Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kuishi Si Kwa Ajili Yetu Wenyewe Tena

Kuishi Si Kwa Ajili Yetu Wenyewe Tena

Kuishi Si Kwa Ajili Yetu Wenyewe Tena

“[Kristo] alikufa kwa ajili ya wote ili wale wanaoishi wasiishi tena kwa ajili yao wenyewe.”—2 WAKORINTHO 5:15.

1, 2. Ni amri gani ya Kimaandiko iliyowachochea wafuasi wa Yesu wa karne ya kwanza kushinda ubinafsi?

ULIKUWA usiku wa mwisho wa Yesu hapa duniani. Baada ya saa chache tu angetoa uhai wake kwa ajili ya wote ambao wangemwamini. Katika usiku huo, Yesu aliwaambia mitume wake waaminifu mambo mengi muhimu. Kati ya mambo hayo, aliwapa amri kuhusu sifa fulani ambayo ingewatambulisha kuwa wafuasi wake. “Ninawapa ninyi amri mpya,” akasema, “kwamba mpendane; kama vile ambavyo nimewapenda ninyi, ninyi nanyi mpendane vivyo hivyo. Kwa jambo hili wote watajua kwamba ninyi ni wanafunzi wangu, mkiwa na upendo kati yenu wenyewe.”—Yohana 13:34, 35.

2 Wakristo wa kweli wanapaswa kuonyeshana upendo wa kujidhabihu na kutanguliza mahitaji ya waamini wenzao. Hawapaswi kusita hata ‘kutoa nafsi yao kwa ajili ya rafiki zao.’ (Yohana 15:13) Wakristo wa mapema waliitikiaje amri hiyo mpya? Katika kitabu chake kinachojulikana sana, Apology, mwandishi wa karne ya pili Tertullian alinukuu mambo ambayo wengine walisema kuhusu Wakristo: ‘Ona jinsi wanavyopendana na jinsi walivyo tayari kufa kwa ajili ya mmoja na mwenzake.’

3, 4. (a) Kwa nini tunapaswa kushinda ubinafsi? (b) Tutazungumzia mambo gani katika makala hii?

3 Sisi pia tunapaswa ‘kuendelea kubebeana mizigo mizito, na hivyo kuitimiza sheria ya Kristo.’ (Wagalatia 6:2) Hata hivyo, ubinafsi ni mojawapo ya mambo makubwa zaidi ambayo hutuzuia kutii sheria ya Kristo na ‘kumpenda Yehova Mungu wetu kwa moyo wetu wote, nafsi, na akili na kuwapenda jirani kama sisi wenyewe.’ (Mathayo 22:37-39) Kwa kuwa sisi ni watu wasio wakamilifu, tuna mwelekeo wa kuwa na ubinafsi. Mwelekeo huo wa asili huongezeka kwa sababu ya mikazo ya maisha ya kila siku, roho ya kushindana shuleni au kazini, na jitihada za kupata mahitaji ya lazima. Mwelekeo huo wa ubinafsi unaongezeka. Mtume Paulo alionya hivi: “Katika siku za mwisho . . . watu watakuwa na ubinafsi.”—2 Timotheo 3:1, 2, BHN.

4 Alipokaribia kumaliza huduma yake duniani, Yesu aliwaonyesha wanafunzi wake hatua tatu ambazo zingeweza kuwasaidia kushinda ubinafsi. Hatua hizo zilikuwa zipi, na maagizo yake yanaweza kutunufaishaje?

Suluhisho Lenye Matokeo!

5. Alipokuwa akihubiri kaskazini mwa Galilaya, Yesu aliwafunulia wanafunzi wake habari gani, na kwa nini habari hiyo iliwashtua?

5 Yesu alikuwa akihubiri karibu na Kaisaria Filipi, kaskazini mwa Galilaya. Huenda ikawa eneo hilo tulivu na maridadi lilionekana kuwa linafaa kuwa mahali pa kujistarehesha badala ya mahali pa kujifunza jinsi ya kujinyima. Hata hivyo, akiwa huko, Yesu alianza kuwafunulia wanafunzi wake kwamba “lazima aende Yerusalemu na kupatwa na mambo mengi kutoka kwa wanaume wazee na wakuu wa makuhani na waandishi, na kuuawa, na siku ya tatu afufuliwe.” (Mathayo 16:21) Lazima habari hiyo mpya iwe iliwashtua sana wanafunzi wa Yesu kwa kuwa kufikia wakati huo walikuwa wakitarajia Kiongozi wao asimamishe Ufalme wake duniani.—Luka 19:11; Matendo 1:6.

6. Kwa nini Yesu alimkemea Petro vikali?

6 Mara moja Petro “akamchukua [Yesu] kando na kuanza kumkemea, akisema: ‘Jitendee kwa fadhili, Bwana; wewe hutapatwa hata kidogo na jambo hili.’” Yesu aliitikiaje? ‘Akimgeuzia mgongo wake, alimwambia Petro: “Nenda nyuma yangu, Shetani! Wewe ni kikwazo kwangu, kwa sababu wewe unafikiri, si fikira za Mungu, bali za wanadamu.”’ Mitazamo hiyo miwili ilitofautiana sana. Yesu alikubali kwa hiari maisha ya kujidhabihu ambayo Mungu alitaka aishi, yaani, maisha ambayo yangeongoza kwenye kifo chake juu ya mti wa mateso miezi michache baadaye. Petro alipendekeza maisha ya starehe. Alisema: “Jitendee kwa fadhili.” Bila shaka, Petro alikuwa na nia nzuri. Hata hivyo, Yesu alimkemea kwa sababu pindi hiyo Petro alijiacha aongozwe na Shetani. Petro hakuwa na “fikira za Mungu, bali za wanadamu.”—Mathayo 16:22, 23.

7. Kama inavyoonyeshwa katika Mathayo 16:24, ni hatua gani ambayo Yesu aliwatajia wafuasi wake wafuate?

7 Maneno kama yale ambayo Petro alimwambia Yesu yanaweza kusikiwa leo. Mara nyingi ulimwengu humhimiza mtu ‘ajihurumie’ au ‘afuatilie maisha rahisi.’ Kwa upande mwingine, Yesu alipendekeza mtazamo wa akili ulio tofauti kabisa na huo. Aliwaambia hivi wanafunzi wake: “Mtu yeyote akitaka kunifuata, na ajikane mwenyewe na kuuchukua mti wake wa mateso na kunifuata sikuzote.” (Mathayo 16:24) Kichapo The New Interpreter’s Bible, kinasema: “Maneno hayo hayakuandikiwa watu ambao hawakuwa bado wanafunzi. Bali yaliandikiwa wale ambao tayari walikuwa wameitikia mwito wa Kristo ili watafakari maana ya kuwa mwanafunzi.” Waamini wanapaswa kufuata hatua tatu ambazo Yesu alitaja katika andiko hilo. Na tuchunguze hatua hizo moja baada ya nyingine.

8. Eleza maana ya kujikana mwenyewe.

8 Kwanza, tunapaswa kujikana wenyewe. Neno la Kigiriki linalomaanisha ‘kujikana mwenyewe’ linaonyesha utayari wa kukataa tamaa au mapendezi ya kibinafsi. Kujikana wenyewe si kukataa tu raha fulani kwa muda; wala hakumaanishi kujinyima raha kabisa au kujiingiza katika raha kupita kiasi. Sisi si ‘mali yetu wenyewe’ tena katika maana ya kwamba tunatoa kwa hiari maisha yetu yote na kila kitu kwa Yehova. (1 Wakorintho 6:19, 20) Badala ya kuishi maisha ya ubinafsi, tunatumia maisha yetu kumtumikia Mungu. Kujikana wenyewe kunamaanisha kuazimia kufanya mapenzi ya Mungu, hata ingawa huenda kufanya hivyo kukawa kinyume cha yale ambayo kwa kawaida tungependa kufanya. Sisi huonyesha kwamba tumejitoa kabisa kwa Mungu tunapojiweka wakfu kwake na kubatizwa. Kisha tunajitahidi kuishi kupatana na wakfu wetu muda wote wa maisha yetu.

9. (a) Mti wa mateso uliwakilisha nini Yesu alipokuwa duniani? (b) Sisi huuchukua mti wetu wa mateso katika njia gani?

9 Hatua ya pili ni kwamba tunapaswa kuuchukua mti wetu wa mateso. Katika karne ya kwanza, mti wa mateso uliwakilisha mateso, aibu, na kifo. Kwa kawaida, wahalifu tu ndio waliouawa kwenye mti wa mateso au miili yao kutundikwa kwenye mti. Kwa maneno hayo, Yesu alionyesha kwamba lazima Mkristo awe tayari kuteswa, kudharauliwa, au hata kufa, kwa kuwa yeye si sehemu ya ulimwengu. (Yohana 15:18-20) Viwango vyetu vya Kikristo hufanya tuwe tofauti na watu wengine, kwa hiyo huenda ulimwengu ‘ukatutukana.’ (1 Petro 4:4) Jambo hilo linaweza kutokea shuleni, kazini, au hata katika familia. (Luka 9:23) Hata hivyo, tuko tayari kudharauliwa na ulimwengu kwa sababu hatuishi kwa ajili yetu wenyewe tena. Yesu alisema: “Wenye furaha ni ninyi wakati watu wanapowashutumu na kuwatesa na kusema kwa uwongo kila namna ya jambo baya juu yenu kwa ajili yangu. Shangilieni na kuruka kwa shangwe, kwa kuwa thawabu yenu ni kubwa mbinguni.” (Mathayo 5:11, 12) Kwa kweli, jambo muhimu ni kupata kibali cha Mungu.

10. Ni nini kinachohusika katika kumfuata Yesu sikuzote?

10 Tatu, Yesu Kristo alisema kwamba tunapaswa kumfuata sikuzote. Kulingana na kichapo An Expository Dictionary of New Testament Words, cha W. E. Vine, neno la Kigiriki linalotafsiriwa “kufuata” linamaanisha kuwa mwandamani, yaani, “mtu anayeelekea upande uleule.” Andiko la 1 Yohana 2:6 linasema: “Yeye anayesema kwamba anakaa katika muungano na [Mungu] yuko chini ya wajibu yeye mwenyewe pia kuendelea kutembea kama vile huyo [Kristo] alivyotembea.” Yesu alitembeaje? Yesu hakuwa na ubinafsi kwa kuwa alimpenda Baba yake wa mbinguni na wanafunzi wake. “Kristo hakujipendeza mwenyewe,” akaandika Paulo. (Waroma 15:3) Hata alipochoka au kuhisi njaa, Yesu alitanguliza mahitaji ya wengine. (Marko 6:31-34) Pia Yesu alijitahidi sana katika kazi ya kuhubiri na kufundisha Ufalme. Je, hatupaswi kumwiga tunapotimiza kwa bidii kazi yetu ya ‘kufanya wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote, tukiwafundisha kushika mambo yote ambayo Yesu ameamuru’? (Mathayo 28:19, 20) Kupitia mwenendo wake, Kristo alituachia kielelezo, nasi tunapaswa ‘kufuata hatua zake kwa ukaribu.’—1 Petro 2:21.

11. Kwa nini ni muhimu kujikana wenyewe, kuuchukua mti wetu wa mateso, na kumfuata Yesu Kristo sikuzote?

11 Ni muhimu kujikana wenyewe, kuuchukua mti wetu wa mateso, na kufuata Kielelezo chetu sikuzote. Kufanya hivyo ni suluhisho la kushinda ubinafsi ambao kwa kweli hutuzuia kuonyesha upendo wa kujidhabihu. Isitoshe, Yesu alisema: “Yeyote yule anayetaka kuiokoa nafsi yake ataipoteza; lakini yeyote yule anayeipoteza nafsi yake kwa ajili yangu ataipata. Kwa maana mtu atapata faida gani akiupata ulimwengu wote lakini aipoteze nafsi yake? au mtu atatoa nini ili aipate nafsi yake?”—Mathayo 16:25, 26.

Hatuwezi Kuwatumikia Mabwana Wawili

12, 13. (a) Ni nini lililokuwa hangaiko la mtawala kijana aliyemwomba Yesu shauri? (b) Yesu alimpa kijana huyo shauri gani, na kwa nini?

12 Miezi kadhaa baada ya Yesu kukazia umuhimu wa wanafunzi wake kujikana wenyewe, mtawala mmoja kijana aliyekuwa tajiri alimfikia na kusema: “Mwalimu, nifanye wema gani ili niupate uzima wa milele?” Yesu alimwambia ‘azishike amri sikuzote’ kisha akanukuu baadhi ya amri hizo. Kijana huyo akasema: “Nimeyashika yote hayo.” Yaonekana kwamba mtu huyo alikuwa mnyoofu naye alikuwa amefanya yote awezayo kutii amri za Sheria. Kwa hiyo akauliza: “Ni nini bado ninachokosa?” Yesu alimjibu mwanamume huyo kijana kwa kumpa mwaliko huu wa pekee: “Ikiwa unataka kuwa mkamilifu [“kamili,” New American Standard Bible], nenda ukauze mali zako na uwape maskini nawe utakuwa na hazina mbinguni, kisha uje uwe mfuasi wangu.”—Mathayo 19:16-21.

13 Yesu aliona kwamba ili kijana huyo amtumikie Yehova kwa nafsi yote, alipaswa kuacha kikengeusha-fikira kikubwa maishani mwake, yaani, mali yake. Mwanafunzi wa kweli wa Kristo hawezi kuwatumikia mabwana wawili. Hawezi “kutumikia Mungu na Utajiri.” (Mathayo 6:24) Anahitaji kuwa na ‘jicho rahisi’ ambalo linakazwa kwenye mambo ya kiroho. (Mathayo 6:22) Kuwapa maskini vitu vyako ni tendo la kujidhabihu. Ikiwa mtawala huyo kijana angedhabihu mali zake, Yesu angempa pendeleo kubwa sana la kujiwekea hazina mbinguni, hazina ambayo ingemaanisha kwamba angepata uzima wa milele na mwishowe awe na tumaini la kutawala pamoja na Kristo mbinguni. Kijana huyo hakuwa tayari kujikana mwenyewe. ‘Alienda zake akiwa amehuzunika, kwa maana alikuwa na mali nyingi.’ (Mathayo 19:22) Hata hivyo, wafuasi wengine wa Yesu waliitikia kwa njia tofauti.

14. Wavuvi wanne waliitikiaje mwaliko wa Yesu wa kumfuata?

14 Miaka miwili hivi mapema, Yesu alikuwa amewapa mwaliko huo wavuvi wanne walioitwa Petro, Andrea, Yakobo, na Yohana. Wakati huo, wawili kati yao walikuwa wakivua, na wale wengine walikuwa wakishona nyavu zao. Yesu aliwaambia: “Nifuateni, nami nitawafanya ninyi kuwa wavuvi wa watu.” Mwishowe wote wanne wakaacha biashara yao ya uvuvi na kumfuata Yesu muda wote wa maisha yao.—Mathayo 4:18-22.

15. Shahidi mmoja wa Yehova wa kisasa alijidhabihu jinsi gani ili kumfuata Yesu?

15 Wakristo wengi leo wameiga kielelezo cha wale wavuvi wanne badala ya kielelezo cha yule mtawala kijana aliyekuwa tajiri. Wamedhabihu utajiri na nafasi ya kuwa watu mashuhuri katika ulimwengu huu ili wamtumikie Yehova. “Nilipokuwa na umri wa miaka 22, ilinibidi kufanya uamuzi mkubwa,” asema Deborah. Anaeleza: “Nilikuwa nimejifunza Biblia kwa miezi sita hivi, nami nilitaka kuweka maisha yangu wakfu kwa Yehova, lakini familia yangu ilinipinga sana. Walikuwa matajiri sana, nao walihisi kwamba ningewaaibisha kwa kuwa Shahidi. Walinipa muda wa saa 24 niamue nilichotaka—maisha ya anasa au kweli. Kama singeacha kushirikiana kabisa na Mashahidi, familia yangu ingeninyima urithi. Yehova alinisaidia kufanya uamuzi unaofaa na kunipa nguvu za kuutekeleza. Kufikia sasa nimekuwa katika utumishi wa wakati wote kwa miaka 42, na sijuti hata kidogo. Kwa kukataa maisha ya ubinafsi na ya starehe, niliepuka kuwa na maisha yasiyo na kusudi na yasiyo na furaha ambayo washiriki wa familia yetu wanaishi. Mimi na mume wangu tumesaidia zaidi ya watu 100 kujifunza kweli. Watoto hao wa kiroho ni wenye thamani zaidi kwangu kuliko mali.” Mamilioni ya Mashahidi wengine wa Yehova wanakubaliana naye. Namna gani wewe?

16. Tunaweza kuonyeshaje kwamba hatuishi kwa ajili yetu wenyewe tena?

16 Tamaa ya kutoishi kwa ajili yao wenyewe tena imewachochea maelfu ya Mashahidi wa Yehova kutumikia wakiwa mapainia, au watangazaji wa Ufalme wa wakati wote. Wengine ambao hali zao haziwaruhusu kuwa katika huduma ya wakati wote, wanasitawisha roho ya upainia na kutegemeza kazi ya kuhubiri Ufalme kadiri wawezavyo. Wazazi huonyesha roho hiyohiyo wanapotumia wakati wao mwingi nao hudhabihu mapendezi yao ili kuwazoeza watoto wao kiroho. Katika njia fulani, sisi sote tunaweza kuonyesha kwamba tunatanguliza Ufalme maishani mwetu.—Mathayo 6:33.

Ni Upendo wa Nani Unaotulazimisha?

17. Ni nini hutuchochea kujidhabihu?

17 Si rahisi kuonyesha upendo wa kujidhabihu maishani. Lakini fikiria jambo linalotuchochea. Paulo aliandika hivi: “Upendo alio nao Kristo hutulazimisha, kwa sababu hili ndilo tumehukumu, kwamba mtu mmoja alikufa kwa ajili ya wote . . . Naye alikufa kwa ajili ya wote ili wale wanaoishi wasiishi tena kwa ajili yao wenyewe, bali kwa ajili ya yeye aliyekufa kwa ajili yao na kufufuliwa.” (2 Wakorintho 5:14, 15) Upendo wa Kristo ndio hutulazimisha tusiishi kwa ajili yetu wenyewe tena. Hicho ni kichocheo kikubwa kama nini! Kwa kuwa Kristo alikufa kwa ajili yetu, je, hatuoni kwamba tuna daraka la kuishi kwa ajili yake? Kwa kweli, kuthamini upendo wenye kina ambao Mungu na Kristo wametuonyesha kulitulazimisha kuweka maisha yetu wakfu kwa Mungu na kuwa wanafunzi wa Kristo.—Yohana 3:16; 1 Yohana 4:10, 11.

18. Kwa nini maisha ya kujidhabihu ni yenye manufaa?

18 Je, kuna manufaa yoyote ya kuishi si kwa ajili yetu wenyewe tena? Baada ya yule mtawala kijana aliyekuwa tajiri kukataa mwaliko wa Kristo na kwenda zake, Petro alimwambia Yesu hivi: “Tazama! Tumeacha vitu vyote na kukufuata wewe; kwa kweli kutakuwa na nini kwa ajili yetu?” (Mathayo 19:27) Kwa kweli, Petro na mitume wengine walikuwa wamejikana wenyewe. Wangepata thawabu gani? Kwanza Yesu alitaja pendeleo ambalo wangekuwa nalo la kutawala pamoja naye mbinguni. (Mathayo 19:28) Pindi hiyohiyo, Yesu alitaja baraka ambazo kila mmoja wa wafuasi wake angepata. Alisema: “Hakuna mtu ambaye ameacha nyumba au ndugu au dada au mama au baba au watoto au mashamba kwa ajili yangu na kwa ajili ya habari njema ambaye hatapata mara mia sasa katika kipindi hiki cha wakati . . . na katika mfumo wa mambo unaokuja uzima wa milele.” (Marko 10:29, 30) Tunapata mengi zaidi kuliko yale tuliyodhabihu. Je, baba, mama, ndugu, dada, na watoto wetu wa kiroho si wenye thamani zaidi kuliko kitu chochote ambacho tumeacha kwa ajili ya Ufalme? Ni nani aliyekuwa na maisha yenye kuthawabisha zaidi—Petro au yule mtawala kijana aliyekuwa tajiri?

19. (a) Furaha ya kweli hutegemea nini? (b) Tutazungumzia nini katika makala inayofuata?

19 Kwa maneno na matendo yake, Yesu alionyesha kwamba furaha hutokana na kutoa na kuwatumikia wengine bali si kuwa na ubinafsi. (Mathayo 20:28; Matendo 20:35) Tunapoacha kuishi si kwa ajili yetu wenyewe tena bali kumfuata Kristo sikuzote, tunapata uradhi mkubwa maishani sasa na kuwa na taraja la kuishi milele wakati ujao. Bila shaka, tunapojikana wenyewe, Yehova anakuwa Mmiliki wetu. Hivyo tunakuwa watumwa wa Mungu. Kwa nini utumwa huo huthawabisha? Unaathirije maamuzi tunayofanya maishani? Maswali hayo yatazungumziwa katika makala inayofuata.

Je, Unakumbuka?

• Kwa nini tunapaswa kupinga mwelekeo wetu wa kuwa na ubinafsi?

• Inamaanisha nini kujikana wenyewe, kuuchukua mti wetu wa mateso, na kumfuata Yesu sikuzote?

• Ni nini hutuchochea kuishi si kwa ajili yetu wenyewe tena?

• Kwa nini inanufaisha kuishi maisha ya kujidhabihu?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 11]

“Jitendee kwa fadhili, Bwana”

[Picha katika ukurasa wa 13]

Ni nini kilichomzuia yule mtawala kijana asimfuate Yesu?

[Picha katika ukurasa wa 15]

Upendo huwachochea Mashahidi wa Yehova kutumikia wakiwa watangazaji wa Ufalme wenye bidii