Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Mambo Makuu Katika Kitabu cha Samweli wa Kwanza

Mambo Makuu Katika Kitabu cha Samweli wa Kwanza

Neno la Yehova Liko Hai

Mambo Makuu Katika Kitabu cha Samweli wa Kwanza

NI MWAKA wa 1117 K.W.K. Miaka 300 hivi imepita tangu Yoshua akamilishe ushindi wa Nchi ya Ahadi. Wanaume wazee wa Israeli wanamjia nabii wa Yehova wakiwa na ombi lisilo la kawaida. Nabii huyo anasali kuhusu jambo hilo, naye Yehova anakubali ombi lao. Hilo linaonyesha wazi mwisho wa kipindi cha Waamuzi na mwanzo wa enzi ya wafalme wa kibinadamu. Kitabu cha Biblia cha Samweli wa Kwanza kinaeleza matukio yenye kusisimua yanayotukia katika kipindi hicho muhimu cha badiliko katika historia ya taifa la Israeli.

Kitabu cha Samweli wa Kwanza kiliandikwa na Samweli, Nathani, na Gadi, nacho kinazungumzia mambo yaliyotukia katika kipindi cha miaka 102, tangu 1180 K.W.K. hadi 1078 K.W.K. (1 Mambo ya Nyakati 29:29) Ni masimulizi kuhusu viongozi wanne wa Israeli. Wawili ni waamuzi, wawili ni wafalme; wawili wanamtii Yehova, na wawili hawamtii. Kinatueleza pia kuhusu wanawake wawili ambao ni vielelezo vizuri na pia shujaa wa vita aliye jasiri lakini mpole. Vielelezo hivyo hutufundisha mambo muhimu kuhusu mitazamo na matendo tunayopaswa kuiga na yale tunayopaswa kuepuka. Hivyo, mambo yanayotajwa katika Samweli wa Kwanza yanaweza kuwa na uvutano juu ya matendo na mwenendo wetu.—Waebrania 4:12.

SAMWELI ACHUKUA NAFASI YA ELI AKIWA MWAMUZI

(1 Samweli 1:1–7:17)

Ni wakati wa Sherehe ya Kukusanya, naye Hana, ambaye anaishi Rama ana furaha nyingi. * Yehova amejibu sala zake, naye amezaa mwana. Ili kutimiza nadhiri yake, Hana anampeleka mwana wake Samweli akatumikie kwenye “nyumba ya Yehova.” Huko, mvulana huyo anakuwa “mhudumu wa Yehova mbele ya Eli kuhani.” (1 Samweli 1:24; 2:11) Samweli akiwa bado mchanga sana, Yehova anazungumza naye na kutoa hukumu dhidi ya nyumba ya Eli. Samweli anapozeeka, watu wote wa Israeli wanatambua kwamba yeye ni nabii wa Yehova.

Mwishowe, Wafilisti wanashambulia Israeli. Wanalichukua Sanduku na kuwauwa wana wawili wa Eli. Anapopata habari hizo, Eli aliye mzee anakufa, akiwa “amehukumu Israeli kwa miaka 40.” (1 Samweli 4:18) Kuwa na Sanduku hilo kunatokeza msiba kwa Wafilisti, hivyo wanalirudisha kwa Waisraeli. Sasa Samweli anakuwa mwamuzi wa Israeli, na kuna amani katika nchi.

Maswali ya Kimaandiko Yajibiwa:

2:10—Kwa nini Hana alisali kwamba Yehova “ampe mfalme wake nguvu” ingawa wakati huo hakukuwa na mfalme wa kibinadamu aliyetawala Israeli? Sheria ya Musa ilikuwa imetabiri kwamba Waisraeli wangekuwa na mfalme wa kibinadamu. (Kumbukumbu la Torati 17:14-18) Katika unabii aliotoa alipokuwa akikaribia kufa, Yakobo alisema hivi: “Fimbo ya enzi [ishara ya mamlaka ya kifalme] haitageuka kando kutoka kwa Yuda.” (Mwanzo 49:10) Isitoshe, kumhusu Sara, nyanya wa Waisraeli, Yehova alisema hivi: “Wafalme wa vikundi vya watu watatoka kwake.” (Mwanzo 17:16) Hivyo, Hana alikuwa akisali kuhusu mfalme wa wakati ujao.

3:3—Je, kweli Samweli alikuwa akilala katika Patakatifu Zaidi? La. Samweli alikuwa Mlawi wa familia ya Wakohathi ambayo haikuwa familia ya kikuhani. (1 Mambo ya Nyakati 6:33-38) Kwa hiyo, hakuruhusiwa “kuingia ndani ili kuviona vitu vitakatifu.” (Hesabu 4:17-20) Sehemu pekee ya patakatifu ambayo Samweli aliruhusiwa kutumia ni ua wa maskani. Lazima iwe alikuwa akilala mahali hapo. Yaonekana Eli pia alikuwa akilala mahali fulani katika ua. Kwa wazi, maneno mahali “palipokuwa sanduku la Mungu” hurejelea eneo la maskani.

7:7-9, 17—Kwa kuwa dhabihu zilipaswa kutolewa kwa ukawaida mahali ambapo tu Yehova alichagua, kwa nini Samweli alitoa toleo la kuteketezwa huko Mispa na kujenga madhabahu huko Rama? (Kumbukumbu la Torati 12:4-7, 13, 14; Yoshua 22:19) Baada ya kuondolewa kwa Sanduku takatifu kutoka kwenye maskani huko Shilo, kuwapo kwa Yehova hakukudhihirishwa tena huko. Hivyo, akiwa mwakilishi wa Mungu, Samweli alitoa dhabihu ya kuteketezwa huko Mispa na pia kujenga madhabahu huko Rama. Yaonekana kwamba mambo hayo yalikubaliwa na Yehova.

Mambo Tunayojifunza:

1:11, 12, 21-23; 2:19. Mtazamo wa Hana kuhusu sala, unyenyekevu wake, kuthamini kwake fadhili za Yehova, na upendo wake wenye kudumu akiwa mama ni kielelezo kizuri kwa wanawake wanaomwogopa Mungu.

1:8. Elkana aliweka kielelezo kizuri kama nini katika kuwaimarisha wengine kwa maneno! (Ayubu 16:5) Kwanza alimwuliza Hana mwenye huzuni swali hili bila kuwa na nia ya kumhukumu: “Kwa nini moyo wako unahisi vibaya?” Swali hilo lilimtia Hana moyo kueleza hisia zake. Kisha Elkana alimhakikishia Hana upendo wake kwa kusema: “Je, mimi si bora kwako kuliko wana kumi?”

2:26; 3:5-8, 15, 19. Kwa kutimiza kwa bidii kazi ambayo tumepewa na Mungu, kunufaika na mazoezi ya kiroho, na kuwa wenye adabu na heshima, ‘tunaendelea kupendwa’ na Mungu na vilevile na wanadamu.

4:3, 4, 10. Hata lile sanduku la agano ambalo lilikuwa takatifu halikuweza kuwalinda. Tunapaswa ‘kujilinda na sanamu.’—1 Yohana 5:21.

MFALME WA KWANZA WA ISRAELI —JE, ALIFANIKIWA AU HAKUFANIKIWA?

(1 Samweli 8:1–15:35)

Samweli ni mwaminifu kwa Yehova maisha yake yote, lakini wanawe hawatembei katika njia za Mungu. Wanaume wa Israeli wanapoomba mfalme wa kibinadamu, Yehova anakubali ombi lao. Samweli anafuata mwongozo wa Yehova naye anamtia mafuta Sauli, Mbenyamini mwenye sura nzuri, awe mfalme. Sauli anaimarisha cheo chake akiwa mfalme kwa kuwashinda Waamoni.

Yonathani, mwana wa Sauli aliye shujaa anashinda kikosi cha askari Wafilisti. Jeshi kubwa la Wafilisti linashambulia Israeli. Sauli anaogopa sana na kwa kutotii, yeye mwenyewe anatoa dhabihu ya kuteketezwa. Akiwa tu na mchukua-silaha wake, Yonathani mwenye ujasiri anashambulia kituo kingine cha Wafilisti. Hata hivyo, Sauli anaapa bila kufikiri, na hivyo ushindi huo unakosa kukamilika. Sauli anaanza “kupiga vita kuzunguka pande zote” juu ya adui zake wote. (1 Samweli 14:47) Ingawa anawashinda Waamaleki, Sauli anakosa kumtii Yehova na kuhifadhi kile ‘kilichotengwa kwa ajili ya kuharibiwa.’ (Mambo ya Walawi 27:28, 29) Kwa sababu hiyo, Yehova anamkataa Sauli kuwa mfalme.

Maswali ya Kimaandiko Yajibiwa:

9:9—Maneno “nabii wa leo alikuwa akiitwa mwonaji nyakati za kale” yanamaanisha nini? Huenda maneno hayo yakamaanisha kwamba manabii walipozidi kuwa mashuhuri nyakati za Samweli na katika enzi za wafalme katika Israeli, neno “nabii” lilichukua nafasi ya neno “mwonaji.” Samweli huonwa kuwa wa kwanza katika orodha ya manabii.—Matendo 3:24.

14:24-32, 44, 45—Je, Yonathani alipoteza kibali cha Mungu kwa kula asali kinyume cha kiapo cha Sauli? Inaonekana tendo hilo halikumfanya Yonathani apoteze kibali cha Mungu. Kwanza, Yonathani hakujua kuhusu kiapo cha baba yake. Isitoshe, kiapo hicho ambacho kilichochewa ama na bidii isiyo ya kweli ama maoni yasiyo sahihi kuhusu mamlaka ya kifalme, kiliwaletea watu matatizo. Kiapo kama hicho kingewezaje kukubaliwa na Mungu? Ingawa Yonathani alikuwa tayari kuadhibiwa kwa sababu ya kuvunja kiapo hicho, hakuuawa.

15:6—Kwa nini Sauli aliwaonyesha Wakeni fadhili kwa njia ya pekee? Wakeni walikuwa wana wa baba-mkwe wa Musa. Waliwasaidia Waisraeli baada ya wao kuondoka kwenye Mlima Sinai. (Hesabu 10:29-32) Katika nchi ya Kanaani, Wakeni waliishi pia pamoja na wana wa Yuda kwa muda fulani. (Waamuzi 1:16) Hata ingawa baadaye waliishi kati ya Waamaleki na watu wa mataifa mengine, Wakeni waliendelea kuwa na uhusiano mzuri pamoja na Israeli. Kwa hiyo, Sauli alikuwa na sababu nzuri ya kuwahifadhi Wakeni.

Mambo Tunayojifunza:

9:21; 10:22, 27. Sifa za kiasi na unyenyekevu ambazo Sauli alikuwa nazo alipoanza kutawala zilimlinda asitende kwa upumbavu wakati ‘watu fulani wasiofaa kitu’ walipokataa asiwe mfalme. Kwa kweli, mtazamo huo hutulinda tusitende bila kufikiri.

12:20, 21. Usiruhusu kamwe “vitu visivyo vya kweli,” kama vile kutegemea watu, kutumaini uwezo wa kijeshi wa mataifa, au ibada ya sanamu, vikukengeushe usimtumikie Yehova.

12:24. Msaada muhimu wa kudumisha woga wenye heshima kwa Yehova na kumtumikia kwa moyo wetu wote ni ‘kuangalia mambo makuu ambayo amewafanyia’ watu wake katika nyakati za kale na pia za kisasa.

13:10-14; 15:22-25, 30. Jihadhari na kimbelembele, iwe kinaonyeshwa kupitia matendo ya kukosa utii au mtazamo wa kiburi.—Methali 11:2.

KIJANA MCHUNGAJI ACHAGULIWA KUWA MFALME

(1 Samweli 16:1–31:13)

Samweli anamtia mafuta Daudi wa kabila la Yuda ili awe mfalme wakati ujao. Muda mfupi baadaye, Daudi anamuua Goliathi, jitu la Wafilisti kwa jiwe la kombeo. Urafiki wa karibu unakua kati ya Daudi na Yonathani. Sauli anamweka Daudi kuwa mkuu wa mashujaa wake wa vita. Ili kushangilia ushindi mwingi wa Daudi, wanawake wa Israeli wanaimba hivi: “Sauli amepiga maelfu yake, na Daudi makumi ya maelfu yake.” (1 Samweli 18:7) Akiwa amejawa na wivu, Sauli anajaribu kumuua Daudi. Baada ya kushambuliwa mara tatu na Sauli, Daudi anatoroka na kuwa mkimbizi.

Katika miaka yake akiwa mkimbizi, Daudi anahifadhi uhai wa Sauli mara mbili. Pia anakutana na Abigaili mrembo na mwishowe anamwoa. Wafilisti wanaposhambulia Israeli, Sauli anamtafuta Yehova. Lakini Yehova amemwacha. Tayari Samweli amekufa. Akiwa na wasiwasi mwingi, Sauli anamwendea mwanamke mwenye kuwasiliana na pepo, naye anamwambia kwamba atauawa vitani na Wafilisti. Wakati wa mapigano hayo, Sauli anajeruhiwa vibaya, nao wana wake wanauawa. Simulizi hilo linamalizia kwa kuonyesha Sauli akifa bila kufanikiwa. Bado Daudi yuko mafichoni.

Maswali ya Kimaandiko Yanajibiwa:

16:14—Ni roho mbaya gani iliyomtia hofu Sauli? Roho mbaya iliyomkosesha Sauli amani ya akili ni mtazamo wake mbaya wa akilini na moyoni, yaani, tamaa yake ya ndani ya kufanya mabaya. Yehova alipoondoa roho yake takatifu, Sauli aliachwa bila ulinzi, hivyo akatawaliwa na roho yake mwenyewe iliyokuwa mbaya. Kwa kuwa Mungu aliruhusu roho hiyo ichukue mahali pa roho Yake takatifu, roho hiyo mbaya inaitwa “roho mbaya kutoka kwa Yehova.”

17:55—Kupatana na 1 Samweli 16:17-23, kwa nini Sauli aliuliza Daudi alikuwa mwana wa nani? Swali la Sauli halikuhusu tu jina la baba ya Daudi. Yaelekea alitaka sana kujua ni mtu wa aina gani aliyemzaa mvulana huyo ambaye alitimiza mambo ya ajabu kwa kuua jitu hilo muda mfupi tu kabla ya hapo.

Mambo Tunayojifunza:

16:6, 7. Badala ya kuvutiwa na sura ya nje ya wengine au kuwahukumu haraka, tunapaswa kujaribu kuwaona jinsi Yehova anavyowaona.

17:47-50. Tunaweza kukabili kwa ujasiri upinzani au mateso kutoka kwa maadui walio kama Goliathi kwa sababu “vita ni vya Yehova.”

18:1, 3; 20:41, 42. Marafiki wa kweli wanaweza kupatikana miongoni mwa wale wanaompenda Yehova.

21:12, 13. Yehova anatarajia tutumie uwezo wetu wa kufikiri na stadi zetu ili kushughulikia hali ngumu maishani. Ametupatia Neno lake lililoongozwa na roho, ambalo hutupa busara, ujuzi, na uwezo wa kufikiri. (Methali 1:4) Pia tuna msaada wa wazee Wakristo waliowekwa rasmi.

24:6; 26:11. Daudi anatuwekea kielelezo bora cha kuheshimu kikweli mtiwa-mafuta wa Yehova.

25:23-33. Busara ya Abigaili ni kielelezo kizuri.

28:8-19. Katika jitihada yao ya kuumiza au kuongoza watu vibaya, roho waovu wanaweza kujifanya kuwa watu fulani waliokufa. Tunapaswa kuepuka kuwasiliana na pepo kwa njia yoyote.—Kumbukumbu la Torati 18:10-12.

30:23, 24. Uamuzi huo unaotegemea Hesabu 31:27, unaonyesha kwamba Yehova anathamini wale wanaotegemeza kutaniko. Lolote tufanyalo, na ‘tulifanye kwa nafsi yote kama kwa Yehova, na si kama kwa wanadamu.’—Wakolosai 3:23.

Ni Nini Kilicho “Bora Kuliko Dhabihu”?

Ni kweli gani muhimu inayokaziwa na mambo yaliyotukia maishani mwa Eli, Samweli, Sauli, na Daudi? Ni hii: “Kutii ni bora kuliko dhabihu, na kusikiliza kuliko mafuta ya kondoo-dume; kwa maana uasi ni sawa na dhambi ya uaguzi, na kwenda kwa kimbelembele ni sawa na kutumia nguvu za uchawi na terafimu.”—1 Samweli 15:22, 23.

Tuna pendeleo kubwa kama nini kushiriki katika kazi ya ulimwenguni pote ya kuhubiri Ufalme na kufanya wanafunzi! Tunapomtolea Yehova “ng’ombe-dume wachanga wa midomo yetu,” tunapaswa kufanya yote tuwezayo kutii mwongozo anaotutolea kupitia Neno lake lililoandikwa na pia sehemu ya kidunia ya tengenezo lake.—Hosea 14:2; Waebrania 13:15.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 7 Kuhusu maeneo mbalimbali yanayotajwa katika kitabu cha Samweli wa Kwanza, ona ukurasa wa 18-19 wa broshua ‘Ona Nchi Nzuri,’ iliyochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

[Picha katika ukurasa wa 23]

Mfalme wa kwanza wa Israeli aliyekuwa mnyenyekevu na mwenye kiasi alibadilika na kuwa mtawala mwenye kiburi na kimbelembele

[Picha katika ukurasa wa 24]

Tunaweza kuwa na uhakika kuhusu jambo gani tunapokabili upinzani kutoka kwa maadui walio kama Goliathi?