Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Uhai Una Thamani au Hauna?

Je, Uhai Una Thamani au Hauna?

Je, Uhai Una Thamani au Hauna?

“Kwa kuwa mtu ameumbwa kwa mfano wa Mungu, hivyo kuua binadamu ni kuharibu kitu chenye thamani zaidi na kitakatifu zaidi ulimwenguni.”—The Plain Man’s Guide to Ethics, kilichoandikwa na William Barclay.

‘KITU chenye thamani zaidi ulimwenguni.’ Je, unakubaliana na maoni hayo kuhusu uhai? Kutokana na jinsi watu wanavyojiendesha, ni wazi kwamba wengi hawakubaliani na mwandikaji huyo. Mamilioni ya watu wameuawa kikatili na watu wenye jeuri wanaofuatia miradi yenye ubinafsi bila kujali hali ya wanadamu wenzao.—Mhubiri 8:9.

Wasiofaa na Wasio na Thamani

Vita vya Kwanza vya Ulimwengu ni mfano halisi. Wakati wa vita hivyo vibaya sana, mara nyingi “watu waliuawa bila kusudi lolote,” anasema mwanahistoria A.J.P. Taylor. Ili kupata umashuhuri na utukufu, viongozi wa kijeshi walitumia askari kana kwamba hawakufaa au hawakuwa na thamani yoyote. Katika vita vilivyopiganwa huko Verdun, Ufaransa, askari zaidi ya nusu milioni waliuawa. Taylor anaandika hivi: “Hakukuwa na tuzo [lenye thamani yoyote] lililopatikana au kupotezwa, ni watu tu waliouawa na wengine kujipatia utukufu.”—The First World War.

Katika sehemu nyingi watu hawathamini uhai. Msomi Kevin Bales anasema kwamba hivi karibuni, “ongezeko kubwa la watu limefanya idadi ya mamilioni ya watu maskini na dhaifu wanaotafuta kazi ulimwenguni iongezeke.” Wanapambana katika muda wote wa maisha yao ili kuendeleza maisha tu katika mfumo wa kibiashara wenye kukandamiza ambamo “maisha hayana thamani.” Bales anasema kwamba, wale wanaowakandamiza huwatendea kama watumwa, yaani, “kama vyombo visivyo na thamani hata kidogo ili kujitajirisha.”—Disposable People.

“Kufuatilia Upepo”

Kuna sababu nyingine nyingi zinazofanya watu wengi wahisi kuwa hawafai na wakate tamaa kwamba hakuna anayejali kama wataendelea kuishi ama watakufa. Mbali na vita na ukosefu wa haki, kuna maafa yanayosababishwa na ukame, njaa, magonjwa, misiba, na mambo mengine mengi ambayo yanawatesa wanadamu wote, na kufanya watu wajiulize ikiwa uhai una thamani yoyote.—Mhubiri 1:8, 14.

Bila shaka, si kila mtu anayekabili hali ngumu na maumivu makali maishani mwake. Lakini hata wale ambao hawapatwi na mateso makali kama hayo hukubaliana na maneno ya Mfalme Sulemani wa Israeli la kale aliyeuliza hivi: “Mwanadamu hupata nini kwa ajili ya kazi yake yote iliyo ngumu na kwa ajili ya jitihada za moyo wake katika kufanya kazi ngumu chini ya jua?” Baada ya kufikiria mambo hayo, wengi wametambua kwamba mengi ya yale waliyotimiza yalikuwa “ubatili na kufuatilia upepo.”—Mhubiri 2:22, 26.

Wanapofikiria yale waliyotimiza maishani, wengi hujiuliza: “Je, uzima ndio huuhuu tu?” Naam, ni wangapi wanaohisi kwa kweli kwamba wametosheka na siku kama alivyohisi mzee wa ukoo Abrahamu? (Mwanzo 25:8) Wengi huhisi kwamba maisha yataendelea kuwa ya ubatili. Hata hivyo, si lazima maisha yawe yenye ubatili. Mungu huona uhai wa kila mwanadamu kuwa wenye thamani, naye hutaka kila mtu awe na maisha makamilifu na yenye kuridhisha. Hilo litatukiaje? Chunguza yale yanayozungumziwa katika makala inayofuata kuhusu habari hiyo.