 12:1.

Baada ya kipindi cha mateso ya Nazi, mimi na Ferdinand aliyekuwa na tumaini la kwenda mbinguni tulimtumikia Yehova pamoja kwa zaidi ya miaka 50 kabla hajafa Desemba 20, 1995. Hivi karibuni, nitafikia umri wa miaka 98. Kila siku, ninamshukuru Yehova kwamba watoto wetu walitutegemeza sana wakati wa miaka hiyo ya matatizo na kwamba bado ninaweza kufanya yale niwezayo katika utumishi wake kwa utukufu wa jina lake. Ninashukuru kwa yote ambayo Yehova amenifanyia, nami natamani kuendelea kuongozwa na maneno haya: “Lakini mimi, namtegemea Yehova.”—Zaburi 31:6.

[Picha katika ukurasa wa 19]

Mimi na Ferdinand, Oktoba 1932

[Picha katika ukurasa wa 19]

Mashua “Almina” iliyotumiwa kuhubiri, pamoja na mabaharia wake

[Picha katika ukurasa wa 22]

Nikiwa na Ferdinand na watoto wetu