Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Mambo Makuu Katika Kitabu cha Ruthu

Mambo Makuu Katika Kitabu cha Ruthu

Neno la Yehova Liko Hai

Mambo Makuu Katika Kitabu cha Ruthu

NI TUKIO halisi lenye kuvutia la ushikamanifu kati ya wanawake wawili. Ni simulizi linaloonyesha uthamini kwa Yehova Mungu na kutumaini mipango yake. Ni hadithi inayokazia hangaiko kubwa la Yehova kuhusu watu waliokuwa katika ukoo wa Masihi. Ni simulizi linalogusa moyo kuhusu shangwe na huzuni ya familia fulani. Kitabu cha Ruthu kinatia ndani mambo hayo yote na mengine zaidi.

Kitabu cha Ruthu kinataja mambo yaliyotukia katika kipindi cha karibu miaka 11, “siku ambazo waamuzi walitekeleza haki” katika Israeli. (Ruthu 1:1) Mambo yanayotajwa katika kitabu hicho lazima yawe yalitukia mapema katika kipindi cha Waamuzi, kwa sababu Boazi mmiliki wa shamba, ambaye ni mmoja wa watu wanaotajwa katika tukio hilo halisi, alikuwa mwana wa Rahabu aliyeishi siku za Yoshua. (Yoshua 2:1, 2; Ruthu 2:1; Mathayo 1:5) Yaelekea simulizi hilo liliandikwa na nabii Samweli mwaka wa 1090 K.W.K. Hiki ndicho kitabu peke yake katika Biblia ambacho kina jina la mwanamke asiye Mwisraeli. Ujumbe ulio katika kitabu hiki ni ‘hai nao ni wenye nguvu.’—Waebrania 4:12.

“UENDAKO NITAENDA”

(Ruthu 1:1–2:23)

Naomi na Ruthu wanapofika Bethlehemu, kila mtu anataka kujua wao ni nani. Wakirejelea yule mwanamke mwenye umri mkubwa zaidi, wanawake wa mjini wanauliza: “Je, huyu ni Naomi?” Naye Naomi anawajibu: “Msiniite Naomi. Niiteni Mara, kwa maana Mweza-Yote amenifanya kuwa na uchungu sana. Nilikuwa nimejaa nilipoenda, naye Yehova amenifanya nirudi mikono mitupu.”—Ruthu 1:19-21.

Wakati njaa inapotokea Israeli na kulazimisha familia yake ihame kutoka Bethlehemu hadi nchi ya Moabu, Naomi ‘amejaa’ katika maana ya kwamba ana mume na wana wawili. Hata hivyo, baada ya kuishi Moabu kwa muda fulani, Elimeleki, mume wake afa. Baadaye, wana hao wawili wanaoa wanawake Wamoabu, Orpa na Ruthu. Miaka kumi hivi inapita, na wana hao wawili wanakufa bila kupata watoto na kuwaacha wanawake hao watatu peke yao. Naomi, mama-mkwe wao anapoamua kurudi Yuda, wajane wa wana wake wanaambatana naye. Wakiwa njiani, Naomi anawasihi binti-wakwe zake warudi Moabu na kutafuta waume miongoni mwa watu wao. Orpa anakubali. Hata hivyo, Ruthu anashikamana na Naomi na kusema: “Uendako nitaenda, na mahali utakapokaa usiku kucha nitakaa. Watu wako watakuwa watu wangu, na Mungu wako Mungu wangu.”—Ruthu 1:16.

Wajane hao wawili, Naomi na Ruthu wanafika Bethlehemu mwanzoni mwa mavuno ya shayiri. Kwa kutumia maandalizi yaliyokuwa katika Sheria ya Mungu, Ruthu anaanza kuokota masalio katika shamba la mtu wa ukoo wa Elimeleki—Myahudi mzee anayeitwa Boazi. Ruthu anapata kibali cha Boazi na anaendelea kuokota masalio katika shamba lake “mpaka mavuno ya shayiri na mavuno ya ngano” yanapokwisha.—Ruthu 2:23.

Maswali ya Kimaandiko Yajibiwa:

1:8—Kwa nini Naomi aliwaambia binti-wakwe zake warudi “kila mmoja nyumbani kwa mama yake” badala ya nyumbani kwa baba yake? Hatuelezwi iwapo baba ya Orpa alikuwa hai wakati huo. Lakini baba ya Ruthu alikuwa hai. (Ruthu 2:11) Hata hivyo, Naomi alitaja nyumba ya mama, labda akifikiri kwamba kutajwa kwa mama zao kungewakumbusha faraja inayotokana na upendo wa mama. Jambo hilo lingewafariji hasa binti ambao wamelemewa na huzuni ya kumwacha mama-mkwe wao mpendwa. Huenda pia maneno hayo yakaonyesha kwamba tofauti na Naomi, mama ya Ruthu na ya Orpa walikuwa na familia imara.

1:13, 21—Je, Yehova alifanya maisha ya Naomi yawe machungu na kumsababishia msiba? La, na Naomi hakumlaumu Mungu kwa kosa lolote. Hata hivyo, kwa sababu ya mambo yote yaliyompata, alifikiri kwamba hakuwa na kibali cha Yehova. Alivunjika moyo na kuhisi uchungu. Isitoshe, siku hizo kuzaa kulionwa kuwa baraka kutoka kwa Mungu na kuwa tasa kulionwa kuwa laana. Kwa kuwa Naomi hakuwa na wajukuu na wana wake wawili walikuwa wamekufa, huenda alihisi kwamba alikuwa na sababu nzuri ya kufikiri kuwa Yehova alimfedhehesha.

2:12—Ruthu alipata ‘malipo gani kamili’ kutoka kwa Yehova? Ruthu alizaa mwana na akapata pendeleo la kuwa mmoja wa watu wa ukoo muhimu zaidi katika historia, yaani, ukoo wa Yesu Kristo.—Ruthu 4:13-17; Mathayo 1:5, 16.

Mambo Tunayojifunza:

1:8; 2:20. Licha ya misiba iliyompata, Naomi aliendelea kutumaini fadhili zenye upendo za Yehova. Tunapaswa kufanya kama yeye, hasa tunapokabili majaribu makali.

1:9. Nyumba haipaswi tu kuwa mahali ambapo washiriki wa familia hula na kulala. Inapaswa kuwa mahali penye amani pa kupumzika na kustarehe.

1:14-16. Orpa ‘alirudi kwa watu wake na kwa miungu yake.’ Ruthu hakufanya hivyo. Aliacha starehe na usalama katika nchi ya kwao na kuendelea kuwa mshikamanifu kwa Yehova. Kusitawisha upendo mshikamanifu kwa Mungu na kudhihirisha roho ya kujidhabihu kutatulinda tusifuatilie tamaa za kibinafsi na ‘kurudi nyuma kwenye maangamizi.’—Waebrania 10:39.

2:2. Ruthu alitaka kutumia maandalizi ya kuokota masalio yaliyokuwako kwa ajili ya wageni na wenye kuteseka. Alikuwa mtu mnyenyekevu. Mkristo mwenye uhitaji hapaswi kuwa na kiburi sana hivi kwamba akatae msaada wa upendo kutoka kwa waamini wenzake au msaada anaostahili kupewa na serikali.

2:7. Licha ya kuwa na haki ya kuokota masalio, Ruthu aliomba ruhusa kabla ya kufanya hivyo. (Mambo ya Walawi 19:9, 10) Hiyo ilikuwa ishara ya upole. Tunakuwa wenye hekima ‘tukitafuta upole’ kwa sababu “wapole wataimiliki dunia, nao watapata furaha yao tele katika wingi wa amani.”—Sefania 2:3; Zaburi 37:11.

2:11. Ruthu hakuwa tu mtu wa ukoo wa Naomi. Alikuwa rafiki wa kweli. (Methali 17:17) Urafiki wao ulikuwa imara kwa sababu ulitegemea sifa kama vile upendo, ushikamanifu, hisia-mwenzi, fadhili, na roho ya kujidhabihu. Jambo muhimu zaidi ni kwamba ulitegemea hali yao ya kiroho, yaani, tamaa yao ya kumtumikia Yehova na kuwa miongoni mwa waabudu wake. Sisi pia tuna nafasi nzuri za kuanzisha urafiki wa kweli na waabudu wa kweli.

2:15-17. Hata baada ya Boazi kufanya kazi ya Ruthu iwe rahisi, ‘aliokota masalio shambani mpaka jioni.’ Ruthu alikuwa mfanyakazi mwenye bidii. Mkristo anapaswa kujulikana kuwa mfanyakazi mwenye bidii.

2:19-22. Naomi na Ruthu walifurahia mazungumzo mazuri jioni, huku Naomi akipendezwa na shughuli za Ruthu, wote wakieleza waziwazi mawazo na hisia zao. Ndivyo familia ya Kikristo inavyopaswa kufanya.

2:22, 23. Tofauti na Dina, binti ya Yakobo, Ruthu alishirikiana na waabudu wa Yehova. Anatuwekea kielelezo kizuri sana.—Mwanzo 34:1, 2; 1 Wakorintho 15:33.

NAOMI ‘AJAA’

(Ruthu 3:1–4:22)

Naomi amezeeka sana hivi kwamba hawezi kupata watoto. Kwa hiyo, anamwagiza Ruthu apate mtoto kwa niaba yake katika ndoa ya ukombozi, au ya ndugu-mkwe. Kwa kufuata mwongozo wa Naomi, Ruthu anamwomba Boazi awe mkombozi. Boazi yuko tayari kufanya hivyo. Hata hivyo, kuna mtu wa ukoo wa karibu ambaye anapaswa kupewa nafasi hiyo kwanza.

Boazi anatatua jambo hilo mara moja. Asubuhi inayofuata, anawakusanya wanaume wazee kumi wa Bethlehemu mbele ya mtu huyo wa ukoo na kumwuliza kama anakubali kuwa mkombozi. Mtu huyo anakataa. Kwa hiyo, Boazi anakuwa mkombozi na kumwoa Ruthu. Wanamzaa Obedi, babu ya Mfalme Daudi. Sasa wanawake wa Bethlehemu wanamwambia Naomi hivi: ‘Abarikiwe Yehova. Amekurudishia nafsi yako na kukutunza katika uzee wako, kwa sababu binti-mkwe wako anayekupenda, ambaye ni bora kwako kuliko wana saba, amemzaa huyo.’ (Ruthu 4:14, 15) Yule mwanamke ambaye alirudi “mikono mitupu” hadi Bethlehemu sasa ‘amejaa’ tena!—Ruthu 1:21.

Maswali ya Kimaandiko Yajibiwa:

3:11—Ni nini kilichofanya Ruthu ajulikane kuwa “mwanamke bora sana”? Watu wengine hawakuvutiwa na Ruthu kwa sababu ya “kusuka nywele kwa nje” au “kujivika mapambo ya dhahabu au kuvaa mavazi ya nje.” Badala yake, walivutiwa na “yule mtu wa siri wa moyoni,” yaani, ushikamanifu na upendo wake, unyenyekevu na upole wake, bidii na roho yake ya kujidhabihu. Mwanamke yeyote anayemwogopa Mungu ambaye anataka kuwa kama Ruthu anapaswa kujitahidi kusitawisha sifa hizo.—1 Petro 3:3, 4; Methali 31:28-31.

3:14—Kwa nini Ruthu na Boazi waliamka kabla hakujapambazuka? Si kwa sababu walikuwa wamefanya jambo fulani lisilo la adili usiku na kutaka kulificha. Yaonekana mambo ambayo Ruthu alifanya usiku huo yalipatana na mambo ambayo kwa kawaida yalifanywa na mwanamke aliyekuwa akitafuta haki ya ndoa ya ndugu-mkwe. Alitenda kulingana na maagizo ya Naomi. Isitoshe, jibu la Boazi linaonyesha wazi kwamba hakuona ubaya wowote katika mambo ambayo Ruthu alifanya. (Ruthu 3:2-13) Yaonekana, Ruthu na Boazi waliamka mapema ili mtu yeyote asiwe na sababu ya kuanzisha uvumi usio na msingi.

3:15—Ni nini kilichomaanishwa na Boazi kumpa Ruthu vipimo sita vya shayiri? Huenda tendo hilo lilionyesha kwamba kama vile kulivyokuwa na siku ya kupumzika baada ya siku sita za kufanya kazi, siku ya Ruthu ya kupumzika ilikuwa imekaribia. Boazi angehakikisha kwamba Ruthu angekuwa na “mahali pa kupumzika” katika nyumba ya mume wake. (Ruthu 1:9; 3:1) Pia huenda ikawa Ruthu angeweza tu kubeba vipimo sita vya shayiri kichwani.

3:16—Kwa nini Naomi alimwuliza Ruthu: “Wewe ni nani, binti yangu?” Je, hakumtambua binti-mkwe wake? Yawezekana kwamba hakumtambua, kwa kuwa wakati Ruthu aliporudi kwa Naomi, huenda bado kulikuwa na giza. Hata hivyo, huenda pia swali hilo likamaanisha kwamba Naomi alitaka kujua ikiwa Ruthu alikuwa sasa mwanamke “mpya,” na ikiwa mkombozi wake alikuwa amekubali kumwoa.

4:6—Mkombozi angewezaje ‘kuharibu’ urithi wake anapokomboa? Kwanza, ikiwa mtu aliyejikuta katika umaskini angeuza shamba lake la urithi, ingembidi mkombozi anunue shamba hilo kwa bei ambayo ingetegemea miaka iliyobaki hadi Yubile ambayo ingefuata. (Mambo ya Walawi 25:25-27) Kufanya hivyo kungepunguza thamani ya shamba lake. Isitoshe, kama Ruthu angezaa mwana, mwana huyo ndiye angerithi shamba hilo lililonunuliwa bali si mtu yeyote wa ukoo wa karibu na mkombozi.

Mambo Tunayojifunza:

3:12; 4:1-6. Boazi alifuata mpango wa Yehova kwa makini sana. Je, sisi hufuata utaratibu wa kitheokrasi kwa makini?—1 Wakorintho 14:40.

3:18. Naomi alimtumaini Boazi. Je, sisi pia hatupaswi kuwatumaini waamini wenzetu? Ruthu alikuwa tayari kufunga ndoa ya ndugu-mkwe na mtu asiyemjua hata kidogo, mtu ambaye hatajwi kwa jina katika Biblia. (Ruthu 4:1) Kwa nini? Kwa sababu alitumaini mipango ya Mungu. Je, sisi pia tuna tumaini kama hilo? Kwa mfano, tunapotafuta mwenzi wa ndoa, je, tunatii shauri la kufunga ndoa “katika Bwana tu”?—1 Wakorintho 7:39.

4:13-16. Ingawa Ruthu alikuwa Mmoabu naye aliabudu mungu Kemoshi hapo awali, alipata pendeleo kubwa sana. Hilo huonyesha ile kanuni ya kwamba “haitegemei yule anayetaka wala yule anayekimbia, bali hutegemea Mungu, aliye na rehema.”—Waroma 9:16.

Mungu, “Awainue Ninyi Katika Wakati Unaofaa”

Kitabu cha Ruthu kinaonyesha Yehova kuwa Mungu mwenye fadhili zenye upendo, ambaye hutenda kwa niaba ya watumishi wake washikamanifu. (2 Mambo ya Nyakati 16:9) Tunapotafakari kuhusu jinsi ambavyo Ruthu alibarikiwa, tunaona umuhimu wa kumtumaini Mungu tukiwa na imani kamili, huku tukiamini kabisa “kwamba yeye yuko na kwamba yeye huwa mthawabishaji wa wale wanaomtafuta kwa bidii.”—Waebrania 11:6.

Ruthu, Naomi, na Boazi walitumaini kabisa mpango wa Yehova, nao wakapata matokeo mazuri. Vivyo hivyo, “Mungu hufanya kazi zake zote zishirikiane pamoja kwa ajili ya mema ya wale wanaompenda Mungu, wale ambao wameitwa kulingana na kusudi lake.” (Waroma 8:28) Basi acheni tutii shauri hili la mtume Petro: “Kwa hiyo, jinyenyekezeni chini ya mkono wenye nguvu wa Mungu, ili awainue ninyi katika wakati unaofaa; huku mkitupa mahangaiko yenu yote juu yake, kwa sababu yeye anawajali ninyi.”—1 Petro 5:6, 7.

[Picha katika ukurasa wa 26]

Je, unajua ni kwa nini Ruthu hakumwacha Naomi?

[Picha katika ukurasa wa 27]

Ni nini kilichofanya Ruthu ajulikane kuwa “mwanamke bora sana”?

[Picha katika ukurasa wa 28]

Ruthu alipata ‘malipo gani kamili’ kutoka kwa Yehova?