Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Tulitumia Hali Zetu Zenye Kubadilika Kuhubiri Maeneo ya Mbali

Tulitumia Hali Zetu Zenye Kubadilika Kuhubiri Maeneo ya Mbali

Simulizi la Maisha

Tulitumia Hali Zetu Zenye Kubadilika Kuhubiri Maeneo ya Mbali

LIMESIMULIWA NA RICARDO MALICSI

Nilipopoteza kazi yangu kwa sababu ya msimamo wangu wa Kikristo wa kutokuwamo, mimi na familia yangu tulimwomba Yehova atusaidie kupanga wakati wetu ujao. Katika sala, tulitaja tamaa yetu ya kupanua huduma yetu. Muda mfupi baadaye, tulianza kuishi maisha ya kuhama-hama na tulihamia nchi nane za kigeni katika mabara mawili. Kwa sababu hiyo, tuliweza kuhubiria watu katika maeneo ya mbali.

NILIZALIWA huko Filipino mwaka wa 1933 katika familia iliyoshirikiana na Kanisa la Independent la Filipino. Washiriki wote 14 wa familia yetu walikuwa wafuasi wa kanisa hilo. Nilipokuwa na umri wa miaka 12, nilimwomba Mungu aniongoze kwenye dini ya kweli. Mmoja wa walimu wangu aliniandikisha katika darasa fulani la kidini na nikawa Mkatoliki aliyejitoa. Sikukosa kwenda kuungama dhambi zangu kamwe Jumamosi au kuhudhuria Misa Jumapili. Hata hivyo, hatua kwa hatua nilianza kukosa uradhi na nikawa mwenye shaka. Nilisumbuliwa na maswali kuhusu hali ya wafu, moto wa mateso, na Utatu. Viongozi wa kidini walitoa majibu yasiyo na maana na yasiyoridhisha.

Kupata Majibu Yenye Kuridhisha

Nilipokuwa chuoni, nilijiunga na kikundi fulani ambacho kilifanya nipigane, nicheze kamari, nivute sigara, na kufanya mambo mengine yasiyo ya adili. Jioni moja, nilikutana na mama ya mmoja wa wanadarasa wenzangu. Alikuwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova. Nilimwuliza maswali yaleyale niliyowauliza walimu wangu wa dini. Alijibu maswali yangu yote kutoka katika Biblia, nami nikasadiki kwamba alisema kweli.

Nilinunua Biblia na nikaanza kujifunza pamoja na Mashahidi. Punde si punde, nilikuwa nikihudhuria mikutano yote ya Mashahidi wa Yehova. Niliacha kushirikiana na marafiki wangu wasio na maadili ili kutii shauri la hekima la Biblia kwamba “mashirika mabaya huharibu tabia nzuri.” (1 Wakorintho 15:33) Hatua hiyo ilinisaidia kufanya maendeleo katika funzo langu la Biblia na mwishowe kujiweka wakfu kwa Yehova. Baada ya kubatizwa mwaka wa 1951, nilitumikia nikiwa mhudumu wa wakati wote (painia) kwa muda fulani. Kisha mnamo Desemba 1953, nikamwoa Aurea Mendoza Cruz, naye akawa mwenzi wangu wa maisha na mfanyakazi mwenzangu mwaminifu katika huduma.

Sala Zetu Zajibiwa

Tulitaka sana kutumikia tukiwa mapainia. Hata hivyo, tamaa yetu ya kumtumikia Yehova haikutimia mara moja. Lakini bado tuliendelea kumwomba Yehova atupe nafasi zaidi katika utumishi wake. Lakini maisha yetu yalikuwa magumu. Bado hatukusahau miradi yetu ya kiroho, na nilipokuwa na umri wa miaka 25, niliwekwa rasmi kuwa mtumishi wa kutaniko, mwangalizi-msimamizi katika kutaniko la Mashahidi wa Yehova.

Nilipoendelea kupata ujuzi wa Biblia na kuelewa vizuri zaidi kanuni za Yehova, nilitambua kwamba kazi yangu ilipingana na msimamo wangu wa Kikristo wa kutokuwamo. (Isaya 2:2-4) Niliamua kuacha kazi hiyo. Jambo hilo lilijaribu imani yetu. Ningetoshelezaje mahitaji ya familia yangu? Tulisali kwa Yehova Mungu tena. (Zaburi 65:2) Tulimweleza mahangaiko na wasiwasi wetu lakini pia tukamweleza tamaa yetu ya kutumikia mahali penye uhitaji mkubwa zaidi wa wahubiri wa Ufalme. (Wafilipi 4:6, 7) Hatukuwazia kwamba tungepata nafasi mbalimbali za kufanya hivyo!

Twaanza Safari Yetu

Mnamo Aprili 1965, nilikubali kazi ya kuwa msimamizi wa kikundi cha waokoaji na wazima-moto kwenye Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Vientiane, Laos, nasi tukahamia huko. Katika jiji la Vientiane, kulikuwa na Mashahidi 24, nasi tulifurahi kuhubiri pamoja na wamishonari na ndugu wachache wenyeji. Baadaye, nilihamishwa hadi kwenye Uwanja wa Ndege wa Udon Thani, Thailand. Hakukuwa na Mashahidi wengine huko. Tulifanya mikutano yote ya kila juma tukiwa familia. Tulihubiri nyumba kwa nyumba, tukafanya ziara za kurudia, na kuanzisha mafunzo ya Biblia.

Tulikumbuka shauri ambalo Yesu aliwapa wanafunzi wake kwamba wanapaswa ‘kuendelea kuzaa matunda mengi.’ (Yohana 15:8) Kwa hiyo, tuliazimia kufuata kielelezo chao na kuendelea kutangaza habari njema. Punde si punde, tulipata matokeo mazuri. Msichana mmoja wa Thailand alikubali kweli na akawa dada yetu wa kiroho. Watu wawili kutoka Amerika Kaskazini walikubali kweli na baada ya muda wakawa wazee Wakristo. Tuliendelea kuhubiri habari njema huko kaskazini mwa Thailand kwa zaidi ya miaka kumi. Tunafurahi sana kujua kwamba sasa kuna kutaniko huko Udon Thani. Baadhi ya mbegu za kweli tulizopanda bado zinazaa matunda.

Hata hivyo, kwa kusikitisha, ilitubidi kuhama tena, na tulisali kwamba “Bwana wa mavuno” atusaidie tuendelee kushiriki katika kazi ya kuhubiri. (Mathayo 9:38) Tulihamishwa hadi Tehran, mji mkuu wa Iran. Huo ulikuwa wakati wa utawala wa Shah.

Kuhubiri Katika Maeneo Magumu

Tulipofika Tehran, tuliwapata ndugu zetu wa kiroho mara moja. Tulishirikiana na kikundi kidogo cha Mashahidi kutoka mataifa 13. Tulihitaji kufanya mabadiliko fulani ili kuhubiri habari njema huko Iran. Ingawa hatukupingwa moja kwa moja, ilitubidi kuwa waangalifu.

Kwa sababu ya ratiba ya kazi ya watu wenye kupendezwa, nyakati nyingine tulilazimika kuongoza mafunzo ya Biblia usiku wa manane au baadaye—hadi alfajiri. Hata hivyo, tulifurahi sana kuona matokeo ya kazi hiyo ngumu. Familia kadhaa za Wafilipino na Wakorea zilikubali kweli ya Kikristo na kujiweka wakfu kwa Yehova.

Nilihamishwa tena nikafanye kazi huko Dhaka, Bangladesh. Tulifika huko Desemba 1977. Haikuwa rahisi kuhubiri katika nchi hii pia. Hata hivyo, sikuzote tulikumbuka kwamba lazima tuendelee kuhubiri. Kupitia mwongozo wa roho ya Yehova, tuliweza kupata familia nyingi zilizodai kuwa za Kikristo. Baadhi ya familia hizo zilikuwa na kiu ya maji yenye kuburudisha ya kweli inayopatikana katika Maandiko Matakatifu. (Isaya 55:1) Kwa sababu hiyo, tulianzisha mafunzo mengi ya Biblia.

Tulikumbuka kuwa mapenzi ya Mungu ni kwamba “watu wa namna zote waokolewe.” (1 Timotheo 2:4) Jambo la kufurahisha ni kwamba hakuna aliyejaribu kututatiza. Ili kushinda ubaguzi wowote, tulihakikisha kwamba tunazungumza na watu kwa urafiki sana. Kama mtume Paulo, tulijaribu ‘kuwa mambo yote kwa watu wa namna zote.’ (1 Wakorintho 9:22) Tulipoulizwa sababu ya ziara yetu, tuliwajibu kwa fadhili, na tuliona kuwa wengi wao walikuwa wenye urafiki sana.

Huko Dhaka, tulipata mwanamke mmoja Shahidi aliyekuwa mwenyeji na tukamtia moyo ajiunge nasi katika mikutano yetu ya Kikristo na baadaye katika kazi ya kuhubiri. Naye mke wangu alijifunza Biblia pamoja na familia fulani na kuwaalika wahudhurie mikutano yetu. Kupitia fadhili zenye upendo za Yehova, familia yote ilikubali kweli. Baadaye, binti zao wawili walisaidia kutafsiri vichapo vya Biblia katika lugha ya Bengali, na pia watu wao wengi wa ukoo walipata kumjua Yehova. Wanafunzi wengine wengi wa Biblia walikubali kweli. Wengi wao sasa ni wazee au mapainia.

Kwa kuwa Dhaka ni jiji lenye watu wengi, tulikaribisha baadhi ya washiriki wa familia yetu watusaidie kuhubiri. Wengi wao walikubali nao wakajiunga nasi huko Bangladesh. Tunafurahi na kumshukuru Yehova kama nini kwa nafasi tuliyopata ya kushiriki kuhubiri habari njema katika nchi hiyo! Kutoka mwanzo huo mdogo wa mtu mmoja, sasa kuna makutaniko mawili huko Bangladesh.

Mnamo Julai 1982, ilitubidi kufunga virago na kuondoka Bangladesh. Tulilia kwa kuwaacha ndugu hao. Muda mfupi baadaye, niliajiriwa katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Entebbe, Uganda, ambako tungekaa kwa miaka minne na miezi saba. Tungefanya nini ili kuliheshimu jina kuu la Yehova katika nchi hiyo?

Kumtumikia Yehova Afrika Mashariki

Tulipofika kwenye Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Entebbe, dereva fulani alinichukua mimi pamoja na mke wangu na kutupeleka mahali ambapo tungeishi. Tulipokuwa tukiondoka kwenye uwanja huo nilianza kumhubiria dereva huyo kuhusu Ufalme wa Mungu. Aliniuliza: “Je, wewe ni mmoja wa Mashahidi wa Yehova?” Nilipojibu ndiyo, dereva huyo alisema: “Mmoja wa ndugu zenu anafanya kazi kwenye mnara wa kuongozea ndege.” Mara moja, nikamwomba anipeleke huko. Tulikutana na ndugu huyo ambaye alifurahi sana kutuona, na mipango ikafanywa kwa ajili ya mikutano na utumishi wa shambani.

Wakati huo kulikuwa na wahubiri wa Ufalme 228 tu nchini Uganda. Tukiwa pamoja na ndugu wawili huko Entebbe, tulitumia mwaka wetu wa kwanza kupanda mbegu za kweli. Kwa kuwa watu wa huko wanapenda kusoma, tuliwaachia vichapo vingi kutia ndani mamia ya magazeti. Tuliwaalika akina ndugu kutoka Kampala, mji mkuu, waje kutusaidia kuhubiri eneo la Entebbe mwisho-juma. Nilipotoa hotuba ya watu wote mara ya kwanza, kulikuwa na hudhurio la watu watano kutia ndani mimi.

Katika miaka mitatu iliyofuata, tulipata furaha nyingi sana maishani kuona watu tuliojifunza nao wakiitikia na kufanya maendeleo haraka. (3 Yohana 4) Kwenye kusanyiko moja la mzunguko, watu sita tuliokuwa tukijifunza Biblia nao walibatizwa. Wengi wao walisema kwamba walitiwa moyo kuwa watumishi wa wakati wote kwa sababu waliona tukifanya upainia hata ingawa tulifanya kazi ya kimwili ya wakati wote.

Tulitambua kwamba mahali petu pa kazi pangeweza pia kuwa eneo lenye matokeo. Pindi moja, nilizungumza na ofisa mmoja wa wazima-moto katika uwanja wa ndege na kumweleza kuhusu tumaini la Biblia la kuishi milele katika paradiso duniani. Nilimwonyesha katika Biblia yake kwamba wanadamu watiifu wataishi kwa amani na umoja, bila umaskini, ukosefu wa makao, vita, magonjwa, au kifo. (Zaburi 46:9; Isaya 33:24; 65:21, 22; Ufunuo 21:3, 4) Alipendezwa sana kusoma habari hizo katika Biblia yake mwenyewe. Funzo la Biblia lilianzishwa mara moja. Alihudhuria mikutano yote. Baada ya muda mfupi alijiweka wakfu kwa Yehova na kubatizwa. Baadaye, alijiunga nasi katika huduma ya wakati wote.

Vita vya wenyewe kwa wenyewe vilizuka mara mbili Uganda tulipokuwa huko, lakini hilo halikukomesha kazi yetu ya kiroho. Familia za watu waliofanya kazi katika mashirika ya kimataifa zilihamishwa hadi Nairobi, Kenya, kwa miezi sita. Sisi tuliobaki Uganda tuliendelea na mikutano yetu ya Kikristo na kazi ya kuhubiri, ingawa tulihitaji kuwa wenye busara na waangalifu.

Mnamo Aprili 1988, kazi yangu iliisha nasi tukahama tena. Tuliondoka katika Kutaniko la Entebbe huku tukiwa tumeridhika sana kwa sababu ya ukuzi wa kiroho uliokuwako. Mnamo Julai 1997, tulipata nafasi ya kutembelea Entebbe tena. Kufikia wakati huo, baadhi ya watu tuliojifunza nao Biblia walikuwa wakitumikia wakiwa wazee. Tulifurahi sana kuona watu 106 waliohudhuria Mkutano wa Watu Wote.

Kuhamia Eneo Ambalo Halijahubiriwa

Je, tungeweza kupata nafasi ya kuhubiri maeneo yasiyohubiriwa? Naam, nilipelekwa kufanya kazi kwenye Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Mogadishu, Somalia. Tuliazimia kutumia vizuri nafasi hiyo kutumikia katika eneo lisilohubiriwa.

Tulihubiria hasa wafanyakazi wa ubalozi, wafanyakazi Wafilipino, na wageni wengine. Mara nyingi tulikutana nao sokoni. Pia tuliwatembelea nyumbani kwao. Kwa kutumia ustadi, ubunifu, busara, na kumtegemea Yehova kabisa, tuliweza kuwahubiria wengine kweli za Biblia na jambo hilo lilikuwa na matokeo mazuri miongoni mwa watu wa mataifa mbalimbali. Baada ya miaka miwili, tuliondoka Mogadishu, kabla tu ya vita kuanza.

Kisha Shirika la Kimataifa la Safari za Ndege za Abiria lilituhamisha hadi Yangon, Myanmar. Huko pia tulipata nafasi za kusaidia watu wenye mioyo minyoofu wajifunze makusudi ya Mungu. Baada ya kutoka Myanmar, tulipelekwa Dar es Salaam, Tanzania. Ilikuwa rahisi zaidi kuhubiri nyumba kwa nyumba huko Dar es Salaam kwa sababu kulikuwa na watu waliozungumza Kiingereza.

Katika nchi zote ambako tulifanya kazi, tulipata matatizo machache sana katika huduma yetu, ingawa mara nyingi kazi ya Mashahidi wa Yehova ilikuwa imezuiliwa. Kwa sababu ya kazi yangu ambayo kwa kawaida ilihusiana na serikali au mashirika ya kimataifa, watu hawakutilia shaka kazi yetu.

Kazi yangu ya kimwili ilifanya mimi na mke wangu tuishi maisha ya kuhama-hama kwa miaka 30. Hata hivyo, tuliona kazi yangu kuwa njia tu ya kutimiza lengo letu kuu. Sikuzote lengo letu la kwanza lilikuwa kuendeleza Ufalme wa Mungu. Tunamshukuru Yehova kwa kutusaidia kutumia vizuri hali zetu zenye kubadilika na kufurahia pendeleo kubwa la kueneza habari njema katika maeneo ya mbali.

Twarudi Tulikotoka

Niliamua kustaafu mapema nikiwa na umri wa miaka 58 na kurudi Filipino. Tuliporudi, tulisali kwa Yehova aongoze hatua zetu. Tulianza kutumikia katika kutaniko la Trece Martires City, katika wilaya ya Cavite. Tulipofika huko mara ya kwanza, kulikuwa na watangazaji wa Ufalme wa Mungu 19 tu. Mipango ya kuhubiri kila siku ilifanywa, na mafunzo mengi ya Biblia yakaanzishwa. Kutaniko likaanza kukua. Pindi moja mke wangu alikuwa na mafunzo ya Biblia ya nyumbani 19, nami nilikuwa na 14.

Baada ya muda, Jumba la Ufalme likawa dogo. Tulisali kwa Yehova kuhusu jambo hilo. Ndugu fulani wa kiroho na mke wake waliamua kutoa uwanja, nayo ofisi ya tawi ikatoa mkopo wa kujenga Jumba jipya la Ufalme. Kumekuwa na matokeo makubwa katika kazi ya kuhubiri baada ya kujengwa kwa jumba hilo jipya, nalo hudhurio limekuwa likiongezeka kila juma. Kwa sasa, sisi husafiri muda wa zaidi ya saa mbili kwenda na kurudi ili kusaidia kutaniko lingine lenye wahubiri 17.

Mimi na mke wangu tunathamini pendeleo ambalo tumekuwa nalo la kutumikia katika nchi nyingi tofauti-tofauti. Tunapokumbuka maisha yetu ya kuhama-hama, tunaridhika sana kwamba tuliyatumia vizuri kabisa, yaani, kuwasaidia wengine wajifunze kumhusu Yehova.

[Ramani katika ukurasa wa 24, 25]

(Ona mpangilio kamili katika nakala iliyochapishwa)

TANZANIA

UGANDA

SOMALIA

IRAN

BANGLADESH

MYANMAR

LAOS

THAILAND

FILIPINO

[Picha katika ukurasa wa 23]

Nikiwa na mke wangu, Aurea