Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Maono ya Kimbele Kuhusu Ufalme wa Mungu Yatimizwa

Maono ya Kimbele Kuhusu Ufalme wa Mungu Yatimizwa

Maono ya Kimbele Kuhusu Ufalme wa Mungu Yatimizwa

“Mnafanya vema kulikazia uangalifu [neno la kinabii] kama vile taa inayoangaza mahali penye giza.”—2 PETRO 1:19.

1. Kuna hali gani zinazotofautiana katika ulimwengu leo?

ULIMWENGU wa leo unakumbwa na misiba daima. Kuanzia kuharibiwa kwa mazingira hadi kuenea kwa ugaidi ulimwenguni pote, matatizo ya wanadamu yanaonekana kuwa yanaongezeka daima. Hata dini za ulimwengu zimeshindwa kusaidia. Kwa kweli, mara nyingi dini hizo hufanya hali iwe mbaya hata zaidi kwa kuchochea ushupavu wa kidini, chuki, na utukuzo wa taifa ambao hugawanya watu. Naam, kama ilivyotabiriwa, “weusi mzito” umevifunika “vikundi vya mataifa.” (Isaya 60:2) Hata hivyo, mamilioni ya watu wanatazamia wakati ujao wakiwa na uhakika. Kwa nini? Kwa sababu wanalikazia uangalifu neno la Mungu la kinabii “kama vile taa inayoangaza mahali penye giza.” Wanaruhusu “neno” au ujumbe wa Mungu unaopatikana katika Biblia, uongoze hatua zao.—2 Petro 1:19.

2. Kulingana na unabii wa Danieli kuhusu “wakati wa mwisho,” ni nani tu wanaopewa ufahamu wa kiroho?

2 Kuhusu “wakati wa mwisho,” nabii Danieli aliandika hivi: “Wengi watakwenda huku na huku, na ujuzi wa kweli utakuwa mwingi. Wengi watajitakasa na kujifanya weupe na kusafishwa. Na waovu watatenda kwa uovu, wala hakuna waovu wowote watakaoelewa; bali wale walio na ufahamu wataelewa.” (Danieli 12:4, 10) Ufahamu wa kiroho hupewa tu wale ambao kwa unyoofu ‘huenda huku na huku’ katika, au kwa kujifunza Neno la Mungu kwa bidii, kukubali viwango vyake, na kujitahidi kufanya mapenzi yake.—Mathayo 13:11-15; 1 Yohana 5:20.

3. Katika miaka ya 1870, wanafunzi wa Biblia wa mapema walitambua kweli gani muhimu?

3 Mapema katika miaka ya 1870, kabla ya “siku za mwisho” kuanza, Yehova Mungu alianza kuangaza nuru zaidi kuhusu “siri takatifu za ufalme wa mbinguni.” (2 Timotheo 3:1-5; Mathayo 13:11) Wakati huo, tofauti na maoni ya wengi, kikundi cha wanafunzi wa Biblia kilitambua kwamba kurudi kwa Kristo hakungeonekana kwa macho. Baada ya kutawazwa mbinguni, Yesu angerudi katika maana ya kwamba angeelekeza fikira zake duniani akiwa mfalme. Ishara yenye mambo mengi ambayo ingeonekana ingewasaidia wanafunzi wake watambue kwamba kuwapo kwake kusikoonekana kumeanza.—Mathayo 24:3-14.

Maono ya Kimbele Yanapotimia

4. Yehova ameimarishaje imani ya watumishi wake leo?

4 Maono ya kugeuka sura yalikuwa wonyesho wa kimbele wa kung’aa kwa Kristo akiwa katika utukufu wa Ufalme. (Mathayo 17:1-9) Maono hayo yaliimarisha imani ya Petro, Yakobo, na Yohana wakati ambapo wengi walikuwa wameacha kumfuata Yesu kwa sababu hakufanya yale waliyotarajia afanye. Vivyo hivyo, wakati huu wa mwisho, Yehova ameimarisha imani ya watumishi wake kwa kuwasaidia wapate uelewaji zaidi kuhusu kutimizwa kwa maono hayo yenye kutia hofu na unabii mwingi unaohusiana na maono hayo. Sasa na tuchunguze baadhi ya mambo hayo halisi ya kiroho yenye kuimarisha imani.

5. Ni nani aliyekuwa Nyota ya Mchana, naye ‘alichomoza’ lini na jinsi gani?

5 Akirejelea maono ya kugeuka sura, mtume Petro aliandika hivi: “Kwa hiyo tuna neno la kinabii likiwa limefanywa hakika zaidi; nanyi mnafanya vema kulikazia uangalifu kama vile taa inayoangaza mahali penye giza, mpaka siku ipambazuke na nyota ya mchana ichomoze, katika mioyo yenu.” (2 Petro 1:19) Nyota hiyo ya Mchana ya mfano, au “nyota nyangavu ya asubuhi” ni Yesu Kristo aliyetukuzwa. (Ufunuo 22:16) ‘Alichomoza’ mwaka wa 1914 wakati Ufalme wa Mungu ulipozaliwa mbinguni, na hivyo enzi mpya ikaanza. (Ufunuo 11:15) Katika maono ya kugeuka sura, Musa na Eliya walitokea kando ya Yesu, wakiongea naye. Wanafananisha nani?

6, 7. Ni nani wanaowakilishwa na Musa na Eliya katika maono ya kugeuka sura, nayo Maandiko yanafunua habari gani muhimu kuhusu wale wanaowakilishwa nao?

6 Kwa kuwa Musa na Eliya walishiriki katika utukufu wa Kristo, lazima mashahidi hao wawili waaminifu wawe wanawakilisha wale watakaotawala na Yesu katika Ufalme wake. Uelewaji wa kwamba Yesu atatawala pamoja na watu wengine unapatana na maono ya kimbele ambayo nabii Danieli alionyeshwa ya Masihi aliyetawazwa. Danieli aliona “mtu fulani kama mwana wa binadamu” akipokea “utawala unaodumu mpaka wakati usio na kipimo” kutoka kwa “Mzee wa Siku,” Yehova Mungu. Lakini ona yale ambayo Danieli anaonyeshwa muda mfupi baadaye. Anaandika hivi: “Ufalme na utawala na ukuu wa falme zote chini ya mbingu zote wakapewa watu ambao ni watakatifu wa Aliye Mkuu Zaidi.” (Danieli 7:13, 14, 27) Naam, zaidi ya karne tano kabla ya maono ya kugeuka sura, Mungu alifunua kwamba “watakatifu” fulani wangeshiriki katika ukuu wa utawala wa Kristo.

7 Katika maono ya Danieli, watakatifu hao ni nani? Mtume Paulo anarejelea watu hao anaposema: “Roho yenyewe hutoa ushahidi pamoja na roho yetu kwamba sisi ni watoto wa Mungu. Basi, ikiwa sisi ni watoto, sisi pia ni warithi: warithi wa Mungu kwelikweli, lakini warithi pamoja na Kristo, mradi tu tunateseka pamoja ili pia tutukuzwe pamoja.” (Waroma 8:16, 17) Watakatifu hao ni wanafunzi wa Yesu waliotiwa mafuta. Yesu anasema hivi katika Ufunuo: “Yeye atakayeshinda nitampa ruhusa ya kuketi pamoja nami katika kiti changu cha ufalme, kama vile nilivyoshinda na kuketi pamoja na Baba yangu katika kiti chake cha ufalme.” ‘Washindi’ hao waliofufuliwa ambao hesabu yao ni 144,000 watatawala pamoja na Yesu juu ya dunia yote.—Ufunuo 3:21; 5:9, 10; 14:1, 3, 4; 1 Wakorintho 15:53.

8. Wanafunzi watiwa-mafuta wa Yesu wamefanyaje kazi inayofanana na ile ya Musa na Eliya, nao wamepata matokeo gani?

8 Hata hivyo, kwa nini Wakristo watiwa-mafuta wanawakilishwa na Musa na Eliya? Ni kwa sababu wakiwa bado duniani, Wakristo hao wanafanya kazi inayofanana na ile iliyofanywa na Musa na Eliya. Kwa mfano, wanatumikia wakiwa mashahidi wa Yehova hata wanapokabili mateso. (Isaya 43:10; Matendo 8:1-8; Ufunuo 11:2-12) Kama Musa na Eliya, wanafunua kwa ujasiri dini ya uwongo huku wakiwahimiza watu wanyoofu wajitoe kikamili kwa Mungu. (Kutoka 32:19, 20; Kumbukumbu la Torati 4:22-24; 1 Wafalme 18:18-40) Je, kazi yao imekuwa na matokeo? Bila shaka! Mbali na kusaidia kukusanya watiwa-mafuta wote, wamewasaidia mamilioni ya “kondoo wengine” kujitiisha kwa hiari chini ya Yesu Kristo.—Yohana 10:16; Ufunuo 7:4.

Kristo Akamilisha Ushindi Wake

9. Andiko la Ufunuo 6:2 linaonyesha Yesu akiwa katika hali gani leo?

9 Sasa Yesu si mwanadamu wa kawaida aliyepanda juu ya mwana-punda bali ni Mfalme mwenye nguvu. Anaonyeshwa akiwa amepanda juu ya farasi. Katika Biblia, farasi ni ishara ya vita. (Methali 21:31) Andiko la Ufunuo 6:2 linasema: “Tazama! farasi mweupe; na yule anayeketi juu yake alikuwa na upinde; naye akapewa taji, naye akaenda akishinda na kukamilisha ushindi wake.” Isitoshe, mtunga-zaburi Daudi aliandika hivi kumhusu Yesu: “Yehova ataituma fimbo ya nguvu zako kutoka Sayuni, akisema: ‘Nenda ukitiisha katikati ya adui zako.’”—Zaburi 110:2.

10. (a) Yesu alianzaje ushindi wake kwa utukufu? (b) Ushindi wa kwanza wa Kristo uliathirije ulimwengu kwa ujumla?

10 Ushindi wa kwanza wa Yesu ulikuwa juu ya maadui wake wenye nguvu zaidi, yaani, Shetani na roho wake waovu. Aliwafukuza kutoka mbinguni na kuwavurumisha duniani. Wakijua kwamba wakati wao ni mfupi, roho hao waovu wameelekeza hasira yao yenye jeuri kwa wanadamu, na kusababisha ole mkubwa. Katika Ufunuo, ole huo unafananishwa na waendeshaji-farasi wengine watatu. (Ufunuo 6:3-8; 12:7-12) Kupatana na unabii wa Yesu kuhusu “ishara ya kuwapo [kwake] na ya umalizio wa mfumo wa mambo,” uendeshaji wao wa farasi umetokeza vita, njaa, na pigo lenye kufisha. (Mathayo 24:3, 7; Luka 21:7-11) Sawa na maumivu ya kuzaa, bila shaka ‘maumivu hayo ya taabu’ yataongezeka mpaka Kristo ‘akamilishe ushindi wake’ kwa kuharibu kabisa sehemu zote za tengenezo linaloonekana la Shetani. *Mathayo 24:8.

11. Historia ya kutaniko la Kikristo inathibitishaje mamlaka ya kifalme ya Kristo?

11 Pia mamlaka ya kifalme ya Yesu yanaonekana wazi katika maana ya kwamba amelilinda kutaniko la Kikristo ili litimize kazi ya kuhubiri ujumbe wa Ufalme ulimwenguni pote. Licha ya upinzani mkali kutoka kwa Babiloni Mkubwa, ile milki ya ulimwengu ya dini ya uwongo, na kutoka kwa serikali zenye uadui, kazi ya kuhubiri imeendelea na kufikia kiwango kisicho na kifani katika historia ya ulimwengu. (Ufunuo 17:5, 6) Huo ni ushuhuda wenye nguvu kama nini kwamba Kristo anatawala!—Zaburi 110:3.

12. Kwa nini watu wengi hawatambui kuwapo kusikoonekana kwa Kristo?

12 Hata hivyo, kwa kusikitisha, wengi kutia ndani mamilioni ya watu wanaodai kuwa Wakristo, hawatambui kwamba matukio muhimu yanayotukia duniani ni ishara ya mambo halisi yasiyoonekana. Hata wanadhihaki wale wanaotangaza Ufalme wa Mungu. (2 Petro 3:3, 4) Kwa nini? Kwa sababu Shetani amepofusha akili zao. (2 Wakorintho 4:3, 4) Kwa kweli, alianza kuwapofusha kiroho watu wanaodai kuwa Wakristo karne nyingi zilizopita, hata kuwafanya watupilie mbali tumaini lao la Ufalme lenye thamani.

Tumaini la Ufalme Latupiliwa Mbali

13. Giza la kiroho kati ya watu wanaojiita Wakristo liliongoza kwenye nini?

13 Yesu alitabiri kwamba kama magugu yaliyopandwa katikati ya ngano, waasi-imani wangepenya katika kutaniko la Kikristo na kuwapotosha wengi. (Mathayo 13:24-30, 36-43; Matendo 20:29-31; Yuda 4) Baada ya muda, watu hao wanaojiita Wakristo walianza kufuata sherehe, mafundisho, na desturi za kipagani, na hata kuziita za “Kikristo.” Kwa mfano, Krismasi ilitokana na desturi zinazotia ndani ibada ya miungu ya kipagani, Mithra na Saturn. Lakini ni nini kilichowachochea watu wanaodai kuwa Wakristo wafuate miadhimisho hiyo isiyo ya Kikristo? Kichapo The New Encyclopædia Britannica (1974) kinasema: “Kuanzishwa kwa Krismasi, sherehe ya kuzaliwa kwa Yesu Kristo kulihusiana na tarajio lililokuwa likididimia la kurudi kwa Kristo ambako kulikuwa kunakaribia.”

14. Mafundisho ya Origen na Augustine yalipotoshaje kweli ya Ufalme?

14 Fikiria pia kupotoshwa kwa maana ya neno “ufalme.” Kitabu The Kingdom of God in 20th-Century Interpretation kinasema: “Origen [mwanatheolojia wa karne ya tatu] ndiye aliyebadili matumizi ya Kikristo ya neno ‘ufalme’ na kufanya limaanishe utawala wa Mungu ndani ya moyo.” Origen alitegemeza mafundisho yake juu ya nini? Hayakutegemea Maandiko, bali yalitegemea “maoni na falsafa za kilimwengu ambazo ni tofauti kabisa na maoni ya Yesu na kanisa la mapema zaidi.” Katika kitabu chake De Civitate Dei (Jiji la Mungu), Augustine wa Hippo (354-430 W.K.) alisema kwamba kanisa lenyewe ndilo Ufalme wa Mungu. Maoni hayo yanayopingana na Maandiko yaliyapa makanisa ya dini zinazojiita za Kikristo sababu za kidini za kutwaa mamlaka ya kisiasa. Nayo makanisa hayo yalitumia mamlaka hayo kwa karne nyingi, mara nyingi kwa ukatili.—Ufunuo 17:5, 18.

15. Andiko la Wagalatia 6:7 limetimizwaje kuhusiana na makanisa mengi ya dini zinazojiita za Kikristo?

15 Hata hivyo, leo makanisa yanavuna yalichopanda. (Wagalatia 6:7) Yaonekana makanisa mengi yanapoteza mamlaka yake na pia wafuasi wake. Mwelekeo huo unaonekana wazi huko Ulaya. Kulingana na gazeti Christianity Today, “sasa makanisa makubwa ya Ulaya [hayatumiki] tena kama nyumba za ibada bali kama majumba ya ukumbusho ambayo hutembelewa tu na watalii.” Mwelekeo huohuo unaonekana katika sehemu nyingine ulimwenguni. Hilo linaonyesha nini kuhusu dini ya uwongo? Je, itatokomea kwa sababu ya kukosa msaada wa kifedha na wafuasi? Nayo ibada ya kweli itaathiriwaje?

Jitayarishe kwa Ajili ya Siku Kuu ya Mungu

16. Kwa nini chuki inayoongezeka kuelekea Babiloni Mkubwa ni jambo la kutiwa maanani?

16 Kama vile moshi na majivu yanayofoka kutoka katika volkeno ambayo ilikuwa imelala huenda yakaonyesha kwamba mlipuko utatokea karibuni, chuki inayoongezeka kuelekea dini katika sehemu nyingi za ulimwengu inaonyesha kwamba siku za dini ya uwongo zimehesabiwa. Hivi karibuni, Yehova atafanya serikali za kisiasa za ulimwengu ziungane katika jitihada ya kumfunua na kumharibu kahaba wa kiroho, Babiloni Mkubwa. (Ufunuo 17:15-17; 18:21) Je, Wakristo wa kweli wanapaswa kuogopa tukio hilo na matukio mengine yanayohusiana na “dhiki kuu” ambayo yatafuata? (Mathayo 24:21) La, hasha! Kwa kweli, watakuwa na sababu za kushangilia Mungu anapowaharibu waovu. (Ufunuo 18:20; 19:1, 2) Fikiria mfano wa Yerusalemu la karne ya kwanza na Wakristo walioishi humo.

17. Kwa nini watumishi waaminifu wa Yehova wanaweza kukabili mwisho wa mfumo huu wakiwa na uhakika?

17 Majeshi ya Roma yalipozingira Yerusalemu mwaka wa 66 W.K., Wakristo waliokuwa macho kiroho hawakushtuka wala kuogopa. Kwa sababu walikuwa wanafunzi wenye bidii wa Neno la Mungu, walijua ‘kwamba kufanywa ukiwa kwake kulikuwa kumekaribia.’ (Luka 21:20) Pia walijua kwamba Mungu angewafungulia njia ya kukimbilia usalama. Alipofanya hivyo, Wakristo walikimbia. (Danieli 9:26; Mathayo 24:15-19; Luka 21:21) Vivyo hivyo leo, wale wanaomjua Mungu na kumtii Mwana wake wanaweza kukabili mwisho wa mfumo huu wakiwa na uhakika. (2 Wathesalonike 1:6-9) Kwa kweli, dhiki kuu itakapofyatuka, ‘watainua vichwa vyao kwa furaha, kwa sababu wanajua kwamba ukombozi wao unakaribia.’—Luka 21:28.

18. Shambulio la mwisho na la moja kwa moja la Gogu juu ya watumishi wa Yehova litakuwa na matokeo gani?

18 Baada ya kuharibiwa kwa Babiloni Mkubwa, Shetani akiwa Gogu wa Magogu atafanya shambulio la mwisho na la moja kwa moja dhidi ya Mashahidi wa Yehova wenye amani. Majeshi ya Gogu yatakayokuja “kama mawingu ili kuifunika nchi,” yatatarajia kupata ushindi kwa urahisi. Lakini yatashtuka sana! (Ezekieli 38:14-16, 18-23) Mtume Yohana anaandika hivi: “Nikaona mbingu imefunguliwa, na, tazama! farasi mweupe. Na yeye aliyeketi juu yake anaitwa Mwaminifu na wa Kweli . . . Upanga mrefu mkali unachomoza kutoka kinywani mwake, ili ayapige mataifa nao.” Huyo “Mfalme wa wafalme” asiyeweza kushindwa atawakomboa waabudu washikamanifu wa Yehova na kuharibu maadui wao wote. (Ufunuo 19:11-21) Huo utakuwa upeo ulioje wa utimizo wa maono ya kugeuka sura!

19. Ushindi kamili wa Kristo utakuwa na matokeo gani kwa wanafunzi wake washikamanifu, nao wanapaswa kujitahidi kufanya nini sasa?

19 Yesu ‘atastaajabiwa katika siku hiyo kuhusiana na wote walioonyesha imani.’ (2 Wathesalonike 1:10) Je, unataka kuwa kati ya wale watakaomstaajabia Mwana wa Mungu atakaposhinda? Basi endelea kuimarisha imani yako na ‘kuwa tayari, kwa sababu Mwana wa binadamu anakuja katika saa usiyofikiria.’—Mathayo 24:43, 44.

Tunzeni Akili Zenu

20. (a) Tunawezaje kuonyesha uthamini wetu kwa Mungu kwa kutupatia “mtumwa mwaminifu na mwenye busara”? (b) Tunapaswa kujiuliza maswali gani?

20 “Mtumwa mwaminifu na mwenye busara” huwahimiza kwa ukawaida watu wa Mungu waendelee kuwa macho kiroho na kutunza akili zao. (Mathayo 24:45, 46; 1 Wathesalonike 5:6) Je, unathamini vikumbusho hivyo vinavyotolewa kwa wakati unaofaa? Je, unavitumia ili kujua mambo utakayotanguliza maishani? Kwa nini usijiulize: ‘Je, ninatambua waziwazi maana ya kiroho ya matukio katika ulimwengu na kwamba Mwana wa Mungu anatawala mbinguni? Je, ninatambua kwamba yuko tayari kutekeleza hukumu ya Mungu juu ya Babiloni Mkubwa na sehemu nyingine ya mfumo wa Shetani?’

21. Kwa nini huenda wengine wakapoteza mtazamo wao wa kiroho, nao wanapaswa kufanya nini haraka?

21 Watu fulani ambao sasa wanashirikiana na watu wa Yehova wamepoteza mtazamo wao wa kiroho. Je, inawezekana kwamba wamekosa subira au uvumilivu, kama baadhi ya wanafunzi wa Yesu wa mapema? Je, wameathiriwa na mahangaiko ya maisha, ufuatiaji wa vitu vya kimwili, au mateso? (Mathayo 13:3-8, 18-23; Luka 21:34-36) Labda wengine wameona ni vigumu kuelewa habari fulani iliyochapishwa na “mtumwa mwaminifu na mwenye busara.” Ikiwa umepatwa na mojawapo ya mambo hayo, tunakuhimiza ujifunze Neno la Mungu ukiwa na bidii mpya na kumwomba Yehova dua ili uwe tena na uhusiano wa karibu na wenye nguvu pamoja naye.—2 Petro 3:11-15.

22. Mazungumzo kuhusu maono ya kugeuka sura na unabii mwingine unaohusiana nayo yamekuwa na matokeo gani kwako?

22 Wanafunzi wa Yesu walipewa maono ya kugeuka sura walipohitaji kitia-moyo. Leo tuna kitu bora zaidi cha kutuimarisha—utimizo wenye kustaajabisha wa maono hayo ya kugeuka sura na unabii mwingi unaohusiana nayo. Tunapofikiria mambo hayo matukufu yaliyo halisi na kile yatakachomaanisha wakati ujao, acheni sisi pia tuonyeshe kwa moyo wetu wote hisia kama za mtume Yohana aliposema: “Amina! Njoo, Bwana Yesu.”—Ufunuo 22:20.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 10 Katika Kigiriki cha awali, neno linalotafsiriwa “maumivu ya taabu” kihalisi linamaanisha “maumivu ya kuzaa.” (Mathayo 24:8, Kingdom Interlinear) Hilo linadokeza kwamba sawa na maumivu ya kuzaa, matatizo ya ulimwengu yataongezeka, yatakuwa makali zaidi, na kutokea kwa muda unaofuatana karibu-karibu na kufikia upeo kwenye dhiki kuu.

Je, Unakumbuka?

• Katika miaka ya 1870, kikundi kidogo cha wanafunzi wa Biblia kilielewa nini kuhusu kurudi kwa Kristo?

• Maono ya kugeuka sura yametimizwaje?

• Uendeshaji-farasi wa Yesu akiwa mshindi una matokeo gani kwa ulimwengu na kwa kutaniko la Kikristo?

• Tunapaswa kufanya nini ili tuwe kati ya wale watakaookoka Yesu atakapokamilisha ushindi wake?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 16, 17]

Maono ya kimbele yatimizwa

[Picha katika ukurasa wa 18]

Je, unajua ni nini kilichotokea Kristo alipoanza ushindi wake?