Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

“Mkaribishane”

“Mkaribishane”

“Mkaribishane”

FIBI, Mkristo wa karne ya kwanza, alikuwa na tatizo. Alikuwa akisafiri kutoka Kenkrea, huko Ugiriki, hadi Roma, lakini hakujuana na Waamini wenzake wa jiji hilo. (Waroma 16:1, 2) Mtafsiri wa Biblia Edgar Goodspeed anasema hivi: “Ulimwengu wa Waroma wakati huo ulikuwa mwovu na wenye ukatili na nyumba za wageni hazikuwa mahali pazuri kwa mwanamke mwenye maadili, hasa mwanamke Mkristo.” Kwa hiyo, Fibi angekaa wapi?

Katika nyakati za Biblia watu walisafiri mbali sana. Yesu Kristo na wanafunzi wake walifanya hivyo ili kuhubiri habari njema katika Yudea na Galilaya yote. Baadaye, wamishonari wa Kikristo kama vile Paulo, walipeleka ujumbe katika sehemu mbalimbali kuzunguka Bahari ya Mediterania, kutia ndani Roma, mji mkuu wa Milki ya Roma. Wakristo wa karne ya kwanza waliposafiri ndani au nje ya eneo la Kiyahudi, walikaa wapi? Ni matatizo gani waliyokabili ili kupata nyumba za kupanga? Tunaweza kujifunza nini kutoka kwao kuhusu kuonyesha ukarimu?

“Leo Lazima Nikae Katika Nyumba Yako”

Ukaribishaji-wageni umefafanuliwa kuwa kuwapokea wageni kwa ukarimu na kwa urafiki, na tangu zamani waabudu wa kweli wa Yehova wamejulikana kwa sifa hiyo. Kwa mfano, Abrahamu, Loti, na Rebeka walionyesha sifa hiyo ya ukaribishaji-wageni. (Mwanzo 18:1-8; 19:1-3; 24:17-20) Akieleza mtazamo wake kuelekea wageni, mzee wa ukoo Ayubu alisema hivi: “Hakuna mkaaji mgeni yeyote aliyelala nje usiku; milango yangu niliiacha wazi kuielekea njia.”—Ayubu 31:32.

Ili wasafiri wakaribishwe kwa ukarimu na Waisraeli wenzao, kwa kawaida ilitosha tu mtu kuketi kwenye uwanja wa umma na kungojea mwaliko. (Waamuzi 19:15-21) Kwa kawaida, wakaribishaji waliosha miguu ya wageni wao na kuwapa chakula na kinywaji, na pia chakula kwa ajili ya wanyama wao. (Mwanzo 18:4, 5; 19:2; 24:32, 33) Wasafiri ambao hawakutaka kuwa mzigo kwa wakaribishaji wao walibeba vyakula vyao, yaani, mkate na divai kwa ajili yao wenyewe na chakula cha punda wao. Waliomba tu mahali pa kulala.

Ingawa Biblia haielezi sana jinsi Yesu alivyopata mahali pa kupanga wakati wa safari zake za kuhubiri, ni lazima yeye na wanafunzi wake wawe walilala mahali fulani. (Luka 9:58) Alipotembelea jiji la Yeriko, Yesu alimwambia Zakayo hivi: “Leo lazima nikae katika nyumba yako.” Zakayo alimpokea mgeni wake “kwa shangwe.” (Luka 19:5, 6) Mara kwa mara Yesu alikaa kwa marafiki wake Martha, Maria, na Lazaro huko Bethania. (Luka 10:38; Yohana 11:1, 5, 18) Na yaelekea huko Kapernaumu, Yesu alikaa kwa Simoni Petro.—Marko 1:21, 29-35.

Maagizo kuhusu huduma ambayo Yesu aliwapa mitume wake 12 yanaonyesha mengi kuhusu aina ya ukaribishaji ambao wangetarajia katika Israeli. Yesu aliwaambia hivi: “Msichukue dhahabu wala fedha wala shaba kwa ajili ya mikoba yenu ya mshipi, wala mfuko wa chakula kwa ajili ya safari, wala mavazi mawili ya ndani, wala viatu wala fimbo; kwa maana mfanyakazi anastahili chakula chake. Katika jiji lolote lile au kijiji chochote kile mtakapoingia, tafuteni ni nani humo anayestahili, mkae humo mpaka mtakapoondoka.” (Mathayo 10:9-11) Alijua kwamba watu wenye mioyo minyoofu wangewakaribisha wanafunzi wake, nao wangewapa chakula, mahali pa kulala, na mahitaji mengine.

Hata hivyo, wakati ungefika ambapo waeneza-injili wangepaswa kutosheleza mahitaji yao wenyewe na kuyagharimia walipokuwa safarini. Kwa kufikiria upinzani ambao wafuasi wake wangepata na mpanuko wa kazi ya kuhubiri hadi maeneo yaliyokuwa nje ya Israeli, Yesu alisema hivi: “Acheni yule ambaye ana mkoba auchukue, vivyo hivyo pia mfuko wa chakula.” (Luka 22:36) Ili kueneza habari njema, ilikuwa lazima wasafiri na kutafuta mahali pa kulala.

“Fuateni Mwendo wa Ukaribishaji-Wageni”

Katika karne ya kwanza, watu walisafiri kwa urahisi kotekote katika Milki ya Roma kwa sababu kulikuwa na amani na barabara nzuri. * Kwa vile wasafiri walikuwa wengi, kulikuwa na uhitaji mkubwa wa mahali pa kulala. Uhitaji huo ulitimizwa na kuwepo kwa nyumba nyingi za kupanga zilizokuwa kando ya barabara kuu. Nyumba hizo zilipatikana kila baada ya safari ya siku moja. Hata hivyo, kichapo The Book of Acts in Its Graeco-Roman Setting kinasema: “Vichapo vinasema kwamba hali zilikuwa mbaya sana katika nyumba hizo. Kwa ujumla, vitabu na vitu vilivyochimbuliwa huonyesha kwamba nyumba hizo zilikuwa zimechakaa sana, chafu, hazikuwa na vyombo vyovyote vya nyumbani, zilikuwa na kunguni, chakula kibaya na maji yasiyofaa, wenye nyumba na wafanyakazi wasioaminika, wateja wenye sifa mbaya, na kwa ujumla maadili yaliyopotoka.” Inaeleweka kwamba msafiri aliyefuata maadili angeepuka kukaa katika nyumba hizo.

Basi haishangazi kwamba Biblia inawahimiza Wakristo kwa kurudia-rudia wawaonyeshe wengine ukaribishaji-wageni. Paulo aliwahimiza Wakristo huko Roma hivi: “Shirikini pamoja na watakatifu kulingana na mahitaji yao. Fuateni mwendo wa ukaribishaji-wageni.” (Waroma 12:13) Aliwakumbusha Wakristo Wayahudi hivi: “Msisahau ukaribishaji-wageni, kwa maana kupitia huo watu wengine, bila wao wenyewe kujua, waliwakaribisha malaika.” (Waebrania 13:2) Petro aliwahimiza waabudu wenzake ‘wakaribishane bila kunung’unika.’—1 Petro 4:9.

Hata hivyo, kulikuwa na hali ambazo haingefaa kuonyesha ukaribishaji-wageni. Kuhusu “kila mtu anayevuka mipaka naye hakai katika fundisho la Kristo,” mtume Yohana alisema hivi: “Msimpokee kamwe nyumbani mwenu wala kumsalimu. Kwa maana yeye anayemsalimu anashiriki katika matendo yake maovu.” (2 Yohana 9-11) Kuhusu watenda-dhambi wasiotubu, Paulo aliandika hivi: “Mwache kuchangamana katika ushirika pamoja na mtu yeyote anayeitwa ndugu ambaye ni mwasherati au mtu mwenye pupa au mwabudu-sanamu au mtukanaji au mlevi au mnyang’anyi, hata msile chakula pamoja na mtu wa namna hiyo.”—1 Wakorintho 5:11.

Lazima wajanja na watu wengine wawe walijaribu kutumia vibaya ukarimu wa Wakristo wa kweli. Kichapo cha kilimwengu cha karne ya pili W.K, kinachoitwa The Didache au Mafundisho ya Mitume Kumi na Wawili na ambacho huzungumzia imani ya Kikristo, kinapendekeza kwamba mhubiri anayesafiri akaribishwe kwa “siku moja, au siku mbili ikiwa ni lazima.” Baada ya hapo, anapoondoka “asikubali chochote ila chakula . . . [Akiomba] pesa, yeye ni nabii wa uwongo.” Kichapo hicho kinaendelea kusema: “Ikiwa angependa kuishi nyumbani kwenu, na ana ustadi wa kazi fulani, acheni afanye kazi ili apate riziki. Ikiwa hana ustadi wa kazi yoyote, mpeni kazi fulani mnayojua kwamba anaweza kufanya ili mtu yeyote asiishi kati yenu kwa uzembe kwa sababu tu ni Mkristo. Lakini ikiwa hatafanya kazi hiyo, basi anatumia Ukristo kujifaidi mwenyewe. Jihadharini na mtu kama huyo.”

Mtume Paulo alijihadhari ili asiwe mzigo kwa watu waliomkaribisha alipokaa kwa muda mrefu katika majiji fulani. Alifanya kazi ya kutengeneza mahema ili kujitegemeza. (Matendo 18:1-3; 2 Wathesalonike 3:7-12) Ili kuwasaidia wasafiri waliostahili ambao walikuwa miongoni mwao, yaelekea Wakristo wa mapema walitumia barua za mapendekezo, kama ile barua ambayo Paulo aliandika ili kumtambulisha Fibi. Paulo aliandika hivi: “Nampendekeza kwenu Fibi dada yetu . . . ili kwamba mkamkaribishe katika Bwana . . . na kwamba mkamsaidie katika jambo lolote ambalo huenda akawahitaji ninyi.”—Waroma 16:1, 2.

Baraka Zinazotokana na Kuwa Mkaribishaji

Wamishonari Wakristo wa karne ya kwanza walimtegemea Yehova ili atosheleze mahitaji yao yote. Lakini, je wangetarajia kufaidika kutokana na ukaribishaji-wageni wa waamini wenzao? Lidia aliwakaribisha Paulo na wengine nyumbani kwake. Mtume huyo alikaa pamoja na Akila na Prisila huko Korintho. Mlinzi mmoja wa jela huko Filipi aliwaalika Paulo na Sila kwenye chakula. Paulo alipokewa kwa ukarimu na Yasoni huko Thesalonike, na Filipo huko Kaisaria, pia na Mnasoni kwenye barabara ya kutoka Kaisaria hadi Yerusalemu. Akiwa safarini kwenda Roma, Paulo alikaribishwa na akina ndugu huko Puteoli. Hizo zilikuwa pindi zenye kuthawabisha kiroho kama nini kwa wale waliomkaribisha!—Matendo 16:33, 34; 17:7; 18:1-3; 21:8, 16; 28:13, 14.

Msomi Frederick F. Bruce anasema hivi: “Sababu moja iliyofanya marafiki hao na wafanyakazi wenzi, wakaribishaji wa kiume na wa kike wamsaidie sana ni kwamba walimpenda Paulo na Bwana ambaye Paulo alitumikia. Walijua kwamba kwa kumhudumia walikuwa wakimhudumia Kristo.” Hiyo ni sababu nzuri sana ya kutuchochea kuwa wakaribishaji.

Uhitaji wa kuonyesha ukaribishaji-wageni bado upo. Maelfu ya wawakilishi wasafirio wa Mashahidi wa Yehova hukaribishwa na waamini wenzao. Baadhi ya wahubiri wa Ufalme husafiri kwa gharama zao wenyewe ili kuhubiri katika maeneo ambayo habari njema haijahubiriwa. Hata kama nyumba zetu ni za hali ya chini, kuwakaribisha wahubiri hao wa Ufalme kunaweza kutokeza faida nyingi. Ukaribishaji mchangamfu ambao huenda ukatia ndani chakula cha kawaida tu, unaweza kutoa nafasi nzuri sana za “ubadilishanaji wa kitia-moyo” na kuonyesha upendo kwa ndugu zetu na kwa Mungu wetu. (Waroma 1:11, 12) Pindi kama hizo ni zenye kuthawabisha hasa kwa wakaribishaji, kwa kuwa “kuna furaha zaidi katika kutoa kuliko ilivyo katika kupokea.”—Matendo 20:35.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 11 Inakadiriwa kwamba kufikia mwaka wa 100 W.K., kulikuwa na barabara za Waroma zenye urefu wa kilometa 80,000 hivi za lami.

[Picha katika ukurasa wa 23]

Wakristo ‘hufuata mwendo wa ukaribishaji-wageni’