Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Wameunganishwa na Upendo Kwa Mungu

Wameunganishwa na Upendo Kwa Mungu

Wameunganishwa na Upendo Kwa Mungu

KUTANIKO la Kikristo lilipoanzishwa katika karne ya kwanza ya Wakati wetu wa Kawaida, umoja ulikuwa mojawapo ya sifa zake zenye kutokeza licha ya kwamba wafuasi wake walitofautiana katika njia mbalimbali. Waabudu hao wa Mungu wa kweli walitoka nchi za Asia, Ulaya, na Afrika. Walitoka katika malezi mbalimbali. Kulikuwa na makuhani, askari-jeshi, watumwa, wakimbizi, wafanyabiashara, na wataalamu. Wengine walikuwa Wayahudi, nao wengine watu wasio Wayahudi. Hapo awali, wengi wao walikuwa wazinzi, walifanya ngono na watu wa jinsia moja, walevi, wezi, au wanyang’anyi. Hata hivyo, walipokuwa Wakristo, waliacha mazoea yao mabaya nao wakaunganishwa kwa umoja katika imani.

Ni nini kilichowezesha Ukristo wa karne ya kwanza kuwaunganisha watu hao wote katika umoja? Kwa nini walikuwa na amani kati yao wenyewe na watu wengine kwa ujumla? Kwa nini hawakujihusisha na maasi na vita? Kwa nini Ukristo wa mapema ulikuwa tofauti sana na dini kubwa leo?

Ni Nini Kilichowaunganisha Washiriki wa Kutaniko?

Upendo kwa Mungu ndilo jambo kuu lililowaunganisha waamini wa karne ya kwanza. Wakristo hao walitambua kwamba daraka lao kuu lilikuwa kumpenda Yehova, Mungu wa kweli kwa moyo, nafsi, na akili yao yote. Kwa mfano, mtume Petro aliyekuwa Myahudi, aliagizwa amtembelee mtu asiye Myahudi, mtu ambaye kwa kawaida hangeshirikiana naye kwa ukaribu. Upendo wake kwa Yehova ndio hasa uliomchochea kutii. Petro na Wakristo wengine wa karne ya kwanza walifurahia uhusiano wa karibu pamoja na Mungu ambao ulitegemea ujuzi sahihi wa utu Wake, yale anayopenda na yale anayochukia. Baada ya muda, waabudu wote walifahamu kwamba yalikuwa mapenzi ya Yehova kwamba ‘waunganishwe katika akili ileile na katika njia ileile ya kufikiri.’—1 Wakorintho 1:10; Mathayo 22:37; Matendo 10:1-35.

Waamini waliunganishwa pia na imani yao katika Yesu Kristo. Walitaka kufuata hatua zake kwa ukaribu. Aliwaamuru hivi: “Mpendane; kama vile ambavyo nimewapenda ninyi . . . Kwa jambo hili wote watajua kwamba ninyi ni wanafunzi wangu, mkiwa na upendo kati yenu wenyewe.” (Yohana 13:34, 35) Huo ulipaswa kuwa upendo wa kujidhabihu bali si hisia ya muda tu. Matokeo yangekuwa nini? Yesu alisali hivi kuhusu wale wanaomwamini: “Ninawaombea . . . wote wapate kuwa kitu kimoja, kama vile ambavyo wewe, Baba, umo katika muungano pamoja na mimi na mimi nimo katika muungano pamoja na wewe, ili wao pia wapate kuwa katika muungano pamoja na sisi.”—Yohana 17:20, 21; 1 Petro 2:21.

Yehova aliwamwagia watumishi wake wa kweli roho yake takatifu, au nguvu yake ya utendaji. Roho hiyo ilichangia umoja miongoni mwao. Iliwawezesha kuelewa mafundisho ya Biblia ambayo yalikubaliwa na makutaniko yote. Waabudu wa Yehova walihubiri ujumbe uleule, yaani, kutakaswa kwa jina la Yehova kupitia Ufalme wa Mungu wa Kimasihi, ambao ni serikali ya kimbingu itakayotawala wanadamu wote. Wakristo wa karne ya kwanza walielewa daraka lao la kutokuwa “sehemu ya ulimwengu huu.” Hivyo, wakati wowote maasi au vita vilipozuka, Wakristo walidumisha msimamo wa kutokuwamo. Walifuatia amani na kila mtu.—Yohana 14:26; 18:36; Mathayo 6:9, 10; Matendo 2:1-4; Waroma 12:17-21.

Waamini wote walichukua daraka lao la kuchangia umoja. Jinsi gani? Kwa kuhakikisha kwamba mwenendo wao ulipatana na Biblia. Hivyo, Mtume Paulo aliwaandikia hivi Wakristo: ‘Ondoleeni mbali utu wa zamani unaolingana na mwenendo wenu wa kwanza,’ na ‘mvae utu mpya.’—Waefeso 4:22-32.

Umoja Wadumishwa

Bila shaka, waamini wa karne ya kwanza walikuwa watu wasio wakamilifu, na kulitokea hali ambazo zilihatarisha umoja wao. Kwa mfano, andiko la Matendo 6:1-6 huzungumzia hali ya kutoelewana kati ya Wakristo Wayahudi waliozungumza Kigiriki na wale waliozungumza Kiebrania. Wale waliozungumza Kigiriki walihisi kwamba walikuwa wakibaguliwa. Hata hivyo, mara tu mitume walipojulishwa jambo hilo, walilishughulikia haraka na bila ubaguzi. Baadaye, swali kuhusu mafundisho lilitokeza mabishano kuhusu madaraka ya wale wasio Wayahudi katika kutaniko la Kikristo. Uamuzi uliotegemea kanuni za Biblia ulifanywa, nao ukakubaliwa na wote katika makutaniko.—Matendo 15:1-29.

Mifano hiyo inaonyesha kwamba hali ya kutoelewana katika kutaniko la Kikristo la karne ya kwanza haikusababisha migawanyiko ya kikabila au migawanyiko kwa sababu ya tofauti za kimafundisho. Kwa nini? Kwa sababu mambo yaliyowaunganisha, yaani, upendo kwa Yehova, imani katika Yesu Kristo, upendo wa kujidhabihu kati yao wenyewe, kukubali mwongozo wa roho takatifu, kuelewa mafundisho yaleyale ya Biblia, na kuwa tayari kubadili mwenendo wao, yalikuwa yenye nguvu sana hivi kwamba kutaniko la karne ya kwanza lilikuwa na umoja na amani.

Umoja wa Ibada Leo

Je, umoja unaweza kupatikana kwa njia hiyohiyo leo? Je, mambo hayohayo yanaweza bado kuwaunganisha watu wenye imani moja na kuwawezesha wawe na amani na watu wa jamii zote katika sehemu zote ulimwenguni? Ndiyo, yanaweza! Mashahidi wa Yehova ni undugu wa ulimwenguni pote wenye umoja katika nchi, visiwa na maeneo zaidi ya 230. Nao wameunganishwa na mambo yaleyale yaliyowaunganisha Wakristo katika karne ya kwanza.

Jambo kuu linalochangia umoja unaofurahiwa na Mashahidi wa Yehova ni ujitoaji wao kwa Yehova Mungu. Hilo linamaanisha kwamba wanajitahidi kuwa waaminifu kwake chini ya hali zote. Mashahidi wa Yehova pia huonyesha imani katika Yesu Kristo na mafundisho yake. Wakristo hao huonyeshana upendo wa kujidhabihu, nao huhubiri ujumbe uleule wa habari njema ya Ufalme wa Mungu kokote wanakohubiri. Wao huwa tayari kuzungumza kuhusu Ufalme huo na watu wa dini, jamii, taifa na matabaka mbalimbali. Pia Mashahidi wa Yehova hawajihusishi na mambo ya ulimwengu, jambo ambalo huwasaidia kukabiliana na mikazo ya kisiasa, kijamii, kibiashara ambayo hugawanya watu. Mashahidi wote hukubali daraka lao la kuchangia umoja kwa kujiendesha kupatana na viwango vya Biblia.

Umoja Huwavutia Wengine

Mara nyingi, umoja huo umewavutia watu mmoja-mmoja ambao si Mashahidi. Kwa mfano, wakati mmoja Ilse, * alikuwa mtawa wa kike Mkatoliki katika makao ya watawa huko Ujerumani. Ni nini kilichofanya avutiwe na Mashahidi wa Yehova? Ilse anasema: “Wao ndio watu bora zaidi ambao nimewahi kukutana nao. Hawaendi vitani; nao hawamdhuru mtu yeyote. Wanataka kuwasaidia watu waishi kwa furaha katika paradiso hapa duniani chini ya Ufalme wa Mungu.”

Mfano mwingine ni wa Günther, ambaye alikuwa mwanajeshi Mjerumani huko Ufaransa wakati wa vita vya pili vya ulimwengu. Siku moja, kasisi Mprotestanti alifanya ibada kwa ajili ya wanajeshi Wajerumani waliokuwa katika kikosi cha Günther. Kasisi huyo alisali kwamba Mungu awasaidie, awalinde, na kuwapa ushindi. Baada ya ibada hiyo, Günther alipewa kazi ya kuwa mlinzi. Kupitia darubini yake, aliona majeshi ya adui yakihudhuria pia ibada ya kidini iliyoongozwa na kasisi. Günther alisema hivi baadaye: “Yaelekea kasisi huyo pia alisali kwamba Mungu awasaidie, awalinde, na kuwapa ushindi. Nilijiuliza inawezekanaje makanisa ya Kikristo yapigane katika vita vilevile.” Günther hakulisahau jambo hilo. Baadaye alipokutana na Mashahidi wa Yehova, ambao hawajihusishi na vita, Günther akawa sehemu ya undugu wao wa ulimwenguni pote.

Ashok na Feema walikuwa wafuasi wa dini moja ya Mashariki. Walikuwa na hekalu la mungu katika nyumba yao. Familia yao ilipopatwa na ugonjwa mbaya, walichunguza tena dini yao. Walipozungumza na Mashahidi wa Yehova, Ashok na Feema walivutiwa sana na mafundisho ya Biblia na upendo kati ya Mashahidi. Sasa wao ni wahubiri wenye bidii wa habari njema ya Ufalme wa Yehova.

Ilse, Günther, Ashok, na Feema wameungana pamoja na mamilioni ya Mashahidi wa Yehova katika undugu wa ulimwenguni pote. Wanaamini ahadi ya Biblia kwamba mambo yanayowaunganisha pamoja katika ibada leo, yatawaunganisha wanadamu wote watiifu hivi karibuni. Wakati huo, hakutakuwa tena na ukatili, ukosefu wa umoja, na migawanyiko inayosababishwa na dini. Ulimwengu mzima utaungana kwa umoja katika ibada ya Mungu wa kweli, Yehova.—Ufunuo 21:4, 5.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 16 Baadhi ya majina katika makala hii yamebadilishwa.

[Picha katika ukurasa wa 4, 5]

Ingawa walitoka malezi mbalimbali, Wakristo wa karne ya kwanza walikuwa na umoja