Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Mwongozo Wenye Hekima kwa Wenzi wa Ndoa

Mwongozo Wenye Hekima kwa Wenzi wa Ndoa

Mwongozo Wenye Hekima kwa Wenzi wa Ndoa

“Wake na wajitiishe kwa waume zao kama kwa Bwana. Enyi waume, endeleeni kuwapenda wake zenu.”—WAEFESO 5:22, 25.

1. Ni maoni gani yanayofaa kuhusu ndoa?

YESU alisema kwamba ndoa ni kuunganishwa kwa mwanamume na mwanamke na Mungu ili wawe “mwili mmoja.” (Mathayo 19:5, 6) Inahusisha watu wawili wenye nyutu mbalimbali ambao wanajifunza kuwa na mapendezi yaleyale na kushirikiana kufikia miradi ileile. Ndoa ni kifungo cha maisha, si mkataba unaoweza kuvunjwa kwa urahisi. Katika nchi nyingi, ni rahisi kupata talaka, lakini Mkristo huiona ndoa kuwa takatifu. Inaweza kuvunjwa tu kukiwa na sababu muhimu.—Mathayo 19:9.

2. (a) Wenzi wa ndoa wanaweza kupata msaada gani? (b) Kwa nini ni muhimu kujitahidi kufanikisha ndoa?

2 Mshauri mmoja wa ndoa alisema hivi: “Ndoa nzuri hubadilika-badilika daima inapotokeza masuala mapya, inaposhughulika na matatizo yanayotokea, na kutumia maandalizi yaliyopo katika kila hatua ya maisha.” Kwa wenzi wa ndoa Wakristo, maandalizi hayo yanatia ndani shauri lenye hekima kutoka katika Biblia, msaada kutoka kwa Wakristo wenzao, na uhusiano wa karibu sana pamoja na Yehova kupitia sala. Ndoa yenye mafanikio hudumu, nayo huletea mume na mke furaha na uradhi kadiri miaka inavyopita. Jambo lililo muhimu zaidi ni kwamba humletea heshima Yehova Mungu, ambaye ndiye Mwanzilishi wa ndoa.—Mwanzo 2:18, 21-24; 1 Wakorintho 10:31; Waefeso 3:15; 1 Wathesalonike 5:17.

Igeni Yesu na Kutaniko Lake

3. (a) Taja mambo makuu katika shauri la Paulo kwa wenzi wa ndoa. (b) Yesu alituwekea kielelezo gani kizuri?

3 Miaka 2,000 iliyopita, mtume Paulo aliwapa wenzi Wakristo shauri hili lenye hekima alipoandika: “Kama vile kutaniko linavyojitiisha kwa Kristo, vivyo hivyo wanawake pia na wajitiishe kwa waume zao katika mambo yote. Enyi waume, endeleeni kuwapenda wake zenu, kama vile Kristo pia alivyolipenda kutaniko na kujitoa mwenyewe kwa ajili yake.” (Waefeso 5:24, 25) Huo ni ulinganisho mzuri sana. Wake Wakristo wanaojitiisha kwa unyenyekevu kwa waume zao huliiga kutaniko katika kutambua na kutii kanuni ya ukichwa. Waume wanaoamini ambao huendelea kuwapenda wake zao katika nyakati nzuri au katika nyakati ngumu, huonyesha kwamba wanafuata kwa ukaribu kielelezo cha Kristo cha kulipenda na kulitunza kutaniko.

4. Waume wanawezaje kufuata kielelezo cha Yesu?

4 Waume Wakristo ni vichwa vya familia zao, lakini wao pia wana kichwa ambaye ni Yesu. (1 Wakorintho 11:3) Hivyo, kama vile Yesu alivyolitunza kutaniko lake, ndivyo waume hutunza familia zao kwa upendo kwa njia ya kiroho na kimwili, hata kama atalazimika kujidhabihu ili kufanya hivyo. Wao hutanguliza masilahi ya familia zao badala ya tamaa na mapendezi yao. Yesu alisema: “Mambo yote mnayotaka watu wawatendee ninyi, lazima mwatendee wao pia vivyo hivyo.” (Mathayo 7:12) Kanuni hiyo inatumika hasa katika ndoa. Paulo alionyesha hilo aliposema: “Waume wanapaswa kuwa wakiwapenda wake zao kama miili yao wenyewe. . . . Hakuna mtu anayeuchukia mwili wake kwa vyovyote; bali huulisha na kuutunza kwa upendo.” (Waefeso 5:28, 29) Mwanamume anapaswa kumlisha na kumtunza mke wake kwa bidii kama anavyojilisha na kujitunza mwenyewe.

5. Wake wanawezaje kuiga kutaniko la Kikristo?

5 Wake wanaomwabudu Mungu huiga kielelezo cha kutaniko la Kikristo. Yesu alipokuwa duniani, wafuasi wake waliacha kwa hiari mambo waliyofuatilia hapo awali na kumfuata. Baada ya kifo chake, waliendelea kujitiisha kwake, na kwa miaka zaidi ya 2,000 hivi iliyopita, kutaniko la Kikristo la kweli limeendelea kujitiisha kwa Yesu na kufuata uongozi wake katika mambo yote. Vivyo hivyo, wake Wakristo hawadharau waume zao au kupuuza mpango wa Kimaandiko wa ukichwa katika ndoa. Badala yake, wao huwasaidia waume zao na kujitiisha kwao, wakishirikiana nao, na hivyo kuwatia moyo. Mume na mke wanapotenda kwa njia hiyo ya upendo, ndoa yao itafanikiwa na wote watapata shangwe katika uhusiano huo.

Endeleeni Kukaa Nao

6. Petro aliwapa waume shauri gani, na kwa nini shauri hilo ni muhimu?

6 Mtume Petro pia aliwashauri wenzi wa ndoa, na shauri lake kwa waume lilikuwa la moja kwa moja. Alisema: “Endeleeni kukaa [na wake zenu] vivyo hivyo kulingana na ujuzi, mkiwapa heshima kama chombo dhaifu zaidi, yaani, mwanamke, kwa kuwa ninyi pia ni warithi pamoja nao wa pendeleo lisilostahiliwa la uzima, kusudi sala zenu zisizuiwe.” (1 Petro 3:7) Uzito wa shauri la Petro unaelezwa katika maneno ya mwisho ya mstari huo. Mume asipomheshimu mke wake, uhusiano wake pamoja na Yehova utaathiriwa. Sala zake zitazuiwa.

7. Mume anapaswa kumheshimu mke wake jinsi gani?

7 Basi, waume wanaweza kuwaonyeshaje wake zao heshima? Kumheshimu mke wako kunamaanisha kumtendea kwa upendo, staha, na hadhi. Wengi wangeona kumtendea mke kwa fadhili kuwa jambo lisilo la kawaida. Msomi mmoja Mgiriki anaandika hivi: “Chini ya sheria ya Waroma, mwanamke hakuwa na haki zozote. Kulingana na sheria, haki zake zilikuwa sawa na za mtoto. . . . Alitiishwa kabisa chini ya mume wake, naye alitawaliwa kabisa na mumewe.” Hilo lilikuwa tofauti sana na mafundisho ya Kikristo. Mume Mkristo alimheshimu mke wake. Alishughulika naye kulingana na kanuni za Kikristo, wala si kulingana na hisia zake za ghafula. Isitoshe, alimtendea kwa ufikirio “kulingana na ujuzi,” akikumbuka kwamba mke ni chombo dhaifu zaidi.

“Chombo Dhaifu Zaidi” Katika Njia Gani?

8, 9. Wanawake ni sawa na wanaume katika njia zipi?

8 Kwa kusema kwamba mwanamke ni “chombo dhaifu zaidi,” Petro hakumaanisha kwamba wanawake ni dhaifu zaidi kiakili au kiroho kuliko wanaume. Ni kweli kwamba wanaume wengi Wakristo wana mapendeleo kutanikoni ambayo wanawake hawatarajii kuwa nayo, na katika familia wanawake hujitiisha kwa waume zao. (1 Wakorintho 14:35; 1 Timotheo 2:12) Hata hivyo, wote, wanaume kwa wanawake, wanapaswa kuwa na imani, uvumilivu, na viwango vilevile vya juu vya maadili. Na kama Petro alivyosema, wote wawili, mume na mke ni “warithi . . . wa pendeleo lisilostahiliwa la uzima.” Kwa habari ya wokovu, wote wana msimamo sawa mbele za Yehova Mungu. (Wagalatia 3:28) Petro alikuwa akiwaandikia Wakristo watiwa-mafuta wa karne ya kwanza. Kwa hiyo, maneno yake yaliwakumbusha waume Wakristo kwamba wakiwa “warithi pamoja na Kristo,” wao pamoja na wake zao walikuwa na tumaini lilelile la kimbingu. (Waroma 8:17) Siku moja, wote watakuwa makuhani na wafalme katika Ufalme wa Mungu wa kimbingu!—Ufunuo 5:10.

9 Bila shaka, wake Wakristo waliotiwa mafuta hawakuwa duni kwa kulinganishwa na waume zao Wakristo waliotiwa mafuta. Na kanuni hiyohiyo inatumika kwa wale walio na tumaini la kidunia. Wote, wanaume na wanawake wa “umati mkubwa” wanafua kanzu zao na kuzifanya nyeupe katika damu ya Mwana-Kondoo. Wote, wanaume na wanawake wanashiriki katika kumtolea Yehova sifa “mchana na usiku” ulimwenguni pote. (Ufunuo 7:9, 10, 14, 15) Wote, wanaume na wanawake wanatazamia kupata “uhuru wenye utukufu wa watoto wa Mungu,” watakapofurahia “uzima ulio wa kweli.” (Waroma 8:21; 1 Timotheo 6:19) Wawe ni watiwa-mafuta au wale wa kondoo wengine, Wakristo wote humtumikia Yehova pamoja wakiwa “kundi moja” chini ya “mchungaji mmoja.” (Yohana 10:16) Hiyo ni sababu yenye kusadikisha sana kwa waume na wake Wakristo kuheshimiana.

10. Wanawake ni ‘vyombo dhaifu zaidi’ katika maana gani?

10 Basi, wanawake ni ‘vyombo dhaifu zaidi’ katika njia gani? Huenda Petro alikuwa akirejelea ukweli wa kwamba, kwa ujumla, wanawake ni wadogo zaidi kimwili na hawana nguvu nyingi kama wanaume. Zaidi ya hayo, kwa sababu ya hali yetu ya kutokamilika, pendeleo la pekee la kuzaa watoto huathiri afya ya wanawake. Huenda wanawake wenye umri wa kuweza kuzaa wakawa na maumivu ya mwili mara kwa mara. Kwa kweli wanahitaji utunzaji na ufikirio wa pekee wanapokuwa na maumivu hayo au uchovu unaosababishwa na kuwa mja-mzito na kujifungua. Mume anayemheshimu mke wake akitambua kwamba anahitaji kutegemezwa kihisia, atachangia sana kufanikiwa kwa ndoa.

Katika Nyumba Iliyogawanyika Kidini

11. Ni katika maana gani ndoa inaweza kufanikiwa hata kama mume na mke ni wa dini tofauti?

11 Hata hivyo, namna gani ikiwa wenzi wa ndoa wana maoni tofauti ya kidini kwa sababu mmoja alikubali kweli ya Kikristo muda fulani baada ya kufunga ndoa na yule mwingine hakuikubali? Je, ndoa hiyo inaweza kufanikiwa? Ndoa nyingi kama hizo zimefanikiwa. Mume na mke ambao wana maoni tofauti ya kidini bado wanaweza kuwa na ndoa yenye mafanikio katika maana ya kwamba wanaweza kuwa na ndoa inayodumu na yenye furaha. Mbali na hilo, bado ndoa hiyo ni halali machoni pa Yehova; bado wao ni “mwili mmoja.” Kwa hiyo, wenzi wa ndoa Wakristo wanashauriwa wakae na mwenzi asiyeamini iwapo mwenzi huyo anakubali. Ikiwa kuna watoto, wananufaika na uaminifu wa mzazi aliye Mkristo.—1 Wakorintho 7:12-14.

12, 13. Kwa kufuata shauri la Petro, wake Wakristo wanaweza kuwasaidiaje waume wasioamini?

12 Petro anatoa shauri lenye fadhili kwa wanawake Wakristo wanaoishi katika nyumba zilizogawanyika kidini. Maneno yake yanaweza kuwahusu pia waume Wakristo walio katika hali kama hiyo. Petro anaandika hivi: “Ninyi wake, jitiisheni kwa waume zenu wenyewe, ili, ikiwa wowote si watiifu kwa lile neno, wavutwe bila neno kupitia mwenendo wa wake zao, kwa sababu wamekwisha kushuhudia kwa macho mwenendo wenu ulio safi kiadili pamoja na heshima kubwa.”—1 Petro 3:1, 2.

13 Ikiwa mke anaweza kumweleza mume wake imani yake kwa busara, hilo ni jambo la kusifiwa. Lakini, namna gani ikiwa hataki kusikiliza? Huo ni uamuzi wake. Hata hivyo, bado kuna tumaini, kwa kuwa mwenendo wa Kikristo pia hutoa ushahidi wenye nguvu. Waume wengi ambao hapo mwanzoni hawakupendezwa au hata walipinga imani ya wake zao baadaye walikuwa na “mwelekeo unaofaa kwa ajili ya uzima wa milele” baada ya kuona mwenendo mzuri wa wake zao. (Matendo 13:48) Hata kama mume hatakubali kweli ya Kikristo, huenda bado akavutiwa na mwenendo wa mke wake, na hilo linaweza kuimarisha kifungo cha ndoa. Mume mmoja ambaye mke wake ni Shahidi wa Yehova alikiri kwamba hawezi kuishi kupatana na viwango vya juu vya Mashahidi wa Yehova. Lakini bado alisema kwamba “alifurahi kuwa mume wa mke mwenye kuvutia” na akamsifu kwa unyoofu mke wake pamoja na Mashahidi wenzake katika barua aliyoandikia gazeti moja.

14. Waume wanaweza kuwasaidiaje wake wasioamini?

14 Vivyo hivyo, waume Wakristo ambao wamefuata kanuni zinazopatikana katika maneno ya Petro wamewavuta wake zao kupitia mwenendo wao. Wake wasioamini wameona waume zao wakichukua madaraka yao kwa uzito, wakiacha kupoteza pesa kwa kuvuta sigara, kunywa pombe, na kucheza kamari, na kuacha kutumia lugha chafu. Baadhi ya wake hao wasioamini wamefahamiana na washiriki wa kutaniko la Kikristo. Walivutiwa na undugu wa Kikristo wenye upendo, na yale waliyoona kati ya akina ndugu yaliwavuta kwa Yehova.—Yohana 13:34, 35.

“Yule Mtu wa Siri wa Moyoni”

15, 16. Mke Mkristo anaweza kumvuta mume asiyeamini kwa mwenendo wa aina gani?

15 Ni mwenendo wa aina gani unaoweza kumvuta mume? Kwa kweli, ni mwenendo ambao kwa kawaida husitawishwa na wanawake Wakristo. Petro anasema: “Kujipamba kwenu kusiwe kule kusuka nywele kwa nje na kule kujivika mapambo ya dhahabu au kuvaa mavazi ya nje, bali kuwe yule mtu wa siri wa moyoni katika vazi lisiloharibika la roho ya utulivu na ya upole, ambayo ni ya thamani kubwa machoni pa Mungu. Kwa maana, pia, ndivyo walivyokuwa wakijipamba wale wanawake watakatifu hapo zamani, waliokuwa wakimtumaini Mungu, wakijitiisha kwa waume zao wenyewe, kama Sara alivyokuwa akimtii Abrahamu, akimwita ‘bwana.’ Nanyi mmekuwa watoto wake, mradi tu mnaendelea kutenda mema na kutokuwa na woga kwa sababu ya kitisho chochote.”—1 Petro 3:3-6.

16 Petro anamshauri mwanamke Mkristo asitegemee sura ya nje. Badala yake, anapaswa kuacha mume wake aone jinsi mafundisho ya Biblia yanavyobadili utu wake wa ndani. Anapaswa kuacha mume wake aone jinsi anavyovaa utu mpya. Labda ataulinganisha na ule utu wa zamani ambao mke wake alikuwa nao. (Waefeso 4:22-24) Bila shaka, ataona “roho ya utulivu na ya upole” ya mke wake kuwa yenye kuburudisha na kuvutia. Roho hiyo haimpendezi tu mume wake bali pia ni “ya thamani kubwa machoni pa Mungu.”—Wakolosai 3:12.

17. Sara ni kielelezo kizuri kwa wake Wakristo jinsi gani?

17 Sara anatajwa kuwa kielelezo, naye ni mfano mzuri wa kuigwa na wake Wakristo iwe waume zao ni waamini au la. Bila shaka, Sara alimwona Abrahamu kuwa kichwa chake. Hata moyoni mwake, alimwita “bwana” wake. (Mwanzo 18:12) Hata hivyo, hilo halikumfanya kuwa duni. Ni wazi kwamba alikuwa mwanamke mwenye nguvu kiroho aliyekuwa na imani thabiti katika Yehova. Kwa kweli, yeye ni sehemu ya ‘wingu kubwa la mashahidi’ ambao kielelezo chao cha imani kinapaswa kutuchochea “tukimbie kwa uvumilivu shindano la mbio lililowekwa mbele yetu.” (Waebrania 11:11; 12:1) Kwa hiyo mke Mkristo hawi duni anapomwiga Sara.

18. Ni kanuni gani zinazopaswa kufuatwa katika nyumba iliyogawanyika kidini?

18 Katika nyumba iliyogawanyika kidini, bado mume ndiye kichwa. Ikiwa yeye ni mwamini, atafikiria imani ya mke wake huku akishikilia imani yake. Ikiwa mke ndiye mwamini, yeye pia atashikilia imani yake. (Matendo 5:29) Hata hivyo, hatapinga ukichwa wa mume wake. Ataheshimu cheo chake na kuendelea kuwa chini ya “sheria ya mume wake.”—Waroma 7:2.

Mwongozo wa Biblia Wenye Hekima

19. Ni mambo gani ambayo huleta mkazo katika kifungo cha ndoa, lakini yanaweza kushindwaje?

19 Leo, kuna mambo mengi yanayoweza kusababisha mkazo katika kifungo cha ndoa. Wanaume fulani hukosa kutimiza madaraka yao. Wanawake fulani hukataa kukubali ukichwa wa waume zao. Katika ndoa fulani, mwenzi mmoja hutendewa vibaya na yule mwingine. Mikazo ya kiuchumi, kutokamilika kwa kibinadamu, na roho ya ulimwengu pamoja na ukosefu wa maadili na viwango vyake vilivyopotoka vinaweza kujaribu ushikamanifu wa Wakristo. Hata hivyo, wanaume na wanawake Wakristo wanaofuata kanuni za Biblia hata hali zao ziweje, hubarikiwa na Yehova. Hata kama mwenzi mmoja tu katika ndoa ndiye anayefuata kanuni za Biblia, hali huwa bora zaidi kuliko wote wawili wanapokosa kuzifuata. Zaidi ya hayo, Yehova huwapenda na kuwasaidia watumishi wake wanaoendelea kuwa waaminifu kwa nadhiri zao za ndoa hata chini ya hali ngumu. Yeye hasahau ushikamanifu wao.—Zaburi 18:25; Waebrania 6:10; 1 Petro 3:12.

20. Petro anatoa shauri gani kwa Wakristo wote?

20 Baada ya kuwashauri wanaume na wanawake waliofunga ndoa, mtume Petro alimalizia kwa maneno machangamfu na yenye kutia moyo. Alisema: “Mwishowe, ninyi nyote iweni na akili zinazopatana, mkionyesha hisia-mwenzi, mkiwa na upendo wa kindugu, wenye huruma nyororo, wanyenyekevu katika akili, msilipe ubaya kwa ubaya au matukano kwa matukano, bali, kinyume chake, mkitoa baraka, kwa sababu mliitwa kwenye mwendo huu, ili mrithi baraka.” (1 Petro 3:8, 9) Hilo ni shauri zuri sana kwa wote, hasa kwa wenzi wa ndoa.

Je, Unakumbuka?

• Waume Wakristo humwigaje Yesu?

• Wake Wakristo huliigaje kutaniko?

• Waume wanaweza kuheshimu wake zao katika njia gani?

• Ni mwenendo gani unaomfaa mke Mkristo ambaye mume wake si mwamini?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 16]

Mume Mkristo humpenda na kumtunza mke wake

Mke Mkristo humstahi na kumheshimu mume wake

[Picha katika ukurasa wa 17]

Tofauti na sheria ya Waroma, mafundisho ya Kikristo yalimtaka mume amheshimu mke wake

[Picha katika ukurasa wa 18]

Wote, wanaume na wanawake wa “umati mkubwa” wanatazamia kuishi milele katika Paradiso

[Picha katika ukurasa wa 20]

Sara alimwona Abrahamu kuwa bwana wake