Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Mikaeli Yule Malaika Mkuu Ni Nani?

Mikaeli Yule Malaika Mkuu Ni Nani?

Mikaeli Yule Malaika Mkuu Ni Nani?

GABRIELI na Mikaeli ndio malaika pekee watakatifu wanaotajwa kwa jina katika Biblia, na Mikaeli tu ndiye anayeitwa “malaika mkuu.” (Yuda 9) Jina hilo linatajwa mara ya kwanza katika sura ya kumi ya Danieli, ambako Mikaeli anatajwa kuwa “mmoja wa hao wakuu wa mbele”; alikuja kumsaidia malaika mdogo ambaye alipingwa na “mkuu wa ufalme wa Uajemi.” Mikaeli aliitwa ‘mkuu wa watu wa Danieli,’ “yule mkuu anayesimama kwa ajili ya wana wa watu [wa Danieli].” (Danieli 10:13, 20, 21; 12:1) Hilo linaonyesha kwamba Mikaeli ndiye malaika aliyewaongoza wana wa Israeli nyikani. (Kutoka 23:20, 21, 23; 32:34; 33:2) Jambo linalounga mkono kauli hiyo ni kwamba ‘Mikaeli, yule malaika mkuu alikuwa na tofauti na Ibilisi na kubishana naye juu ya mwili wa Musa.’—Yuda 9.

Uthibitisho wa Kimaandiko unaonyesha kwamba Mwana wa Mungu aliitwa Mikaeli kabla hajaondoka mbinguni ili awe Yesu Kristo na pia baada ya kurudi huko. Mikaeli tu ndiye anayetajwa kuwa “malaika mkuu.” Neno hilo hupatikana kwenye Biblia katika umoja tu. Yaelekea hilo linaonyesha kwamba Mungu amemchagua malaika mmoja tu kuwa mkuu, au kichwa cha jeshi la malaika. Kwenye 1 Wathesalonike 4:16 sauti ya Bwana Yesu Kristo aliyefufuliwa inafafanuliwa kuwa ile ya malaika mkuu, jambo linaloonyesha kwamba kwa kweli yeye ndiye malaika mkuu. Katika andiko hilo, anaonyeshwa akishuka kutoka mbinguni akiwa na “mwito wenye amri.” Kwa hiyo, ni jambo linalopatana na akili kwamba sauti inayotoa mwito huo wenye amri ifafanuliwe kwa neno ambalo halitapunguza mamlaka kuu ambayo Kristo Yesu anayo sasa akiwa Mfalme wa wafalme na Bwana wa mabwana. (Mathayo 28:18; Ufunuo 17:14) Ikiwa jina “malaika mkuu” halingemhusu Yesu Kristo bali malaika wale wengine, basi maneno “sauti ya malaika mkuu” hayangefaa. Ikiwa ndivyo, basi jina hilo lingekuwa linafafanua sauti ya mtu mwenye mamlaka ya chini zaidi kuliko yale ya Mwana wa Mungu.

Pia kuna habari nyingine zinazolingana na hizo ambazo huthibitisha kwamba kwa kweli Mikaeli ni Mwana wa Mungu. Baada ya Danieli kumtaja Mikaeli mara ya kwanza, aliandika unabii ambao ungehusu “wakati wa mwisho” kisha akasema: “Na Mikaeli atasimama wakati huo, yule mkuu anayesimama kwa ajili ya wana wa watu [wa Danieli].” ‘Kusimama’ kwa Mikaeli kungehusianishwa na “wakati wa taabu ambayo haijapata kutokea tangu kuwapo kwa taifa lolote mpaka wakati huo.” (Danieli 11:40; 12:1) Katika unabii wa Danieli, mara nyingi, ‘kusimama’ hurejelea tendo la mfalme, ama akichukua mamlaka yake ya kifalme au akitenda katika cheo chake akiwa mfalme. (Danieli 11:2-4, 7, 16b, 20, 21) Jambo hilo linaunga mkono mkataa wa kwamba Mikaeli ni Yesu Kristo, kwa kuwa Yesu ndiye Mfalme aliyewekwa rasmi na Yehova, na kupewa kazi ya kuharibu mataifa yote kwenye Har–Magedoni.—Ufunuo 11:15; 16:14-16.

Kitabu cha Ufunuo humtaja Mikaeli hasa kuhusiana na kusimamishwa kwa Ufalme wa Mungu na kuhusianisha tukio hilo na ole kwa dunia: “Na vita vikatokea ghafula mbinguni: Mikaeli na malaika zake wakapigana na yule joka mkubwa, naye joka mkubwa na malaika zake wakapigana . . . Nami nikaisikia sauti kubwa mbinguni ikisema: ‘Sasa kumekuwa na wokovu na nguvu na ufalme wa Mungu wetu na mamlaka ya Kristo wake, kwa sababu mshtaki wa ndugu zetu ametupwa chini . . . Kwa sababu hiyo furahini, enyi mbingu nanyi mnaokaa ndani yake! Ole wa dunia na wa bahari.’” (Ufunuo 12:7, 10, 12) Baadaye Yesu Kristo anaonyeshwa akiongoza majeshi ya kimbingu kupigana na mataifa ya dunia. (Ufunuo 19:11-16) Hiki kingekuwa kipindi chenye taabu kwa mataifa, ambacho bila shaka kingemalizika katika “wakati wa taabu” unaohusianishwa na kusimama kwa Mikaeli. (Danieli 12:1) Kwa kuwa Mwana wa Mungu atapigana na mataifa, ni jambo linalopatana na akili kukata kauli kwamba yeye pamoja na malaika zake ndiye aliyepigana na joka lenye nguvu zipitazo za wanadamu, Shetani Ibilisi, pamoja na malaika zake.

Kabla hajawa mwanadamu, Yesu aliitwa “Neno.” (Yohana 1:1) Pia alikuwa na jina la kibinafsi, Mikaeli. Kwa kuendelea kuitwa Yesu baada ya kufufuliwa, “Neno” anaonyesha kwamba yeye ndiye aliyekuwa Mwana wa Mungu duniani. (Matendo 9:5) Kwa kurudia jina lake la kimbingu Mikaeli na jina la cheo “Neno la Mungu” hilo humhusianisha na kipindi alichoishi kabla ya yeye kuwa mwanadamu. (Ufunuo 19:13) Jina lenyewe Mikaeli, ambalo ni swali, “Ni Nani Aliye Kama Mungu?” huonyesha kwamba hakuna aliye kama Yehova Mungu, au hakuna anayelingana naye, na kwamba malaika wake mkuu, Mikaeli, ndiye Bingwa au Mteteaji wake mkuu.