Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Miujiza Ambayo Wewe Umeona!

Miujiza Ambayo Wewe Umeona!

Miujiza Ambayo Wewe Umeona!

NENO “muujiza” lina maana nyingine. Linamaanisha “tukio, kitu, au utimizo wenye kutokeza sana au usio wa kawaida.” Sote tumeona muujiza wa aina hiyo ambao hutukia pasipo Mungu kuingilia kati.

Kwa sababu ya kuwa na ujuzi zaidi wa sheria za asili, wanadamu wameweza kutimiza mambo ambayo hapo awali yalionwa kuwa hayawezekani. Kwa mfano, huenda mamia ya miaka iliyopita watu wengi wangeona yale ambayo yametimizwa na kompyuta, televisheni, teknolojia ya mambo ya anga, na maendeleo mengine kuwa mambo yasiyowezekana.

Wakitambua kwamba hawana ujuzi kamili wa mambo ya kisayansi yenye kustaajabisha yanayoonekana katika uumbaji wa Mungu, wanasayansi fulani wanakiri kwamba hawawezi kusema kwa uhakika kwamba jambo fulani haliwezi kutukia kamwe. Wanaweza tu kusema kwamba huenda lisitukie. Hivyo, hawapingi uwezekano wa kutokea kwa “miujiza” wakati ujao.

Hata kama tunatumia maana ya msingi ya neno “muujiza,” na hivyo kurejelea mambo “ambayo husababishwa na nguvu zipitazo za kibinadamu,” tunaweza kusema kwamba kila mmoja wetu ameona miujiza. Kwa mfano, tunaona jua, mwezi, na nyota, vitu ambavyo vilitokezwa na “nguvu zipitazo za kibinadamu,” yaani, Muumba mwenyewe. Isitoshe, ni nani anayeweza kueleza kikamili jinsi mwili wa mwanadamu hufanya kazi? jinsi ubongo unavyofanya kazi, au jinsi kijusi cha mwanadamu hukua? Kitabu The Body Machine kinasema: “Mwili wa mwanadamu ambao huongozwa na kuelekezwa na mfumo wa neva, ni mfumo tata wa hisi, mashini inayoweza kujiendesha yenyewe, kompyuta inayoweza kujifanya upya. Huo ni uumbaji wa ajabu sana na usioweza kueleweka kabisa.” Kwa kweli, Mungu aliyeumba “mwili wa mwanadamu” alifanya muujiza ambao bado unatushangaza. Kuna miujiza mingine ambayo wewe umeona ingawa huenda usitambue kuwa ni miujiza.

Je, Kitabu Kinaweza Kuwa Muujiza?

Hakuna kitabu ambacho kimesambazwa kwa wingi kama Biblia. Je, wewe unaiona kuwa muujiza? Je, tunaweza kusema kwamba ilitokezwa na “nguvu zipitazo za kibinadamu”? Ni kweli kwamba Biblia ni kitabu kilichoandikwa na wanadamu, lakini walidai kwamba waliandika mawazo ya Mungu, na si mawazo yao wenyewe. (2 Samweli 23:1, 2; 2 Petro 1:20, 21) Hebu fikiria. Kulikuwa na watu 40 hivi walioishi katika kipindi cha miaka 1,600. Walitoka katika malezi mbalimbali, walikuwa wachungaji, wanajeshi, wavuvi, wafanyakazi wa umma, madaktari, makuhani, na wafalme. Hata hivyo, waliweza kuandika ujumbe unaopatana na wenye tumaini ambao ni sahihi na wa kweli.

Kwa kujifunza Biblia kwa bidii, Mashahidi wa Yehova wameikubali “si kama neno la wanadamu, bali, kama vile lilivyo kwa kweli, kama neno la Mungu,” kama alivyoandika mtume Paulo. (1 Wathesalonike 2:13) Kwa miaka mingi, vichapo vyao vimeonyesha jinsi maandiko yanayoonwa kuwa yanapingana yanavyoweza kupatanishwa na ujumbe wa ujumla wa Biblia. Kupatana huko kunathibitisha kwamba Biblia ilitungwa na Mungu. *

Hakuna kitabu kingine chochote ambacho kimekabili jitihada nyingi za kukiangamiza kama Biblia. Hata hivyo, Biblia bado ipo angalau kwa sehemu katika lugha zaidi ya 2,000. Kuhifadhiwa kwa Biblia yenyewe na pia kuhifadhiwa kwa maandishi yake yakiwa sahihi huthibitisha kwamba Mungu aliingilia kati. Kwa kweli Biblia ni muujiza!

Muujiza Ulio ‘Hai na Wenye Nguvu’

Miujiza ya zamani kama vile uponyaji wa kimuujiza na ufufuo haitukii tena. Lakini tuna sababu ya kuwa na uhakika kwamba katika ulimwengu mpya wa Mungu unaokuja, miujiza kama hiyo itatukia ulimwenguni pote. Italeta kitulizo cha kudumu nayo itatimiza mambo ambayo kwa sasa hatuwezi kuyaelewa.

Hata leo, Biblia, ambayo imetufikia kwa njia ya kimuujiza inaweza kufanya miujiza kwa kuwachochea watu wabadili nyutu zao. (Ona mfano katika sanduku, “Nguvu za Neno la Mungu,” kwenye ukurasa wa 8.) Andiko la Waebrania 4:12 linasema: “Neno la Mungu liko hai nalo lina nguvu na ni lenye makali zaidi kuliko upanga wowote wenye makali kuwili nalo huchoma hata kufikia kugawanya nafsi na roho, na viungo na urojorojo wake, nalo linaweza kutambua fikira na makusudio ya moyo.” Naam, Biblia imechangia sana kubadili maisha ya watu zaidi ya milioni sita wanaoishi ulimwenguni, na kuwapa kusudi maishani na tumaini bora sana la wakati ujao.

Acha Biblia ifanye miujiza maishani mwako.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 8 Ikiwa ungependa kuchunguza jinsi maandiko yanayoonwa kuwa yanapingana yanavyoweza kupatanishwa, kuna mifano mingi inayozungumziwa katika sura ya 7 ya kitabu Biblia—Neno la Mungu au la Binadamu?, kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 7]

JE, ALIKUWA TAYARI AMEKUFA AU BADO ALIKUWA HAI?

Kulingana na Yohana 19:33, 34, Yesu alikuwa tayari amekufa wakati ‘mmoja wa askari-jeshi alipouchoma ubavu wake kwa mkuki, na mara moja damu na maji vikatoka.’ Hata hivyo, andiko la Mathayo 27:49, 50 linaonyesha kwamba Yesu bado alikuwa hai jambo hilo lilipotukia. Kwa nini Maandiko hayo yanatofautiana?

Sheria ya Musa ilisema kwamba mhalifu hakupaswa kuachwa ametundikwa usiku kucha juu ya mti. (Kumbukumbu la Torati 21:22, 23) Hivyo, katika siku za Yesu, ikiwa mhalifu aliyetundikwa mtini bado alikuwa hai kufikia jioni, kulikuwa na desturi ya kuvunja miguu yake ili afe haraka. Hangeweza tena kujiinua wima ili aweze kupumua vizuri. Kwa kuwa askari-jeshi alivunja miguu ya watenda-maovu waliotundikwa mtini kando ya Yesu lakini hakuvunja miguu ya Yesu, hilo linaonyesha kwamba alifikiri kwamba alikuwa amekufa. Inawezekana kwamba askari-jeshi huyo aliuchoma ubavu wake kwa mkuki ili kuondoa shaka yoyote na baadaye kusiwe na dai lolote kwamba alifufuliwa.

Andiko la Mathayo 27:49, 50 linasimulia kwa njia tofauti jinsi matukio yalivyofuatana. Linasema: “Mtu mwingine akachukua mkuki na kumchoma ubavuni, na damu na maji vikatoka. Tena Yesu akapaaza sauti kubwa, akaitoa roho yake.” Hata hivyo, maneno yaliyo katika maandishi ya mlazo hayapatikani katika hati za Biblia za zamani. Waandikaji wengi huamini kwamba maneno hayo ya ziada yalitolewa baadaye katika Injili ya Yohana na kupachikwa mahali pasipofaa. Hivyo, tafsiri nyingi huweka maneno hayo katika mabano, na kutoa maelezo ya chini, au kuiondoa sentensi hiyo kabisa.

Chapa ya maandishi ya Kigiriki ya Agano Jipya ya Westcott na Hort, ambayo ilitumiwa sana kutafsiri New World Translation, huweka sentensi hiyo katika mabano maradufu. Inasema kwamba ‘kuna uwezekano mkubwa sana kwamba sentensi hiyo iliingizwa humo na waandishi.’

Kwa hiyo, uthibitisho huo wote unaonyesha kwamba simulizi la Yohana 19:33, 34 ni la kweli na kwamba Yesu alikuwa tayari amekufa wakati askari-jeshi Mroma alipomchoma kwa mkuki.

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 8]

NGUVU ZA NENO LA MUNGU

Akiwa kijana kutoka familia iliyovunjika, Detlef alianza kutumia dawa za kulevya, pombe, na kusikiliza muziki wa mdundo mzito. * Alishirikiana na magenge ya vijana wahalifu walionyoa upara, na punde si punde, mwenendo wake wa jeuri ulifanya ajikute matatani na polisi.

Mwaka wa 1992, genge la vijana 60 walionyoa upara lilipigana vikali na wahuni 35 hivi wanaopenda muziki wa roki katika mkahawa mmoja wenye baa huko kaskazini-mashariki mwa Ujerumani. Thomas, mmoja wa wahuni hao alipigwa vibaya na akafa kutokana na majeraha aliyopata. Wengi wa viongozi wa vikundi hivyo, kutia ndani Detlef, walifungwa gerezani, baada ya kufanywa kwa kesi iliyoripotiwa sana na vyombo vya habari.

Muda mfupi baada ya Detlef kufunguliwa kutoka gerezani, alipewa broshua fulani na Mashahidi wa Yehova. Broshua hiyo ilikuwa na kichwa, “Kwa Nini Maisha Yamejaa Matatizo Sana?” Mara moja Detlef alitambua ukweli wa yale ambayo broshua hiyo ilisema, na akaanza kujifunza Biblia pamoja na Mashahidi. Funzo hilo lilibadili maisha yake kabisa. Tangu mwaka wa 1996, amekuwa Shahidi wa Yehova mwenye bidii.

Siegfried, aliyekuwa mmoja wa wale wahuni, alikuwa rafiki wa karibu wa Thomas, kijana aliyeuawa. Baadaye Siegfried pia alikuwa Shahidi na sasa ni mzee kutanikoni. Siegfried alipoenda kutoa hotuba ya Biblia katika kutaniko ambalo Detlef anashirikiana nalo (mama ya Thomas pia huhudhuria mikutano huko mara kwa mara), Detlef alimwalika kwa chakula cha mchana. Miaka kumi hivi iliyopita, hawangeweza kudhibiti chuki yao. Leo, upendo wao wa kindugu unaonekana wazi.

Detlef na Siegfried wanatarajia kumkaribisha Thomas atakapofufuliwa katika dunia paradiso. Detlef anasema hivi: “Ninapofikiria jambo hilo, mimi hutokwa na machozi. Nasikitika sana kwa yale niliyofanya.” Tamaa yao kubwa ni kumsaidia Thomas wakati huo, kama wanavyowasaidia wengine leo, kumjua Yehova na kufurahia tumaini ambalo Biblia hutoa.

Naam, Neno la Mungu lina nguvu sana.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 25 Majina yamebadilishwa.

[Picha katika ukurasa wa 6]

Mwili wa mwanadamu ni uumbaji wa ajabu sana

[Hisani]

Anatomy Improved and Illustrated, London, 1723, Bernardino Genga