Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Sikuzote Yehova Hufanya Yaliyo Sawa

Sikuzote Yehova Hufanya Yaliyo Sawa

Sikuzote Yehova Hufanya Yaliyo Sawa

“Yehova ni mwadilifu katika njia zake zote.”—ZABURI 145:17.

1. Wewe huhisije mtu fulani anapokata kauli kimakosa kukuhusu, na tunaweza kujifunza nini kutokana na hilo?

JE, MTU fulani amewahi kukata kauli kimakosa kukuhusu, labda akitilia shaka matendo au nia yako, bila kuwa na habari kamili? Ikiwa ndivyo, inaelekea kwamba uliumia moyoni, na inaeleweka kwa nini ulihisi hivyo. Tunaweza kujifunza jambo fulani muhimu kutokana na hilo: Ni jambo la hekima kuepuka kukata kauli haraka ikiwa hatuna habari kamili.

2, 3. Wengine huitikiaje wanaposoma masimulizi fulani ya Biblia ambayo hayana habari za kutosha kujibu kila swali, lakini Biblia hutuambia nini kumhusu Yehova?

2 Tunapaswa kukumbuka jambo hilo tunapokata kauli kumhusu Yehova Mungu. Kwa nini? Kwa sababu huenda masimulizi fulani ya Biblia yakaonekana kuwa yenye kutatanisha mara ya kwanza. Masimulizi hayo, ambayo labda yanahusu matendo ya baadhi ya waabudu wa Mungu au hukumu za Mungu za wakati uliopita, huenda yasiwe na habari za kutosha kujibu maswali yetu yote. Kwa kusikitisha, wengine huchambua masimulizi hayo na hata kutilia shaka iwapo Mungu ni mwadilifu na mwenye haki. Hata hivyo, Biblia hutuambia kwamba “Yehova ni mwadilifu katika njia zake zote.” (Zaburi 145:17) Neno lake pia linatuhakikishia kwamba yeye “hatendi kwa uovu.” (Ayubu 34:12; Zaburi 37:28) Basi wazia jinsi anavyohisi wengine wanapokata kauli kimakosa kumhusu!

3 Acheni tuzungumzie sababu tano ambazo hufanya tukubali hukumu za Yehova. Kisha, tukiwa na sababu hizo akilini, tutachunguza masimulizi mawili ya Biblia ambayo huenda wengine wakaona kuwa vigumu kuyaelewa.

Kwa Nini Tukubali Hukumu za Yehova?

4. Kwa nini tunapaswa kuwa wanyenyekevu tunapofikiria matendo ya Mungu? Toa mfano.

4 Kwanza, kwa sababu Yehova anajua habari zote zinazohusika ambazo sisi hatuna, tunapaswa kuwa wanyenyekevu tunapofikiria matendo ya Mungu. Fikiria mfano huu: Hakimu fulani anayejulikana kuwa hana upendeleo, amekata hukumu mahakamani. Ungemwonaje mtu ambaye anachambua uamuzi wa hakimu huyo bila kuwa na habari kamili au kuelewa kabisa sheria zinazohusika? Lingekuwa jambo la upumbavu mtu kuchambua jambo fulani bila kuwa na habari kamili kulihusu. (Methali 18:13) Lingekuwa jambo la upumbavu hata zaidi kwa wanadamu duni kumchambua “Mwamuzi wa dunia yote.”—Mwanzo 18:25.

5. Hatupaswi kusahau nini tunaposoma masimulizi ya Biblia kuhusu kutekelezwa kwa hukumu za Mungu juu ya watu fulani?

5 Sababu ya pili ya kukubali hukumu za Mungu ni kwamba tofauti na wanadamu, Mungu anaweza kusoma mioyo. (1 Samweli 16:7) Neno lake linasema: “Mimi, Yehova, ninauchunguza moyo, ninazikagua figo, ili kumpa kila mmoja kulingana na njia zake, kulingana na matunda ya matendo yake.” (Yeremia 17:10) Kwa hiyo, tunaposoma masimulizi ya Biblia kuhusu hukumu za Mungu juu ya watu fulani, na tusisahau kwamba kwa kuwa yeye huona kila kitu, aliona mawazo yaliyofichwa, nia, na makusudio ambayo hayakuandikwa katika Neno lake.—1 Mambo ya Nyakati 28:9.

6, 7. (a) Yehova ameonyeshaje kwamba yeye hushikilia viwango vyake vya haki na uadilifu hata kama itamgharimu sana? (b) Tunapaswa kukumbuka nini tukisoma habari fulani katika Biblia ambayo hufanya tutilie shaka kama Mungu alitenda kwa njia iliyo sawa au ya haki?

6 Ona sababu ya tatu ya kukubali hukumu za Yehova: Yeye hushikilia viwango vyake vya uadilifu hata kama itamgharimu sana. Fikiria mfano mmoja. Kwa kumtoa Mwana wake kuwa fidia ili kuwakomboa wanadamu watiifu kutoka katika dhambi na kifo, Yehova alitimiza viwango vyake vya haki na vya uadilifu. (Waroma 5:18, 19) Hata hivyo, lazima Yehova awe aliumia sana kumwona Mwana wake akiteseka na kufa kwenye mti wa mateso. Hilo hutufunza nini kumhusu Mungu? Kuhusu “fidia ambayo Kristo Yesu alilipa,” Biblia inasema: ‘Ilikuwa hivyo ili kuonyesha wazi uadilifu wa Mungu mwenyewe.’ (Waroma 3:24-26) Biblia nyingine hutafsiri andiko la Waroma 3:25 hivi: “Hilo lilionyesha kwamba sikuzote Mungu hufanya yaliyo sawa na haki.” (New Century Version) Naam, yote ambayo Yehova alikuwa tayari kufanya ili kutoa fidia yanaonyesha kwamba yeye hushikilia sana “yaliyo sawa na haki.”

7 Hivyo basi, tunaposoma habari fulani katika Biblia ambayo hufanya wengine watilie shaka kama Mungu alitenda kwa njia iliyo sawa au ya haki, tunapaswa kukumbuka jambo hili: Kwa sababu ya kushikamana na viwango vyake vya uadilifu na haki, Yehova hakujizuia kumtoa hata Mwana wake apatwe na kifo chenye maumivu. Je, atakiuka viwango hivyo kuhusiana na mambo mengine? Ukweli ni kwamba, Yehova hakiuki kamwe viwango vyake vya haki na uadilifu. Hivyo, tuna sababu za kutosha kusadiki kwamba sikuzote yeye hufanya yaliyo sawa na haki.—Ayubu 37:23.

8. Kwa nini lingekuwa jambo lisilopatana na akili kwa wanadamu kufikiri kwamba labda Yehova hana sifa ya haki na uadilifu?

8 Fikiria sababu ya nne ya kukubali hukumu za Yehova: Yehova aliumba mwanadamu kwa mfano Wake. (Mwanzo 1:27) Kwa hiyo, wanadamu wamepewa sifa kama za Mungu, kutia ndani haki na uadilifu. Lingekuwa jambo lisilopatana na akili ikiwa haki na uadilifu wetu ungefanya tufikiri kwamba labda Yehova hana sifa hizo. Tukitatanishwa na simulizi fulani la Biblia, tunapaswa kukumbuka kwamba kwa sababu ya dhambi tuliyorithi, njia yetu ya kufanya yaliyo haki na uadilifu si kamilifu. Yehova Mungu, ambaye tumeumbwa kwa mfano wake, ni mkamilifu katika haki na uadilifu. (Kumbukumbu la Torati 32:4) Ungekuwa upumbavu kama nini kufikiri kwamba wanadamu wanaweza kuwa wenye haki na waadilifu zaidi kuliko Mungu!—Waroma 3:4, 5; 9:14.

9, 10. Kwa nini Yehova hana wajibu wa kuwaeleza wanadamu sababu ya matendo yake au kujitetea mbele yao?

9 Sababu ya tano ya kukubali hukumu za Yehova ni kwamba yeye ndiye ‘Aliye Juu Zaidi, juu ya dunia yote.’ (Zaburi 83:18) Kwa hiyo, hana wajibu wa kuwaeleza wanadamu sababu ya matendo yake au kujitetea mbele yao. Yeye ni Mfinyanzi Mkuu, na sisi ni kama udongo wa mfinyanzi ambao umetumiwa kutengeneza vyombo mbalimbali, ili avitumie apendavyo. (Waroma 9:19-21) Sisi, tukiwa vyombo vya mikono yake, tunawezaje kutilia shaka maamuzi au matendo yake? Mzee wa ukoo Ayubu, alipoelewa vibaya jinsi Mungu alivyoshughulika na wanadamu, Yehova alimsahihisha kwa kumuuliza: “Kwa kweli, je, utaifanya haki yangu kuwa bure? Je, utanitangaza mimi kuwa mwovu ili wewe uwe upande wa haki?” Baadaye Ayubu alipotambua kwamba alizungumza bila kuelewa, alitubu. (Ayubu 40:8; 42:6) Na tusifanye kosa la kumlaumu Mungu kamwe!

10 Ni wazi kwamba tuna sababu nzuri za kuamini kwamba sikuzote Yehova hufanya yaliyo sawa. Tukiwa na sababu hizo za kutusaidia kuelewa njia za Yehova, acheni tuchunguze masimulizi mawili ya Biblia ambayo huenda yakawatatanisha wengine. Simulizi la kwanza linahusu matendo ya mwabudu mmoja wa Mungu, nalo lingine linahusu kutekelezwa kwa hukumu na Mungu mwenyewe.

Kwa Nini Loti Alitaka Kuupa Umati Wenye Hasira Binti Zake?

11, 12. (a) Simulia yale yaliyotukia Mungu alipowatuma malaika wawili waliojivika miili ya kibinadamu huko Sodoma. (b) Simulizi hilo limetokeza maswali gani akilini mwa watu fulani?

11 Katika Mwanzo sura ya 19, tunasoma kuhusu yale yaliyotukia wakati Mungu alipowatuma malaika wawili waliojivika miili ya kibinadamu huko Sodoma. Loti alisisitiza wageni hao wakae nyumbani kwake. Hata hivyo, usiku huo, umati wa wanaume kutoka jijini ulizingira nyumba hiyo na kudai wageni hao watolewe nje ili wafanye ngono nao. Loti alijaribu kusihi umati huo, lakini hakufanikiwa. Akijaribu kuwalinda wageni wake, Loti alisema: “Tafadhali, ndugu zangu, msitende vibaya. Tafadhali, hapa nina binti wawili ambao hawajapata kamwe kulala na mwanamume. Tafadhali, acheni niwatoe nje kwenu. Kisha mwatendee kama ilivyo vema machoni penu. Ila tu wanaume hawa msiwatendee jambo, kwa kuwa ndiyo sababu wamekuja chini ya kivuli cha paa yangu.” Umati huo haukutaka kusikiliza nao ulikuwa karibu kuvunja mlango. Mwishowe, malaika hao wakapiga umati huo wenye kichaa kwa upofu.—Mwanzo 19:1-11.

12 Ni jambo linaloeleweka kwamba simulizi hilo limetokeza maswali akilini mwa watu fulani. Wanajiuliza: ‘Loti angewezaje kuwalinda wageni wake kwa kutaka kuupa umati huo wenye uchu binti zake? Je, hakutenda kwa njia isiyofaa, na hata kwa woga?’ Kwa kuzingatia simulizi hilo, kwa nini Petro, chini ya uongozi wa roho ya Mungu alimwita Loti ‘mtu mwadilifu’? Je, Loti alikuwa na kibali cha Mungu alipofanya hivyo? (2 Petro 2:7, 8) Acheni tufikirie jambo hilo ili tusikate kauli kimakosa.

13, 14. (a) Tunapaswa kutambua nini kuhusiana na simulizi la Biblia kuhusu matendo ya Loti? (b) Ni nini kinachoonyesha kwamba Loti hakutenda kwa woga?

13 Kwanza, tunapaswa kutambua kwamba badala ya kutetea au kushutumu matendo ya Loti, Biblia inaeleza tu yale yaliyotukia. Pia Biblia haituambii Loti alikuwa akifikiria nini au ni nini kilichomchochea kufanya hivyo. Pengine Loti atatueleza habari zaidi atakapofufuliwa katika “ufufuo wa waadilifu.”—Matendo 24:15.

14 Loti hakuwa mwoga hata kidogo. Alikuwa katika hali ngumu. Kwa kusema kwamba wageni hao walikuwa “wamekuja chini ya kivuli” cha paa yake, Loti alionyesha kwamba alihisi alipaswa kuwalinda na kuwapa makao. Lakini haingekuwa rahisi kufanya hivyo. Mwanahistoria Myahudi Yosefu anasema kwamba watu wa Sodoma “waliwatendea watu isivyo haki, nao walikuwa waovu machoni pa Mungu . . . Waliwachukia wageni, nao walijihusisha katika ngono zilizopotoka.” Hata hivyo, Loti hakuogopa umati huo wenye chuki. Badala yake, alitoka nje na kujadiliana na wanaume hao wenye hasira. Hata ‘aliufunga mlango nyuma yake.’—Mwanzo 19:6.

15. Kwa nini inaweza kusemwa kwamba Loti alitenda kwa imani?

15 ‘Hata hivyo,’ huenda wengine wakauliza, ‘kwa nini Loti alitaka kuupa umati huo binti zake?’ Badala ya kukata kauli kwamba alikuwa na nia mbaya, kwa nini usifikirie hali fulani ambazo huenda zilihusika? Kwanza, huenda Loti alitenda kwa imani. Jinsi gani? Bila shaka, Loti alijua jinsi Yehova alivyomlinda Sara, mke wa Abrahamu, mjomba wake. Kumbuka kwamba kwa sababu Sara alikuwa mrembo sana, Abrahamu alikuwa amemwambia aseme kwamba yeye ni ndugu yake kwa sababu aliogopa watu wangemuua ili wamchukue Sara. * Baadaye, Sara alipelekwa nyumbani kwa Farao. Hata hivyo, Yehova aliingilia kati na kumzuia Farao asimnajisi Sara. (Mwanzo 12:11-20) Yawezekana Loti aliamini kwamba binti zake wangeweza kulindwa vivyo hivyo. Jambo lenye kutokeza ni kwamba, Yehova, kupitia malaika wake aliingilia kati na kuwalinda wanawake hao vijana.

16, 17. (a) Huenda Loti alikuwa akijaribu kuwashtua au kuwatatanisha wanaume wa Sodoma kwa njia gani? (b) Hata iwe Loti alikuwa akifikiria nini, tunaweza kuwa na uhakika kuhusu jambo gani?

16 Pia fikiria uwezekano mwingine. Huenda pia Loti alikuwa akijaribu kuwashtua au kuwatatanisha wanaume hao. Labda aliamini kwamba umati huo haungewatamani binti zake kwa sababu watu wa Sodoma walikuwa walawiti. (Yuda 7) Isitoshe, wanawake hao vijana walikuwa wamechumbiwa na wanaume wa jiji hilo, kwa hiyo, huenda watu wa jamaa, marafiki, au watu waliofanya biashara pamoja na wana-wakwe wa Loti walikuwa kati ya umati huo. (Mwanzo 19:14) Huenda Loti alitumaini kwamba kwa sababu ya mahusiano hayo, baadhi ya wanaume katika umati huo wangewatetea binti zake. Umati uliogawanyika haungekuwa hatari sana. *

17 Hata iwe Loti alikuwa na fikira au nia gani, tunaweza kuwa na uhakika kuhusu jambo hili: Kwa kuwa sikuzote Yehova hufanya yaliyo sawa, lazima awe alikuwa na sababu nzuri ya kumwona Loti kuwa ‘mtu mwadilifu.’ Na tunapofikiria matendo ya umati huo wa watu wa Sodoma wenye kichaa, je, tunaweza kuwa na shaka yoyote kwamba Yehova alikuwa na haki kamili ya kutekeleza hukumu juu ya wakaaji wa jiji hilo lenye uovu?—Mwanzo 19:23-25.

Kwa Nini Yehova Alimuua Uza?

18. (a) Ni nini kilichotukia Daudi alipojaribu kupeleka Sanduku Yerusalemu? (b) Simulizi hilo linatokeza swali gani?

18 Simulizi lingine ambalo huenda likawatatanisha watu fulani linahusu jaribio la Daudi la kuleta sanduku la agano Yerusalemu. Sanduku hilo liliwekwa juu ya gari la kukokotwa ambalo liliongozwa na Uza na ndugu yake. Biblia inasema hivi: “Nao mwishowe wakaja mpaka uwanja wa kupuria wa Nakoni, na sasa Uza akanyoosha mkono wake kwenye lile sanduku la Mungu wa kweli, akalishika, kwa maana wale ng’ombe karibu waliangushe. Ndipo hasira ya Yehova ikamwakia Uza, na Mungu wa kweli akampiga hapo kwa sababu ya hilo tendo lisilo la heshima kwa Mungu, naye akafa hapo karibu na lile sanduku la Mungu wa kweli.” Miezi kadhaa baadaye, jaribio la pili lilifanikiwa wakati Sanduku hilo liliposafirishwa kwa njia ambayo Mungu aliagiza, lilibebwa kwenye mabega ya Wakohathi Walawi. (2 Samweli 6:6, 7; Hesabu 4:15; 7:9; 1 Mambo ya Nyakati 15:1-14) Huenda wengine wakauliza: ‘Kwa nini Yehova alichukua hatua kali hivyo? Uza alikuwa akijaribu tu kukinga Sanduku hilo.’ Ili tusikate kauli kimakosa, ingefaa tufikirie habari fulani zinazoweza kutusaidia.

19. Kwa nini Yehova hawezi kutenda isivyo haki kamwe?

19 Tunapaswa kukumbuka kwamba Yehova hawezi kutenda isivyo haki kamwe. (Ayubu 34:10) Lingekuwa jambo lisilo la upendo yeye kufanya hivyo, na kutokana na yale ambayo tumejifunza katika Biblia tunajua kwamba “Mungu ni upendo.” (1 Yohana 4:8) Kwa kuongezea, Maandiko hutuambia kwamba “uadilifu na hukumu ndizo mahali palipofanywa imara pa kiti [cha Mungu] cha ufalme.” (Zaburi 89:14) Basi, Yehova angewezaje kutenda isivyo haki? Kama angefanya hivyo, angekuwa akidhoofisha msingi hasa wa enzi yake kuu.

20. Kwa nini Uza alipaswa kujua masharti yaliyohusu Sanduku?

20 Kumbuka kwamba Uza alipaswa kuijua Sheria. Sanduku liliwakilisha kuwapo kwa Yehova. Sheria ilitaja kwamba halikupaswa kuguswa na watu wasiostahili, na kuonya wazi kwamba watu waliokiuka sheria hiyo wangepewa adhabu ya kifo. (Hesabu 4:18-20; 7:89) Kwa hiyo, kuhamishwa kwa Sanduku hilo takatifu kulipaswa kuonwa kuwa jambo nzito. Yaelekea Uza alikuwa Mlawi (ingawa hakuwa kuhani), hivyo alipaswa kuijua Sheria. Isitoshe, miaka kadhaa mapema Sanduku hilo lilikuwa limehamishwa kwa nyumba ya baba yake ili lilindwe. (1 Samweli 6:20–7:1) Lilikuwa limekaa huko kwa miaka 70 hivi hadi Daudi alipoamua kulihamisha. Hivyo, tangu utotoni yaelekea Uza alijua sheria zilizohusu Sanduku hilo.

21. Katika kisa cha Uza, kwa nini ni muhimu kukumbuka kwamba Yehova huona nia ya moyo?

21 Kama ilivyotajwa mapema, Yehova anaweza kusoma mioyo. Kwa kuwa Neno lake linataja tendo la Uza kuwa “tendo lisilo la heshima,” huenda Yehova aliona nia fulani ya kibinafsi ambayo haitajwi kihususa katika simulizi hilo. Je, labda Uza alikuwa mtu mwenye kimbelembele, ambaye alikuwa na mwelekeo wa kuvuka mipaka? (Methali 11:2) Je, kusafirisha hadharani Sanduku hilo ambalo familia yao ilililinda kisiri kulimfanya ahisi kuwa mtu wa maana? (Methali 8:13) Je, Uza alikosa imani sana hivi kwamba afikiri kuwa mkono wa Yehova ulikuwa mfupi sana asiweze kulinda sanduku hilo takatifu ambalo liliwakilisha kuwapo Kwake? Vyovyote vile, tunaweza kuwa na uhakika kwamba Yehova alifanya yaliyo sawa. Yaelekea aliona jambo fulani katika moyo wa Uza ambalo lilifanya atekeleze hukumu bila kukawia.—Methali 21:2.

Msingi Thabiti wa Kuwa na Uhakika

22. Hekima ya Yehova inaonekanaje wakati Neno lake halitaji habari fulani?

22 Hekima ya Yehova isiyo na kifani inaonekana katika maana ya kwamba nyakati nyingine Neno lake hukosa kutaja habari fulani. Kwa kufanya hivyo, Yehova hutupatia nafasi ya kuonyesha kwamba tunamtumaini. Kutokana na mambo ambayo tumezungumzia, je, si wazi kwamba tuna sababu nzuri za kukubali hukumu za Yehova? Naam, tunapojifunza Neno la Mungu tukiwa na moyo mnyoofu na akili iliyo wazi, tunajifunza mambo mengi kumhusu Yehova yanayotusadikisha kwamba sikuzote yeye hufanya yaliyo sawa na haki. Hivyo, ikiwa simulizi fulani la Biblia linatokeza maswali tusiyoweza kupata majibu yaliyo wazi mara moja, acheni tuwe na uhakika kabisa kwamba Yehova alifanya yaliyo sawa.

23. Tunaweza kuwa na uhakika gani kuhusu mambo ambayo Yehova atafanya wakati ujao?

23 Tunaweza kuwa na uhakika huohuo kuhusu mambo ambayo Yehova atafanya wakati ujao. Hivyo, tunaweza kuwa na uhakika kwamba atakapotekeleza hukumu wakati wa dhiki kuu inayokaribia, ‘hatafagilia mbali mwadilifu pamoja na mwovu.’ (Mwanzo 18:23) Hawezi kufanya hivyo kamwe kwa kuwa anapenda uadilifu na haki. Pia tunaweza kuwa na uhakika kwamba katika ulimwengu wake mpya unaokuja, atatosheleza mahitaji yetu yote kwa njia bora kabisa.—Zaburi 145:16.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 15 Abrahamu alikuwa na sababu ya kuogopa kwa kuwa mafunjo fulani ya zamani yanataja Farao mmoja ambaye aliwatuma wanaume wenye silaha wamkamate mwanamke fulani mrembo na kumuua mume wake.

^ fu. 16 Kwa habari zaidi, ona Mnara wa Mlinzi, (Kiingereza) Desemba 1, 1979, ukurasa wa 31.

Je, Unakumbuka?

• Tuna sababu zipi za kukubali hukumu za Yehova?

• Ni nini kinachoweza kutusaidia tuepuke kukata kauli kimakosa kuhusu tendo la Loti la kutaka kuupa umati wenye hasira binti zake?

• Ni mambo gani yanayoweza kutusaidia kuelewa kwa nini Yehova alimuua Uza?

• Tunaweza kuwa na uhakika gani kuhusu mambo ambayo Yehova atafanya wakati ujao?

[Maswali ya Funzo]