Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kupanda Kwenye Kijiji cha Bottom Huko Saba

Kupanda Kwenye Kijiji cha Bottom Huko Saba

Kupanda Kwenye Kijiji cha Bottom Huko Saba

WAKATI mmoja kisiwa cha Saba cha Uholanzi kilitumiwa kama ngome na mabaharia waliosafiri katika Bahari ya Karibea kutafuta nyara. Leo, kisiwa hiki kidogo, kilicho umbali wa kilometa 240 mashariki ya Puerto Riko kina wakaaji 1,600 hivi, na 5 kati yao ni Mashahidi wa Yehova. Hata hivyo, wahudumu hao jasiri wanatafuta kitu fulani chenye thamani zaidi kuliko nyara. Wanatafuta kwa bidii watu ambao wana “mwelekeo unaofaa kwa ajili ya uzima wa milele.”—Matendo 13:48.

Habari njema ya Ufalme wa Mungu ilifika kisiwani humo mara ya kwanza Juni 22, 1952, wakati merikebu iliyoitwa Sibia yenye urefu wa meta 18 ambayo iliendeshwa na Mashahidi wa Yehova ilipotia nanga katika pwani ya Saba. (Mathayo 24:14) Wamishonari Gust Maki na Stanley Carter walipanda Ngazi yenye mawe zaidi ya 500 kuelekea kwenye kijiji cha Bottom, jiji kuu la Saba. * Kwa karne nyingi, njia hiyo nyembamba ndiyo iliyokuwa njia pekee ya kuwafikia wakaaji wa kisiwa hicho.

Ripoti ya kwanza rasmi iliyochapishwa kuhusu kazi ya Kikristo ya kuhubiri huko Saba ilichapishwa katika 1966 Yearbook of Jehovah’s Witnesses. Kulingana na ripoti hiyo, kulikuwa na Shahidi mmoja tu aliyekuwa akihubiri kisiwani humo. Baadaye, familia moja kutoka Kanada ilihubiri habari njema huko miaka kadhaa. Hivi karibuni, Russel na Kathy, wenzi wa ndoa kutoka Marekani ambao wamestaafu, walienda Saba na kuanza kuhubiri huko. Ona yale wanayosimulia.

Kutembelea Saba

Mimi na mke wangu tunawasili kwa ndege tukiwa wageni wa Ronald, ambaye ndiye aliyekuwa Shahidi peke yake katika kisiwa hicho katika miaka ya 1990. Mkaribishaji wetu anatungojea kwenye uwanja wa ndege. Anafurahia zawadi tuliyomletea ya sanduku dogo la mboga kwa kuwa katika kisiwa hicho hakuna biashara ya ukulima wa mboga. Twasafiri polepole kwa lori dogo huku tukipanda Mlima Scenery hadi kilele cha volkeno hiyo ambayo imeacha kulipuka.

Tunasimama katika kijiji cha Hell’s Gate, huku Ronald akiangalia ubao wa matangazo wa umma ili kuona kama mwaliko wa hotuba ya watu wote ya Jumapili ungali katika ubao huo. Tunafurahi kuona bado upo. Anapanda juu ya lori hiyo tena, na tunaendelea na safari yetu ya kupanda hadi kwenye kijiji cha Windwardside ambacho ndicho kikubwa zaidi kisiwani humo. Kama jina lake linavyodokeza, kijiji hicho chenye kuvutia kiko upande wenye upepo wa kisiwa hicho, meta 400 hivi juu ya usawa wa bahari. Tunaposafiri katika barabara inayoelekea kwenye nyumba ya Ron, tunaona ubao maridadi kwenye ukumbi wa nyumba hiyo ambao umeandikwa, Jumba la Ufalme la Mashahidi wa Yehova.

Wakati wa chakula cha mchana, ninauliza swali ambalo limefanya tutembelee kisiwa hicho, “Ilikuwaje hata ukaja kuhubiri kuhusu Ufalme huku Saba?”

“Ujenzi wa ofisi ya tawi ya Mashahidi wa Yehova ya Puerto Riko ulipomalizika mwaka wa 1993,” asema Ron, “mimi na mke wangu tulitaka kuendelea kutumikia katika nchi ya kigeni. Kabla ya hapo, mimi na mke wangu pamoja na ndugu mwingine na mke wake waliokuwa mapainia tulitembelea Saba na kupata habari kwamba kulikuwa na wakaaji 1,400 lakini hakukuwa na Mashahidi. Kwa hiyo tulizungumza na Halmashauri ya Tawi ya Puerto Riko kuhusu kuhamia huko.

“Mipango ilikamilika, na mwishowe tukaruhusiwa kuhamia huko. Kwa kusikitisha, miaka miwili baadaye, mke wangu alikuwa mgonjwa sana, na tukarudi California. Alipokufa, nilirudi Saba. Kwa kawaida, sipendi kuanza jambo na kukosa kulimaliza.”

Kuhubiri Nyumba kwa Nyumba Huko Saba

Sebule ya nyumba ya Ron ambayo imedumu kwa miaka mia moja hutumiwa kama Jumba la Ufalme. * Tunapoendelea kufurahia kiamsha-kinywa na kujitayarisha kwenda kuhubiri, mvua ya rasharasha inafanya kuwe na unyevu jikoni. Baada ya kiamsha-kinywa, tunaondoka kwenda kuhubiri nyumba kwa nyumba katika kisiwa cha Bottom huku mawingu yakiwa yametanda. Kwenye kila nyumba, Ron anamsalimu mwenye nyumba kwa jina. Mazungumzo yetu yanategemea jambo ambalo limetukia hivi karibuni kwenye kisiwa hicho. Watu wengi wanamfahamu Ron na huduma yake, na wengi wanakubali bila kusita vichapo vya Biblia.

Si jambo rahisi kuandika rekodi ya wale wanaopendezwa na ujumbe wa Ufalme ikiwa hufahamiani na wana-kijiji. Kwa nini? Kwa sababu “ni takwa la kisheria kwamba nyumba zote zipakwe rangi moja,” asema Ron. Na kweli, ninapotazama pande zote, ninaona kwamba nyumba zote za Saba ni nyeupe na zina paa nyekundu.

Baada ya kumaliza mazungumzo yetu ya Biblia, tunamwalika mwenye nyumba aje kusikiliza hotuba ya Biblia ya watu wote itakayotolewa Jumapili kwenye Jumba la Ufalme. Ron anapokuwa kisiwani, yeye hutoa hotuba ya watu wote kila juma. Kwa sasa, mafunzo ya Biblia 17 yanaongozwa huko Saba. Watu 20 walihudhuria Ukumbusho wa Kifo cha Kristo mwaka wa 2004. Na ingawa huenda hesabu hiyo ikaonekana kuwa ndogo sana, inawakilisha asimilia 1 ya watu wote wa Saba!

Kwa kweli, Mashahidi wa Yehova wamejitahidi sana kuwapelekea watu wengi iwezekanavyo ujumbe wa Mungu wa wokovu. Iwe ni katika kisiwa kidogo kama vile Saba au katika bara zima, Mashahidi wa Yehova wanatimiza kwa uaminifu kazi ya ‘kufanya wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote.’—Mathayo 28:19.

Kwa kusikitisha, ziara yetu imemalizika. Tunapoingia ndani ya ndege yetu, tunaaga kisiwa hicho. Sikuzote tutakumbuka ziara yetu huko Saba na wakati tuliotumia kupanda kwenye kijiji cha Bottom.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 3 Inaonekana kwamba maharamia walikiita kijiji hicho Bottom kwa sababu walifikiri kwamba kilikuwa sehemu ya chini ya shimo lililosababishwa na volkeno.

^ fu. 12 Katika Septemba 28, 2003, wafanyakazi wa kujitolea kutoka Florida, Marekani, walienda Saba nao wakarekebisha jengo moja lililokuwa karibu ambalo sasa linatumiwa kama Jumba la Ufalme.

[Ramani katika ukurasa wa 10]

(Ona mpangilio kamili katika nakala iliyochapishwa)

PUERTO RIKO

[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 10]

Background: www.sabatourism.com