Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Unaweza Kuamua Wakati Wako Ujao Utakuwaje?

Je, Unaweza Kuamua Wakati Wako Ujao Utakuwaje?

Je, Unaweza Kuamua Wakati Wako Ujao Utakuwaje?

JE, WAKATI wetu ujao umeamuliwa mapema? Je, maamuzi tunayofanya maishani yanaathiri wakati wetu ujao?

Tuseme kwamba mwanadamu anaweza kuamua jinsi wakati wake ujao utakavyokuwa. Basi, je, mtu yeyote anaweza kupangiwa mapema afanye kazi fulani hususa au kuwa na cheo fulani? Naye Mungu angewezaje kutimiza mapenzi yake kuelekea dunia iwapo wanadamu wangekuwa na uhuru wa kubadili wakati wao ujao? Biblia inatoa majibu yenye kuridhisha kwa maswali hayo.

Kupangiwa Mambo Mapema na Uhuru wa Kuchagua—Je, Kunapatana?

Fikiria jinsi Yehova Mungu alivyotuumba. “Kwa mfano wa Mungu alimuumba [mtu]; mwanamume na mwanamke aliwaumba,” yasema Biblia. (Mwanzo 1:27) Kwa kuwa tumeumbwa kwa mfano wa Mungu, tunaweza kuonyesha sifa zake kama vile upendo, haki, hekima, na nguvu. Pia Mungu ametupatia zawadi ya uhuru wa kuchagua. Hilo hufanya tuwe tofauti na viumbe wengine duniani. Tunaweza kuchagua kama tutafuata mwongozo wa kiadili wa Mungu au la. Ndiyo sababu nabii Musa angeweza kusema hivi: “Nachukua mbingu na dunia kuwa mashahidi juu yenu leo, kwamba nimeweka uzima na kifo mbele yako, baraka na laana; nawe lazima uchague uzima ili uendelee kuwa hai, wewe na uzao wako, kwa kumpenda Yehova Mungu wako, kwa kuisikiliza sauti yake na kwa kushikamana naye.”—Kumbukumbu la Torati 30:19, 20.

Hata hivyo, zawadi ya uhuru wa kuchagua haimaanishi kuwa na uhuru kamili. Uhuru huo hautupatii sababu ya kupuuza sheria za asili na za kiadili ambazo Mungu aliweka ili kuwe na usalama na amani katika ulimwengu wote. Sheria hizo ziliwekwa kwa faida yetu, na tunapozivunja tunapatwa na matokeo mabaya sana. Hebu wazia jambo ambalo lingetokea iwapo tungeamua kupuuza nguvu za uvutano na kuruka kutoka kwenye paa ya jengo refu!—Wagalatia 6:7.

Pia uhuru wa kuchagua hutupa wajibu fulani ambao viumbe wasio na uhuru huo hawana. Mwandikaji Corliss Lamont auliza: “Tunawezaje kusema kwamba wanadamu wana wajibu wa kiadili na kuwaadhibu wanapokosea ikiwa tunakubali . . . kwamba maamuzi na matendo yao yameamuliwa mapema?” Kwa kweli hatuwezi. Wanyama ambao huongozwa na silika hawana wajibu wa kiadili kwa mambo wanayofanya, wala kompyuta hazina wajibu wowote kwa mambo ambayo zimepangiwa kufanya. Kwa hiyo, uhuru wa kuchagua hutupa daraka zito na kufanya tuwe na wajibu kwa matendo yetu.

Yehova Mungu angekosa upendo na haki kama nini iwapo kabla hatujazaliwa, angepanga mapema jinsi maisha yetu yatakavyokuwa kisha atutoze hesabu kwa matendo yetu! Yeye hafanyi hivyo, kwa kuwa “Mungu ni upendo,” na “njia zake zote ni haki.” (1 Yohana 4:8; Kumbukumbu la Torati 32:4) Mungu hakutupatia uhuru wa kuchagua na wakati uleule ‘kuamua tangu milele yule ambaye ataokoa na yule atakayeangamiza,’ kama wanavyosisitiza watu wanaoamini kwamba watu hupangiwa mambo mapema. Uhuru wa kuchagua hupingana na wazo la kwamba watu hupangiwa mambo mapema.

Biblia inaonyesha wazi kwamba uchaguzi tunaofanya utabadili wakati wetu ujao. Kwa mfano, Mungu anawasihi hivi wakosaji: “Tafadhali, geukeni kila mmoja kutoka katika njia yake mbaya . . . ili nisiwaletee ninyi msiba.” (Yeremia 25:5, 6) Ombi hilo halingekuwa na maana yoyote iwapo tayari Mungu angekuwa ameamua jinsi wakati ujao wa kila mtu utakavyokuwa. Zaidi ya hayo, Neno la Mungu linasema: “Tubuni na mgeuke ili dhambi zenu zipate kufutwa, ili majira ya kuburudisha yapate kuja kutoka kwa uso wa Yehova.” (Matendo 3:19) Kwa nini Yehova anawasihi watu watubu na kugeuka ikiwa alijua tangu mwanzo kwamba hawawezi kufanya jambo lolote ili kubadili wakati wao ujao?

Maandiko hutaja watu fulani ambao wamealikwa na Mungu watawale wakiwa wafalme pamoja na Yesu Kristo mbinguni. (Mathayo 22:14; Luka 12:32) Hata hivyo, Biblia inasema kwamba watapoteza pendeleo hilo ikiwa hawatavumilia hadi mwisho. (Ufunuo 2:10) Kwa nini Mungu awape mwaliko huo ikiwa tayari alikuwa ameamua kwamba hawatachaguliwa? Pia fikiria maneno ya mtume Paulo kwa waamini wenzake. Aliandika hivi: “Tukizoea kutenda dhambi kimakusudi baada ya kupokea ujuzi sahihi juu ya kweli, hakuna tena dhabihu yoyote iliyobaki kwa ajili ya dhambi.” (Waebrania 10:26) Onyo hilo halingekuwa na maana yoyote iwapo Mungu alikuwa ameagiza kimbele wakati wao ujao. Lakini je, Mungu hajaagiza kimbele angalau watu fulani wawe watawala pamoja na Yesu Kristo?

Je, Aliagiza Kimbele Mtu Mmoja-Mmoja au Kikundi cha Watu?

Mtume Paulo aliandika hivi: “[Mungu] ametubariki kwa kila aina ya baraka ya kiroho katika mahali pa kimbingu katika muungano na Kristo, kama vile alivyotuchagua katika muungano naye kabla ya kuwekwa msingi wa ulimwengu . . . Kwa maana alituagiza kimbele ili tufanywe kuwa wana kwake kupitia Yesu Kristo.” (Waefeso 1:3-5) Ni nini ambacho Mungu ameagiza kimbele, na kuchaguliwa “kabla ya kuwekwa msingi wa ulimwengu” kunamaanisha nini?

Andiko hilo linasema kwamba Mungu amechagua baadhi ya wazao wa mwanadamu wa kwanza Adamu, watawale pamoja na Kristo mbinguni. (Waroma 8:14-17, 28-30; Ufunuo 5:9, 10) Hata hivyo, wazo la kwamba Yehova Mungu aliagiza kimbele watu fulani wapokee pendeleo hilo maelfu ya miaka kabla hawajazaliwa linapingana na uhakika wa kwamba wanadamu wana uhuru wa kuchagua. Mungu aliagiza kimbele kikundi, au jamii ya watu, bali si mtu mmoja-mmoja.

Kwa mfano: Tuseme serikali inaamua kuanzisha shirika fulani. Inaamua kimbele kazi, mamlaka, na ukubwa wa shirika hilo. Mwishowe shirika hilo linaanza kufanya kazi muda fulani baada ya kuanzishwa, nao wanachama wake wanatoa taarifa wakisema: “Serikali iliamua miaka mingi iliyopita kazi yetu itakuwa nini. Sasa tunaanza kazi tuliyopewa.” Je, ungekata kauli kwamba lazima serikali iwe iliamua miaka kadhaa mapema kuhusu wale ambao wangekuwa wanachama wa shirika hilo? La. Vivyo hivyo, Yehova aliamua mapema kwamba angeanzisha shirika fulani la kipekee ili kuondoa madhara ya dhambi ya Adamu. Aliagiza kimbele jamii ya watu ambao wangetumika kwenye shirika hilo—lakini si mtu mmoja-mmoja. Wangechaguliwa baadaye, na maamuzi ambayo wangefanya maishani yangeamua kama mwishowe wangekubaliwa au la.

Mtume Paulo alikuwa akifikiria ulimwengu gani aliposema: ‘Mungu alituchagua katika muungano naye kabla ya kuwekwa msingi wa ulimwengu’? Ulimwengu ambao Paulo anataja hapa si ulimwengu ambao Mungu alianzisha alipowaumba Adamu na Hawa. Ulimwengu huo ulikuwa ‘mwema sana’—bila dhambi au upotovu wowote. (Mwanzo 1:31) Haukuhitaji “kuachiliwa huru” kutoka katika dhambi.—Waefeso 1:7.

Ulimwengu ambao Paulo alimaanisha ni ule ambao ulianza baada ya Adamu na Hawa kuasi huko Edeni—ulimwengu ulio tofauti sana na ule uliokusudiwa na Mungu hapo mwanzoni. Ni ulimwengu ambao ulianza na watoto wa Adamu na Hawa. Ulimwengu huo ulifanyizwa na watu waliotengwa na Mungu na watumwa wa dhambi na uharibifu. Ni ulimwengu wa watu ambao wangeweza kukombolewa, tofauti na Adamu na Hawa waliotenda dhambi kimakusudi.—Waroma 5:12; 8:18-21.

Yehova Mungu aliweza kushughulikia mara moja hali iliyotokana na uasi huo huko Edeni. Mara tu uhitaji ulipotokea, aliagiza kimbele shirika la kipekee—Ufalme wa Kimasihi mikononi mwa Yesu Kristo—ambao ungewakomboa wanadamu kutoka katika dhambi ya Adamu. (Mathayo 6:10) Mungu alifanya hivyo “kabla ya kuwekwa msingi wa ulimwengu” wa wanadamu wanaoweza kukombolewa, yaani, kabla ya Adamu na Hawa walioasi kuzaa watoto.

Kwa kawaida wanadamu huhitaji kufanya mipango hususa ili kutimiza yale wanayotaka kufanya. Kupanga mambo mapema kunahusianishwa na wazo la kwamba lazima Mungu awe alipangia mapema kila kitu katika ulimwengu wote. Roy Weatherford aandika hivi: “Yaelekea, kwa wanafalsafa wengi maoni ya kwamba Mungu hakupanga kila tukio kimbele hayapatani na Enzi yake Kuu.” Je, kweli Mungu anahitaji kupanga kimbele kila tukio?

Kwa kuwa ana nguvu zisizo na mipaka na hekima isiyo na kifani, Yehova anaweza kushughulika kwa mafanikio na hali yoyote ya dharura au isiyotazamiwa ambayo inaweza kutokea viumbe wake wanapotumia uhuru wao wa kuchagua. (Isaya 40:25, 26; Waroma 11:33) Anaweza kufanya hivyo mara moja bila kufikiria kimbele. Tofauti na wanadamu wasio wakamilifu ambao uwezo wao una mipaka, Mungu Mweza-Yote hahitaji mpango hususa unaoonyesha kimbele jinsi wakati ujao wa kila mwanadamu duniani utakavyokuwa. (Methali 19:21) Katika tafsiri nyingi za Biblia, andiko la Waefeso 3:11 husema juu ya “kusudi la milele” la Mungu badala ya mpango hususa.

Jinsi Unavyoweza Kubadili Wakati Wako Ujao

Mungu ana kusudi fulani kuelekea dunia, na kusudi hilo limeagizwa kimbele. Andiko la Ufunuo 21:3, 4 linasema: “Tazama! Hema la Mungu liko pamoja na wanadamu, naye atakaa pamoja nao, nao watakuwa watu wake. Na Mungu mwenyewe atakuwa pamoja nao. Naye atafuta kila chozi kutoka katika macho yao, na kifo hakitakuwapo tena, wala maombolezo wala kilio wala maumivu hayatakuwapo tena. Mambo ya zamani yamepitilia mbali.” Naam, dunia hii itakuwa paradiso, kama Yehova alivyokusudia tangu mwanzo. (Mwanzo 1:27, 28) Swali ni, Je, utakuwepo? Hilo linategemea maamuzi unayofanya sasa. Yehova hajaamua mapema jinsi wakati wako ujao utakavyokuwa.

Dhabihu ya fidia ya Mwana wa Mungu, Yesu Kristo, hufanya iwezekane kwa kila mtu anayemwamini apate uzima wa milele. (Yohana 3:16, 17; Matendo 10:34, 35) Biblia inasema, “Yule anayemwamini Mwana ana uzima wa milele; yule asiyemtii Mwana hataona uzima.” (Yohana 3:36) Unaweza kuchagua uzima kwa kujifunza yale ambayo Biblia inasema kumhusu Mungu, Mwana wake, na mapenzi Yake na kwa kutumia mambo unayojifunza. Mtu anayetenda kwa hekima ya kweli iliyoandikwa katika Neno la Mungu anahakikishiwa kwamba “atakaa salama wala hatasumbuliwa na hofu ya msiba.”—Methali 1:20, 33.

[Picha katika ukurasa wa 5]

Tofauti na wanyama, wanadamu wana wajibu wa kiadili kwa matendo yao

[Hisani]

Eagle: Foto: Cortesía de GREFA