Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

“Kupata Lulu Moja ya Thamani Kubwa”

“Kupata Lulu Moja ya Thamani Kubwa”

“Kupata Lulu Moja ya Thamani Kubwa”

“Ufalme wa mbinguni ndio mradi ambao watu wanajikaza kuufikia, na wale wanaojikaza wanaufikia.”—MATHAYO 11:12.

1, 2. (a) Yesu alionyesha sifa gani isiyo ya kawaida katika mojawapo ya mifano yake kuhusu Ufalme? (b) Yesu alisema nini katika mfano wa lulu ya thamani kubwa?

JE, KUNA kitu fulani unachothamini sana hivi kwamba unaweza kuwa tayari kuacha kila kitu ulicho nacho ili kukipata? Ingawa watu hujitoa ili kufuatilia mradi fulani kama vile kupata pesa, umashuhuri, mamlaka, au cheo, si jambo la kawaida mtu kupata kitu fulani kinachotamanika sana kiasi cha kwamba yuko tayari kuacha kila kitu ili kukipata. Katika mojawapo ya mifano mingi yenye kuchochea fikira kuhusu Ufalme wa Mungu, Yesu Kristo alitaja sifa isiyo ya kawaida lakini yenye kuvutia.

2 Mfano huo ambao Yesu aliwaeleza wanafunzi wake faraghani mara nyingi huitwa mfano wa lulu ya thamani kubwa. Yesu alisema hivi: “Ufalme wa mbinguni ni kama mwanabiashara msafiri anayetafuta lulu nzuri. Akiisha kupata lulu moja ya thamani kubwa, alienda zake na mara moja akauza vitu vyote alivyokuwa navyo na kuinunua.” (Mathayo 13:36, 45, 46) Yesu alitaka wasikilizaji wake wajifunze nini kutokana na mfano huo? Nasi tunaweza kunufaikaje na maneno ya Yesu?

Thamani Kubwa ya Lulu

3. Kwa nini lulu nzuri zilikuwa zenye thamani sana nyakati za kale?

3 Tangu zamani, lulu zimeonwa kuwa vitu vya kujipamba vyenye thamani. Kichapo kimoja kinasema kwamba kulingana na msomi Mroma Pliny Mkubwa, lulu zilikuwa na “thamani kubwa zaidi kati ya vitu vyote vyenye thamani.” Tofauti na dhahabu, fedha, au mawe mengi yenye thamani, lulu hutokezwa na viumbe vilivyo hai. Inajulikana kwamba aina fulani za chaza wanaweza kugeuza vitu vinavyowasha mwilini kama vile vipande vidogo vya mawe kuwa lulu zenye kumetameta kwa kuvifunika kwa umajimaji unaoitwa lulumizi. Nyakati za kale, lulu bora zaidi zilipatikana hasa katika Bahari Nyekundu, Ghuba ya Uajemi, na Bahari ya Hindi, maeneo yaliyokuwa mbali na nchi ya Israeli. Bila shaka, hiyo ndiyo sababu Yesu alisema kuhusu “mwanabiashara msafiri anayetafuta lulu nzuri.” Ili kupata lulu zenye thamani ya kweli, jitihada kubwa inahitajika.

4. Ni nini lililo jambo muhimu zaidi katika mfano wa Yesu wa mwanabiashara msafiri?

4 Hata ingawa kwa muda mrefu lulu nzuri zimekuwa zenye bei, yaonekana kwamba si bei yake iliyokuwa jambo muhimu zaidi katika mfano wa Yesu. Katika mfano huo, Yesu hakufananisha tu Ufalme wa Mungu na lulu ya thamani kubwa; alielekeza fikira kwa “mwanabiashara msafiri anayetafuta lulu nzuri” na yale aliyofanya baada ya kuipata. Tofauti na mwenye duka wa kawaida, huenda mwanabiashara msafiri wa lulu, au muuzaji alikuwa mtu mwenye ujuzi katika biashara hiyo, mtu ambaye ni makini au anayeweza kutofautisha uzuri wa nje na uzuri uliojificha ambao hufanya lulu iwe ya kipekee. Angejua lulu halisi kwa kuiona tu na hangedanganywa na lulu bandia.

5, 6. (a) Tunapaswa kufikiria jambo gani hasa kuhusu mwanabiashara katika mfano wa Yesu? (b) Mfano wa hazina iliyofichwa huonyesha nini kuhusu mwanabiashara msafiri?

5 Kuna jambo lingine tunalopaswa kufikiria katika mfano huo wa mwanabiashara. Huenda mwanabiashara wa kawaida kwanza akataka kujua bei ya lulu ili aweze kuamua atainunua kwa bei gani kusudi apate faida. Huenda pia akafikiria ikiwa ataweza kuiuza haraka. Yaani, angetaka kupata faida haraka iwezekanavyo kutokana na rasilimali yake, bali si kuiweka iwe yake. Lakini mwanabiashara katika mfano wa Yesu hataki kupata faida ya haraka. Pesa au faida halisi si muhimu kwake. Kwa kweli, alikuwa tayari kuacha “vitu vyote alivyokuwa navyo”—labda vitu vyake vyote na mali zake—ili kupata kile alichokuwa akitafuta.

6 Huenda wanabiashara wengi wangeona kile ambacho yule mtu katika mfano wa Yesu alifanya kuwa jambo lisilo la hekima. Mwanabiashara mwerevu hangefikiria kufanya biashara hiyo ya kujasiria. Lakini mwanabiashara katika mfano wa Yesu alikuwa na maoni tofauti kuhusu vitu vyenye thamani. Shangwe na uradhi wake haikutokana na faida yoyote ya kifedha bali ilitokana na kumiliki kitu chenye thamani kubwa sana. Jambo hilo linafafanuliwa katika mfano mwingine unaofanana na huo ambao Yesu alitoa. Alisema: “Ufalme wa mbinguni ni kama hazina iliyofichwa katika shamba, ambayo mtu aliipata na kuificha; na kwa sababu ya shangwe aliyo nayo, anaenda na kuuza vitu alivyo navyo na kulinunua shamba hilo.” (Mathayo 13:44) Naam, shangwe inayotokana na kuvumbua na kumiliki hazina ilitosha kumchochea mtu huyo auze vitu vyote alivyokuwa navyo. Je, kuna watu kama hao leo? Je, kuna hazina inayoweza kufanya mtu auze vitu vyote alivyo navyo?

Wale Waliotambua Thamani Kubwa ya Ufalme

7. Yesu alionyeshaje kwamba alitambua thamani kubwa ya Ufalme?

7 Yesu alitoa mfano huo alipokuwa akizungumza juu ya “ufalme wa mbinguni.” Bila shaka yeye mwenyewe alitambua thamani kubwa ya Ufalme. Masimulizi ya Injili hutoa uthibitisho wenye nguvu kuhusu jambo hilo. Baada ya kubatizwa mwaka wa 29 W.K., Yesu “alianza kuhubiri na kusema: ‘Tubuni, kwa maana ufalme wa mbinguni umekaribia.’” Kwa miaka mitatu na nusu, alifundisha umati wa watu kuhusu Ufalme. Alivuka kutoka upande mmoja wa nchi hadi mwingine na “kusafiri kutoka jiji mpaka jiji na kutoka kijiji mpaka kijiji, akihubiri na kutangaza habari njema ya ufalme wa Mungu.”—Mathayo 4:17; Luka 8:1.

8. Yesu alifanya nini ili kuonyesha mambo ambayo Ufalme utatimiza?

8 Pia kwa kufanya miujiza mingi nchini kote, kutia ndani kuwaponya wagonjwa, kuwalisha wenye njaa, na kutiisha nguvu za asili, na hata kuwafufua wafu, Yesu alionyesha mambo ambayo Ufalme wa Mungu utatimiza. (Mathayo 14:14-21; Marko 4:37-39; Luka 7:11-17) Mwishowe, alithibitisha ushikamanifu wake kwa Mungu na kwa Ufalme huo kwa kutoa uhai wake na kufia imani kwenye mti wa mateso. Kama vile mwanabiashara msafiri alivyokuwa tayari kuuza kila kitu alichokuwa nacho ili kupata “lulu moja ya thamani kubwa,” Yesu aliishi na kufa kwa ajili ya Ufalme.—Yohana 18:37.

9. Wanafunzi wa Yesu wa mapema walikuwa na sifa gani isiyo ya kawaida?

9 Ingawa Yesu alikazia fikira Ufalme maishani mwake, alikusanya pia kikundi kidogo cha wafuasi. Hao pia walitambua thamani kubwa ya Ufalme. Miongoni mwao kulikuwa na Andrea ambaye hapo mwanzoni alikuwa mwanafunzi wa Yohana Mbatizaji. Baada ya kumsikia Yohana akitoa ushahidi kwamba Yesu alikuwa “Mwana-Kondoo wa Mungu,” Andrea na mwanafunzi mwingine wa Yohana, yaelekea mmoja wa wana wa Zebedayo ambaye pia aliitwa Yohana, walivutiwa mara moja kumkaribia Yesu nao wakawa waamini. Lakini mambo hayakuishia hapo. Mara moja, Andrea alienda kwa ndugu yake Simoni na kumwambia: “Tumempata Masihi.” Muda mfupi baadaye, Simoni (ambaye baadaye aliitwa Kefa, au Petro) na vilevile Filipo na rafiki yake Nathanaeli pia walimtambua Yesu kuwa Masihi. Kwa kweli, Nathanaeli alichochewa kumwambia Yesu hivi: “Wewe ndiye Mwana wa Mungu, wewe ndiye Mfalme wa Israeli.”—Yohana 1:35-49.

Wachochewa Kutenda

10. Wanafunzi waliitikiaje Yesu alipokuja na kuwaita muda fulani baada ya kukutana nao mara ya kwanza?

10 Msisimuko ambao Andrea, Petro, Yohana, na wengine walipata walipompata Masihi unaweza kulinganishwa na msisimuko wa mwanabiashara msafiri alipopata lulu ya thamani kubwa. Sasa wangefanya nini? Vitabu vya Injili havituelezi mengi kuhusu yale waliyofanya punde tu baada ya kukutana na Yesu mara ya kwanza. Yaelekea wengi wao walirudia maisha yao ya kawaida. Hata hivyo, yapata miezi sita hadi mwaka mmoja hivi baadaye, Yesu alikutana tena na Andrea, Petro, Yohana, na Yakobo ndugu ya Yohana walipokuwa kwenye biashara yao ya uvuvi kando ya Bahari ya Galilaya. * Alipowaona, Yesu alisema: “Nifuateni, nami nitawafanya ninyi kuwa wavuvi wa watu.” Waliitikiaje? Simulizi la Mathayo linasema hivi kuhusu Petro na Andrea: “Mara moja wakaziacha nyavu, wakamfuata.” Kwa habari ya Yakobo na Yohana, tunasoma hivi: “Mara moja wakaacha ile mashua na baba yao, wakamfuata.” Simulizi la Luka linaongeza kwamba ‘waliacha kila kitu, wakamfuata.’—Mathayo 4:18-22; Luka 5:1-11.

11. Ni nini ambacho huenda kilifanya wanafunzi waitikie kwa haraka mwito wa Yesu?

11 Je, wanafunzi hao walifanya uamuzi wa haraka-haraka? La, sivyo! Hata ingawa walirudia biashara ya familia yao ya uvuvi baada ya kukutana na Yesu mara ya kwanza, hakuna shaka kwamba yale waliyokuwa wameona na kusikia pindi hiyo yalibaki akilini na kugusa mioyo yao. Muda wa mwaka moja hivi ambao ulikuwa umepita, uliwapa wakati wa kutosha kutafakari mambo hayo. Sasa wakati wa kufanya uamuzi ulikuwa umefika. Je, wangekuwa kama mwanabiashara msafiri ambaye moyo wake ulichochewa sana alipopata lulu ya thamani kubwa, hivi kwamba kama Yesu alivyoeleza, “alienda zake na mara moja” akafanya kile alichopaswa kufanya ili anunue lulu hiyo? Ndiyo. Mambo waliyoona na kusikia yalichochea mioyo yao. Walitambua kwamba wakati wa kuchukua hatua ulikuwa umefika. Hivyo, kama masimulizi hayo yanavyotuambia, pasipo kusita-sita waliacha kila kitu walichokuwa nacho na kuwa wafuasi wa Yesu.

12, 13. (a) Wengi waliomsikia Yesu waliitikiaje? (b) Yesu alisema nini kuhusu wanafunzi wake waaminifu, nayo maneno yake yanamaanisha nini?

12 Wanafunzi hao waaminifu walikuwa tofauti sana na watu wengine waliotajwa baadaye katika vitabu vya Injili. Wengi walikuwa wameponywa au kulishwa na Yesu lakini waliendelea tu na shughuli zao za kawaida. (Luka 17:17, 18; Yohana 6:26) Baadhi yao hata walitoa visingizio Yesu alipowaalika wawe wafuasi wake. (Luka 9:59-62) Tofauti na hao, Yesu alisema hivi baadaye kuhusu wanafunzi wake waaminifu: “Tangu siku za Yohana Mbatizaji mpaka sasa ufalme wa mbinguni ndio mradi ambao watu wanajikaza kuufikia, na wale wanaojikaza wanaufikia.”—Mathayo 11:12.

13 Neno “Kujikaza” linamaanisha nini? Kitabu Vine’s Expository Dictionary of Old and New Testament Words kinasema hivi kuhusu kitenzi cha Kigiriki ambacho neno hilo limetolewa: “Kitenzi hicho kinadokeza jitihada yenye bidii.” Naye msomi wa Biblia Heinrich Meyer anasema hivi kuhusu mstari huo: “Neno hilo linafafanua hamu, jitihada isiyozuilika na pambano la kuufikia ufalme wa Kimasihi unaokaribia . . . Wanafuatia ufalme kwa hamu na kwa bidii sana (si kungoja kwa utulivu tu na kutarajia).” Kama yule mwanabiashara msafiri, watu hao wachache walitambua haraka kitu kilichokuwa na thamani ya kweli nao wakawa tayari kuacha vitu vyote walivyokuwa navyo kwa ajili ya Ufalme.—Mathayo 19:27, 28; Wafilipi 3:8.

Wengine Walijiunga Katika Kutafuta

14. Yesu aliwatayarishaje mitume kwa ajili ya kazi ya kuhubiri Ufalme, na matokeo yalikuwa nini?

14 Yesu alipokuwa akiendelea na huduma yake, aliwazoeza na kuwasaidia wengine waufikie Ufalme. Kwanza alichagua 12 kutoka kati ya wanafunzi wake ili wawe mitume, au wale aliowatuma. Yesu aliwapa maagizo mengi kuhusu jinsi ya kutimiza huduma yao na pia maonyo kuhusu majaribu na magumu ambayo wangekabili. (Mathayo 10:1-42; Luka 6:12-16) Kwa miaka miwili hivi iliyofuata, waliambatana na Yesu katika safari zake za kuhubiri nchini kote, nao walifurahia uhusiano wa karibu pamoja naye. Walisikia maneno yake, wakashuhudia kazi zake zenye nguvu, na kuona kielelezo chake. (Mathayo 13:16, 17) Bila shaka, mambo hayo yote yaligusa sana mioyo yao hivi kwamba kama mwanabiashara msafiri, walikuwa na bidii na walijitoa kwa moyo wote kufuatilia Ufalme.

15. Yesu alisema ni kitu gani hasa kingefanya wafuasi wake washangilie?

15 Kwa kuongezea wale mitume 12, Yesu ‘alichagua wengine 70 na kuwatuma wawili-wawili, wamtangulie kuingia katika kila jiji na mahali ambako yeye mwenyewe alikuwa aende.’ Aliwaambia pia kuhusu majaribu na magumu ambayo wangekabili na kuwaagiza wawaambie watu: “Ufalme wa Mungu umekuja karibu nanyi.” (Luka 10:1-12) Wale 70 waliporudi, walikuwa na shangwe na walimwambia Yesu hivi: “Bwana, hata roho waovu wanatiishwa kwetu kwa kutumia jina lako.” Lakini huenda walishangaa Yesu alipowaeleza kuhusu shangwe kubwa ambayo wangepata kwa sababu ya bidii yao kwa ajili ya Ufalme. Aliwaambia: “Msishangilie juu ya hili, kwamba roho wanatiishwa kwenu, bali shangilieni kwa sababu majina yenu yameandikwa mbinguni.”—Luka 10:17, 20.

16, 17. (a) Yesu aliwaambia nini mitume wake waaminifu usiku wa mwisho ambao alikuwa pamoja nao? (b) Maneno ya Yesu yaliwapa mitume shangwe na uhakika gani?

16 Mwishowe, usiku wa mwisho ambao Yesu alikuwa pamoja na mitume wake, Nisani 14, 33 W.K., alianzisha Mlo wa Jioni wa Bwana na kuwaamuru waadhimishe tukio hilo. Usiku huo, Yesu aliwaambia hivi wale 11 waliobaki: “Ninyi ndio mmeshikamana nami katika majaribu yangu; nami ninafanya agano pamoja nanyi, sawa na vile Baba yangu alivyofanya agano pamoja nami, kwa ajili ya ufalme, ili mpate kula na kunywa mezani pangu katika ufalme wangu, na kuketi juu ya viti vya ufalme kuyahukumu makabila kumi na mawili ya Israeli.”—Luka 22:19, 20, 28-30.

17 Mitume hao waliposikia maneno hayo ya Yesu, mioyo yao ilijawa na furaha na uradhi kama nini! Walikuwa wakipewa pendeleo kubwa sana ambalo mwanadamu anaweza kupata. (Mathayo 7:13, 14; 1 Petro 2:9) Kama yule mwanabiashara msafiri, walikuwa wameacha vitu vingi ili kumfuata Yesu katika kufuatilia Ufalme. Sasa walihakikishiwa kwamba hawakuwa wameacha vitu hivyo bure.

18. Mbali na wale mitume 11, ni nani wengine wangenufaika na Ufalme?

18 Mbali na mitume waliokuwa pamoja na Yesu usiku huo, wengine pia wangenufaika na Ufalme. Mapenzi ya Yehova yalikuwa kwamba jumla ya watu 144,000 waingizwe katika agano la Ufalme wakiwa watawala pamoja na Yesu Kristo katika Ufalme wa mbinguni wenye utukufu. Isitoshe, mtume Yohana aliona katika maono “umati mkubwa, ambao hakuna mtu aliyeweza kuuhesabu, . . . wamesimama mbele ya kiti cha ufalme na mbele ya Mwana-Kondoo, . . . wakisema: ‘Wokovu unatoka kwa Mungu wetu, anayeketi juu ya kiti cha ufalme, na Mwana-Kondoo.’” Hao ndio raia wa kidunia wa Ufalme huo. *Ufunuo 7:9, 10; 14:1, 4.

19, 20. (a) Watu wa mataifa yote wamepewa nafasi gani? (b) Ni swali gani litakalozungumziwa katika makala inayofuata?

19 Muda mfupi kabla ya Yesu kupaa mbinguni, aliwaamuru hivi wafuasi wake waaminifu: “Kwa hiyo nendeni mkafanye wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote, mkiwabatiza katika jina la Baba na la Mwana na la roho takatifu, na kuwafundisha kushika mambo yote ambayo nimewaamuru ninyi na tazama! mimi nipo pamoja nanyi siku zote mpaka umalizio wa mfumo wa mambo.” (Mathayo 28:19, 20) Hivyo, watu wa mataifa yote wangekuwa wanafunzi wa Yesu Kristo. Sawa na vile mwanabiashara msafiri alivyofanya kuhusiana na lulu nzuri, hao pia wangeelekeza mioyo yao kwenye Ufalme—iwe ni kwa ajili ya uzima mbinguni au duniani.

20 Maneno ya Yesu yalionyesha kwamba kazi ya kufanya wanafunzi ingeendelea mpaka “umalizio wa mfumo wa mambo.” Kwa hiyo, je, leo bado kuna watu ambao kama yule mwanabiashara msafiri, wako tayari kuacha vyote walivyo navyo ili kufuatilia Ufalme wa Mungu? Swali hilo litazungumziwa katika makala inayofuata.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 10 Huenda Yohana, mwana wa Zebedayo alimfuata Yesu na kushuhudia baadhi ya mambo aliyofanya baada ya kukutana naye mara ya kwanza, na hivyo kumwezesha Yohana kuyaandika mambo hayo waziwazi katika masimulizi yake ya Injili. (Yohana, sura ya 2-5) Hata hivyo, alirudia biashara ya familia yao ya uvuvi kwa muda fulani kabla ya kuitwa na Yesu.

^ fu. 18 Kwa habari zaidi, ona sura ya 10 ya kitabu Ujuzi Uongozao Kwenye Uhai Udumuo Milele, kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

Je, Unaweza Kueleza?

• Ni nini lililo jambo muhimu zaidi katika mfano wa mwanabiashara msafiri?

• Yesu alionyeshaje kwamba alitambua thamani kubwa ya Ufalme?

• Ni nini kilichofanya Andrea, Petro, Yohana, na wengine waitikie kwa haraka mwito wa Yesu?

• Watu wa mataifa yote wamepewa nafasi gani?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 10]

‘Waliacha kila kitu, wakamfuata Yesu’

[Picha katika ukurasa wa 12]

Kabla ya kupaa mbinguni, Yesu aliwaamuru wafuasi wake wafanye wanafunzi