Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Sehemu Kuu ya Unabii Ilielekezwa Kwa Kristo

Sehemu Kuu ya Unabii Ilielekezwa Kwa Kristo

Sehemu Kuu ya Unabii Ilielekezwa Kwa Kristo

“Kutoa ushahidi kumhusu Yesu ndilo kusudi la unabii.”—UFUNUO 19:10.

1, 2. (a) Kuanzia mwaka wa 29 W.K., Waisraeli walikabili uamuzi gani? (b) Ni nini kitakachozungumziwa katika makala hii?

NI MWAKA wa 29 W.K. Wakaaji wa Israeli wanazungumza kwa shauku kuhusu Masihi aliyeahidiwa. Mahubiri ya Yohana Mbatizaji yamechochea tarajio hilo. (Luka 3:15) Yohana anakataa kuwa yeye ndiye Kristo. Badala yake, akielekeza kwa Yesu wa Nazareti anasema: “Nimetoa ushahidi kwamba huyo ndiye Mwana wa Mungu.” (Yohana 1:20, 34) Punde si punde, umati unamfuata Yesu ili kusikiliza mafundisho yake na kuponywa naye.

2 Miezi inayofuata, Yehova anatoa ushuhuda mwingi sana kuhusu Mwana wake. Wale ambao wamejifunza Maandiko na kuona kazi za Yesu wana msingi thabiti wa kumwamini. Hata hivyo, kwa ujumla watu waliofanya agano pamoja na Mungu wanaonyesha ukosefu wa imani. Ni wachache tu wanaokubali kwamba Yesu ni Kristo, Mwana wa Mungu. (Yohana 6:60-69) Ungefanya nini iwapo ungeishi wakati huo? Je, ungechochewa kumkubali Yesu kuwa Masihi na hivyo kuwa mfuasi wake mwaminifu? Fikiria uthibitisho kuhusu utambulisho wake ambao Yesu mwenyewe anatoa anaposhtakiwa kwamba anavunja Sabato, na ona uthibitisho anaotoa baadaye ili kuimarisha imani ya wanafunzi wake washikamanifu.

Yesu Mwenyewe Atoa Uthibitisho

3. Ni hali gani zilizomsukuma Yesu atoe uthibitisho kuhusu utambulisho wake?

3 Ni wakati wa Pasaka mwaka wa 31 W.K. Yesu yuko Yerusalemu. Ametoka tu kumponya mtu aliyekuwa mgonjwa kwa miaka 38. Hata hivyo, Wayahudi wanamtesa Yesu kwa kuwa amemponya mtu huyo siku ya Sabato. Pia wanamshutumu kuwa amekufuru, nao wanatafuta kumwua kwa sababu anamwita Mungu Baba yake. (Yohana 5:1-9, 16-18) Yesu anajitetea kwa kutoa sababu tatu zenye nguvu ambazo zingemsadikisha Myahudi yeyote aliye na moyo mnyoofu kuhusu utambulisho halisi wa Yesu.

4, 5. Ni nini lililokuwa kusudi la huduma ya Yohana, naye aliitimiza kikamili kadiri gani?

4 Kwanza, Yesu anataja ushahidi wa mtangulizi wake, Yohana Mbatizaji, akisema: “Ninyi mmetuma watu kwa Yohana, naye ametoa ushahidi kwa ile kweli. Mtu huyo alikuwa taa yenye kuwaka na yenye kung’aa, nanyi kwa wakati mfupi mlikuwa na nia ya kushangilia sana katika nuru yake.”—Yohana 5:33, 35.

5 Yohana Mbatizaji alikuwa “taa yenye kuwaka na yenye kung’aa” katika maana ya kwamba kabla Herode hajamfunga gerezani isivyo haki, alikuwa ametimiza kazi aliyopewa na Mungu ya kumtayarishia Masihi njia. Yohana alisema: “Nilikuja nikibatiza katika maji ili [Masihi] apate kufunuliwa kwa Israeli. . . . Niliona roho ikishuka kama njiwa kutoka mbinguni, nayo ikakaa juu yake. Hata sikumjua, bali Yule aliyenituma nibatize katika maji aliniambia, ‘Yeyote yule ambaye utaona roho ikishuka na kukaa juu yake, huyo ndiye ambaye hubatiza katika roho takatifu.’ Nami nimeona, na nimetoa ushahidi kwamba huyo ndiye Mwana wa Mungu.” * (Yohana 1:26-37) Yohana alimtambulisha Yesu waziwazi kuwa Mwana wa Mungu, yaani, Masihi aliyeahidiwa. Ushahidi wa Yohana ulikuwa wazi sana hivi kwamba miezi minane hivi baada ya kifo chake, Wayahudi wengi wenye mioyo minyoofu walikiri hivi: “Mambo mengi ambayo Yohana alisema juu ya mtu huyu, yote yalikuwa ya kweli.”—Yohana 10:41, 42.

6. Kwa nini kazi za Yesu zilipaswa kuwasadikisha watu kwamba alikuwa anaungwa mkono na Mungu?

6 Kisha, Yesu anatumia sababu nyingine yenye nguvu ili kuthibitisha kwamba yeye ndiye Masihi. Anataja kazi zake nzuri kuwa uthibitisho wa kwamba anaungwa mkono na Mungu. Yeye anasema: “Mimi nina ushahidi ulio mkubwa zaidi kuliko ule wa Yohana, kwa maana kazi zilezile ambazo Baba yangu alinigawia kutimiza, kazi hizo zenyewe ambazo ninafanya, hutoa ushahidi juu yangu kwamba Baba alinituma.” (Yohana 5:36) Hata maadui wa Yesu hawangeweza kukanusha uthibitisho huu ambao ulitia ndani miujiza mingi. Baadhi yao wanauliza hivi baadaye: “Tufanye nini, kwa sababu mtu huyu anafanya ishara nyingi?” (Yohana 11:47) Hata hivyo, wengine wanaitikia vizuri na kusema: “Kristo atakapofika, je, atafanya ishara zaidi ya zile ambazo mtu huyu amefanya?” (Yohana 7:31) Wasikilizaji wa Yesu walikuwa na nafasi nzuri sana ya kuona sifa za Baba zikionyeshwa na Mwana.—Yohana 14:9.

7. Maandiko ya Kiebrania hutoaje ushahidi kumhusu Yesu?

7 Mwishowe, Yesu anaelekeza fikira kwenye ushahidi usioweza kukanushwa. Anasema: “Maandiko . . . ndiyo yanayotoa ushahidi juu yangu,” kisha anaongezea: “Ikiwa mngalimwamini Musa mngaliniamini mimi, kwa maana huyo aliandika juu yangu.” (Yohana 5:39, 46) Bila shaka, Musa alikuwa tu mmoja wa mashahidi wengi waliokuwako kabla ya Ukristo ambao waliandika juu ya Kristo. Maandishi yao yalitia ndani unabii mwingi na nasaba kamili ambayo ingemtambulisha Masihi. (Luka 3:23-38; 24:44-46; Matendo 10:43) Namna gani Sheria ya Musa? Mtume Paulo aliandika: “Sheria imekuwa mtunzaji wetu kutuongoza kwa Kristo.” (Wagalatia 3:24) Naam, “kutoa ushahidi kumhusu Yesu ndilo kusudi [au, mwelekeo wote, au lengo] la unabii.”—Ufunuo 19:10.

8. Kwa nini Wayahudi wengi hawakumwamini Masihi?

8 Je, uthibitisho huo wote, yaani, ushahidi ulio wazi wa Yohana, kazi zenye nguvu na sifa za kimungu za Yesu, na ushuhuda mwingi sana wa Maandiko haukusadikishi kwamba Yesu alikuwa Masihi? Mtu yeyote aliyempenda Mungu kikweli na Neno lake angetambua jambo hilo mara moja na kuamini kwamba Yesu ndiye Masihi aliyeahidiwa. Hata hivyo, kwa ujumla Waisraeli hawakuwa na upendo huo. Yesu aliwaambia hivi wapinzani wake: “Ninajua vizuri kwamba ninyi hammpendi Mungu ndani yenu.” (Yohana 5:42) Badala ya ‘kutafuta utukufu unaotoka kwa Mungu wa pekee,’ walikuwa ‘wakikubali utukufu kutoka kwa mtu na mwenzake.’ Haishangazi kwamba hawakukubaliana na Yesu ambaye kama Baba yake, huchukia maoni kama hayo!—Yohana 5:43, 44; Matendo 12:21-23.

Waimarishwa na Maono ya Kinabii

9, 10. (a) Kwa nini ishara ambayo wanafunzi wa Yesu walipewa ilitukia wakati unaofaa? (b) Yesu alitoa ahadi gani muhimu kwa wanafunzi wake?

9 Mwaka mmoja hivi umepita tangu Yesu atoe uthibitisho ambao umetajwa kwamba yeye ndiye Masihi. Pasaka ya mwaka wa 32 W.K. imepita. Wengi waliomwamini Yesu wameacha kumfuata pengine kwa sababu ya mateso, ufuatiaji wa vitu vya kimwili, au mahangaiko ya maisha. Huenda wengine wametatanika au kukata tamaa kwa sababu Yesu alikataa jitihada za watu za kumfanya mfalme. Alipojaribiwa na viongozi wa kidini Wayahudi, alikataa kuwapa ishara kutoka mbinguni ili kujitukuza. (Mathayo 12:38, 39) Huenda watu fulani walichanganyikiwa alipokataa kufanya hivyo. Isitoshe, Yesu ameanza kuwafunulia wanafunzi wake jambo fulani ambalo wanaona ni vigumu sana kulielewa—“lazima aende Yerusalemu na kupatwa na mambo mengi kutoka kwa wanaume wazee na wakuu wa makuhani na waandishi, na kuuawa.”—Mathayo 16:21-23.

10 Katika muda wa miezi tisa au kumi hivi, wakati ungefika ‘wa Yesu kutoka katika ulimwengu huu kwenda kwa Baba.’ (Yohana 13:1) Kwa kuwahangaikia sana wanafunzi wake washikamanifu, Yesu anawaahidi baadhi yao jambo lilelile alilokataa kuwapa Wayahudi wasio na imani, yaani, ishara kutoka mbinguni. “Kwa kweli ninawaambia ninyi,” Yesu anasema, “kuna baadhi ya wale wanaosimama hapa ambao hawataonja kifo kamwe mpaka kwanza wamwone Mwana wa binadamu akija katika ufalme wake.” (Mathayo 16:28) Ni wazi kwamba Yesu hamaanishi kuwa baadhi ya wanafunzi hao watakuwa hai wakati Ufalme wa Kimasihi unaposimamishwa mbinguni mwaka wa 1914. Yesu anafikiria kuwaonyesha wanafunzi wake wa karibu sana maono ya kimbele yenye kustaajabisha ya utukufu atakaokuwa nao akiwa Mtawala wa Ufalme. Maono hayo yanaitwa mgeuko-sura.

11. Eleza maono ya kugeuka sura.

11 Siku sita baadaye, Yesu anawachukua Petro, Yakobo, na Yohana na kuwapandisha katika mlima mrefu—yaelekea ni safu ya Mlima Hermoni. Wakiwa huko, ‘sura ya Yesu inageuka mbele yao, na uso wake unang’aa kama jua, na mavazi yake ya nje yanang’aa kama nuru.’ Pia manabii Musa na Eliya wanatokea, nao wanaongea na Yesu. Yaelekea jambo hilo lenye kutia hofu linatokea usiku, hivyo linaonekana waziwazi. Kwa kweli, linakuwa halisi sana hivi kwamba Petro anajitolea kusimamisha mahema matatu—moja la Yesu, moja la Musa, na moja la Eliya. Petro akiwa bado anaongea, wingu jangavu linawafunika na sauti kutoka katika lile wingu inasema: “Huyu ni Mwanangu, mpendwa, ambaye nimemkubali; msikilizeni.”—Mathayo 17:1-6.

12, 13. Maono ya kugeuka sura yalikuwa na matokeo gani kwa wanafunzi wa Yesu, na kwa nini?

12 Ni kweli kwamba muda mfupi kabla ya hapo, Petro alikuwa ametoa ushuhuda kwamba Yesu “ndiye Kristo, Mwana wa Mungu aliye hai.” (Mathayo 16:16) Lakini hebu wazia ukisikia Mungu mwenyewe akitoa ushuhuda kuthibitisha utambulisho na daraka la Mwana wake mtiwa-mafuta! Kwa kweli maono hayo ya kugeuka sura yanaimarisha sana imani ya Petro, Yakobo, na Yohana. Wakiwa na imani iliyoimarishwa sana, sasa wako tayari kukabiliana na mambo yaliyo mbele na daraka muhimu ambalo watatimiza katika kutaniko la wakati ujao.

13 Maono hayo ya kugeuka sura yanabaki akilini mwa wanafunzi hao. Zaidi ya miaka 30 baadaye, Petro anaandika: “[Yesu] alipokea kutoka kwa Mungu Baba heshima na utukufu, wakati maneno ya namna hii yalipotolewa kwake kwa utukufu wenye fahari: ‘Huyu ni mwanangu, mpendwa wangu, ambaye mimi mwenyewe nimemkubali.’ Ndiyo, maneno hayo tuliyasikia yakitoka mbinguni tulipokuwa tungali pamoja naye katika ule mlima mtakatifu.” (2 Petro 1:17, 18) Yohana pia anachochewa na tukio hilo. Zaidi ya miaka 60 baadaye, yaelekea Yohana analitaja tukio hilo anaposema maneno haya: ‘Tuliutazama utukufu wake, utukufu kama ule ulio wa mwana mzaliwa-pekee kutoka kwa baba.’ (Yohana 1:14) Hata hivyo, maono ya kugeuka sura hayakuwa maono ya mwisho waliopewa wafuasi wa Yesu.

Nuru Zaidi kwa Washikamanifu wa Mungu

14, 15. Ni katika njia gani mtume Yohana angekaa mpaka Yesu aje?

14 Baada ya kufufuliwa, Yesu anawatokea wanafunzi wake kando ya Bahari ya Galilaya. Huko, anamwambia Petro: “Ikiwa ni mapenzi yangu [Yohana] akae mpaka nije, hilo linakuhusu nini wewe?” (Yohana 21:1, 20-22, 24) Je, maneno hayo yanaonyesha kwamba mtume Yohana angeishi muda mrefu zaidi kuliko mitume wengine? Yaelekea hivyo, kwa kuwa Yohana anamtumikia Yehova kwa uaminifu kwa miaka mingine 70 hivi. Hata hivyo, maneno ya Yesu yanaonyesha jambo muhimu zaidi kuliko muda ambao Yohana angeishi.

15 Maneno “mpaka nije” yanatukumbusha maneno ya Yesu kuhusu “Mwana wa binadamu akija katika ufalme wake.” (Mathayo 16:28) Yohana anakaa hadi Yesu aje katika maana ya kwamba baadaye Yohana anapewa maono ya kinabii ya Yesu akija akiwa Mtawala wa Ufalme. Yohana anapokaribia mwisho wa maisha yake akiwa uhamishoni kwenye kisiwa cha Patmo, anapokea Ufunuo wenye ishara za kinabii zenye kushangaza za mambo ambayo yatatukia katika “siku ya Bwana.” Yohana anachochewa sana na maono hayo yenye kustaajabisha hivi kwamba Yesu anaposema: “Ndiyo; mimi ninakuja upesi,” Yohana anapaaza sauti na kusema: “Amina! Njoo, Bwana Yesu.”—Ufunuo 1:1, 10; 22:20.

16. Kwa nini ni muhimu tuendelee kuimarisha imani yetu?

16 Watu wenye mioyo minyoofu wanaoishi katika karne ya kwanza wanamkubali Yesu kuwa Masihi na kumwamini. Wale wanaokuwa waamini wanahitaji kuimarishwa kwa sababu ya kazi wanayopaswa kufanya, wengine kukosa imani, na majaribu yaliyo mbele yao. Yesu ametoa uthibitisho wa kutosha kwamba yeye ndiye Masihi, naye ametoa maono ya kinabii yenye kuelimisha ili kuwaimarisha wafuasi wake washikamanifu. Leo, tunaishi wakati wa mwisho-mwisho wa “siku ya Bwana.” Hivi karibuni, Kristo ataharibu mfumo wote mwovu wa mambo wa Shetani na kuwakomboa watu wa Mungu. Lazima sisi pia tuimarishe imani yetu kwa kutumia kikamili maandalizi yote ya Yehova kwa ajili ya hali yetu njema ya kiroho.

Kuhifadhiwa Wakati wa Giza na Dhiki

17, 18. Katika karne ya kwanza, kulikuwa na tofauti gani kubwa kati ya wafuasi wa Yesu na wale waliopinga kusudi la Mungu, na matokeo yalikuwaje kwa kila kikundi?

17 Baada ya kifo cha Yesu, wanafunzi wanatii kwa ujasiri amri yake ya kutoa ushahidi juu yake “katika Yerusalemu na pia katika Yudea yote na Samaria na mpaka sehemu ya mbali zaidi ya dunia.” (Matendo 1:8) Licha ya pindi zenye mateso makali, Yehova analibariki kutaniko jipya la Kikristo kwa nuru ya kiroho na pia kulipatia wanafunzi wapya wengi.—Matendo 2:47; 4:1-31; 8:1-8.

18 Kwa upande mwingine, matarajio ya wale wanaopinga habari njema yanazidi kudidimia hatua kwa hatua. Methali 4:19 inasema: “Njia ya waovu ni kama giza; hawajui ni nini kinachoendelea kuwakwaza.” “Giza” hilo linaongezeka mwaka wa 66 W.K. majeshi ya Roma yanapozingira Yerusalemu. Baada ya kuondoka kwa muda kwa sababu isiyojulikana, Waroma wanarudi mwaka wa 70 W.K., na kuliharibu jiji. Kulingana na mwanahistoria Myahudi Yosefu, zaidi ya Wayahudi milioni moja wanakufa. Hata hivyo, Wakristo waaminifu wanatoroka. Kwa nini? Kwa sababu majeshi ya Roma yanapoondoka kwa muda, wanatii amri ya Yesu na kukimbia.—Luka 21:20-22.

19, 20. (a) Kwa nini watu wa Mungu hawapaswi kuogopa mwisho wa mfumo huu wa mambo unapokaribia? (b) Yehova aliwapa watu wake ufahamu gani wenye kutokeza makumi ya miaka kabla ya 1914?

19 Hali yetu inafanana na hiyo. Dhiki kuu inayokuja itamaanisha mwisho wa mfumo wote mwovu wa Shetani. Lakini watu wa Mungu hawapaswi kuogopa, kwa kuwa Yesu aliahidi: “Tazama! mimi nipo pamoja nanyi siku zote mpaka umalizio wa mfumo wa mambo.” (Mathayo 28:20) Ili kuimarisha imani ya wanafunzi wake wa mapema na kuwatayarisha kukabiliana na mambo yaliyokuwa mbele, Yesu aliwapa maono kuhusu utukufu wake wa kimbingu akiwa Mfalme wa Kimasihi. Namna gani leo? Maono hayo yalitimizwa mwaka wa 1914. Nayo yameimarisha sana imani ya watu wa Mungu. Yanatoa ahadi ya wakati ujao ulio mzuri, nao watumishi wa Yehova wamepewa ufahamu unaoongezeka kuhusu Ufalme huo wa Kimasihi. Katikati ya hali za ulimwengu zinazozidi kuzorota, “njia ya waadilifu ni kama nuru inayong’aa, inayozidi kuongezeka mpaka mchana mkamilifu.”—Methali 4:18.

20 Hata kabla ya mwaka wa 1914, kikundi kidogo cha Wakristo watiwa-mafuta kilianza kuelewa kweli muhimu kuhusu kurudi kwa Bwana. Kwa mfano, walitambua kwamba kurudi kwa Bwana hakutaonekana kwa macho, kama ilivyodokezwa na malaika wawili waliowatokea wanafunzi mwaka wa 33 W.K., Yesu alipokuwa akipaa mbinguni. Baada ya wingu kumchukua Yesu juu kutoka machoni pao, malaika hao walisema: “Yesu huyu aliyepokewa juu angani kutoka kwenu atakuja vivyo hivyo kama vile ambavyo mmemwona akienda angani.”—Matendo 1:9-11.

21. Ni nini kitakachozungumziwa katika makala inayofuata?

21 Ni wafuasi washikamanifu wa Yesu peke yao waliomwona akiondoka. Si kila mtu aliyeona maono ya kugeuka sura; ulimwengu kwa ujumla hata haukujua kilichotokea. Ingekuwa hivyo wakati ambapo Kristo angerudi akiwa Mtawala wa Ufalme. (Yohana 14:19) Ni wanafunzi wake waaminifu walio watiwa-mafuta ambao wangetambua kuwapo kwake akiwa Mfalme. Katika makala inayofuata, tutaona jinsi ambavyo ufahamu huo ungekuwa na matokeo makubwa kwao, na kufikia upeo katika kukusanywa kwa mamilioni ya watu ambao watakuwa raia wa Yesu duniani.—Ufunuo 7:9, 14.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 5 Yaonekana kwamba wakati wa ubatizo wa Yesu, Yohana peke yake ndiye aliyesikia sauti ya Mungu. Wayahudi ambao Yesu anazungumza nao ‘hawajasikia sauti ya Mungu wakati wowote wala kuona umbo lake.’—Yohana 5:37.

Je, Unakumbuka?

• Yesu aliposhutumiwa kwamba alivunja Sabato na kukufuru, alitoa uthibitisho gani ili kuonyesha kwamba alikuwa Masihi?

• Wanafunzi wa Yesu wa mapema walifaidikaje na maono ya kugeuka sura?

• Yesu alimaanisha nini aliposema kwamba Yohana angekaa mpaka aje?

• Ni maono gani ya kimbele yaliyotimizwa katika mwaka wa 1914?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 10]

Yesu alitoa uthibitisho kwamba alikuwa Masihi

[Picha katika ukurasa wa 12]

Maono ya kugeuka sura yaliimarisha imani

[Picha katika ukurasa wa 13]

Yohana angekaa mpaka Yesu ‘aje’