Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Jivunieni Kuwa Wakristo

Jivunieni Kuwa Wakristo

Jivunieni Kuwa Wakristo

“Yeye anayejisifu, na ajisifu katika Yehova.”—1 WAKORINTHO 1:31.

1. Watu wana mtazamo gani kuelekea dini?

UBARIDI kuelekea dini. Hivyo ndivyo mchanganuzi mmoja wa masuala ya kidini alivyosema hivi karibuni kuhusu mtazamo wa watu kuelekea dini yao. Alisema: “Mwelekeo uliopo katika dini za kisasa si wa kidini hata kidogo, unaweza kufafanuliwa kwa kufaa kuwa ubaridi kuelekea dini.” Alifafanua mtazamo huo kuwa “kutotaka kujishughulisha sana na dini.” Alisema kwamba watu wengi “wanamwamini Mungu . . . ; ni kwamba tu hawajishughulishi sana naye.”

2. (a) Kwa nini haishangazi kwamba watu wamekuwa na ubaridi wa kiroho? (b) Ubaridi hutokeza hatari gani kwa Wakristo wa kweli?

2 Wanafunzi wa Biblia hawashangazwi na mtazamo huo wa ubaridi. (Luka 18:8) Na mtazamo huo unatazamiwa kuhusu dini kwa ujumla. Dini ya uwongo imewapotosha watu na kuwakatisha tamaa kwa muda mrefu. (Ufunuo 17:15, 16) Hata hivyo, ni hatari kwa Wakristo wa kweli kudhihirisha mtazamo ulioenea wa kuwa na moyo nusu-nusu na kutokuwa na bidii. Tutapatwa na madhara ikiwa tutakuwa na ubaridi kuelekea imani yetu na kupoteza hamu yetu ya kweli ya Biblia na bidii yetu ya kumtumikia Mungu. Yesu alitoa onyo hili kuhusu uvuguvugu wa namna hiyo kwa Wakristo wa karne ya kwanza walioishi Laodikia: “Wewe si baridi wala si moto. Laiti ungalikuwa baridi au moto. . . . Wewe ni vuguvugu.”—Ufunuo 3:15-18.

Kutambua Sisi Ni Nani

3. Wakristo wanaweza kujivunia mambo gani yanayowatambulisha?

3 Ili kupambana na ubaridi wa kiroho, Wakristo wanapaswa kutambua waziwazi wao ni nani, nao wanapaswa kujivunia kwa kadiri fulani utambulisho wao wa pekee. Tukiwa watumishi wa Yehova na wanafunzi wa Kristo, tunaweza kupata ufafanuzi wa utambulisho wetu katika Biblia. Sisi ni “mashahidi” wa Yehova, “wafanyakazi wenzi wa Mungu,” tunapowaeleza wengine kwa bidii “habari njema.” (Isaya 43:10; 1 Wakorintho 3:9; Mathayo 24:14) Sisi ni watu ‘wanaopendana.’ (Yohana 13:34) Wakristo wa kweli ni watu ambao “kwa kutumia, nguvu zao za ufahamu zimezoezwa kutofautisha yaliyo sawa na yaliyo makosa pia.” (Waebrania 5:14) Sisi ni “mianga katika ulimwengu.” (Wafilipi 2:15) Sisi hujitahidi ‘kudumisha mwenendo wetu ukiwa mzuri katikati ya mataifa.’—1 Petro 2:12; 2 Petro 3:11, 14.

4. Mwabudu wa Yehova anawezaje kujua yeye si mtu wa aina gani?

4 Pia waabudu wa kweli wa Yehova wanajua wao si watu wa aina gani. “Wao si sehemu ya ulimwengu,” kama vile Kiongozi wao Yesu Kristo hakuwa sehemu ya ulimwengu. (Yohana 17:16) Wao hujitenga na “mataifa,” ambayo ‘yako katika giza kiakili, na kutenganishwa mbali na uzima ambao ni wa Mungu.’ (Waefeso 4:17, 18) Kwa sababu hiyo, wafuasi wa Yesu ‘hukataa kabisa kutomwogopa Mungu na tamaa za kilimwengu na kuishi kwa utimamu wa akili na uadilifu na ujitoaji-kimungu katikati ya mfumo wa mambo wa sasa.’—Tito 2:12.

5. Ni nini maana ya kitia moyo ‘kujisifu katika Yehova’?

5 Kuelewa waziwazi utambulisho wetu na uhusiano wetu pamoja na Mtawala Mwenye Enzi Kuu ya ulimwengu wote hutuchochea ‘tujisifu katika Yehova.’ (1 Wakorintho 1:31) Huko ni kujisifu kwa aina gani? Tukiwa Wakristo wa kweli, tunajivunia Yehova kuwa Mungu wetu. Tunafuata kitia moyo hiki: “Yule anayejigamba na ajigambe kwa sababu ya jambo hili, kuwa na ufahamu na kuwa na ujuzi kunihusu mimi, kwamba mimi ni Yehova, Yeye anayeonyesha fadhili zenye upendo, haki na uadilifu duniani.” (Yeremia 9:24) ‘Tunajisifu’ kwa kuwa na pendeleo la kumjua Mungu na kutumiwa naye kuwasaidia wengine.

Ugumu Uliopo

6. Kwa nini watu fulani huona ni vigumu kudumisha utambulisho wao wa Kikristo ulio wazi?

6 Ni kweli kwamba, sikuzote si rahisi kudumisha utambulisho wetu wa Kikristo ulio wa pekee. Mwanamume mmoja kijana aliyelelewa akiwa Mkristo alikumbuka kwamba kwa kipindi fulani alikuwa na udhaifu wa kiroho. Anasema hivi: “Nyakati nyingine, nilihisi kwamba sikujua kwa nini nilikuwa Shahidi wa Yehova. Nilifunzwa kweli tangu utotoni. Nyakati nyingine nilihisi kwamba hii ilikuwa tu dini nyingine kubwa inayokubaliwa na wengi.” Huenda wengine wameruhusu vitumbuizo, vyombo vya habari, na mtazamo wa kutomwogopa Mungu uathiri utambulisho wao. (Waefeso 2:2, 3) Nyakati nyingine huenda baadhi ya Wakristo wakajitilia shaka na kuchunguza upya viwango na miradi yao.

7. (a) Ni kujichunguza kwa aina gani kunakofaa watumishi wa Mungu? (b) Hatari iko wapi?

7 Je, ni vibaya kujichunguza kwa makini kwa kiasi fulani? La. Huenda ukakumbuka kwamba mtume Paulo aliwatia moyo Wakristo waendelee kujichunguza wenyewe: “Endeleeni kujijaribu kama ninyi mko katika imani, endeleeni kuthibitisha ninyi wenyewe jinsi mlivyo.” (2 Wakorintho 13:5) Hapa mtume huyo alikuwa akiwatia moyo Wakristo wajitahidi kuchunguza udhaifu wowote wa kiroho ambao huenda wakawa nao, wakiwa na kusudi la kuchukua hatua ifaayo kuurekebisha. Mkristo anapojijaribu kama yuko katika imani anapaswa kuhakikisha ikiwa maneno na matendo yake yanapatana na mambo anayodai kuamini. Hata hivyo, kujichunguza kusikofaa ambako hutuchochea kutafuta “utambulisho” wetu au kutafuta majibu yasiyohusu uhusiano wetu pamoja na Yehova au na kutaniko la Kikristo ni kwa bure na kunaweza kuwa hatari kiroho. * Hatungependa ‘imani yetu ivunjike’ kamwe.—1 Timotheo 1:19.

Sisi Pia Hupatwa na Magumu

8, 9. (a) Musa alielezaje hisia zake za kujitilia shaka? (b) Yehova alifanyaje Musa alipohisi kuwa hana uwezo? (c) Uhakikisho wa Yehova una matokeo gani juu yako?

8 Je, Wakristo ambao pindi kwa pindi hujitilia shaka wanapaswa kuhisi kuwa wameshindwa? La. Kwa kweli, wanaweza kupata faraja kwa kujua kwamba hisia hizo zimekuwako. Mashahidi waaminifu wa Mungu wa nyakati za kale walipatwa nayo. Kwa mfano, fikiria Musa aliyeonyesha imani isiyo ya kawaida, ushikamanifu, na ujitoaji-kimungu. Alipopewa mgawo ulioonekana kuwa mgumu, Musa alisitasita na kuuliza hivi: “Mimi ni nani?” (Kutoka 3:11) Yaelekea jibu alilokuwa nalo akilini lilikuwa, ‘Mimi si mtu wa maana!’ au ‘Mimi sina uwezo!’ Huenda Musa alihisi hivyo kwa sababu ya mambo yaliyompata mapema maishani: Alitokana na taifa la watumwa. Alikuwa amekataliwa na Waisraeli. Hakuwa msemaji mwenye ufasaha. (Kutoka 1:13, 14; 2:11-14; 4:10) Alifanya kazi ya uchungaji, kazi ambayo ilichukiwa na Wamisri. (Mwanzo 46:34) Haishangazi kwamba alihisi hafai kuwa mkombozi wa watu wa Mungu waliokuwa utumwani!

9 Yehova alimpa Musa uhakikisho zaidi kupitia ahadi hizi mbili zenye nguvu: “Nitakuwa pamoja nawe, nayo hii ndiyo ishara kwako ya kwamba mimi ndiye niliyekutuma: Baada ya kuwatoa watu hao Misri, ninyi mtamtumikia Mungu wa kweli kwenye mlima huu.” (Kutoka 3:12) Mungu alikuwa akimwambia mtumishi wake mwenye kusita-sita kwamba angekuwa pamoja naye daima. Isitoshe, Yehova alikuwa akionyesha kwamba hakika angewakomboa watu wake. Katika karne zote, Mungu ametoa ahadi kama hizo za kuwasaidia watu wake. Kwa mfano, kupitia Musa aliliambia hivi taifa la Israeli lilipokuwa karibu kuingia katika Nchi ya Ahadi: “Iweni hodari na wenye nguvu. . . . Yehova Mungu wako ndiye anayepiga mwendo pamoja nawe. Hatakutupa wala kukuacha kabisa.” (Kumbukumbu la Torati 31:6) Pia Yehova alimhakikishia Yoshua hivi: “Hakuna yeyote atakayesimama imara mbele yako siku zote za maisha yako. Nitakuwa pamoja nawe, . . . Sitakutupa wala kukuacha kabisa.” (Yoshua 1:5) Naye anawaahidi Wakristo hivi: “Sitakuacha wala kukutupa hata kidogo.” (Waebrania 13:5) Kwa kuwa tuna msaada huo wenye nguvu, tunapaswa kujivunia kuwa Wakristo.

10, 11. Mlawi Asafu alisaidiwaje kudumisha mtazamo unaofaa kuhusu pendeleo la kumtumikia Yehova?

10 Karibu karne tano baada ya kifo cha Musa, Mlawi mwaminifu aliyeitwa Asafu aliandika kwa unyoofu shaka zake kuhusu umuhimu wa kufuatilia mwenendo wa uadilifu. Alipokuwa akijitahidi kumtumikia Mungu licha ya majaribu na vishawishi, Asafu aliona watu fulani waliomdhihaki Mungu wakifanikiwa na kuwa wenye nguvu zaidi. Hilo lilimwathirije Asafu? “Mimi nami karibu miguu yangu igeuke kando,” akakiri. “Hatua zangu zilikuwa karibu kuteleza. Kwa maana niliwaonea wivu wenye kujisifu, nilipokuwa nikiiona amani ya watu waovu.” Alianza kutilia shaka umuhimu wa kuwa mwabudu wa Yehova. “Hakika nimeusafisha moyo wangu bure na kuiosha mikono yangu katika kutokuwa na hatia,” akawaza Asafu. “Nami nikapata mapigo mchana kutwa.”—Zaburi 73:2, 3, 13, 14.

11 Asafu alishughulikaje na hisia hizo zenye kusumbua? Je, alipuuza hisia hizo? La. Alizitaja katika sala kwa Mungu kama tunavyoona katika Zaburi ya 73. Asafu alibadili kabisa mtazamo wake alipotembelea patakatifu pa hekalu. Akiwa huko, alitambua kwamba kujitoa kwa Mungu ndiyo njia bora zaidi. Baada ya kuthamini tena umuhimu wa kumtumikia Yehova, alifahamu kwamba Yehova anachukia ubaya na kwamba katika wakati wake unaofaa waovu wataadhibiwa. (Zaburi 73:17-19) Baada ya kurekebisha mtazamo wake, Asafu aliimarisha utambulisho wake wa kuwa na pendeleo la kumtumikia Yehova. Alimwambia Mungu hivi: “Niko pamoja nawe daima; umeushika mkono wangu wa kuume. Utaniongoza kwa shauri lako, na baadaye utanipeleka kwenye utukufu.” (Zaburi 73:23, 24) Baadaye, Asafu alijivunia Mungu wake tena.—Zaburi 34:2.

Walitambua Vizuri Wao Ni Nani

12, 13. Toa mifano ya watu wanaotajwa katika Biblia ambao walijivunia uhusiano wao pamoja na Mungu.

12 Njia moja ya kujitambulisha waziwazi kuwa Wakristo ni kuchunguza na kuiga imani ya waabudu washikamanifu, ambao licha ya magumu walijivunia uhusiano wao pamoja na Mungu. Fikiria Yosefu, mwana wa Yakobo. Akiwa mchanga, aliuzwa kwa hila kama mtumwa na kupelekwa Misri, mamia ya kilometa mbali na baba yake mwenye kumwogopa Mungu na mbali sana na watu waliompenda na kumjali. Akiwa Misri, Yosefu hakuwa na mtu wa kumpa shauri la kimungu, naye alilazimika kukabiliana na hali ngumu zilizojaribu maadili yake na tegemeo lake katika Mungu. Hata hivyo, aliazimia kujitambulisha waziwazi kuwa mtumishi wa Mungu, naye akaendelea kuwa mwaminifu katika mambo aliyojua kuwa ya haki. Alijivunia kuwa mwabudu wa Yehova hata katika mazingira yasiyofaa, naye hakusita kuonyesha jinsi alivyohisi.—Mwanzo 39:7-10.

13 Yapata karne nane baadaye, msichana Mwisraeli aliyetekwa ambaye alikuwa mtumwa wa Naamani, mkuu wa jeshi la Siria, hakusahau kujitambulisha kuwa mwabudu wa Yehova. Nafasi ilipotokea, kwa ujasiri alitoa ushahidi mzuri kumhusu Yehova alipomtambulisha Elisha kuwa nabii wa Mungu wa kweli. (2 Wafalme 5:1-19) Miaka mingi baadaye, licha ya kuwa katika mazingira yaliyopotoka, Mfalme Yosia aliyekuwa kijana, alianzisha marekebisho ya kidini ya muda mrefu, akarekebisha hekalu la Mungu, na kurudisha ibada ya Yehova katika taifa hilo. Alijivunia imani na ibada yake. (2 Mambo ya Nyakati sura ya 34, 35) Danieli na Waebrania wenzake watatu huko Babiloni hawakusahau kujitambulisha kuwa watumishi wa Yehova, na hata walidumisha utimilifu wao chini ya mkazo na vishawishi. Ni wazi kwamba walijivunia kuwa watumishi wa Yehova.—Danieli 1:8-20.

Jivunieni Kuwa Wakristo

14, 15. Ni nini kinachotiwa ndani katika kujivunia kuwa Wakristo?

14 Watumishi hao wa Mungu walifanikiwa kwa sababu walijivunia ifaavyo msimamo wao mbele za Mungu. Namna gani sisi leo? Ni nini kinachotiwa ndani katika kujivunia kuwa Wakristo?

15 Kwanza, hii inatia ndani uthamini mwingi wa kuwa mmoja wa watu wanaoitwa kwa jina la Yehova ambao wana baraka na kibali chake. Mungu hana shaka kuhusu walio wake. Mtume Paulo ambaye aliishi katika kipindi kilichokuwa na mvurugo mkubwa wa kidini aliandika hivi: “Yehova anawajua walio wake.” (2 Timotheo 2:19; Hesabu 16:5) Yehova hujivunia “walio wake.” Anasema: “Yeye anayewagusa ninyi anaigusa mboni ya jicho langu.” (Zekaria 2:8) Ni wazi kwamba Yehova anatupenda. Kwa hiyo, uhusiano wetu pamoja naye unapaswa kutegemea upendo mwingi kumwelekea. Paulo alisema: “Ikiwa yeyote anampenda Mungu, huyo anajulikana naye.”—1 Wakorintho 8:3.

16, 17. Kwa nini Wakristo, vijana kwa wazee, hujivunia urithi wao wa kiroho?

16 Vijana ambao wamelelewa wakiwa Mashahidi wa Yehova wanapaswa kuchunguza ikiwa utambulisho wao wa Kikristo unazidi kuwa wenye nguvu kwa sababu ya kuwa na uhusiano wa karibu pamoja na Mungu. Hawawezi kutegemea tu imani ya wazazi wao. Paulo aliandika hivi kuhusu kila mtumishi wa Mungu: “Kwa bwana wake mwenyewe yeye husimama au kuanguka.” Hivyo, Paulo anaendelea kusema: “Kila mmoja wetu atatoa hesabu kwa Mungu kwa ajili yake mwenyewe.” (Waroma 14:4, 12) Ni wazi kwamba, kufuata tu kwa moyo nusu-nusu dini ya wazazi hakuwezi kumsaidia kijana aendelee kuwa na uhusiano wa karibu pamoja na Yehova kwa muda mrefu.

17 Katika historia yote, kumekuwa na mstari wa mashahidi wengi wa Yehova. Ulianza na Abeli mwaminifu—ambaye aliishi yapata miaka 6,000 iliyopita—hadi “umati mkubwa” wa Mashahidi wa kisasa na waabudu wengi wa Yehova watakaoishi milele wakati ujao. (Ufunuo 7:9; Waebrania 11:4) Sisi ndio wa karibuni zaidi katika mstari huo wa waabudu hao wengi walio waaminifu. Tuna urithi wa kiroho ulio mzuri kama nini!

18. Viwango na kanuni zetu hututofautishaje na ulimwengu?

18 Pia utambulisho wetu wa Kikristo unatia ndani kanuni, sifa, na viwango ambavyo hututambulisha kuwa Wakristo. Hiyo ndiyo “Ile Njia,” njia pekee ya maisha yenye mafanikio na ya kumpendeza Mungu. (Matendo 9:2; Waefeso 4:22-24) Wakristo ‘huhakikisha mambo yote’ na ‘kushika sana yaliyo mazuri’! (1 Wathesalonike 5:21) Tunaelewa waziwazi tofauti kubwa iliyopo kati ya Ukristo na ulimwengu uliotenganishwa na Mungu. Yehova anaonyesha waziwazi tofauti iliyopo kati ya ibada ya kweli na ibada ya uwongo. Alisema hivi kupitia nabii wake Malaki: “Mtaona tena tofauti kati ya mwadilifu na mwovu, kati ya mtu anayemtumikia Mungu na mtu ambaye hajamtumikia.”—Malaki 3:18.

19. Wakristo wa kweli hawawezi kamwe kuwa na mtazamo gani?

19 Kwa kuwa kujisifu katika Yehova ni muhimu sana katika ulimwengu huu uliovurugika, ni nini kinachoweza kutusaidia kujivunia ifaavyo Mungu wetu na kujitambulisha waziwazi kuwa Wakristo? Makala inayofuata ina madokezo yanayofaa. Unapofikiria madokezo hayo, unaweza kuwa na uhakika kuhusu jambo hili: Wakristo wa kweli hawawezi kamwe kuwa na ubaridi kuelekea dini.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 7 Hapa tunarejelea tu utambulisho wetu wa kiroho. Kwa wale wachache walio na matatizo fulani ya akili, huenda ikawabidi kumwona daktari.

Je, Unakumbuka?

• Wakristo wanawezaje ‘kujisifu katika Yehova’?

• Umejifunza nini kutokana na kielelezo cha Musa na Asafu?

• Ni watu gani wanaotajwa katika Biblia ambao walijivunia kumtumikia Mungu?

• Ni nini kinachotiwa ndani katika kujivunia kuwa Wakristo?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 14]

Kwa muda fulani, Musa alijitilia shaka

[Picha katika ukurasa wa 15]

Watumishi wengi wa Yehova wa kale walijivunia utambulisho wao wa pekee