Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kipimo Fulani cha “Pimu” Chathibitisha Kwamba Biblia Ni Sahihi Kihistoria

Kipimo Fulani cha “Pimu” Chathibitisha Kwamba Biblia Ni Sahihi Kihistoria

Kipimo Fulani cha “Pimu” Chathibitisha Kwamba Biblia Ni Sahihi Kihistoria

NENO “pimu” hupatikana mara moja tu katika Biblia. Katika siku za Mfalme Sauli, iliwabidi Waisraeli kwenda kunoa vifaa vyao vya chuma kwa wafua-vyuma Wafilisti. Biblia inasema hivi: “Bei ya kunoa ikawa ni pimu moja kwa majembe na kwa majembetezo na kwa vifaa vyenye meno matatu na kwa mashoka na kwa kuimarisha mchokoo wa ng’ombe.”—1 Samweli 13:21.

Pimu ilikuwa nini? Jibu la swali hilo liliendelea kuwa fumbo hadi mwaka wa 1907 W.K. wakati jiwe la kwanza la pimu la kupimia uzito lilipopatikana katika jiji la kale la Gezeri. Watafsiri wa Biblia wa nyakati za kale walitatizika kutafsiri neno “pimu.” Kwa mfano, tafsiri ya Union Version ilitafsiri 1 Samweli 13:21 hivi: “Ila walikuwa na tupa za kunolea sululu, na miundu, na mauma, na mashoka; na kwa kuinoa michokoo.”

Leo wasomi wanajua kwamba pimu ilikuwa kipimo cha uzito wa wastani wa gramu 7.82, au yapata sehemu mbili ya tatu ya shekeli, ambayo ilikuwa kipimo cha uzito cha kawaida kilichotumiwa na Waebrania. Wafilisti waliwatoza Waisraeli mabaki ya chuma yenye uzito wa pimu moja kama malipo ya kuwanolea vifaa vyao. Kipimo cha shekeli kiliacha kutumiwa wakati ufalme wa Yuda na mji wake mkuu, Yerusalemu, ulipoharibiwa mwaka wa 607 K.W.K. Kwa hiyo, kipimo cha pimu kinathibitishaje kwamba maandishi ya Kiebrania ni sahihi kihistoria?

Wasomi fulani hudai kwamba maandishi ya Maandiko ya Kiebrania, kutia ndani kitabu cha Samweli wa Kwanza, yaliandikwa katika enzi ya Wagiriki na Waroma, au hata yaliandikwa baadaye kuanzia karne ya pili na ya kwanza K.W.K. Kwa hiyo, inadaiwa kwamba “maandishi hayo . . . ‘si ya kihistoria,’ hayawezi kutoa habari ya kweli ya kihistoria kuhusu taifa la Israeli linalotajwa katika Biblia au ‘Israeli la kale,’ ambalo limebuniwa na waandikaji wa vichapo vya Wayahudi na Wakristo tu.”

Hata hivyo, akirejelea kipimo cha pimu kinachotajwa katika 1 Samweli 13:21, William G. Dever, profesa wa akiolojia na anthropolojia wa Mashariki ya Karibu, anasema: “Haiwezekani kwamba taifa hilo ‘lilibuniwa’ na waandikaji walioishi katika enzi ya Wagiriki na Waroma karne nyingi baada ya vipimo hivyo kutoweka na kusahauliwa. Kwa kweli, sehemu hii ndogo ya maandishi ya Biblia . . . haingeeleweka hadi mapema katika karne ya 20 W.K., wakati baadhi ya vitu vya kwanza kuvumbuliwa vilipopatikana vikiwa na neno la Kiebrania pîm.” Profesa huyo anaendelea kusema: “Ikiwa hadithi zote za Biblia ‘zimebuniwa na waandikaji’ walioishi katika enzi ya Wagiriki na Waroma, simulizi hili lilipataje kuwa katika Biblia ya Kiebrania? Bila shaka, huenda mtu akakanusha kwamba kuvumbuliwa kwa pîm ni ‘jambo dogo tu.’ Hiyo ni kweli; lakini inajulikana kwamba ‘historia hufanyizwa na mambo madogo-madogo.’”

[Picha katika ukurasa wa 29]

Kipimo cha uzito cha pimu moja kilikuwa sehemu mbili ya tatu hivi ya shekeli