Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Twazoezwa Kutoa Ushahidi Kamili

Twazoezwa Kutoa Ushahidi Kamili

Twazoezwa Kutoa Ushahidi Kamili

“Mtakuwa mashahidi wangu katika Yerusalemu na pia katika Yudea yote na Samaria na mpaka sehemu ya mbali zaidi ya dunia.”—MATENDO 1:8.

1, 2. Petro alikuwa na kazi gani, na ni nani aliyempa kazi hiyo?

“YESU aliyekuwa ametoka Nazareti . . . alituagiza sisi tuwahubirie watu na kutoa ushahidi kamili kwamba Huyu ndiye aliyeagizwa na Mungu kuwa mwamuzi wa walio hai na wafu.” (Matendo 10:38, 42) Kwa maneno hayo, mtume Petro alimweleza Kornelio na familia yake kazi aliyopokea ya kuwa mweneza-injili.

2 Yesu aliwapa kazi hiyo wakati gani? Yaelekea, Petro alikuwa akifikiria yale ambayo Yesu aliyekuwa amefufuliwa, alisema muda mfupi kabla ya kupaa mbinguni. Pindi hiyo, Yesu aliwaambia hivi wanafunzi wake waaminifu: “Mtakuwa mashahidi wangu katika Yerusalemu na pia katika Yudea yote na Samaria na mpaka sehemu ya mbali zaidi ya dunia.” (Matendo 1:8) Hata hivyo, muda fulani kabla ya hapo, Petro alikuwa amejua kwamba akiwa mwanafunzi wa Yesu, angepaswa kuwaeleza wengine imani yake katika Yesu.

Wazoezwa kwa Miaka Mitatu

3. Yesu alifanya muujiza gani, naye alitoa mwaliko gani kwa Petro na Andrea?

3 Miezi kadhaa baada ya kubatizwa mwaka wa 29 W.K., Yesu alihubiri kwenye Bahari ya Galilaya, mahali ambapo Petro na ndugu yake Andrea walifanya kazi ya uvuvi. Walikuwa wamefanya kazi usiku wote bila kuvua chochote. Hata hivyo, Yesu aliwaambia hivi: ‘Vuteni mpaka mahali penye kilindi, nanyi mshushe nyavu zenu, mvue.’ Walipofanya kama Yesu alivyowaambia, ‘walikusanya samaki wengi sana. Kwa kweli, nyavu zao zikaanza kupasuka.’ Alipoona muujiza huo, Petro aliogopa sana, lakini Yesu alimtuliza na kumwambia: “Acha kuogopa. Tangu sasa na kuendelea utakuwa ukiwavua watu wakiwa hai.”—Luka 5:4-10.

4. (a) Yesu aliwatayarishaje wanafunzi wake kutoa ushahidi? (b) Huduma ya wanafunzi wa Yesu ingetofautianaje na ile ya Yesu?

4 Mara moja, Petro na Andrea na pia Yakobo na Yohana, wana wa Zebedayo, wakaacha mashua zao na kumfuata Yesu. Kwa miaka mitatu hivi, waliandamana na Yesu alipokuwa akihubiri nao wakazoezwa kuwa waeneza-injili. (Mathayo 10:7; Marko 1:16, 18, 20, 38; Luka 4:43; 10:9) Baada ya mazoezi hayo, Nisani 14, 33 W.K., Yesu aliwaambia hivi: “Yule anayeniamini, huyo pia atafanya kazi ambazo mimi hufanya; naye atafanya kazi kubwa kuliko hizi.” (Yohana 14:12) Wanafunzi wa Yesu wangetoa ushahidi kamili kama alivyofanya Yesu, lakini kwa kiwango kikubwa zaidi. Kama walivyotambua baadaye, wao na wale ambao wangekuwa wanafunzi wa Yesu, wangetoa ushahidi katika “mataifa yote,” mpaka “umalizio wa mfumo wa mambo.”—Mathayo 28:19, 20.

5. Tunaweza kunufaika na mazoezi ambayo Yesu aliwapa wafuasi wake katika njia zipi?

5 Tunaishi katika “umalizio wa mfumo wa mambo.” (Mathayo 24:3) Tofauti na wanafunzi hao wa kwanza, sisi hatuwezi kuandamana na Yesu na kuona jinsi anavyowahubiria watu. Hata hivyo, bado tunaweza kunufaika na mazoezi aliyotoa kwa kusoma katika Biblia kuhusu jinsi alivyohubiri na maagizo aliyowapa wafuasi wake. (Luka 10:1-11) Hata hivyo, makala hii itazungumzia jambo lingine muhimu ambalo Yesu aliwaonyesha wanafunzi wake, yaani, mtazamo unaofaa kuelekea kazi ya kuhubiri.

Kuwajali Watu

6, 7. Ni sifa gani ya Yesu iliyomwezesha awe na matokeo mazuri katika huduma yake, nasi tunawezaje kumwiga?

6 Kwa nini Yesu alitoa ushahidi wenye matokeo mazuri? Sababu mmoja ni kwamba alipendezwa sana na watu na kuwajali. Mtunga-zaburi alitabiri kwamba Yesu ‘angemsikitikia mtu wa hali ya chini na maskini.’ (Zaburi 72:13) Bila shaka alitimiza unabii huo. Biblia inasema hivi kuhusu pindi moja: “Alipouona umati akawasikitikia, kwa sababu walikuwa wamechunwa ngozi na kutupwa huku na huku kama kondoo wasio na mchungaji.” (Mathayo 9:36) Hata wale waliotenda dhambi nzito walihisi kwamba aliwajali nao walimkaribia.—Mathayo 9:9-13; Luka 7:36-38; 19:1-10.

7 Leo sisi pia tutafanikiwa ikiwa tutawajali watu vivyo hivyo. Kabla ya kushiriki katika huduma, mbona usitafakari kidogo jinsi watu wanavyohitaji haraka habari unazowapelekea? Fikiria matatizo waliyo nayo ambayo yatatatuliwa tu na Ufalme. Azimia kuwa na maoni yanayofaa kumhusu kila mtu, kwa kuwa hujui ni nani atakayekubali ujumbe. Labda mtu mwingine utakayehubiria amekuwa akisali akutane na mtu kama wewe ili amsaidie!

Chochewa na Upendo

8. Kama Yesu, ni nini huwachochea wafuasi wake kuhubiri habari njema?

8 Habari njema ambayo Yesu alitangaza ilihusiana na masuala muhimu yaliyowakabili wanadamu, yaani, kutimizwa kwa mapenzi ya Yehova, kutakaswa kwa jina Lake, na kutetewa kwa enzi Yake kuu. (Mathayo 6:9, 10) Kwa sababu alimpenda Baba yake, Yesu alichochewa kudumisha utimilifu hadi mwisho na kutoa ushahidi kamili kuhusu Ufalme ambao utatatua masuala hayo. (Yohana 14:31) Kwa kuwa wafuasi wa Yesu leo wanachochewa vivyo hivyo, wanashiriki kwa bidii katika huduma. Mtume Yohana alisema hivi: “Kwa maana kumpenda Mungu humaanisha hivi, kwamba tuzishike amri zake,” kutia ndani amri ya kuhubiri habari njema na kufanya wanafunzi.—1 Yohana 5:3; Mathayo 28:19, 20.

9, 10. Mbali na kumpenda Mungu, ni upendo gani mwingine hutuchochea kutoa ushahidi kamili?

9 Yesu aliwaambia wafuasi wake: “Ikiwa mnanipenda, mtazishika amri zangu. Yule aliye na amri zangu na kuzishika, huyo ndiye ambaye hunipenda.” (Yohana 14:15, 21) Kwa hiyo, kumpenda Yesu kunapaswa kutuchochea tutoe ushahidi kuhusu kweli na kushika mambo yote ambayo Yesu aliamuru. Katika pindi moja alipowatokea wanafunzi wake baada ya kufufuliwa, Yesu alimhimiza Petro hivi: “Lisha wana-kondoo wangu. . . . Chunga kondoo wangu wadogo. . . . Lisha kondoo wangu wadogo.” Ni nini kinachopaswa kumchochea Petro kufanya hivyo? Yesu alidokeza jibu alipomwuliza Petro hivi mara kadhaa: “Je, unanipenda? . . . Je, unanipenda? . . . Je, unanipenda?” Naam, upendo wa Petro kwa Yesu ungemchochea kutoa ushahidi kamili, kutafuta ‘kondoo wadogo’ wa Yesu na kisha kuwa mchungaji wa kiroho wa kondoo hao.—Yohana 21:15-17.

10 Leo, hatumjui Yesu kibinafsi kama Petro. Lakini tunaelewa umuhimu wa yale ambayo Yesu alitufanyia. Mioyo yetu huchochewa na upendo mwingi ambao ulimfanya “aonje kifo kwa ajili ya kila mwanadamu.” (Waebrania 2:9; Yohana 15:13) Tunahisi kama Paulo alivyohisi alipoandika: “Upendo alio nao Kristo hutulazimisha . . . Alikufa kwa ajili ya wote ili wale wanaoishi wasiishi tena kwa ajili yao wenyewe, bali kwa ajili ya yeye.” (2 Wakorintho 5:14, 15) Tunaonyesha kwamba tunachukua kwa uzito upendo wa Yesu kutuelekea na kwamba tunampenda kwa kuchukua kwa uzito kazi ya kutoa ushahidi kamili. (1 Yohana 2:3-5) Hatungependa kamwe kuwa na mtazamo wa kivivi hivi kuhusu kazi ya kuhubiri, kana kwamba tunaiona dhabihu ya Yesu kuwa yenye thamani ya kawaida tu.—Waebrania 10:29.

Kukazia Fikira Mambo Muhimu

11, 12. Yesu alikuja duniani kwa kusudi gani, naye alionyeshaje kwamba aliona kazi hiyo kuwa muhimu?

11 Yesu alipokuwa mbele ya Pontio Pilato, alisema: “Kwa ajili ya hili mimi nimezaliwa, na kwa ajili ya hili nimekuja ulimwenguni, ili nitoe ushahidi juu ya ile kweli.” (Yohana 18:37) Yesu hakuruhusu chochote kimkengeushe fikira asitoe ushahidi juu ya ile kweli. Hayo ndiyo yaliyokuwa mapenzi ya Mungu kwake.

12 Bila shaka, Shetani alimjaribu Yesu kuhusiana na jambo hilo. Muda mfupi baada ya Yesu kubatizwa, Shetani alimwambia kwamba angemfanya kuwa mtu mashuhuri ulimwenguni na kumpa “falme zote za ulimwengu na utukufu wazo.” (Mathayo 4:8, 9) Baadaye, Wayahudi walitaka kumfanya kuwa mfalme. (Yohana 6:15) Huenda leo wengine wakafikiri kwamba wanadamu wangenufaika kama Yesu angekubali mambo hayo, labda wakifikiri kwamba akiwa mfalme wa kibinadamu, Yesu angeweza kuwafanyia wanadamu mambo mengi mazuri. Hata hivyo, Yesu alikataa kufikiri kwa namna hiyo. Alikazia fikira kutoa ushahidi juu ya ile kweli.

13, 14. (a) Ni nini ambacho hakikumkengeusha Yesu kuacha kazi yake kuu? (b) Ingawa Yesu alikuwa maskini kimwili, alitimiza nini?

13 Isitoshe, Yesu hakukengeushwa fikira na ufuatiaji wa mali. Hivyo, hakuwa tajiri. Hakuwa hata na nyumba yake mwenyewe. Yeye alisema hivi pindi moja: “Mbweha wana mapango na ndege wa mbinguni wana viota, lakini Mwana wa binadamu hana mahali popote pa kulaza kichwa chake.” (Mathayo 8:20) Kulingana na Biblia, Yesu alipokufa, kitu pekee chenye thamani alichokuwa nacho ni vazi ambalo askari-jeshi Waroma walilipigia kura. (Yohana 19:23, 24) Hata hivyo, je, hilo lilimaanisha kwamba Yesu hakufanikiwa maishani? La, hasha!

14 Yesu alitimiza mambo mengi zaidi kuliko mfadhili aliye tajiri zaidi. Paulo alisema: “Mnazijua fadhili zisizostahiliwa za Bwana wetu Yesu Kristo, kwamba ingawa alikuwa tajiri, alikuja kuwa maskini kwa ajili yenu, ili muwe matajiri kupitia umaskini wake.” (2 Wakorintho 8:9; Wafilipi 2:5-8) Ingawa Yesu alikuwa maskini kimwili, alifanya iwezekane kwa watu wanyenyekevu kupata uzima wa milele katika ukamilifu. Tunamshukuru kama nini! Nasi tunashangilia katika thawabu aliyopokea kwa sababu alikazia fikira kufanya mapenzi ya Mungu.—Zaburi 40:8; Matendo 2:32, 33, 36.

15. Ni nini chenye thamani zaidi kuliko mali?

15 Leo Wakristo ambao hujitahidi kumwiga Yesu pia hukataa kukengeushwa na ufuatiaji wa mali. (1 Timotheo 6:9, 10) Wanatambua kwamba mali zinaweza kufanya maisha yawe yenye kustarehesha, lakini pia wanajua kwamba wakati wao ujao wa milele hautegemei mali. Mkristo anapokufa, mali zake za kimwili hazina thamani kwake sawa tu na vile lile vazi halikuwa na thamani kwa Yesu alipokufa. (Mhubiri 2:10, 11, 17-19; 7:12) Mkristo anapokufa, jambo pekee lenye thamani ya kweli ni uhusiano wake pamoja na Yehova na Yesu Kristo.—Mathayo 6:19-21; Luka 16:9.

Hakuvunjwa Moyo na Upinzani

16. Yesu alikabilianaje na upinzani?

16 Upinzani haukumkengeusha Yesu fikira asitoe ushahidi juu ya ile kweli. Hata hakuvunjika moyo kwa kujua kwamba huduma yake hapa duniani ingeishia kwenye kifo chake cha kidhabihu. Paulo alisema hivi kumhusu Yesu: “Kwa ajili ya shangwe iliyowekwa mbele yake, yeye alivumilia mti wa mateso, akaidharau aibu, naye ameketi kwenye mkono wa kuume wa kiti cha ufalme cha Mungu.” (Waebrania 12:2) Ona kwamba Yesu ‘aliidharau aibu.’ Hakubabaishwa na jinsi wapinzani wake walivyomwona. Hakukengeushwa fikira aache kufanya mapenzi ya Mungu.

17. Tunaweza kujifunza nini kutokana na uvumilivu wa Yesu?

17 Akitumia uvumilivu wa Yesu kuwa mfano, Paulo aliwatia moyo Wakristo hivi: “Mfikirieni sana yeye ambaye amevumilia maneno ya aina hii yenye kupinga yanayotolewa na watenda-dhambi kinyume cha faida zao wenyewe, ili ninyi msichoke na kuzimia katika nafsi zenu.” (Waebrania 12:3) Ni kweli kwamba linaweza kuwa jambo lenye kuchosha kukabiliana na upinzani au dhihaka siku baada ya siku. Linaweza kuwa jambo lenye kuchosha kuendelea kupinga vishawishi vya ulimwengu, jambo ambalo huenda likafanya watu wa jamaa watuchambue na kututia moyo tuwe watu mashuhuri. Hata hivyo, kama Yesu tunategemea msaada wa Yehova tunapoazimia kutanguliza Ufalme maishani mwetu.—Mathayo 6:33; Waroma 15:13; 1 Wakorintho 2:4.

18. Tunaweza kujifunza jambo gani zuri kutokana na yale ambayo Yesu alimwambia Petro?

18 Yesu alionyesha kwamba hakutaka kukengeushwa na chochote alipoanza kuwaambia wanafunzi wake kuhusu kifo chake. Petro alimtia Yesu moyo ‘ajitendee kwa fadhili’ na kumhakikishia kwamba ‘hangepatwa hata kidogo na jambo hilo.’ Yesu alikataa kusikiliza jambo lolote ambalo lingevunja azimio lake la kufanya mapenzi ya Yehova. Alimgeuzia Petro mgongo wake na kusema: “Nenda nyuma yangu, Shetani! Wewe ni kikwazo kwangu, kwa sababu wewe unafikiri, si fikira za Mungu, bali za wanadamu.” (Mathayo 16:21-23) Sisi pia na tuazimie sikuzote kukataa maoni ya wanadamu. Badala yake, sikuzote na tuongozwe na maoni ya Mungu.

Utaleta Manufaa ya Kudumu

19. Ingawa Yesu alifanya miujiza, ni jambo gani lililokuwa muhimu zaidi katika huduma yake?

19 Yesu alifanya miujiza mingi ili kuonyesha kwamba alikuwa Masihi. Hata aliwafufua wafu. Umati ulivutiwa na kazi hizo lakini Yesu hakuja duniani ili kutoa huduma za kijamii tu. Alikuja kutoa ushahidi kuhusu ile kweli. Alijua kwamba manufaa yoyote ya kimwili ambayo alitoa yalikuwa ya muda tu. Hata wale waliofufuliwa wangekufa tena. Angeweza tu kuwasaidia wengine wapate uzima wa milele kwa kutoa ushahidi kuhusu kweli.—Luka 18:28-30.

20, 21. Wakristo wa kweli hudumisha usawaziko gani kuhusiana na kazi nzuri?

20 Leo watu fulani hujaribu kuiga kazi nzuri za Yesu kwa kujenga hospitali au kutoa huduma nyingine za kijamii kwa watu walio maskini ulimwenguni. Nyakati nyingine, wao hutumia pesa nyingi kufanya mambo hayo. Wanapaswa kupongezwa kwa unyoofu wao; lakini kitulizo chochote wanachotoa ni cha muda tu. Ni Ufalme tu utakaoleta kitulizo cha kudumu. Kwa hiyo, kama Yesu, Mashahidi wa Yehova hukazia fikira kazi ya kutoa ushahidi juu ya ile kweli kuhusu Ufalme huo.

21 Bila shaka, Wakristo wa kweli hufanya kazi nzuri. Paulo aliandika: “Kwa kweli, basi, tukiwa na wakati unaofaa kwa ajili ya hilo, tuwatendee wote mema, na hasa wale ambao katika imani ni jamaa zetu.” (Wagalatia 6:10) Nyakati za shida au mtu anapokuwa na uhitaji, hatusiti ‘kutenda mema’ kwa jirani zetu au ndugu zetu Wakristo. Hata hivyo, sisi huiona kazi ya kutoa ushahidi kuhusu ile kweli kuwa muhimu zaidi sawa na vile Yesu alivyoiona.

Jifunze Kutokana na Kielelezo cha Yesu

22. Kwa nini Wakristo huwahubiria jirani zao?

22 Paulo aliandika: “Kwa kweli, ole wangu mimi ikiwa sitangazi habari njema!” (1 Wakorintho 9:16) Hakuchukua habari njema kivivi hivi kwa sababu ilimaanisha uzima kwake na kwa wale waliomsikiliza. (1 Timotheo 4:16) Sisi huiona huduma yetu kama Paulo. Tunataka kuwasaidia jirani zetu. Tunataka kuonyesha upendo wetu kwa Yehova. Tunataka kuthibitisha upendo wetu kwa Yesu na kuthamini upendo wake mwingi kwetu. Kwa hiyo, tunahubiri habari njema na hivyo kuishi “si kwa ajili ya tamaa za wanadamu tena, bali kwa ajili ya mapenzi ya Mungu.”—1 Petro 4:1, 2.

23, 24. (a) Tunajifunza jambo gani kutokana na muujiza wa samaki? (b) Ni nani wanaotoa ushahidi kamili leo?

23 Kama Yesu, hatukengeushwi fikira kutoka katika kazi yetu muhimu wengine wanapotudhihaki au kukataa ujumbe wetu kwa hasira. Tunajifunza jambo fulani kutokana na muujiza ambao Yesu alifanya alipowaita Petro na Andrea wamfuate. Tunaona kwamba tukimtii Yesu na kushusha nyavu zetu kwa njia ya mfano katika maji yasiyo na samaki, tunaweza kuvua samaki wengi. Wavuvi wengi Wakristo wamevua samaki wengi baada ya kufanya kazi kwa miaka mingi katika maji yasiyoonekana kuwa na samaki. Wengine wamehamia mahali ambako kuna samaki wengi nao wamepata matokeo mazuri. Lolote tunalofanya, hatutaacha kushusha nyavu zetu. Tunajua kwamba bado Yesu hajasema kazi ya kuhubiri imekwisha katika sehemu yoyote ya dunia.—Mathayo 24:14.

24 Zaidi ya Mashahidi wa Yehova milioni sita sasa wanafanya kazi hiyo kwa bidii katika nchi zaidi ya 230. Toleo la Mnara wa Mlinzi la Februari 1, 2005, litakuwa na ripoti ya ulimwenguni pote ya utendaji wao katika mwaka wa utumishi wa 2004. Ripoti hiyo itaonyesha jinsi Yehova amebariki sana kazi ya kuhubiri. Katika wakati uliobaki wa mfumo huu wa mambo, acheni tuendelee kutii maneno haya ya Paulo yenye kuchochea: “Lihubiri neno, fanya hivyo kwa bidii.” (2 Timotheo 4:2) Na tuendelee kutoa ushahidi kamili mpaka Yehova aseme kwamba kazi hiyo imekwisha.

Kuanzia mwaka huu, Ripoti ya Mwaka wa Utumishi ya Mashahidi wa Yehova Ulimwenguni Pote haitachapishwa katika toleo la Mnara wa Mlinzi la Januari 1. Badala yake, itachapishwa katika toleo la Februari 1.

Je, Unaweza Kujibu?

• Tunaweza kunufaikaje na mazoezi ambayo Yesu aliwapa wanafunzi wake?

• Yesu aliwaonaje watu aliowahubiria?

• Ni nini hutuchochea kutoa ushahidi kamili?

• Tunaweza kukaza fikira zetu kufanya mapenzi ya Mungu katika njia zipi?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 15]

Tutakuwa wenye matokeo katika huduma yetu ikiwa tutawahangaikia watu kama vile Yesu alivyofanya

[Picha katika ukurasa wa 16]

Yesu alikuja duniani hasa ili kutoa ushahidi juu ya ile kweli

[Picha katika ukurasa wa 17]

Mashahidi wa Yehova hukazia fikira kazi ya kutoa ushahidi kamili