Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Uzee Unapokuwa “Taji la Uzuri”

Uzee Unapokuwa “Taji la Uzuri”

“Msaada Wangu Unatoka Kwa Yehova”

Uzee Unapokuwa “Taji la Uzuri”

“HAYO ndiyo maisha bora zaidi,” akasema Muriel mwenye umri wa miaka 101. “Ni pendeleo kwelikweli!” ndivyo alivyosema Theodoros mwenye umri wa miaka 70. “Singeweza kutumia maisha yangu kwa njia bora zaidi kuliko hii,” akasema Maria mwenye umri wa miaka 73. Wote hao wametumia maisha yao katika utumishi wa Yehova Mungu.

Wazee hao wanawakilisha waabudu wengi wa Yehova wenye bidii ulimwenguni pote. Licha ya uzee, mahangaiko ya afya, na hali nyingine ngumu, bado wanamtumikia Mungu kwa nafsi yote. Katika kutaniko la Kikristo, waaminifu hao walio wazee kwa umri wanaheshimiwa na kuonwa kuwa vielelezo vya ujitoaji-kimungu. Yehova anathamini sana utumishi wa wale walio wazee hata ingawa huenda hali zao zisiwaruhusu kufanya mengi. *2 Wakorintho 8:12.

Kitabu cha Zaburi kinataja mambo mazuri kuhusu maisha ambayo waaminifu walio wazee wanaweza kutarajia. Wanaweza kuwa kama mti wa zamani na wenye fahari ambao unaendelea kuzaa matunda. Mtunga-zaburi aliimba hivi kuhusu wazee waaminifu: “Bado wataendelea kusitawi wakati wa kuwa na kichwa chenye mvi, wataendelea kuwa wanono na wabichi.”—Zaburi 92:14.

Huenda wengine wakaogopa kwamba watakataliwa na kupuuzwa watakapoishiwa na nguvu kwa sababu ya uzee. Daudi alimsihi Mungu hivi: “Usinitupe wakati wa uzee; wakati tu nguvu zangu zinapungua, usiniache.” (Zaburi 71:9) Ni nini kinachoweza kufanya mtu asitawi badala ya kudhoofika anapozeeka? Ni sifa ya kimungu ya uadilifu. Mtunga-zaburi aliimba hivi: “Mwadilifu atachanua kama mtende.”—Zaburi 92:12.

Yaelekea wale ambao wametumia maisha yao kikamili katika kumtumikia Mungu kwa uaminifu huendelea kuzaa matunda mazuri wanapozeeka. Kwa kweli, mbegu nyingi ambazo wamepanda katika maisha yao au katika maisha ya wengine huchipuka na kukomaa na hivyo kutokeza mavuno mazuri. (Wagalatia 6:7-10; Wakolosai 1:10) Bila shaka, wale ambao wametumia maisha yao kwa kufuatia mambo ya kibinafsi ambayo hukiuka njia za Mungu, kwa kawaida hawaoni maisha yao kuwa yenye thamani wanapozeeka.

Pia kitabu cha Biblia cha Methali kinakazia kwamba uadilifu ni kama pambo la uzee. Tunasoma hivi katika kitabu hicho: “Kichwa chenye mvi ni taji la uzuri kinapopatikana katika njia ya uadilifu.” (Methali 16:31) Naam, uadilifu huonyesha uzuri wa ndani. Kufuata njia ya uadilifu maishani huleta heshima. (Mambo ya Walawi 19:32) Mtu ambaye ana mvi kwa sababu ya uzee na ambaye pia ana hekima na wema wa adili huheshimiwa.—Ayubu 12:12.

Yehova hufurahi sana mtu anapotumia maisha yake kwa unyoofu kumtumikia. Maandiko husema: “Hata uzeeni mwa mtu mimi [Yehova] ni Yeye yuleyule; na hata wakati wa kichwa chenye mvi cha mtu nitaendelea kubeba. Mimi mwenyewe hakika nitatenda, ili mimi mwenyewe nichukue na ili mimi mwenyewe nibebe na kuponyosha.” (Isaya 46:4) Inafariji kama nini kujua kwamba Baba yetu wa mbinguni mwenye upendo anaahidi kuwasaidia na kuwategemeza washikamanifu wake wanapozeeka!—Zaburi 48:14.

Kwa kuwa Yehova hufurahi mtu anapotumia maisha yake kwa uaminifu kumtumikia, je, wengine pia hawapaswi kumheshimu mtu huyo? Kuwa na maoni ya Mungu hufanya tuwathamini waamini wenzetu walio wazee. (1 Timotheo 5:1, 2) Kwa hiyo na tufikirie njia halisi za kuonyesha upendo wa Kikristo kwa kuwatimizia mahitaji yao.

Kutembea Katika Mapito ya Uadilifu Uzeeni

Sulemani anatuhakikishia hivi: “Katika mapito ya uadilifu kuna uzima.” (Methali 12:28) Uzee haumzuii mtu kutembea katika mapito hayo. Kwa mfano, nchini Moldova, mzee mmoja mwenye umri wa miaka 99 alikuwa ametumia ujana wake kuendeleza siasa za Kikomunisti. Alijigamba kwamba alizungumza uso kwa uso na viongozi mashuhuri wa Kikomunisti, kama vile V. I. Lenin. Hata hivyo, baada ya Ukomunisti kuporomoka, mwanamume huyo mzee alipoteza mwelekeo na kusudi la maisha. Lakini Mashahidi wa Yehova walipomwonyesha kwamba Ufalme wa Mungu ndio suluhisho pekee kwa matatizo ya wanadamu, alikubali kweli ya Biblia na kuwa mwanafunzi wa Biblia mwenye bidii. Kwa kusikitisha, alikufa kabla ya kubatizwa na kuwa mtumishi wa Yehova.

Alipokuwa akijifunza matakwa ya Mungu ya maadili, mwanamke mmoja mwenye umri wa miaka 81 huko Hungaria alitambua kwamba alihitaji kuolewa na mwanamume aliyeishi naye miaka kadhaa. Mwanamke huyo alijipa ujasiri na kumweleza mwanamume huyo maoni yake yanayotegemea Biblia. Alishangaa na kufurahi sana mwanamume huyo alipokubali kumwoa. Baada ya kuhalalisha ndoa yao, mwanamke huyo alifanya maendeleo ya kiroho haraka. Miezi minane baada ya kuanza kujifunza Biblia, akawa mhubiri asiyebatizwa, naye akabatizwa muda mfupi baada ya hapo. Ni kweli kwamba uadilifu unaweza kufanya wazee waonyeshe uzuri halisi.

Naam, Wakristo waaminifu walio wazee wanaweza kuwa na hakika kwamba Mungu anapendezwa nao. Yehova hatawaacha wale wanaoendelea kuwa washikamanifu kwake. Badala yake, anaahidi kuwaongoza, kuwasaidia, na kuwategemeza hata wanapozeeka. Nao wanathibitisha maneno haya ya mtunga-zaburi: “Msaada wangu unatoka kwa Yehova.”—Zaburi 121:2.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 4 Ona Kalenda ya Mwaka wa 2005 ya Mashahidi wa Yehova, Januari/Februari.

[Blabu katika ukurasa wa 9]

“Kichwa chenye mvi ni taji la uzuri kinapopatikana katika njia ya uadilifu.”—METHALI 16:31

[Sanduku katika ukurasa wa 8]

YEHOVA ANAWAJALI WATUMISHI WAKE WALIO WAZEE

“Unapaswa kusimama mbele ya mtu mwenye mvi, nawe umwonyeshe ufikirio mtu mzee.”—Mambo ya Walawi 19:32.

“Hata uzeeni mwa mtu mimi ni Yeye yuleyule; na hata wakati wa kichwa chenye mvi cha mtu nitaendelea kubeba.”—Isaya 46:4.