Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Uhai Wako Ni Wenye Thamani Kadiri Gani?

Uhai Wako Ni Wenye Thamani Kadiri Gani?

Uhai Wako Ni Wenye Thamani Kadiri Gani?

WATU wengi walipokuwa wakiuawa huko Ulaya wakati wa Vita vya Kwanza vya Ulimwengu, jitihada kubwa zilikuwa zikifanywa kuokoa uhai huko Antaktika. Mvumbuzi Mwingireza-Muairishi Ernest Shackleton na wenzake walipatwa na msiba wakati meli yao Endurance ilipogonga mapande ya barafu na kuzama. Shackleton alifaulu kuwaokoa watu wake na kuwapeleka mahali penye usalama wa kadiri fulani kwenye Kisiwa cha Elephant katika Bahari ya Atlantiki Kusini. Lakini bado walikabili hatari kubwa sana.

Shackleton alitambua kwamba tumaini lao la kuokoka lilitegemea tu kuomba msaada kutoka kituo cha kuwinda nyangumi katika kisiwa cha South Georgia. Kituo hicho kilikuwa umbali wa kilometa 1,100, naye alikuwa tu na mashua ndogo ya kuokoa uhai yenye urefu wa meta 6.7 aliyokuwa ameokoa kutoka kwenye meli Endurance. Matarajio yao hayakuwa mazuri.

Hata hivyo, baada ya siku 17 zenye kutisha, Mei 10, 1916, Shackleton na kikundi kidogo walifika South Georgia, lakini hali mbaya ya hewa baharini iliwalazimisha kutia nanga upande usiofaa wa kisiwa. Iliwabidi kutembea kwenye kijia kisicho na alama yoyote umbali wa kilometa 30 juu ya milima iliyofunikwa na theluji ili kufika mahali walipokuwa wakienda. Chini ya hali ngumu sana—hali ya hewa yenye baridi kali na bila vifaa vizuri vya kupanda milima—Shackleton na wenzake walifika mahali walipokuwa wakienda na mwishowe akawaokoa watu wake wote waliokuwa wamekwama kwenye Kisiwa cha Elephant. Kwa nini Shackleton alifanya jitihada hiyo yenye bidii? Roland Huntford, mwandikaji wa historia ya maisha ya watu, anaandika hivi: “Kusudi lake kuu lilikuwa kuwaokoa watu wake wote.”

“Hakuna Hata Moja Kati ya Hizo Inayokosekana”

Ni nini kilichowasaidia watu wa Shackleton wasikate tamaa kabisa walipokuwa wamejikunyata huku wakingoja kwenye “kipande cha mwamba chenye barafu, kilichokuwa ukiwa na kisichofikika, chenye urefu wa kilometa 30”? Walikuwa na uhakika kwamba kiongozi wao angetimiza ahadi yake ya kuwaokoa.

Leo wanadamu ni kama watu hao waliokuwa wamekwama kwenye Kisiwa cha Elephant. Wengi huishi katika hali ngumu sana wakijitahidi ili kuendelea tu kuwa hai. Hata hivyo, wanaweza kuwa na uhakika kabisa kwamba Mungu “atamwokoa mwenye kuteseka” kutoka katika ukandamizaji na taabu. (Ayubu 36:15) Uwe na uhakika kwamba Mungu huona uhai wa kila mtu kuwa wenye thamani. Yehova Mungu, Muumba anasema hivi: ‘Uniite katika siku ya taabu, nami nitakuokoa.’—Zaburi 50:15.

Je, unaona ni vigumu kuamini kwamba Muumba hukuona wewe binafsi—ukiwa mtu mmoja kati ya mabilioni duniani—kuwa mwenye thamani? Basi, ona yale ambayo nabii Isaya aliandika kuhusu mabilioni ya nyota katika mabilioni ya makundi ya nyota katika ulimwengu mkubwa unaotuzunguka. Tunasoma hivi: “Inueni macho yenu juu, mwone. Ni nani ameviumba vitu hivi? Ni Yeye anayelileta jeshi lake kulingana na hesabu, ambaye zote anaziita kwa jina. Kutokana na wingi wa nguvu zenye msukumo, yeye pia akiwa hodari katika nguvu, hakuna hata moja kati ya hizo inayokosekana.”—Isaya 40:26.

Je, unaelewa maneno hayo yanamaanisha nini? Mfumo wetu wa jua ni sehemu ndogo tu ya kundi letu la nyota liitwalo Kilimia, ambalo lina nyota bilioni 100 hivi. Kuna makundi mengine mangapi ya nyota? Kwa kweli hakuna anayejua, lakini makadirio fulani yanasema ni bilioni 125. Hiyo ni hesabu ya nyota yenye kustaajabisha kama nini! Hata hivyo, Biblia inatueleza kwamba Muumba wa ulimwengu anajua kila nyota kwa jina.

“Nywele Zenyewe za Kichwa Chenu Zimehesabiwa Zote”

‘Lakini,’ huenda mtu akabisha, ‘kujua tu majina ya mabilioni ya nyota au mabilioni ya watu hakumaanishi unamjali mtu mmoja-mmoja.’ Kompyuta yenye kumbukumbu ya kutosha inaweza kuorodhesha majina ya mabilioni ya watu. Lakini hakuna mtu ambaye angefikiri kwamba kompyuta hiyo inajali kila mmoja wa watu hao. Hata hivyo, Biblia inaonyesha kwamba Yehova Mungu anajua majina ya mabilioni ya watu, na pia huwajali wakiwa mtu mmoja-mmoja. Mtume Petro aliandika hivi: ‘Tupeni mahangaiko yenu yote juu yake, kwa sababu yeye anawajali ninyi.’—1 Petro 5:7.

Yesu Kristo alisema: “Je, shomoro wawili hawauzwi kwa sarafu ya thamani ndogo? Na bado hakuna hata mmoja wao atakayeanguka chini bila Baba yenu kujua. Lakini nywele zenyewe za kichwa chenu zimehesabiwa zote. Kwa hiyo msiogope: ninyi ni bora kuliko shomoro wengi.” (Mathayo 10:29-31) Ona kwamba Yesu hakusema kwamba Mungu angejua tu kile kilichotukia kwa shomoro na watu. Alisema: “Ninyi ni bora kuliko shomoro wengi.” Kwa nini wewe ni bora zaidi? Kwa sababu uliumbwa “kwa mfano wa Mungu,” yaani, ukiwa na uwezo wa kukuza na kudhihirisha sifa za kiadili, kiakili, na kiroho, ambazo Mungu mwenyewe hudhihirisha kwa hali ya juu zaidi.—Mwanzo 1:26, 27.

Matokeo ya Utendaji Wenye Akili”

Usiogozwe vibaya na maneno ya watu wanaokana kwamba kuna Muumba. Kulingana na maoni yao, umefanyizwa na nguvu za asili zisizo na utu. Wanadai kwamba, mbali na kuumbwa “kwa mfano wa Mungu,” wewe si tofauti na wanyama wengine wote walio katika sayari hii, kutia ndani shomoro.

Je, ni jambo linalopatana na akili kuamini kwamba uhai ulitokana na nguvu fulani au ulitokea kiaksidenti tu? Kulingana na mwana-biolojia wa molekuli Michael J. Behe “miundo ya kikemia iliyo tata sana” ambayo huongoza uhai hufanya wazo hilo kuwa lisilo la akili kabisa. Anasema kwamba, uthibitisho wa biokemia unaongoza kwenye mkataa thabiti kwamba ‘kimsingi, uhai ulitokea duniani kwa sababu ya utendaji wenye akili.’ —Darwin’s Black Box—The Biochemical Challenge to Evolution.

Biblia inatueleza kwamba uhai wote duniani ulitokana na utendaji wenye akili. Nayo inatueleza kwamba Chanzo cha utendaji huo wote wenye akili ni Yehova Mungu, Muumba wa ulimwengu wote.—Zaburi 36:9; Ufunuo 4:11.

Usiache wazo la kwamba tunapaswa kuvumilia katika ulimwengu huu ulio na maumivu na mateso mengi likuzuie kuamini kwamba kuna Muumba na Mbuni wa dunia na uhai wote uliomo. Kumbuka kweli mbili za msingi. Moja ni kwamba Mungu hakusababisha kutokamilika ambako kumeenea leo. Pili, Muumba wetu ana sababu thabiti ya kuruhusu kwa muda kutokamilika huko. Kama vile gazeti hili limeeleza mara kwa mara, Yehova Mungu ameruhusu uovu uendelee kwa muda tu ili kutatua kwa umilele wote masuala ya kiadili yaliyozushwa wakati wanadamu walipokataa kwa mara ya kwanza enzi yake kuu. *Mwanzo 3:1-7; Kumbukumbu la Torati 32:4, 5; Mhubiri 7:29; 2 Petro 3:8, 9.

“Atamkomboa Maskini Anayelilia Msaada”

Bila shaka, hata katika hali mbaya ambazo huwapata watu wengi leo, bado uhai ni zawadi bora. Nasi hufanya yote tuwezayo ili kuulinda. Uhai ambao Mungu anaahidi wakati ujao hautakuwa na hali ngumu na zenye mateso kama yale ambayo watu wa Shackleton walivumilia katika Kisiwa cha Elephant. Kusudi la Mungu ni kutuokoa kutoka katika hali za sasa zenye taabu na ubatili ‘ili tuushike imara uzima ulio wa kweli’ ambao Mungu alikusudia hapo mwanzoni kwa viumbe wake wa kibinadamu.—1 Timotheo 6:19.

Mungu atafanya yote hayo kwa sababu kila mmoja wetu ni mwenye thamani machoni pake. Alifanya mpango ili Mwana wake, Yesu Kristo, atoe dhabihu ya fidia iliyohitajiwa kutuweka huru na dhambi, kutokamilika, na kifo tulichorithi kutoka kwa wazazi wetu wa kwanza, Adamu na Hawa. (Mathayo 20:28) Yesu Kristo alisema hivi: “Mungu aliupenda ulimwengu sana hivi kwamba akamtoa Mwana wake mzaliwa-pekee, ili kila mtu anayemwamini . . . awe na uzima wa milele.”—Yohana 3:16.

Mungu atafanya nini kwa wale ambao sasa maisha yao yanaathiriwa na mateso na ukandamizaji? Neno la Mungu lililoongozwa na roho yake linatuambia hivi kumhusu Mwana wake: “Atamkomboa maskini anayelilia msaada, pia mwenye kuteseka na yeyote ambaye hana msaidizi. Atamsikitikia mtu wa hali ya chini na maskini, naye ataziokoa nafsi za maskini. Ataikomboa nafsi yao kutoka katika ukandamizaji na katika jeuri.” Kwa nini atafanya hivyo? Kwa sababu “damu yao [au, uhai wao] itakuwa na thamani machoni pake.”Zaburi 72:12-14.

Kwa karne nyingi, wanadamu wameteseka kwa kulemewa na dhambi na kutokamilika, na “kuugua” katika maumivu na mateso mengi. Mungu aliruhusu hilo tu huku akijua kwamba angesuluhisha madhara yoyote ambayo yangetokana nayo. (Waroma 8:18-22) Hivi karibuni, ataleta mabadiliko kwa ‘kurudisha mambo yote’ kupitia serikali yake ya Ufalme inayoongozwa na Mwana wake, Yesu Kristo.—Matendo 3:21; Mathayo 6:9, 10.

Hilo linatia ndani ufufuo wa watu ambao wameteseka na kufa nyakati za kale. Wako katika kumbukumbu la Mungu. (Yohana 5:28, 29; Matendo 24:15) Hivi karibuni, watapokea uhai “kwa wingi,” yaani, uzima wa milele katika ukamilifu kwenye dunia paradiso isiyo na maumivu na mateso. (Yohana 10:10; Ufunuo 21:3-5) Kila mwanadamu anayeishi ataweza kufurahia uhai mkamilifu na kukuza sifa bora na uwezo mbalimbali unaoonyeshwa na wale walioumbwa “kwa mfano wa Mungu.”

Je, utakuwa hai ili kufurahia uhai ambao Yehova ameahidi? Uamuzi ni wako. Tunakuhimiza ufaidike na mipango ambayo Mungu ameandaa ili kuleta baraka hizo zote. Wachapishaji wa gazeti hili watafurahi kukusaidia kufanya hivyo.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 17 Kwa maelezo zaidi kuhusu habari hii, ona sura ya 8, “Sababu Gani Mungu Huruhusu Kuteseka?” katika kitabu Ujuzi Uongozao Kwenye Uhai Udumuo Milele, kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

[Picha katika ukurasa wa 4, 5]

Watu wa Shackleton waliokuwa wamekwama walikuwa na uhakika kwamba angetimiza ahadi yake ya kuwaokoa

[Hisani]

© CORBIS

[Picha katika ukurasa wa 6]

“Ninyi ni bora kuliko shomoro wengi”