Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Kweli Miujiza Hutukia?

Je, Kweli Miujiza Hutukia?

Je, Kweli Miujiza Hutukia?

MTU huyo alivutiwa papo hapo na kibandiko kilichokuwa nyuma ya gari lililopita, “Miujiza Hutukia—Waulize Malaika.” Ingawa alikuwa mtu anayependa dini, mwanamume huyo hakuelewa maneno hayo yalimaanisha nini. Je, kibandiko hicho kilionyesha kwamba dereva huyo aliamini miujiza? Au ilikuwa njia ya kimzaha tu ya kuonyesha kwamba watu hawaamini miujiza wala malaika?

Huenda ukapendezwa kujua yale ambayo mwandikaji Mjerumani Manfred Barthel alisema: “Muujiza ni neno ambalo mara moja hugawanya wasomaji katika pande mbili zinazopingana.” Wale wanaoamini miujiza wanasadiki kwamba miujiza hutukia, nayo hutukia mara nyingi. * Kwa mfano, imeripotiwa kwamba huko Ugiriki katika miaka ya hivi karibuni, waamini wamedai kwamba miujiza hutukia karibu mara moja kwa mwezi. Jambo hilo lilifanya askofu wa Kanisa Othodoksi la Ugiriki kuonya hivi: “Mtu anayeamini miujiza huelekea kumwona Mungu, Maria, na watakatifu kuwa wana sifa za kibinadamu. Waamini hawapaswi kutilia sana chumvi mambo hayo.”

Katika nchi nyingine, watu hawaamini sana miujiza. Kulingana na uchunguzi uliofanywa nchini Ujerumani na kuchapishwa mwaka wa 2002, asilimia 71 ya Wajerumani hawaamini kwamba miujiza hutukia. Hata hivyo, miongoni mwa watu wanaopungua theluthi moja ambao huamini miujiza, kuna wanawake watatu wanaodai kwamba walipokea ujumbe kutoka kwa Bikira Maria. Miezi michache baada ya kudaiwa kwamba Maria aliwatokea akiwa pamoja na malaika na njiwa mmoja, gazeti la Ujerumani, Westfalenpost liliripoti hivi: “Kufikia sasa watu wapatao 50,000 wanaotembelea sehemu takatifu ambao wanataka kuponywa, na pia wadadisi wamependezwa sana na maono yaliyoonwa na wanawake hao.” Watu wengine 10,000 walitarajiwa kwenda kwenye kijiji hicho kuona maono zaidi ya Maria. Inasemekana kwamba maono mengine ya Bikira Maria yalionekana huko Lourdes, Ufaransa, mwaka wa 1858, na huko Fátima, Ureno, mwaka wa 1917.

Namna Gani Dini Zisizo za Kikristo?

Karibu dini zote huamini miujiza. Kichapo The Encyclopedia of Religion kinaeleza kwamba waanzilishi wa Ubudha, Ukristo, na Uislamu walikuwa na maoni mbalimbali kuhusu miujiza, lakini kinasema: “Historia ya baadaye ya dini hizo huonyesha wazi kwamba miujiza na masimulizi kuhusu miujiza yamekuwa sehemu muhimu ya imani ya kidini ya wanadamu.” Kichapo hicho kinasema kwamba “nyakati nyingine Buddha mwenyewe alifanya miujiza.” Baadaye, “dini ya Ubudha ilipopelekwa China, mara nyingi wamishonari wake walifanya miujiza.”

Baada ya kutaja miujiza kadhaa inayodaiwa kwamba ilitukia, kichapo hicho kinamalizia hivi: “Huenda mtu asikubali masimulizi yote ya miujiza yanayosimuliwa na waandikaji wa wasifu wanaofuata sana dini, lakini bila shaka masimulizi hayo yalitungwa kwa nia nzuri ya kumtukuza Buddha, ambaye alikuwa na uwezo wa kuwapa wafuasi wake wenye bidii nguvu hizo za kimuujiza.” Kichapo hichohicho kinasema hivi kuhusu Uislamu: “Waislamu wengi bado hutarajia miujiza itukie. Mapokeo (hadīths) yanasema kwamba Muhammad alifanya miujiza pindi nyingi hadharani. . . . Hata baada ya watakatifu kufa, inaaminika kwamba wao hufanya miujiza wakiwa makaburini ili kuwafaidi waumini, nao watu hutafuta msaada wao kwa bidii.”

Namna Gani Miujiza Katika Dini za Kikristo?

Wengi ambao wamekubali Ukristo wana maoni yanayotofautiana. Wengine hukubali kwamba miujiza inayotajwa katika Biblia kuwa ilifanywa na Yesu Kristo au watumishi wa Mungu kabla ya Ukristo ilitukia. Hata hivyo, wengi wanakubaliana na Mprotestanti Martin Luther aliyeleta marekebisho ya kidini. Kichapo The Encyclopedia of Religion kinasema hivi kumhusu: “Wote wawili, Luther na Calvin waliandika kwamba enzi za miujiza zilikuwa zimepita na kwamba watu hawapaswi kutarajia miujiza itukie.” Kichapo hicho kinasema kwamba Kanisa Katoliki liliendelea kuamini miujiza, “pasipo kueleza jinsi miujiza hiyo ilivyotukia.” Hata hivyo, “baadaye wasomi Waprotestanti waliamini kwamba Ukristo ulihusiana sana na maadili na kwamba wala Mungu wala viumbe wa roho hawana uvutano mkubwa katika maisha ya wanadamu.”

Watu wengine wanaojidai kuwa Wakristo, kutia ndani baadhi ya viongozi wa kidini hutilia shaka kama kweli miujiza inayotajwa katika Biblia ilitukia. Kwa mfano, fikiria lile simulizi la mti uliokuwa ukiteketea linalotajwa katika Biblia kwenye Kutoka 3:1-5. Kitabu What the Bible Really Says kinaeleza kwamba wanatheolojia wengi Wajerumani hawaoni simulizi hilo kuwa muujiza. Badala yake, wanasema kwamba “lilifananisha Musa akipambana na dhamiri iliyokuwa ikimsumbua.” Kitabu hicho kinaendelea kusema: “Miali inaweza kuonwa kuwa maua yaliyochanua kwa ghafula katika nuru ya kuwapo kwa Mungu.”

Huenda usiridhishwe na maelezo hayo. Hivyo basi, uamini nini? Je, ni jambo linalopatana na akili kuamini kwamba miujiza ilitukia? Namna gani miujiza inayotukia leo? Kwa kuwa hatuwezi kuwauliza malaika, tutamuuliza nani?

Maoni ya Biblia

Hakuna mtu anayeweza kukana kwamba hapo zamani nyakati nyingine Mungu aliingilia kati na kufanya mambo yasiyoweza kufanywa na wanadamu. Tunasoma hivi kumhusu: “Nawe ukawatoa watu wako Israeli katika nchi ya Misri, kwa ishara na kwa miujiza na kwa mkono wenye nguvu na kwa mkono ulionyooshwa na kwa hali kuu ya kuogopesha.” (Yeremia 32:21) Hebu wazia, taifa lililokuwa na nguvu sana wakati huo lilinyenyekezwa kwa mapigo kumi kutoka kwa Mungu, kutia ndani kuuawa kwa wazaliwa wake wa kwanza. Mapigo hayo yalikuwa kweli miujiza.—Kutoka, sura ya 7 hadi 14.

Karne nyingi baadaye, wale waandikaji wanne wa Injili walitaja miujiza 35 hivi iliyofanywa na Yesu. Kwa kweli, maneno yao yanaonyesha kwamba Yesu alifanya miujiza mingi zaidi ya ile waliyotaja. Je, kweli miujiza hiyo ilitukia? *Mathayo 9:35; Luka 9:11.

Ikiwa kweli Biblia ni Neno la Mungu kama inavyodai, basi una sababu nzuri ya kuamini miujiza ambayo inataja. Biblia inataja wazi miujiza iliyotukia hapo zamani, yaani, miujiza ya kuponywa, kufufuliwa, na kadhalika, lakini pia inaeleza wazi kwamba miujiza hiyo haitukii tena. (Ona sanduku “Kwa Nini Miujiza Haitukii Tena Kama Zamani?” kwenye ukurasa wa 4.) Je, hilo linamaanisha kwamba hata wale wanaoiamini Biblia hawaamini miujiza inayotukia leo? Acha makala inayofuata itujibu.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 3 Neno “miujiza” kama linavyotumiwa katika makala haya linafafanuliwa hivi katika kamusi mmoja ya Biblia: “Matokeo katika ulimwengu halisi ambayo hupita nguvu za kibinadamu au za kiasili zinazojulikana na kwa hiyo huonwa kuwa yanasababishwa na nguvu zipitazo za kibinadamu.”

^ fu. 14 Unaweza kuchunguza uthibitisho wa kwamba kweli tunaweza kuiamini Biblia. Uthibitisho huo unapatikana katika kitabu BibliaNeno la Mungu au la Binadamu? kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

[Sanduku katika ukurasa wa 4]

Kwa Nini Miujiza Haitukii Tena Kama Zamani?

Biblia inataja miujiza mbalimbali. (Kutoka 7:19-21; 1 Wafalme 17:1-7; 18:22-38; 2 Wafalme 5:1-14; Mathayo 8:24-27; Luka 17:11-19; Yohana 2:1-11; 9:1-7) Mingi ya miujiza hiyo ilisaidia kumtambulisha Yesu kuwa Masihi, na kuthibitisha kwamba alikuwa akiungwa mkono na Mungu. Wafuasi wa Yesu wa mapema walikuwa na zawadi za kufanya miujiza, kama vile kusema katika lugha na utambuzi wa maneno yaliyoongozwa na roho. (Matendo 2:5-12; 1 Wakorintho 12:28-31) Zawadi hizo za kufanya miujiza zililinufaisha sana kutaniko la Kikristo lilipokuwa bado jipya. Jinsi gani?

Kwanza, kulikuwa na nakala chache tu za Maandiko. Kwa kawaida, ni matajiri tu waliokuwa na vitabu vya kukunjwa au vitabu vingine vyovyote. Katika nchi za kipagani, watu hawakuijua Biblia au Mtungaji wake, Yehova. Watu walifundishwa mafundisho ya Kikristo kwa mdomo. Zawadi za kufanya miujiza zilisaidia kuonyesha kwamba Mungu alikuwa akilitumia kutaniko la Kikristo.

Lakini Paulo alieleza kwamba zawadi hizo zingekoma baada ya makusudi yake kutimia. “Kama kuna zawadi za kutoa unabii, zitaondolewa mbali; kama kuna lugha, zitakoma; kama kuna ujuzi, utaondolewa mbali. Kwa maana tuna ujuzi wa sehemu tu nasi tunatoa unabii kwa sehemu tu; lakini wakati kile kilicho kamili kitakapofika, kile kilicho kwa sehemu tu kitaondolewa mbali.”—1 Wakorintho 13:8-10.

Leo, watu wanaweza kupata Biblia, na pia konkodansi na ensaiklopedia. Wakristo zaidi ya milioni sita waliozoezwa wanawasaidia wengine kupata ujuzi kumhusu Mungu kutoka katika Biblia. Hivyo, miujiza haihitajiki tena ili kuthibitisha kwamba Yesu Kristo ndiye Mkombozi aliyewekwa na Mungu au ili kuthibitisha kwamba Yehova anawaunga mkono watumishi wake.