Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Manufaa ya Kufanya Amani

Manufaa ya Kufanya Amani

Manufaa ya Kufanya Amani

ED ALIKUWA anakaribia kufa, naye Bill alimchukia. Miaka 20 kabla ya hapo, Ed alifanya uamuzi ambao ulifanya Bill apoteze kazi yake, na hilo likawatenganisha wanaume hao ambao hapo zamani walikuwa marafiki wa karibu. Sasa Ed alijaribu kuomba msamaha ili afe kwa amani. Hata hivyo, Bill alikataa kumsikiliza.

Karibu miaka 30 baadaye Bill alipokaribia kufa, alieleza kwa nini hakumsamehe Ed. “Ed hakupaswa kufanya yale aliyomfanyia rafiki yake mkubwa. Sikutaka kufanya mapatano baada ya miaka 20. . . . Huenda nilikosea, lakini hivyo ndivyo nilivyohisi.” *

Kwa kawaida, tofauti za kibinafsi haziwi na matokeo yenye kusikitisha kama hayo, lakini mara nyingi huacha watu wakihisi kuwa wameumia au wenye uchungu. Hebu fikiria mtu fulani anayehisi kama alivyohisi Ed. Baada ya kutambua kwamba uamuzi wake ulisababisha madhara, huenda mtu huyo akasumbuliwa na dhamiri na kuhisi kwamba amempoteza rafiki mzuri. Hata hivyo, yeye huhisi ameumia anapofikiria jinsi rafiki yake aliyekosewa alivyovunja urafiki wao kana kwamba haukuwa na thamani yoyote.

Hata hivyo, mtu aliye na maoni kama ya Bill, hujiona kuwa asiye na hatia naye huenda akawa mwenye uchungu na kinyongo. Kwa maoni yake, rafiki yake wa zamani hakupaswa kutenda jinsi alivyotenda na huenda alimtia uchungu kimakusudi. Mara nyingi, watu wawili wanapokosa kuelewana, kila mmoja huwa na uhakika kwamba hajakosea na kwamba yule mwingine ndiye anayepaswa kulaumiwa. Hivyo, marafiki wawili wa zamani wanajikuta wakipigana vita.

Wanaendelea kupigana vita kwa kunyamaziana, yaani, mmoja hufuata njia nyingine anapokutana na mwenzake, nao hawazungumziani wanapokutana katika kikundi. Kwa mbali, wanatazamana kichini-chini au kuangaliana kwa uadui na chuki. Wanapozungumziana, wao hufanya hivyo kwa ukali au kwa kutupiana matusi ambayo hukata kama kisu.

Hata hivyo, ingawa wanapingana kabisa, yaelekea wanakubaliana katika mambo fulani. Huenda wakatambua kwamba wana matatizo mazito na kwamba inasikitisha kuvunja uhusiano na rafiki wa karibu. Yaelekea kila mmoja wao anahisi uchungu wa kidonda kilichotunga usaha, na wote wanajua kwamba wanapaswa kufanya jambo fulani ili kukiponya. Lakini ni nani atakayechukua hatua ya kwanza kurekebisha uhusiano huo ulioharibika na kufanya amani? Hakuna mmoja aliye tayari kufanya hivyo.

Miaka 2,000 iliyopita, mitume wa Yesu Kristo nyakati nyingine walijikuta katika mabishano yenye hasira. (Marko 10:35-41; Luka 9:46; 22:24) Baada ya mojawapo ya mabishano yao makali, Yesu aliwauliza hivi: “Mlikuwa mkibishania nini barabarani?” Huku wakinyamaza kwa aibu, hakuna yeyote aliyejibu. (Marko 9:33, 34) Mafundisho ya Yesu yaliwasaidia kusuluhisha tofauti zao. Mashauri yake, na yale ya baadhi ya wanafunzi wake, yanaendelea kuwasaidia watu kusuluhisha ugomvi na kurekebisha urafiki uliovunjika. Na tuone jinsi mashauri hayo yanavyowasaidia watu.

Jitahidi Kufanya Amani

“Sitaki kuzungumza na mtu huyo. Sitaki kumwona tena.” Ikiwa umesema maneno kama hayo kuhusu mtu fulani, unahitaji kufanya jambo fulani kama maandiko ya Biblia yafuatayo yanavyoonyesha.

Yesu alifundisha hivi: “Basi, ikiwa unaleta zawadi yako kwenye madhabahu na hapo ukumbuke kwamba ndugu yako ana jambo fulani juu yako, acha zawadi yako hapo mbele ya madhabahu, na uende zako; kwanza fanya amani yako pamoja na ndugu yako.” (Mathayo 5:23, 24) Pia alisema: “Ndugu yako akitenda dhambi, nenda ufunue kosa lake kati yako na yeye peke yake.” (Mathayo 18:15) Iwe umemkosea mtu mwingine au ni wewe uliyekosewa, maneno ya Yesu yanakazia uhitaji wa wewe kuzungumza haraka na yule mtu mwingine. Unapaswa kufanya hivyo “katika roho ya upole.” (Wagalatia 6:1) Kusudi la mazungumzo hayo si kujaribu kudumisha heshima yako kwa kujitetea au kumlazimisha mpinzani wako aombe msamaha, lakini ni kufanya amani. Je, shauri hilo la Biblia lina matokeo?

Ernest ni msimamizi katika ofisi moja kubwa. * Kwa miaka mingi, akiwa kazini imembidi ashughulikie mambo mazito yanayohusu watu wa aina zote na kudumisha uhusiano mzuri wa kikazi pamoja nao. Ameona jinsi kutoelewana kunavyoweza kutokea kwa urahisi. Anasema hivi: “Nyakati nyingine, nimekuwa na matatizo na watu wengine. Lakini hilo linapotukia, ninaketi na mtu huyo na kuzungumzia tatizo hilo. Nenda ukawaone moja kwa moja. Wakabili ukiwa na kusudi la kufanya amani. Kufanya hivyo huwa na matokeo sikuzote.”

Alicia ana marafiki kutoka tamaduni nyingi mbalimbali, naye anasema hivi: “Nyakati fulani ninasema jambo, na baadaye ninahisi kwamba huenda nimemkosea mtu fulani. Mimi huenda kumwomba mtu huyo msamaha. Huenda ikawa ninaomba msamaha mara nyingi zaidi kuliko ninavyostahili kwa sababu hata ikiwa sikumkosea mtu huyo, ninahisi vizuri zaidi kwamba nimeomba msamaha. Hivyo ninajua kwamba hakuna kutoelewana kokote.”

Kushinda Vizuizi

Hata hivyo, mara nyingi jitihada za kutafuta amani kunapokuwa na ugomvi hukatizwa na vizuizi. Je, umewahi kusema: “Kwa nini niwe wa kwanza kufanya amani? Ni yeye aliyesababisha tatizo hilo.” Au je, umewahi kwenda kumwona mtu fulani ili kutatua tatizo fulani na kumsikia akisema: “Sina jambo lolote la kuzungumza nawe”? Watu wengine huitikia hivyo kwa sababu wamewahi kupatwa na mfadhaiko wa kihisia-moyo. Methali 18:19 inasema hivi: “Ndugu aliyekosewa ni mgumu kuliko mji wenye nguvu; na kuna magomvi yaliyo kama pingo la mnara wa makao.” Kwa hiyo, fikiria hisia za yule mwingine. Ikiwa anakataa kufanya amani, basi ngoja muda mfupi upite kisha jaribu tena. Huenda wakati huo “mji wenye nguvu” ukafunguliwa na huenda “pingo” ikaondolewa mlangoni na hivyo kufanya mapatano.

Huenda kizuizi kingine cha kufanya amani kikawa woga wa mtu kupoteza heshima yake. Watu wengine huona kwamba ni aibu kuomba msamaha au hata kuzungumza na adui. Ni jambo linalofaa kujiheshimu, lakini je, kukataa kufanya amani huzidisha au hupunguza heshima ya mtu? Je, inawezekana kwamba hangaiko letu la kujiheshimu linasababishwa na kiburi?

Mwandikaji wa Biblia, Yakobo, anaonyesha kwamba kuna uhusiano kati ya roho ya ugomvi na kiburi. Baada ya kueleza kuhusu “vita” na “mapigano” ambayo Wakristo fulani hufanya kati yao, anaendelea kusema hivi: “Mungu huwapinga wenye majivuno, lakini huwapa wanyenyekevu fadhili zisizostahiliwa.” (Yakobo 4:1-3, 6) Majivuno, au kiburi huzuiaje watu kufanya amani?

Kiburi huwadanganya watu, na kuwafanya waamini kwamba wao ni bora zaidi kuliko wengine. Watu wenye majivuno huhisi kwamba wana mamlaka ya kuhukumu maadili ya wengine. Katika njia gani? Kutoelewana kunapotokea, mara nyingi wao huwaona wapinzani wao kuwa watu wasioweza kubadilika. Kiburi huwafanya watu fulani wawahukumu wale walio na maoni tofauti na yao kuwa watu wanaostahili kupuuzwa na hata wasiopaswa kuombwa msamaha wa kweli. Hivyo, mara nyingi wale wanaochochewa na kiburi huruhusu ugomvi kuendelea badala ya kuusuluhisha kwa njia ifaayo.

Kama vile kizuizi huzuia magari katika barabara kuu, mara nyingi kiburi huzuia watu wasichukue hatua za kufanya amani. Kwa hiyo, ikiwa wewe unakataa jitihada za mtu mwingine za kufanya amani, huenda unasumbuliwa na kiburi. Unawezaje kushinda kiburi? Kwa kukuza sifa iliyo kinyume cha kiburi, yaani, unyenyekevu.

Tenda Kinyume cha Kiburi

Biblia hutuhimiza tuwe na unyenyekevu. “Matokeo ya unyenyekevu na kumwogopa Yehova ni utajiri na utukufu na uzima.” (Methali 22:4) Kwenye Zaburi 138:6, tunasoma juu ya maoni ya Mungu kuhusu watu wanyenyekevu na wale wenye kiburi: “Yehova yuko juu, hata hivyo yeye humwona mnyenyekevu; lakini yeye anamjua mwenye kiburi kutoka mbali tu.”

Watu wengi huhusianisha unyenyekevu na aibu. Inaonekana viongozi wa ulimwengu wana maoni hayo. Ingawa mataifa mazima hujitiisha chini ya viongozi wa kisiasa, viongozi hao hawana ujasiri wa kukubali kwa unyenyekevu makosa yao. Ni jambo linalostahili kuripotiwa kumsikia kiongozi fulani akisema “naomba msamaha.” Hivi karibuni, wakati mtu mmoja aliyekuwa ofisa wa serikali alipoomba msamaha kwa kukosa kuzuia msiba uliosababisha vifo vya watu wengi, maneno yake yalipewa umuhimu katika vyombo vya habari.

Unyenyekevu ni sifa ya kuwa mnyenyekevu au kujiona kuwa mtu wa hali ya chini. Ni kinyume cha kiburi au majivuno. Kwa hiyo, kuwa mnyenyekevu kunaonyesha maoni ambayo mtu anayo kujihusu mwenyewe, na si maoni ambayo wengine wanayo kumhusu. Kukubali makosa kwa unyenyekevu na kuomba msamaha kwa unyoofu hakumwaibishi mtu; badala yake, kunaboresha sifa yake. Biblia inasema hivi: “Kabla ya kuanguka moyo wa mwanadamu huwa na kiburi, na kabla ya utukufu kuna unyenyekevu.”—Methali 18:12.

Kuhusu wanasiasa ambao hawaombi msamaha kwa sababu ya makosa yao, mchunguzi mmoja alisema hivi: “Kwa kusikitisha, yaelekea wao hufikiri kwamba kukubali makosa ni dalili ya udhaifu. Ni mara chache sana watu dhaifu na wasio imara husema, ‘Samahani.’ Watu jasiri na wenye moyo mkunjufu ndio huona kwamba si kujishushia heshima kusema, ‘Nimekosea.’” Hiyo ni kweli pia hata ikiwa wewe si mwanasiasa. Ukijitahidi kuwa mnyenyekevu badala ya kuwa na kiburi, itakuwa rahisi zaidi kwako kufanya amani ugomvi unapotokea. Ona jinsi familia moja ilivyoona ukweli wa jambo hilo.

Kutoelewana kulisababisha mvutano kati ya Julie na ndugu yake William. William aliwakasirikia sana Julie na mume wake, Joseph, naye akaacha kabisa kuwasiliana nao. Hata alirudisha zawadi zote ambazo Julie na Joseph walimpa miaka mingi iliyopita. Kadiri miezi ilivyopita, kinyongo kiliwatenganisha William na dada yake Julie, ambao hapo mwanzoni walikuwa na uhusiano wa karibu.

Hata hivyo, Joseph, aliazimia kutumia shauri la Mathayo 5:23, 24. Alijaribu kumfikia shemeji yake katika roho ya upole na kumtumia barua za kuomba msamaha kwa kumkosea. Joseph alimtia moyo mke wake amsamehe ndugu yake. Baadaye, William aliona kwamba Julie na Joseph kwa kweli walitaka kufanya amani, naye akalegeza mtazamo wake. William na mke wake walikutana na Julie na Joseph; wote waliombana msamaha, wakakumbatiana, nao wakawa marafiki tena.

Ikiwa unatamani kusuluhisha ugomvi pamoja na mtu fulani, tumia kwa subira mafundisho ya Biblia na jitahidi kufanya amani pamoja na mtu huyo. Yehova atakusaidia. Yale ambayo Mungu aliliambia taifa la Israeli la kale yatatimia kwako: “Laiti ungesikiliza amri zangu! Ndipo amani yako ingekuwa kama mto.”—Isaya 48:18.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 3 Habari hiyo inategemea kichapo The Murrow Boys—Pioneers on the Front Lines of Broadcast Journalism, kilichoandikwa na Stanley Cloud na Lynne Olson.

^ fu. 12 Majina fulani yamebadilishwa.

[Picha katika ukurasa wa 7]

Mara nyingi kuomba msamaha kunarudisha tena uhusiano wenye amani