Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Wewe Hujilinganisha na Wengine?

Je, Wewe Hujilinganisha na Wengine?

Je, Wewe Hujilinganisha na Wengine?

NI NANI kati yetu ambaye hajawahi kukutana na mtu mwenye sura nzuri zaidi kuliko yeye, anayejulikana zaidi, anayeelewa mambo kwa haraka zaidi, au ambaye ni mwanafunzi bora zaidi? Pengine wengine wana afya bora au kazi nzuri zaidi, wanafanikiwa zaidi, au inaonekana wana marafiki wengi zaidi. Huenda wakawa na mali zaidi, pesa zaidi, gari lipya, au huenda wakaonekana kuwa wenye furaha zaidi. Kwa kutaja mambo hayo, je, sisi tunajilinganisha na wengine? Je, ni lazima tujilinganishe na wengine? Kwa nini huenda Mkristo akataka kuepuka kujilinganisha na wengine? Nasi tunawezaje kuridhika pasipo kujilinganisha na mtu yeyote?

Kwa Nini na Ni Wakati Gani Huenda Tukajilinganisha na Wengine?

Huenda watu wakajilinganisha na wengine kwa kuwa inadhaniwa kwamba kufanya hivyo kutawafanya wajiheshimu. Mara nyingi watu huridhika wanapoona kwamba wanafanikiwa kama watu wa rika lao. Inadhaniwa kwamba sisi hujilinganisha na wengine ili kupunguza wasiwasi, kuelewa mambo tunayoweza kufanya na yale tusiyoweza kufanya. Tunaona mambo ambayo wengine wametimiza. Ikiwa wao ni kama sisi katika mambo mengi na wamefikia miradi fulani, huenda tukahisi kwamba sisi pia tunaweza kufikia miradi kama hiyo.

Mara nyingi watu hujilinganisha na wale wanaofanana nao kwa njia fulani, yaani, watu wa jinsia moja, wa umri mmoja, wa tabaka moja na wanaojuana. Yaelekea hatutajilinganisha na mtu mwingine ikiwa tunaona kwamba kuna tofauti kubwa kati yetu na yeye. Kwa maneno mengine, yaelekea msichana tineja hatajilinganisha na mwonyesha-mitindo mashuhuri, bali atajilinganisha na wanafunzi wenzake, na yaelekea mwonyesha-mtindo hatajilinganisha na tineja.

Watu hujilinganisha katika mambo gani? Kitu au sifa yoyote inayoonwa kuwa muhimu katika jamii, kama vile, kuwa na akili, urembo, mali, mavazi. Hata hivyo, tuna mwelekeo wa kujilinganisha na wengine katika mambo yanayotupendeza. Kwa mfano, huenda tusimwonee wivu rafiki ambaye amekusanya stempu nyingi sana ikiwa sisi hatupendezwi na kukusanya stempu.

Kujilinganisha na wengine hutokeza hisia mbalimbali, kama vile uradhi, kushuka moyo, husuda, tamaa ya kutaka kuigwa, wasiwasi au uadui. Baadhi ya hisia hizo hutokeza madhara, nazo hazipatani na sifa za Kikristo.

Kujilinganisha Kunakotokeza Mashindano

Wengi wanaojitahidi kuwashinda wengine wanapojilinganisha nao huonyesha roho ya kushindana. Wao hutaka kuwa bora kuliko wengine, nao hawaridhiki hadi wanapojihisi kuwa bora zaidi. Haifurahishi kushirikiana na watu kama hao. Urafiki kama huo husababisha hali ya kutoelewana. Watu kama hao si wanyenyekevu na pia hawafuati shauri la Biblia la kuwapenda wanadamu wenzao, kwa kuwa mtazamo wao unaweza kuwashushia wengine heshima na kuwafanya wajihisi kuwa hawafai kitu.—Mathayo 18:1-5; Yohana 13:34, 35.

Kufanya watu wajihisi kuwa duni huwaumiza kwa njia fulani. Kulingana na mwandikaji mmoja, “sisi huumia sana tunapokosa kutimiza mambo fulani hasa tunapoona watu walio katika hali kama zetu wametimiza mambo tuliyotaka.” Kwa hiyo, roho ya kushindana husababisha wivu, kinyongo, na chuki kuelekea mtu mwingine kwa sababu ya mali, ufanisi, cheo, sifa, mafanikio yake, na kadhalika. Hilo husababisha mashindano zaidi. Biblia inashutumu “kuchochea mashindano.”—Wagalatia 5:26.

Watu wenye wivu hujaribu kujitukuza kwa kudharau mafanikio ya washindani wao. Huenda hisia hizo zikaonekana kuwa mambo madogo, lakini zisipotambuliwa na kuzuiwa, zinaweza kumfanya mtu atende mambo maovu kwa sababu ya chuki. Fikiria masimulizi mawili ya Biblia yaliyohusisha wivu.

Alipokuwa akiishi kati ya Wafilisti, Isaka alibarikiwa kuwa na “makundi ya kondoo na mifugo ya ng’ombe na kundi kubwa la watumishi, hivi kwamba Wafilisti wakaanza kumwonea wivu.” Wivu wao uliwachochea wafunike visima ambavyo vilichimbwa na Abrahamu, baba ya Isaka, naye mfalme wao akamwamuru Isaka aondoke katika eneo hilo. (Mwanzo 26:1-3, 12-16) Wivu wao ulikuwa wenye chuki na wenye madhara. Hawakuweza tena kuvumilia ufanisi wa Isaka katika nchi yao.

Karne nyingi baadaye, Daudi alijipatia sifa kwenye uwanja wa vita. Uhodari wake ulisifiwa na wanawake wa Israeli, ambao waliimba hivi: “Sauli amepiga maelfu yake, na Daudi makumi ya maelfu yake.” Ingawa Sauli alisifiwa kwa kadiri fulani, aliona ulinganisho huo kuwa jambo la kumshushia heshima, naye akaanza kuona wivu. Tangu hapo na kuendelea, alikuza uadui kuelekea Daudi. Punde tu baada ya hapo akafanya jaribio la kwanza kati ya majaribio mengi ya kumuua Daudi. Wivu unaweza kumfanya mtu atende uovu mkubwa.—1 Samweli 18:6-11.

Hivyo, ikiwa kujilinganisha na matendo au mafanikio ya wengine kunachochea hisia kama hizo za wivu au roho ya kushindana, tujihadhari! Hizo ni hisia zenye kudhuru ambazo hazipatani na kufikiri kwa Mungu. Lakini kabla ya kuchunguza jinsi tunavyoweza kukabiliana na mitazamo kama hiyo, acheni tuchunguze jambo lingine ambalo hufanya tujilinganishe na wengine.

Kujichunguza na Kuridhika

‘Je, mimi ni mwenye akili, ninavutia, nina uwezo wa kufanya mambo vizuri, nina afya nzuri, ninaheshimiwa, ninapendwa? Na ni kwa kadiri gani?’ Kwa kawaida hatusimami mbele ya kioo na kujiuliza maswali kama hayo. Hata hivyo, kulingana na mwandikaji mmoja, “kwa wazi sisi hujiuliza maswali kama hayo mara nyingi nayo hutokeza akilini majibu ya kimya-kimya yasiyoridhisha kabisa.” Huenda mtu ambaye hana uhakika wa mambo anayoweza kutimiza, akafikiria mambo bila kuwa na roho ya kushindana au wivu. Anajaribu tu kujichunguza. Hakuna ubaya wowote wa kufanya hivyo. Lakini si lazima ajilinganishe na wengine ili kutimiza hilo.

Tuna uwezo tofauti-tofauti, ikitegemea mambo mbalimbali. Sikuzote kutakuwa na watu ambao yaelekea watafanya mambo kwa njia bora zaidi kuliko sisi. Kwa hiyo, badala ya kuwaonea wivu, tunapaswa kupima uwezo wetu kupatana na viwango vya Mungu vya uadilifu, ambavyo hutoa mwongozo ulio hakika kuhusu yaliyo maadilifu na mema. Yehova anapendezwa nasi tukiwa mtu mmoja-mmoja. Hahitaji kutulinganisha na mtu mwingine. Mtume Paulo anatushauri hivi: “Kila mmoja na athibitishe kazi yake mwenyewe ni nini, kisha atakuwa na sababu ya kufurahi kwa habari yake mwenyewe peke yake, na si kwa kujilinganisha na mtu yule mwingine.”—Wagalatia 6:4.

Kushinda Wivu

Kwa sababu wanadamu wote si wakamilifu, huenda jitihada yenye bidii na yenye kuendelea ikahitajiwa ili kushinda wivu. Tunajua kwamba Maandiko yanatuambia: “Katika kuonyeshana heshima iweni wa kwanza,” lakini ni vigumu zaidi kufanya hivyo. Paulo alitambua kwamba ana mwelekeo wa dhambi. Ili kushindana nao, alipaswa ‘kuupigapiga mwili wake na kuuongoza kama mtumwa.’ (Waroma 12:10; 1 Wakorintho 9:27) Kwa upande wetu, huenda hilo likamaanisha kupinga mawazo ya kushindana, na kuwa na mawazo yenye kujenga. Tunahitaji kumwomba Yehova ili atusaidie ‘tusijifikirie wenyewe zaidi kuliko ilivyo lazima kufikiri.’—Waroma 12:3.

Funzo la Biblia na kutafakari kunasaidia pia. Kwa mfano, fikiria ahadi ya Mungu kuhusu Paradiso ya wakati ujao. Wakati huo, watu wote watakuwa na amani, afya njema, chakula kingi, nyumba nzuri, na kazi yenye kuridhisha. (Zaburi 46:8, 9; 72:7, 8, 16; Isaya 65:21-23) Je, kuna yeyote atakayekuwa na mwelekeo wa kushindana? La. Hakutakuwa na sababu ya kufanya hivyo. Kwa kweli, Yehova hajatueleza kikamili jinsi maisha yatakavyokuwa wakati huo, lakini ni jambo linalopatana na akili kuwazia kwamba watu wote wataweza kufanya mambo yanayowapendeza na ambayo wana ujuzi wa kuyafanya. Huenda mtu mmoja akajifunza kuhusu mambo ya anga, na mwingine kutengeneza vitambaa maridadi. Hakutakuwa na sababu ya kuoneana wivu. Kazi za wengine hazitatufanya tuwe na kinyongo, bali zitatuchochea kutimiza mambo mengi. Hisia za kushindana hazitakuwepo tena.

Ikiwa hayo ndiyo maisha tunayotaka, je, hatupaswi kujitahidi kukuza mtazamo huo sasa? Tayari tunafurahia paradiso ya kiroho, nasi hatupatwi na matatizo mengi ya ulimwengu unaotuzunguka. Kwa kuwa hakutakuwa na roho ya kushindana katika ulimwengu mpya wa Mungu, tuna sababu nzuri ya kuiepuka sasa.

Basi je, ni vibaya kujilinganisha na wengine? Au je, kuna nyakati huenda kufanya hivyo kukafaa?

Kujilinganisha Kunakofaa

Mara nyingi kujilinganisha na wengine kumetokeza huzuni au mshuko wa moyo, lakini si lazima sikuzote hali iwe hivyo. Kuhusiana na hilo, ona shauri hili la mtume Paulo: “Muwe waigaji wa wale ambao kupitia imani na subira huzirithi ahadi.” (Waebrania 6:12) Kujitahidi kukuza sifa kama zile za watumishi wa Yehova wa kale kunaweza kuwa na matokeo mazuri. Ni kweli kwamba ili kufanya hivyo, huenda tukahitaji kujilinganisha nao kwa kadiri fulani. Hata hivyo, jambo hilo linaweza kutusaidia kuona mifano ambayo tunaweza kuiga na sehemu ambazo tunahitaji kuboresha.

Fikiria mfano wa Yonathani. Kwa njia fulani, alikuwa na sababu nzuri ya kuwa na wivu. Kwa kuwa yeye ndiye aliyekuwa mwana mkubwa wa Mfalme Sauli wa Israeli, huenda wakati mmoja Yonathani alitarajia kuwa mfalme, lakini Yehova alimchagua mwanamume aliyekuwa mdogo wake kwa miaka 30 hivi, kijana Daudi. Badala ya kuweka kinyongo, Yonathani alijipatia sifa kwa kuwa rafiki asiye na ubinafsi na kumuunga Daudi mkono akiwa mfalme aliyeteuliwa na Yehova. Kwa kweli, Yonathani alikuwa mwanamume wa kiroho. (1 Samweli 19:1-4) Tofauti na baba yake, ambaye alimwona Daudi kuwa mshindani wake, Yonathani alitambua kwamba Yehova ndiye aliyekuwa akiongoza mambo, naye akajitiisha chini ya mapenzi Yake; hakujilinganisha na Daudi, huku akiuliza, “Kwa nini Daudi ndiye aliyechaguliwa wala si mimi?”

Tunapokuwa miongoni mwa Wakristo wenzetu hatupaswi kamwe kujihisi kuwa hatarini, kana kwamba wengine wanajaribu kutupita au kuchukua mahali petu. Kushindana ni jambo lisilofaa. Wakristo wakomavu hutambuliwa kwa ushirikiano, umoja, na upendo, si kwa kushindana. Mwanasosiolojia Francesco Alberoni anasema hivi: “Upendo ni adui mkubwa wa wivu. Ikiwa tunampenda mtu, tunamtakia mema, nasi tunafurahi anapofanikiwa na kuwa mwenye furaha.” Hivyo, ikiwa mtu fulani katika kutaniko la Kikristo anapewa mapendeleo fulani, tunapaswa kuridhika na hilo. Yonathani aliridhika na jinsi hali ilivyokuwa. Kama Yonathani, tutabarikiwa tukiwaunga mkono wale walio na madaraka na wanaotumikia kwa uaminifu katika tengenezo la Yehova.

Kielelezo bora kinachowekwa na Wakristo wenzetu kinaweza kuvutia. Kujilinganisha nao tukiwa na usawaziko kunaweza kutuchochea kwa njia inayofaa kuiga imani yao. (Waebrania 13:7) Lakini tusipokuwa waangalifu, kuwaiga wengine kunaweza kugeuka kuwa mashindano. Ikiwa tunahisi kwamba mtu fulani tunayevutiwa naye anatushinda nasi tunajaribu kumharibia sifa au kumchambua, hatutakuwa tukimwiga, bali tutakuwa tukimwonea wivu.

Mwanadamu asiye mkamilifu hawezi kuwa kielelezo bora kabisa. Kwa hiyo, Maandiko yanasema: “Iweni waigaji wa Mungu, kama watoto wapendwa.” Pia, “Kristo aliteseka kwa ajili yenu, akiwaachia ninyi kielelezo ili mfuate hatua zake kwa ukaribu.” (Waefeso 5:1, 2; 1 Petro 2:21) Tunapaswa kujitahidi kuiga sifa za Yehova na Yesu, yaani, upendo, shauku, hisia-mwenzi, na unyenyekevu wao. Tunapaswa kujitahidi kuwa na sifa na makusudi kama yao, na kuiga njia yao ya kufanya mambo. Kujilinganisha huko kunaweza kuboresha maisha yetu, kutupa mwongozo ulio hakika, utulivu, na usalama, na kunaweza kutusaidia kufikia kimo cha wanaume na wanawake Wakristo wakomavu. (Waefeso 4:13) Ikiwa tunajitahidi kufanya yote tuwezayo ili kuiga kielelezo chao bora, bila shaka hatutakuwa na mwelekeo wa kujilinganisha na wanadamu wenzetu.

[Picha katika ukurasa wa 29]

Mfalme Sauli alimwonea Daudi wivu

[Picha katika ukurasa wa 31]

Yonathani hakumwona kijana Daudi kuwa mshindani kamwe