Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Mahubiri ya Sauli Yachochea Uadui

Mahubiri ya Sauli Yachochea Uadui

Mahubiri ya Sauli Yachochea Uadui

WAYAHUDI huko Damasko hawangeweza kuamini kwamba mteteaji mwenye bidii wa imani ya kimapokeo angeweza kugeuka na kuwa mwasi-imani. Sauli alijulikana kuwa mtu aliyewatesa wale walioliitia jina la Yesu huko Yerusalemu. Alikuwa ameenda Damasko ili kuwatesa wanafunzi huko. Lakini sasa yeye mwenyewe alikuwa akihubiri kwamba Yesu ni Masihi, mtu aliyeonwa kuwa mhalifu, aliyedharauliwa, na aliyetundikwa kwa sababu ya kukufuru. Je, Sauli alikuwa amepatwa na wazimu?—Matendo 9:1, 2, 20-22.

Labda kulikuwa na ufafanuzi fulani. Yaelekea wengine waliosafiri pamoja na Paulo kutoka Yerusalemu walizungumza kuhusu yale yaliyotukia barabarani. Walipokuwa wakikaribia Damasko, ghafula nuru nyangavu ilimulika kuwazunguka, na wote wakaanguka chini. Pia sauti ilisikika. Sauli peke yake ndiye aliyejeruhiwa. Alikuwa amelala barabarani. Mwishowe aliposimama, wasafiri wengine walimwongoza kuingia Damasko, kwa kuwa hangeweza kuona chochote.—Matendo 9:3-8; 26:13, 14.

Mpinzani Awa Mteteaji

Ni nini kilichompata Sauli akiwa njiani kuelekea Damasko? Je, alidhoofishwa na safari ndefu au joto la alasiri? Huku wakiwa wameazimia kutafuta kisababishi cha asili, watu wenye kutilia shaka wa leo hutaja mambo ambayo huenda yalitukia, ambayo yanatia ndani kuchanganyikiwa, kuona na kusikia mambo yasiyokuwepo, tatizo baya la akili lililofanya Sauli asumbuliwe na dhamiri, matatizo ya akili, na kudhaniwa kwamba alikuwa na kifafa.

Kwa kweli, kile kilichotukia ni kwamba Yesu Kristo alimtokea Sauli katika nuru hiyo yenye kupofusha na kumthibitishia kwamba alikuwa Masihi. Michoro fulani inaonyesha Sauli akianguka kutoka juu ya farasi. Ingawa hilo linawezekana, Biblia inasema tu kwamba ‘alianguka chini.’ (Matendo 22:6-11) Iwe Sauli alianguka kihalisi hilo kwa kweli halikuwa jambo muhimu likilinganishwa na aibu kubwa ya kuanguka kutoka kwenye cheo chake cha awali. Sasa Sauli alipaswa kutambua kwamba mambo ambayo wafuasi wa Yesu walikuwa wakihubiri yalikuwa ya kweli. Alipaswa tu kujiunga nao. Sauli aliyekuwa adui mwenye kutaka mapambano wa ujumbe wa Yesu, aligeuka na kuwa mmoja wa wahubiri waaminifu zaidi wa ujumbe huo. Baada ya kuweza kuona tena na kubatizwa, ‘Sauli aliendelea kupata nguvu hata zaidi naye alikuwa akiwafadhaisha Wayahudi waliokuwa wakikaa Damasko alipokuwa akithibitisha kupatana na akili kwamba huyu ndiye Kristo.’—Matendo 9:22.

Njama ya Kumuua Yashindwa

Sauli, ambaye baadaye aliitwa Paulo, alienda wapi baada ya kugeuza imani? Alisema hivi alipowaandikia Wagalatia: “Nilienda nikaingia Arabia, nami nikarudi tena Damasko.” (Wagalatia 1:17) Neno “Arabia” linaweza kumaanisha kusafiri katika sehemu yoyote ile ya Rasi ya Arabia. Wasomi fulani wanadokeza kwamba huenda Paulo alienda katika Jangwa la Siria au kwingineko katika ufalme wa Nabatae wa Areta wa Nne. Yaelekea baada ya ubatizo wake, Sauli alienda mahali penye utulivu ili kutafakari sawa na vile Yesu alivyoenda nyikani baada ya kubatizwa.—Luka 4:1.

Sauli aliporudi Damasko, “Wayahudi walikata shauri pamoja kumwangamiza.” (Matendo 9:23) Gavana aliyetumikia kama mwakilishi wa Mfalme Areta huko Damasko alikuwa akilinda jiji ili Sauli akamatwe. (2 Wakorintho 11:32) Hata hivyo, maadui walipokuwa wakipanga njama ya kumuua Sauli, wanafunzi wa Yesu walikuwa wakitafuta njia ya kumtorosha.

Anania na wanafunzi walioshirikiana na Sauli baada tu ya kugeuza kwake imani walikuwa kati ya wale waliomsaidia mtume huyo kutoroka. * (Matendo 9:17-19) Huenda pia baadhi ya wale walioamini baada ya kusikia mahubiri ya Sauli huko Damasko walimsaidia, kwa kuwa andiko la Matendo 9:25 linasema hivi: “Wanafunzi wake wakamchukua na kumshusha usiku kupitia shimo ukutani, wakamshusha katika kapu.” Maneno “wanafunzi wake” huenda yakamaanisha wale ambao Sauli alifundisha. Vyovyote vile, yaelekea kufanikiwa kwa huduma yake kulizidisha uadui ambao tayari ulikuwepo kumwelekea.

Yale Tunayojifunza

Tunapochunguza baadhi ya matukio yanayoambatana na kugeuza imani na kubatizwa kwa Sauli tunaona wazi kwamba hakuhangaika kupita kiasi kuhusu jinsi wengine walivyomwona; wala hakuacha kuhubiri kwa sababu ya upinzani mkali. Jambo muhimu zaidi kwa Sauli lilikuwa kazi ya kuhubiri aliyopokea.—Matendo 22:14, 15.

Je, hivi karibuni umesadikishwa kuhusu umuhimu wa kuhubiri habari njema? Ikiwa ndivyo, basi unatambua kwamba Wakristo wote wa kweli wanapaswa kuwa wahubiri wa Ufalme. Hupaswi kushangaa ikiwa nyakati fulani huduma yako inatokeza upinzani. (Mathayo 24:9; Luka 21:12; 1 Petro 2:20) Sauli alituwekea kielelezo kizuri kwa jinsi alivyokabiliana na upinzani. Wakristo wanaovumilia majaribu bila kufa moyo watapata kibali cha Mungu. Yesu aliwaambia wanafunzi wake hivi: “Mtachukiwa na watu wote kwa sababu ya jina langu.” Hata hivyo, aliwahakikishia hivi: “Nanyi kwa kuvumilia mtajipatia nafsi zenu.”—Luka 21:17-19.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 10 Huenda Ukristo ulifika Damasko kutokana na mahubiri ya Yesu huko Galilaya au baada ya Pentekoste 33 W.K.—Mathayo 4:24; Matendo 2:5.

[Picha katika ukurasa wa 28]

Sauli ‘alianguka chini’ Yesu alipomtokea

[Picha katika ukurasa wa 29]

Sauli alitoroka njama ya kutaka kumuua huko Damasko