Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kufuatilia ‘Lulu ya Thamani Kubwa’ Leo

Kufuatilia ‘Lulu ya Thamani Kubwa’ Leo

Kufuatilia ‘Lulu ya Thamani Kubwa’ Leo

“Hii habari njema ya ufalme itahubiriwa katika dunia yote inayokaliwa ili kuwa ushahidi.”—MATHAYO 24:14.

1, 2. (a) Wayahudi katika siku za Yesu walikuwa na maoni gani kuhusu Ufalme wa Mungu? (b) Yesu alifanya nini ili kuwasaidia wanafunzi waelewe vizuri zaidi kuhusu Ufalme, na matokeo yalikuwa nini?

YESU alipokuwa duniani, Wayahudi walipendezwa sana kuzungumza kuhusu Ufalme wa Mungu. (Mathayo 3:1, 2; 4:23-25; Yohana 1:49) Hata hivyo, mwanzoni wengi wao hawakuelewa kikamili mamlaka ya Ufalme huo na ukubwa wa eneo ambalo ungetawala; wala hawakuelewa kwamba ungekuwa serikali ya kimbingu. (Yohana 3:1-5) Hata watu fulani ambao walipata kuwa wafuasi wa Yesu hawakuelewa kikamili Ufalme wa Mungu ni nini au mambo waliyopaswa kufanya ili wapate kibali cha kuwa watawala pamoja na Kristo.—Mathayo 20:20-22; Luka 19:11; Matendo 1:6.

2 Kadiri wakati ulivyopita, Yesu aliwafundisha kwa subira wanafunzi wake mambo mengi kutia ndani ule mfano wa lulu ya thamani kubwa ambao tulizungumzia katika makala iliyotangulia, na kuwatajia umuhimu wa kujitahidi kufuatilia Ufalme wa mbinguni. (Mathayo 6:33; 13:45, 46; Luka 13:23, 24) Lazima mambo hayo yawe yaligusa sana mioyo yao kwa sababu punde si punde walitangaza kwa ujasiri na bila kuchoka habari njema ya Ufalme hadi sehemu za mbali za dunia kama kitabu cha Matendo kinavyothibitisha.—Matendo 1:8; Wakolosai 1:23.

3. Kwa habari ya siku zetu,Yesu alisema nini kuhusu Ufalme?

3 Basi, namna gani leo? Mamilioni ya watu wanahubiriwa kuhusu baraka za paradiso hapa duniani chini ya Ufalme. Katika unabii wake muhimu kuhusu “umalizio wa mfumo wa mambo,” Yesu alisema hivi kihususa: “Hii habari njema ya ufalme itahubiriwa katika dunia yote inayokaliwa ili kuwa ushahidi kwa mataifa yote; na ndipo ule mwisho utakapokuja.” (Mathayo 24:3, 14; Marko 13:10) Pia alieleza kwamba kazi hiyo kubwa itafanywa licha ya vizuizi na magumu yenye kutisha, na hata mateso. Hata hivyo, alitoa uhakikisho huu: “Yule ambaye atavumilia mpaka mwisho ndiye atakayeokolewa.” (Mathayo 24:9-13) Mambo hayo yote hutaka tujidhabihu na kujitoa kama yule mwanabiashara msafiri katika mfano wa Yesu. Je, leo kuna watu wanaoonyesha imani na bidii kama hiyo katika kufuatilia Ufalme?

Shangwe ya Kupata Ukweli

4. Kweli ya Ufalme ina matokeo gani kwa watu leo?

4 Mwanabiashara katika mfano wa Yesu alikuwa na shangwe kubwa alipopata kile alichoona kuwa ‘lulu ya thamani kubwa.’ Shangwe hiyo ilimchochea kufanya yote awezayo ili kupata lulu hiyo. (Waebrania 12:1) Vivyo hivyo leo, kweli kumhusu Mungu na Ufalme wake huwavuta na kuwachochea watu. Hilo hutukumbusha maneno ya Ndugu A. H. Macmillan aliyeandika kuhusu jinsi alivyomtafuta Mungu na kusudi Lake kwa wanadamu, katika kitabu Faith on the March. Alisema hivi: “Kile ambacho nimepata, maelfu ya watu bado wanakipata kila mwaka. Nao ni watu kama mimi na wewe, kwa sababu wametoka katika mataifa, rangi, na matabaka mbalimbali na ni wa umri mbalimbali. Kweli haibagui mtu yeyote. Huwavuta watu wa aina zote.”

5. Ni matokeo gani mazuri yanayoonekana katika ripoti ya mwaka wa utumishi wa 2004?

5 Ukweli wa maneno hayo huonekana kila mwaka mamia ya maelfu ya watu wanyoofu wanapochochewa na habari njema ya Ufalme wa Mungu na kujiweka wakfu kwa Yehova na kufanya mapenzi yake. Ndivyo ilivyokuwa mwaka wa utumishi wa 2004 ambao ulianza Septemba 2003 hadi Agosti 2004. Katika miezi hiyo 12, watu 262,416 walionyesha hadharani wakfu wao kwa kubatizwa katika maji. Jambo hilo lilitukia katika nchi 235, ambako Mashahidi wa Yehova wanaongoza mafunzo ya Biblia ya nyumbani 6,085,387 kila juma ili kuwasaidia watu wa matabaka, mataifa, kabila, na lugha zote wapate kweli inayotoa uhai kutoka katika Neno la Mungu.—Ufunuo 7:9.

6. Ni nini kimechangia ongezeko lenye kuendelea kila mwaka?

6 Mambo hayo yote yaliwezekanaje? Hapana shaka kwamba Yehova huwavuta watu hao wenye mwelekeo unaofaa. (Yohana 6:65; Matendo 13:48) Hata hivyo, hatupaswi kupuuza roho ya kujidhabihu na jitihada yenye bidii ya wale ambao wamejitoa kabisa kufuatilia Ufalme. Akiwa na umri wa miaka 79, Ndugu Macmillan aliandika: “Tangu nilipojifunza kwa mara ya kwanza kuhusu ahadi za Biblia kwa wanadamu wanaopatwa na ugonjwa na kifo, tumaini langu katika ujumbe wa Biblia halijafifia. Papo hapo, niliazimia kujifunza mengi kuhusu mafundisho ya Biblia ili niweze kuwasaidia wengine ambao, kama mimi, wanatafuta kumjua Mungu Mweza-Yote, Yehova, na makusudi yake mazuri kuelekea wanadamu.”

7. Ni jambo gani lililoonwa ambalo linaonyesha shangwe na bidii ya wale wanaopata kweli ya Biblia?

7 Bidii hiyo inaonekana pia miongoni mwa watumishi wa Yehova leo. Kwa mfano, fikiria Daniela, kutoka Vienna, Austria. Alisema: “Tangu utoto wangu, Mungu amekuwa rafiki yangu mkubwa zaidi. Sikuzote nilitaka kujua jina lake kwa sababu neno ‘Mungu’ halikuwa na utu hata kidogo. Lakini ilinibidi kungoja hadi nilipofika umri wa miaka 17, wakati Mashahidi wa Yehova waliponitembelea. Walinieleza yote niliyotaka kujua kumhusu Mungu. Mwishowe, nilipata kweli, nayo ilikuwa nzuri sana! Nilisisimuka sana hivi kwamba nilianza kuhubiria kila mtu.” Punde si punde, shauku yake ilifanya wanafunzi wenzake wamdhihaki. Daniela aliendelea kusema, “Hata hivyo, mimi niliona jambo hilo kuwa utimizo wa unabii wa Biblia kwa sababu nilikuwa nimejifunza kwamba Yesu alisema wafuasi wake wangechukiwa na kuteswa kwa ajili ya jina lake. Nilifurahi sana na kushangaa.” Punde si punde, Daniela alijiweka wakfu kwa Yehova na kubatizwa na akaanza kufuatilia mradi wa kuwa mmishonari. Baada ya kuolewa, Daniela pamoja na mume wake, Helmut, walianza kuwahubiria Waafrika, Wachina, Wafilipino, na Wahindi walioishi Vienna. Sasa Daniela na Helmut wanatumika wakiwa wamishonari kusini-magharibi mwa Afrika.

Hawafi Moyo

8. Wengi wameonyesha upendo wao kwa Mungu na ushikamanifu wao kwa Ufalme wake katika njia gani yenye kuthawabisha?

8 Kwa kweli, utumishi wa umishonari ni mojawapo ya njia ambazo watu wa Yehova leo huonyesha upendo wao kwa Mungu na ushikamanifu wao kwa Ufalme wake. Kama mwanabiashara katika mfano wa Yesu, wale wanaofanya utumishi huo huwa tayari kusafiri hadi sehemu za mbali sana kwa ajili ya Ufalme. Bila shaka, wamishonari hao hawasafiri ili kwenda kutafuta habari njema ya Ufalme; wanapeleka habari hiyo kwa watu wanaoishi sehemu za mbali sana za dunia, wakiwafundisha na kuwasaidia wawe wanafunzi wa Yesu Kristo. (Mathayo 28:19, 20) Katika nchi nyingi, inawabidi kuvumilia magumu yasiyo ya kawaida. Lakini wanathawabishwa sana kwa sababu ya kuvumilia.

9, 10. Ni mambo gani yenye kusisimua ambayo wamishonari wamejionea katika sehemu za mbali, kama vile Jamhuri ya Afrika ya Kati?

9 Kwa mfano, fikiria Jamhuri ya Afrika ya Kati, ambako mwaka jana, watu 16,184, walihudhuria Ukumbusho wa kifo cha Kristo. Idadi hiyo ilikuwa karibu mara saba ya idadi ya wahubiri wa Ufalme katika nchi hiyo. Kwa kuwa sehemu nyingi za nchi hiyo hazina umeme, kwa kawaida watu hufanya kazi zao za kawaida nje, chini ya kivuli cha mti. Kwa hiyo ni jambo la kawaida kwa wamishonari kufanya kazi yao kwa njia hiyo, yaani, kuongoza mafunzo ya Biblia chini ya kivuli cha mti. Si kwamba tu nje kuna baridi na mwangaza bali pia kuna faida nyingine. Watu wanapenda sana Biblia, na ni jambo la kawaida kuzungumzia mambo ya dini kama vile ilivyo kawaida kuzungumzia habari za michezo au hali ya hewa katika sehemu nyingine za ulimwengu. Mara nyingi, wapita-njia hutazama kinachoendelea na kujiunga na funzo.

10 Hivyo, wakati mmishonari mmoja alipokuwa akiongoza funzo la Biblia nje, kijana mmoja mwanamume aliyeishi ng’ambo ya barabara alikuja na kusema kwamba kwa kuwa hakuwa ametembelewa na Shahidi yeyote, mmishonari huyo alipaswa kwenda kwake na kujifunza Biblia pamoja naye. Bila shaka, mmishonari huyo alikubali kwa furaha, na kijana huyo anafanya maendeleo haraka. Katika nchi hiyo, mara nyingi polisi huwasimamisha Mashahidi barabarani, si ili kuwapa notisi ya kufika mahakamani au kuwatoza faini, bali ili kuomba matoleo ya karibuni ya Mnara wa Mlinzi na Amkeni! au ili kuwashukuru kwa makala fulani waliyofurahia kusoma.

11. Licha ya majaribu, wamishonari ambao wametumika kwa muda mrefu huonaje utumishi wao?

11 Wengi ambao walianza utumishi wa umishonari miaka 40 au 50 iliyopita bado wanatumikia kwa uaminifu. Imani na uvumilivu wao ni kielelezo kizuri kama nini kwetu! Kwa miaka 42 iliyopita, wenzi fulani wa ndoa wametumikia wakiwa wamishonari katika nchi tatu. Mume huyo anasema: “Kumekuwa na magumu. Kwa mfano, tumepambana na malaria kwa miaka 35. Hata hivyo, hatukujuta kamwe uamuzi wetu wa kuwa wamishonari.” Mke wake anaongezea hivi: “Sikuzote tumekuwa na sababu nyingi za kuwa wenye shukrani. Huduma ya shambani inaleta shangwe sana, na ni rahisi kuanzisha mafunzo ya Biblia. Kila mara unapowaona wanafunzi wakija kwenye mikutano na kufahamiana, ni kama kikusanyiko cha familia.”

‘Wanaviona Vitu Vyote Kuwa Hasara’

12. Mtu huonyeshaje kwamba anatambua kikweli thamani ya Ufalme?

12 Mwanabiashara msafiri alipopata lulu ya thamani kubwa, “alienda zake na mara moja akauza vitu vyote alivyokuwa navyo na kuinunua.” (Mathayo 13:46) Kuwa tayari kuacha vitu vinavyoonekana kuwa vyenye thamani ni sifa moja ya wale wanaotambua kikweli thamani ya Ufalme. Akiwa mmoja wa wale ambao wangeshiriki na Kristo katika utukufu wa Ufalme, mtume Paulo alisema: “Kwa kweli naviona vitu vyote kuwa hasara kwa sababu ya thamani bora zaidi ya kumjua Kristo Yesu Bwana wangu. Kwa sababu yake nimekubali hasara ya vitu vyote nami naviona kuwa takataka nyingi, ili niweze kumpata Kristo.”—Wafilipi 3:8.

13. Mtu mmoja katika Jamhuri ya Cheki alionyeshaje kwamba anaupenda Ufalme?

13 Kwa njia hiyohiyo, wengi leo wako tayari kufanya mabadiliko makubwa maishani mwao ili kupata baraka za Ufalme. Kwa mfano, Oktoba 2003, mwalimu-mkuu mwenye umri wa miaka 60 wa shule moja katika Jamhuri ya Cheki alipata kitabu cha kujifunzia Biblia Ujuzi Uongozao Kwenye Uhai Udumuo Milele. Baada ya kukisoma, aliwasiliana mara moja na Mashahidi wa Yehova katika eneo lake ili apate funzo la Biblia. Alifanya maendeleo mazuri ya kiroho na punde si punde akaanza kuhudhuria mikutano yote. Hata hivyo, namna gani mipango yake ya kugombea kiti cha meya na baadaye cha seneta? Aliamua kufuatilia mradi tofauti, yaani, kuwa mtangazaji wa Ufalme. Alisema, “niliwapa wanafunzi wangu shuleni vichapo vingi vya Biblia.” Alionyesha wakfu wake kwa Yehova alipobatizwa katika kusanyiko moja mnamo Julai 2004.

14. (a) Habari njema ya Ufalme imewachochea mamilioni kufanya nini? (b) Kila mmoja wetu anaweza kujiuliza maswali gani yenye kuamsha fikira?

14 Katika njia hiyohiyo, mamilioni ya watu ulimwenguni pote wameitikia habari njema ya Ufalme. Wametoka katika ulimwengu mwovu, wakavua utu wao wa zamani, wakaacha marafiki wao wa zamani, na kuacha kufuatilia mambo ya ulimwengu. (Yohana 15:19; Waefeso 4:22-24; Yakobo 4:4; 1 Yohana 2:15-17) Kwa nini wanafanya mambo hayo yote? Kwa sababu wanaona baraka za Ufalme wa Mungu kuwa muhimu zaidi kuliko kitu chochote ambacho mfumo huu unaweza kuwapa. Je, wewe unahisi vivyo hivyo kuhusu habari njema ya Ufalme? Je, inakuchochea kufanya mabadiliko yanayohitajiwa ili kupatanisha maisha yako, viwango, na miradi yako na matakwa ya Yehova? Ukifanya hivyo, utapata baraka nyingi sasa na wakati ujao.

Mavuno Yanafikia Upeo

15. Ilitabiriwa kwamba watu wa Mungu wangefanya nini katika siku za mwisho?

15 Mtunga-zaburi aliandika hivi: “Watu wako watajitoa kwa hiari katika siku ya jeshi lako.” Wale ambao wamejitoa kwa hiari wanatia ndani ‘kundi la vijana kama matone ya umande’ na “jeshi kubwa” la “wanawake wanaotangaza habari njema.” (Zaburi 68:11; 110:3) Katika siku hizi za mwisho, kujidhabihu na jitihada za watu wa Yehova—wanaume kwa wanawake, vijana kwa wazee—zimekuwa na matokeo gani?

16. Toa mfano kuonyesha jinsi watumishi wa Yehova wanavyojitahidi kuwasaidia wengine wajifunze kuhusu Ufalme.

16 Dada mmoja painia au mtangazaji wa Ufalme wa wakati wote nchini India alijiuliza jinsi ambavyo watu zaidi ya milioni mbili viziwi katika nchi hiyo wangeweza kusaidiwa kujifunza kuhusu Ufalme. (Isaya 35:5) Aliamua kujiunga na chuo cha kujifunza lugha ya ishara huko Bangalore. Akiwa huko, aliwaeleza viziwi wengi kuhusu tumaini la Ufalme na vikundi vya kujifunza Biblia vikaanzishwa. Katika muda wa majuma machache, zaidi ya watu 12 walianza kuhudhuria mikutano kwenye Jumba la Ufalme. Baadaye, akiwa kwenye sherehe ya arusi, painia huyo alikutana na mwanamume mmoja kijana ambaye ni kiziwi kutoka Calcutta aliyekuwa na maswali mengi na aliyetaka sana kujua mengi kumhusu Yehova. Hata hivyo, kulikuwa na tatizo. Mwanamume huyo kijana alipaswa kurudi Calcutta, umbali wa kilometa 1,600 hivi ili aende chuoni, na huko hakukuwa na Mashahidi waliojua lugha ya ishara. Alijitahidi sana kumshawishi baba yake amruhusu kwenda shule huko Bangalore ili aweze kuendelea kujifunza Biblia. Alifanya maendeleo mazuri ya kiroho, na baada ya mwaka mmoja hivi, alijiweka wakfu kwa Yehova. Yeye pia alijifunza Biblia pamoja na viziwi wengi, kutia ndani rafiki yake mmoja wa tangu utotoni. Sasa ofisi ya tawi nchini India inafanya mipango mapainia wajifunze lugha ya ishara ili waweze kusaidia katika eneo hilo.

17. Simulia mambo unayoona kuwa hasa yenye kutia moyo katika ripoti ya mwaka wa utumishi wa 2004 kwenye ukurasa wa 19 hadi 22.

17 Utapata ripoti ya utendaji ya Mashahidi wa Yehova ya ulimwenguni pote ya mwaka wa utumishi wa 2004 kwenye ukurasa wa 19 hadi 22 wa gazeti hili. Tumia wakati kuichunguza, na ujionee mwenyewe uthibitisho wa kwamba watu wa Yehova ulimwenguni pote wanakazia fikira kufuatilia ‘lulu ya thamani kubwa’ leo.

Endeleeni “Kuutafuta Kwanza Ufalme”

18. Ni habari gani ambayo Yesu hakutaja katika ule mfano wa mwanabiashara msafiri, na kwa nini?

18 Tukirudia mfano wa Yesu wa mwanabiashara msafiri, tunaona kwamba Yesu hakueleza jinsi mwanabiashara huyo angetosheleza mahitaji yake baada ya kuuza vitu vyote alivyokuwa navyo. Kwa kufaa, huenda wengine wakauliza: ‘Mwanabiashara huyo angepataje chakula, nguo, na makao kwa kuwa sasa hakuwa na akiba yoyote? Lulu hiyo ya thamani ingekuwa na faida gani kwake?’ Kwa maoni ya kimwili, maswali hayo yangeonekana kuwa yanafaa. Lakini je, Yesu hakuwahimiza wanafunzi wake hivi: “Basi, endeleeni kuutafuta kwanza ufalme na uadilifu wake, nanyi mtaongezewa hivi vitu vingine vyote”? (Mathayo 6:31-33) Jambo kuu katika mfano huo ni uhitaji wa kujitoa kwa moyo wote kwa Mungu na kuwa na bidii kwa ajili ya Ufalme. Je, tunaweza kujifunza jambo fulani kutokana na hilo?

19. Tunajifunza jambo gani muhimu kutokana na mfano wa Yesu wa lulu ya thamani kubwa?

19 Iwe tumejifunza kuhusu habari njema hivi karibuni au tumekuwa tukifuatilia Ufalme na kuwaeleza wengine kuhusu baraka zake kwa miaka mingi, lazima tuendelee kupendezwa na kukazia fikira Ufalme. Hizi ni nyakati ngumu, lakini tuna sababu nzuri za kuamini kwamba kile tunachofuatilia ni halisi na hakiwezi kulinganishwa na kitu chochote—kama lulu ambayo mwanabiashara alipata. Matukio ya ulimwengu na unabii wa Biblia ambao umetimizwa unatoa uthibitisho wenye kusadikisha kwamba tunaishi katika “umalizio wa mfumo wa mambo.” (Mathayo 24:3) Kama mwanabiashara msafiri, acheni tuwe na bidii ya kutoka moyoni kwa ajili ya Ufalme wa Mungu na kufurahia pendeleo la kutangaza habari njema.—Zaburi 9:1, 2.

Je, Unakumbuka?

• Ni nini ambacho kimechangia ongezeko miongoni mwa waabudu wa kweli kila mwaka?

• Wale wanaotumikia wakiwa wamishonari wana mtazamo gani?

• Watu mmoja-mmoja wamefanya mabadiliko gani kwa sababu ya habari njema ya Ufalme?

• Tunajifunza jambo gani muhimu kutokana na mfano wa Yesu wa lulu ya thamani kubwa?

[Maswali ya Funzo]

[Chati katika ukurasa wa 19-22]

RIPOTI YA MWAKA WA UTUMISHI WA 2008 YA MASHAHIDI WA YEHOVA ULIMWENGUNI POTE

(Ona buku lililojalidiwa)

[Picha katika ukurasa wa 14]

“Kweli . . . huwavuta watu wa aina zote.”—A. H. Macmillan

[Picha katika ukurasa wa 15]

Daniela na Helmut walihubiri katika eneo la lugha ya kigeni huko Vienna

[Picha katika ukurasa wa 16, 17]

Kama yule mwanabiashara msafiri, wamishonari leo wanapata baraka nyingi

[Picha katika ukurasa wa 17]

“Watu wako watajitoa kwa hiari”