Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Ndoa Inaweza Kufanikiwa Katika Ulimwengu wa Leo

Ndoa Inaweza Kufanikiwa Katika Ulimwengu wa Leo

Ndoa Inaweza Kufanikiwa Katika Ulimwengu wa Leo

“Jivikeni upendo, kwa maana huo ni kifungo kikamilifu cha muungano.”—WAKOLOSAI 3:14.

1, 2. (a) Ni jambo gani linalotia moyo kuhusiana na kutaniko la Kikristo? (b) Ndoa yenye mafaniko ni ipi?

TUNAPOTAZAMA washiriki mbalimbali wa kutaniko la Kikristo, je, haichangamshi moyo kuona watu wengi waliofunga ndoa ambao wamekuwa washikamanifu kwa wenzi wao kwa miaka 10, 20, 30, au hata kwa muda mrefu zaidi? Wamekuwa washikamanifu kwa wenzi wao kwa heri na kwa shari.—Mwanzo 2:24.

2 Wengi wao watakubali kwamba wamekuwa na matatizo katika ndoa zao. Mchunguzi mmoja aliandika hivi: “Ndoa zenye furaha hazikosi mahangaiko na matatizo. Kuna nyakati zenye furaha na nyakati za matatizo . . . Lakini . . . ndoa hizo zimedumu licha ya msukosuko wa maisha ya kisasa.” Wenzi ambao wamefanikiwa wamejifunza kukabiliana na misukosuko na misiba isiyoepukika ambayo husababishwa na mikazo ya maisha, hasa ikiwa wamelea watoto. Kutokana na mambo ambayo wamejionea, wenzi hao wamejifunza kwamba upendo wa kweli “haushindwi kamwe.”—1 Wakorintho 13:8.

3. Takwimu zinaonyesha nini kuhusu ndoa na talaka, na hilo linatokeza maswali gani?

3 Tofauti na hilo, ndoa nyingi zimevunjika. Ripoti moja inasema hivi: “Nusu ya ndoa zote huko Marekani leo zinatarajiwa kuishia katika talaka. Na nusu ya [talaka] hizo zitatokea katika miaka 7.8 ya kwanza ya ndoa . . . Kati ya asilimia 75 ya wale wanaofunga ndoa tena, asilimia 60 watatalikiana tena.” Talaka zimeongezeka hata katika nchi ambazo hapo awali zilikuwa na idadi ya chini ya talaka. Kwa mfano, huko Japani, idadi ya talaka imeongezeka karibu maradufu katika miaka ya hivi karibuni. Ni mikazo gani imechangia hali hiyo, mikazo ambayo nyakati nyingine huwaathiri hata washiriki wa kutaniko la Kikristo? Ni nini kinachohitajiwa ili ndoa ifanikiwe licha ya jitihada za Shetani za kudhoofisha mpango huo?

Mitego ya Kuepukwa

4. Ni baadhi ya mambo gani ambayo yanaweza kudhoofisha ndoa?

4 Neno la Mungu hutusaidia kuelewa baadhi ya mambo yanayoweza kudhoofisha ndoa. Kwa mfano, fikiria yale ambayo mtume Paulo alisema kuhusu hali ambazo zingekuwapo katika siku hizi za mwisho: “Katika siku za mwisho kutakuwa na nyakati za hatari zilizo ngumu kushughulika nazo. Kwa maana watu watakuwa wenye kujipenda wenyewe, wenye kupenda pesa, wenye kujidai, wenye majivuno, wakufuru, wasiotii wazazi, wasio na shukrani, wasio washikamanifu, wasio na upendo wa asili, wasiotaka makubaliano yoyote, wachongezi, wasiojizuia, wakali, wasiopenda wema, wasaliti, wenye vichwa vigumu, wenye kujivuna kwa kiburi, wanaopenda raha badala ya kumpenda Mungu wakiwa na namna ya ujitoaji-kimungu lakini wakizikana nguvu zake; nawe geukia mbali kutoka kwa hao.”—2 Timotheo 3:1-5.

5. Kwa nini mtu ‘anayejipenda mwenyewe’ anahatarisha ndoa yake, nayo Biblia inatoa shauri gani kuhusiana na hilo?

5 Tunapochunguza maneno ya Paulo, tunaona kwamba mambo mengi aliyoorodhesha yanaweza kuharibu mahusiano ya ndoa. Kwa mfano, watu “wenye kujipenda wenyewe” wana ubinafsi na hawawafikirii wengine. Waume au wake wanaojipenda wenyewe hutaka tu kutimiza makusudi yao. Hawako tayari kubadilika. Je, mtazamo kama huo unaweza kuchangia furaha katika ndoa? Sivyo kabisa. Kwa hekima, mtume Paulo aliwashauri hivi Wakristo, kutia ndani wenzi wa ndoa: “[Hampaswi] kufanya jambo lolote kwa ugomvi au kwa kujisifu, bali kwa unyenyekevu wa akili mkiwaona wengine kuwa ni bora kuliko ninyi, mkiendelea kuangalia, si faida za kibinafsi za mambo yenu wenyewe tu, bali pia faida za kibinafsi za wengine.”—Wafilipi 2:3, 4.

6. Kupenda pesa kunaweza kudhoofishaje uhusiano wa ndoa?

6 Kupenda pesa kunaweza kusababisha mgawanyiko kati ya mume na mke. Paulo alionya hivi: “Wale ambao wameazimia kuwa matajiri huanguka katika jaribu na mtego na tamaa nyingi za kijinga na zenye kudhuru, ambazo hutumbukiza watu katika maangamizi na uharibifu. Kwa maana kupenda pesa ni chanzo cha mambo mabaya ya namna zote, na kwa kujitahidi kufikia upendo huo wengine wamepotoshwa kutoka kwenye imani nao wamejichoma wenyewe kila mahali kwa maumivu mengi.” (1 Timotheo 6:9, 10) Kwa kusikitisha, maneno hayo ya Paulo yametimia katika ndoa nyingi leo. Katika kufuatia mali, watu wengi wamepuuza mahitaji ya wenzi wao kutia ndani uhitaji wa kutegemezwa kihisia na kuwa na urafiki mchangamfu wenye kudumu.

7. Katika visa fulani, ni mwenendo gani umesababisha ukosefu wa ushikamanifu katika ndoa?

7 Paulo alisema pia kwamba katika siku hizi za mwisho watu fulani wangekuwa “wasio washikamanifu, wasio na upendo wa asili, wasiotaka makubaliano yoyote.” Nadhiri ya ndoa ni ahadi nzito ambayo inapaswa kuongoza kwenye kifungo chenye kudumu, haipaswi kuvunjwa kwa hila. (Malaki 2:14-16) Hata hivyo, wengine wamependezwa kimapenzi na watu ambao si wenzi wao wa ndoa. Mwanamke mmoja mwenye umri wa miaka 30 na kitu, ambaye mume wake alimwacha anasema kwamba hata kabla ya kumwacha, mume wake alikuwa na uhusiano wa karibu na wanawake wengine naye aliwapenda sana. Alikosa kutambua kwamba alikuwa akijihusisha na mwenendo usiomfaa mwanamume aliyeoa. Aliumia sana alipoona jambo hilo likitukia, na kwa busara alijaribu kumwonya mume wake kwamba alikuwa akijihusisha na mwenendo hatari. Hata hivyo, mume wake alifanya uzinzi. Hata ingawa alionywa kwa fadhili, mwenzi huyo hakutaka kusikiliza. Alitumbukia kwenye mtego.—Methali 6:27-29.

8. Ni jambo gani linaloweza kuongoza kwenye uzinzi?

8 Biblia inaonya waziwazi kuhusu uzinzi. “Yeyote anayefanya uzinzi na mwanamke amepungukiwa moyoni; yule anayefanya hivyo anaiangamiza nafsi yake mwenyewe.” (Methali 6:32) Kwa kawaida, uzinzi si tendo linalofanywa ghafula bila kufikiriwa. Kama Yakobo, mwandikaji wa Biblia alivyoonyesha, kwa kawaida dhambi kama vile uzinzi hutukia baada tu ya wazo hilo kutungwa akilini na kufikiriwa kwa muda. (Yakobo 1:14, 15) Pole kwa pole, mwenzi anayezini huacha kuwa mshikamanifu kwa mwenzi wake ambaye aliapa atakuwa mwaminifu kwake katika maisha yake yote. Yesu alisema: “Ninyi mlisikia kwamba ilisemwa, ‘Usifanye uzinzi.’ Lakini mimi ninawaambia ninyi kwamba kila mtu ambaye anaendelea kumtazama mwanamke na kumtamani tayari amefanya uzinzi pamoja naye moyoni mwake.”—Mathayo 5:27, 28.

9. Tunapata shauri gani lenye hekima kwenye Methali 5:18-20?

9 Kwa hiyo, mwenendo wenye hekima na mshikamanifu ni ule unaotajwa katika kitabu cha Methali: “Chemchemi yako ya maji na ibarikiwe, na ushangilie pamoja na mke wa ujana wako, paa mwenye kupendeka na mbuzi wa milimani mwenye kuvutia. Na maziwa yake yakuleweshe nyakati zote. Upendo wake na ukufurahishe sikuzote. Basi mwanangu, kwa nini umfurahie mwanamke mgeni au kukumbatia kifua cha mwanamke wa kigeni?”—Methali 5:18-20.

Usikimbilie Ndoa

10. Kwa nini ni jambo la hekima kuchukua wakati kumjua yule unayetazamia awe mwenzi wako wa ndoa?

10 Huenda matatizo yakatokea katika ndoa wenzi wa ndoa wanapoingia kwenye mpango huo haraka-haraka bila kufikiri. Huenda wakawa wachanga mno na wasio na uzoefu. Au labda hawachukui wakati kujuana, yaani, kujua mapendezi yao, miradi yao maishani, na malezi yao. Ni jambo la hekima kuwa na subira na kuchukua wakati kumjua yule unayetazamia awe mwenzi wako wa ndoa. Mfikirie Yakobo, mwana wa Isaka. Ilibidi kumfanyia kazi kwa miaka saba yule aliyetazamia kuwa baba-mkwe wake ili akubaliwe kumwoa Raheli. Alikuwa tayari kufanya hivyo kwa sababu hisia zake zilitegemea upendo wa kweli, na si kuvutiwa tu na urembo wa nje.—Mwanzo 29:20-30.

11. (a) Kifungo cha ndoa huunganisha nini? (b) Kwa nini ni muhimu kutumia usemi unaofaa katika ndoa?

11 Ndoa inahusisha mengi zaidi ya uhusiano wa kimapenzi. Kifungo cha ndoa huwaunganisha watu wawili kutoka malezi tofauti na wenye nyutu, hisia, na mara nyingi elimu tofauti. Mara nyingine kinaunganisha tamaduni mbili, na hata lugha mbili. Hata kama kifungo hicho hakiwaunganishi watu katika njia zilizotajwa, kinawaunganisha watu wawili wanaoweza kuwa na maoni tofauti. Watu hao wenye maoni tofauti ndio hufanyiza kifungo cha ndoa. Wanaweza kuwa wachambuzi na walalamikaji daima au wanaweza kuwa wenye kutia moyo na kujenga. Naam, maneno yetu yanaweza kuumiza au kuponya mwenzi wetu. Usemi usiodhibitiwa unaweza kutokeza mkazo mkubwa katika ndoa.—Methali 12:18; 15:1, 2; 16:24; 21:9; 31:26.

12, 13. Tunatiwa moyo tuwe na maoni gani halisi kuhusu ndoa?

12 Kwa hiyo, ni jambo la hekima kuchukua wakati kumjua vizuri yule unayetazamia awe mwenzi wako wa ndoa. Dada mmoja Mkristo ambaye ameolewa kwa muda mrefu alisema hivi pindi moja: “Unapomchunguza yule unayetazamia awe mwenzi wako wa ndoa, fikiria sifa kumi hivi muhimu ambazo ungependa awe nazo. Ikiwa mtu huyo ana sifa saba tu, jiulize, ‘Je, niko tayari kupuuza zile sifa tatu ambazo hana? Je, kila siku nitavumilia upungufu huo?’ Ikiwa una shaka yoyote, tua na ufikirie tena.” Bila shaka, unapaswa kuona mambo kihalisi. Ukitaka kufunga ndoa, kumbuka kwamba hutapata kamwe mwenzi mkamilifu. Hata hivyo, yule ambaye utafunga naye ndoa hatapata mwenzi mkamilifu pia!—Luka 6:41.

13 Ndoa hutia ndani kujidhabihu. Paulo alikazia jambo hilo aliposema: “Nataka ninyi msiwe na mahangaiko. Mwanamume ambaye hajaoa huhangaikia mambo ya Bwana, jinsi anavyoweza kupata kibali cha Bwana. Lakini mwanamume aliyeoa huhangaikia mambo ya ulimwengu, jinsi anavyoweza kupata kibali cha mke wake, naye amegawanyika. Zaidi ya hayo, mwanamke mseja, na bikira, huhangaikia mambo ya Bwana, ili awe mtakatifu katika mwili wake na pia katika roho yake. Hata hivyo, mwanamke aliyeolewa huhangaikia mambo ya ulimwengu, jinsi anavyoweza kupata kibali cha mume wake.”—1 Wakorintho 7:32-34.

Kwa Nini Ndoa Fulani Hazifanikiwi?

14, 15. Ni nini kinachoweza kuchangia kudhoofika kwa kifungo cha ndoa?

14 Mwanamke mmoja Mkristo alipatwa na mfadhaiko wa talaka mume wake alipomwacha baada ya miaka 12 ya ndoa na kuanza urafiki na mwanamke mwingine. Je, aliona dalili zozote mbaya kabla ya ndoa yao kuvunjika? Anaeleza hivi: “Ilifikia wakati mume wangu hakuwa akisali tena. Alitoa visababu vya kukosa mikutano ya Kikristo na kwenda kuhubiri. Alidai kwamba alikuwa na shughuli nyingi mno au alikuwa amechoka sana hivi kwamba hakuwa na wakati wa kuwa pamoja nami. Alikataa kuzungumza nami. Hakuzungumza nami mambo ya kiroho. Inasikitisha kwamba alibadilika sana. Hakuwa tena yule mwanamume niliyefunga naye ndoa.”

15 Wengine wamesema kwamba wameona dalili hizohizo, kutia ndani kupuuzwa kwa funzo la kibinafsi la Biblia, sala, au kuhudhuria mikutano ya Kikristo. Yaani, watu wengi ambao mwishowe waliwaacha wenzi wao waliruhusu uhusiano wao na Yehova udhoofike. Waliacha kukazia fikira mambo ya kiroho. Hawakumwona tena Yehova kuwa Mungu aliye hai. Ulimwengu mpya wa uadilifu unaoahidiwa haukuwa tena halisi kwao. Katika visa fulani, hali ya kiroho ilidhoofika hata kabla mwenzi aliyezini kuwa na uhusiano nje ya ndoa.—Waebrania 10:38, 39; 11:6; 2 Petro 3:13, 14.

16. Ni nini huimarisha ndoa?

16 Tofauti na hilo, mume na mke fulani ambao wana furaha sana katika ndoa yao wanasema kwamba ndoa yao imefanikiwa kwa sababu wana uhusiano wa kiroho wenye nguvu. Wao husali na kujifunza pamoja. Mume huyo anasema hivi: “Sisi husoma Biblia pamoja. Tunahubiri pamoja. Sisi hufurahia kufanya mambo pamoja.” Somo liko wazi: Kudumisha uhusiano mzuri na Yehova kutachangia sana kuimarisha ndoa.

Oneni Mambo Kihalisi na Mwasiliane

17. (a) Ni mambo gani mawili ambayo huchangia kufanikiwa kwa ndoa? (b) Paulo anafafanuaje upendo wa Kikristo?

17 Mambo mengine mawili ambayo huchangia kufanikiwa kwa ndoa ni: upendo wa Kikristo na kuwasiliana. Watu wawili wanapopendana, kila mmoja huwa na mwelekeo wa kupuuza kasoro za mwenzake. Huenda wenzi hao wakaingia katika ndoa wakitarajia mambo mengi kwa sababu ya yale wanayosoma katika vitabu vya mahaba au wanayoona katika sinema. Hata hivyo, mwishowe wenzi hao watalazimika kuona mambo kihalisi. Wakati huo, huenda kasoro ndogo-ndogo au tabia zenye kuudhi zikasababisha matatizo makubwa. Hali hiyo ikitokea, Wakristo wanahitaji kuonyesha matunda ya roho, mojawapo likiwa upendo. (Wagalatia 5:22, 23) Kwa kweli, upendo wa Kikristo, na si upendo wa kimahaba, una nguvu sana. Paulo alifafanua upendo huo wa Kikristo aliposema hivi: “Upendo ni wenye ustahimilivu na wenye fadhili. . . . Hautafuti faida zake wenyewe, hauchokozeki. Hauweki hesabu ya ubaya. . . . Huhimili mambo yote, huamini mambo yote, hutumaini mambo yote, huvumilia mambo yote.” (1 Wakorintho 13:4-7) Kwa wazi, upendo wa kweli huvumilia udhaifu wa kibinadamu. Huona mambo kihalisi, kwa hiyo hautarajii ukamilifu.—Methali 10:12.

18. Mawasiliano yanawezaje kuimarisha ndoa?

18 Mawasiliano pia ni muhimu. Hata wenzi wa ndoa wawe wameoana kwa muda mrefu kadiri gani, wanapaswa kuzungumziana na kila mmoja amsikilize mwenzake kikweli. Mume mmoja anasema hivi: “Sisi huonyeshana wazi hisia zetu lakini kwa njia ya kirafiki.” Baada ya kukaa pamoja kwa muda mrefu, mume au mke hujifunza si kusikiliza tu yale yanayosemwa bali pia kusikiliza mambo ambayo hayajasemwa. Yaani, kadiri miaka inavyopita, wenzi wa ndoa wenye furaha hujifunza kutambua mawazo ambayo hayajasemwa au hisia ambazo hazijaonyeshwa. Wake fulani wamesema kwamba waume zao hawawasikilizi kikweli. Waume fulani wamelalamika kwamba wake zao hutaka kuzungumza nyakati zisizofaa. Mawasiliano hutia ndani kuwa na huruma na kuwafikiria wengine. Mawasiliano mazuri humfaidi mume na mke.—Yakobo 1:19.

19. (a) Kwa nini inaweza kuwa vigumu kuomba msamaha? (b) Ni nini kitakachotuchochea kuomba msamaha?

19 Nyakati nyingine, mawasiliano hutia ndani kuomba msamaha. Si rahisi sikuzote kufanya hivyo. Mtu anahitaji kuwa mnyenyekevu ili akubali makosa yake. Lakini jambo hilo linaweza kuimarisha sana ndoa. Kuomba msamaha kwa unyoofu kunaweza kuondoa hali ambayo inaweza kusababisha ugomvi wakati ujao na kufanya iwe rahisi kusamehe kikweli na kusuluhisha tatizo hilo. Paulo alisema hivi: “Endeleeni kuvumiliana na kusameheana kwa hiari ikiwa yeyote ana sababu ya kulalamika juu ya mwingine. Kama vile Yehova alivyowasamehe ninyi kwa hiari, nanyi fanyeni vivyo hivyo pia. Lakini, zaidi ya mambo haya yote, jivikeni upendo, kwa maana huo ni kifungo kikamilifu cha muungano.”—Wakolosai 3:13, 14.

20. Mkristo anapaswa kumtendeaje mwenzi wake wa ndoa wakiwa faraghani na mbele za watu?

20 Pia kutegemezana ni muhimu katika ndoa. Mume na mke Mkristo wanapaswa kuaminiana na kutegemezana. Hawapaswi kuharibiana sifa au kwa njia fulani kumfanya mwingine ahisi kuwa hafai. Tukiwa Wakristo waliofunga ndoa, sisi huwapongeza wenzi wetu kwa upendo na hatuwachambui vikali. (Methali 31:28b) Bila shaka, hatuwashushii heshima kwa kuwafanyia mizaha ya kipumbavu. (Wakolosai 4:6) Kutegemezana huko huimarishwa kwa kuonyeshana upendo kwa ukawaida. Mguso au neno fulani linaweza kumwonyesha mwenzi wako kwamba bado unampenda na unafurahia kuwa naye. Hayo ni baadhi ya mambo yanayoweza kusaidia uhusiano na kufanya ndoa ifanikiwe katika ulimwengu wa leo. Kuna mambo mengine, na makala inayofuata itatoa mwongozo zaidi wa Kimaandiko kuhusu jinsi ya kufanikisha ndoa. *

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 20 Kwa habari zaidi, ona kichapo Siri ya Kupata Furaha ya Familia, kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

Je, Unaweza Kueleza?

• Ni baadhi ya mambo gani ambayo yanaweza kudhoofisha ndoa?

• Kwa nini si jambo la hekima kukimbilia ndoa?

• Hali ya kiroho huathirije ndoa?

• Ni mambo gani husaidia kuimarisha ndoa?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 12]

Ndoa inahusisha mengi zaidi ya uhusiano wa kimapenzi

[Picha katika ukurasa wa 14]

Kuwa na uhusiano wenye nguvu pamoja na Yehova husaidia wenzi wa ndoa kufanikisha ndoa yao